Uhai—Zawadi ya Kuthaminiwa
YEHOVA MUNGU alipopatia familia ya kibinadamu pendeleo la uzazi, ilikuwa ni zawadi nzuri kama nini! Mtoto mwenye sura nzuri angefika na kukaribishwa kwa mikono inayongoja ya wenzi wa ndoa wenye furaha waliopendana na waliokuwa tayari kutunza na kulea tokeo hilo la muungano wao wa ndoa. Ni shangwe tu ingetokea kwa familia kadiri maisha ya mtoto yalipoanza kufunguka.
Lakini dhambi ya Adamu na Hawa ilileta matokeo yenye msiba kwa watoto waliozaliwa katika jamii ya kibinadamu. Likiwa tokeo la dhambi, mama yetu wa kwanza alilaaniwa apate maumivu na uchungu wa kimwili wakati alipozaa watoto. Na yale mazingira yenye dhambi ambamo watoto waliletwa ndani yayo yalifanya uzazi kuwa jambo gumu sana. Kwa hiyo, katika ulimwengu wa leo wenye mambo mengi, haishangazi kwamba kutungwa kwa mimba ya mtoto hakufurahiwi hata kidogo. Lakini, maoni ya Muumba juu ya watoto ambao hawajazaliwa ni nini? Je! maoni yake yamebadilika kwa kufuatana na viwango vinavyobadilika vya adili? Kwa hakika sivyo. Maoni yake na hangaiko lake kwa watoto ambao hawajazaliwa hayabadiliki.
Maandiko yaonyesha wazi kwamba ndani ya mama kuna mtu wa pekee anayekua. Maisha huanza wakati wa kutunga mimba. Kuzaliwa katika ulimwengu huonyesha tu binadamu mtoto ambaye ameonwa tayari na Mungu. Ezekieli azungumzia “kila mtoto anayefungua mimba.” (Ezekieli 20:26, New World Translation) Ayubu aeleza juu ya “milango ya tumbo la mamangu,” na kuita mimba zilizoharibika “wachanga wasiouona mwanga kabisa.”—Ayubu 3:10, 16.
Tazama maoni ya Yehova ya wororo kwa uhai dhaifu unapokua katika tumbo la uzazi. Alimwambia Yeremia: “Kabla sijakuumba katika tumbo nilikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa.” (Yeremia 1:5) Daudi alisema hivi: “Mifupa yangu haikusitirika kwako, nilipoumbwa kwa siri, nilipoungwa kwa ustadi pande za chini za nchi; macho yako yaliniona kabla sijakamilika.” (Zaburi 139:15, 16) Ayubu amwita Mungu “huyo aliyenifanya mimi ndani ya tumbo,” aliyeendelea ‘kutufinyanga tumboni.’—Ayubu 31:15.
Lakini vipi hangaiko la Mungu kwa mama mwenye mimba anayefadhaika na asiyetaka mtoto huyo? Kwa watu wote, ni Muumba anayetambua madaraka mazito ya uzazi. Ikiwa mama mwenye mimba, ingawa ana magumu mengi, achagua kuhifadhi mimba kwa sababu ya kustahi matakwa ya kimungu, je, Mungu hatabariki uamuzi wake? Mzazi anaweza na anapaswa ifaavyo kumwomba msaada wake katika kulea mtoto mwenye furaha. Katika kurasa za Neno lake, Mungu tayari ametoa mashauri bora zaidi yanayopatikana juu ya kulea watoto. Kutumia kanuni za Biblia katika maisha ya familia kutaleta matokeo mazuri sana. Zile shangwe na thawabu za kulea watoto wanaomcha Mungu zinashinda kwa mbali dhabihu zozote zinazofanywa wakati wa malezi, kama vile mzazi yeyote mwenye fahari anavyoweza kuthibitisha.
Je! Yehova huona mambo kwa njia tofauti ikiwa mtoto huyo alitokana na kunajisiwa au ugoni wa kifamilia? Ingawa kitendo hicho dhidi ya mama kilikuwa kinyume cha sheria, mtoto si wa kulaumiwa. Kukomesha uhai wake kungekuwa tu kukinza kitendo kimoja cha jeuri kwa kingine cha jeuri. Kwa hakika Yehova anatambua maumivu makali ya kihisia-moyo ambayo hao akina mama hupitia na anaweza kumsaidia mama na mtoto wakabiliane na matokeo ya baadaye kwa njia inayofaa.
Namna gani ikiwa daktari amjulisha mwanamke mwenye mimba kwamba uhai wake waweza kuhatarishwa akibeba mimba hiyo mpaka wakati wa uzazi? Dkt. Alan Guttmacher alisema hivi: “Leo inawezekana kwa karibu kila mgonjwa kupitia uzazi akiwa hai, ijapokuwa tu akiwa anaugua ugonjwa mbaya wa kuua kama kansa au leukemia, na ikiwa hivyo, utoaji-mimba hautaongeza urefu wa maisha licha ya kuokoa uhai.” The Encyclopedia Americana yasema hivi: “Kwa kuwa wanawake wengi wanaweza kupitia uzazi hata wakiwa na matatizo makubwa ya afya, ni visa vichache sana vya utoaji-mimba vinavyohitajiwa ili kulinda afya ya mama. Utoaji-mimba mwingi hufanywa ili kuepuka kuwa na mtoto.” Kwa hiyo, hali kama hizo ni chache sana. Hata hivyo, ikitokea wakati wa uzazi, basi wazazi wanapaswa kuchagua kati ya uhai wa mama na ule wa mtoto. Ni uamuzi wao.
Je! ni ajabu kwamba Muumba wa uhai ameweka kanuni zilizo wazi juu ya matumizi ya uwezo wetu wa uzazi? Machoni pake, kutunga uhai ambao mtu hayuko tayari kutunza ni dhambi, kama vile ilivyo dhambi kuondoa uhai.
Kwa hakika, mzozo huo wa utoaji-mimba utaendelea mpaka mwisho wa mfumo huu. Lakini kwa habari ya Muumba wa uhai, Yehova Mungu, pamoja na wale wanaothamini sheria zake, hakuna shaka lolote. Uhai ni kitu cha thamani kubwa—zawadi ya kutunzwa vizuri na kuthaminiwa kuanzia mwanzo wao kabisa.
[Sanduku katika ukurasa wa 11]
Kuuona Utoaji-Mimba kwa Njia ya Mungu
ITAKUWAJE kwa msichana mdogo anayeshika mimba nje ya ndoa na ambaye hayuko tayari hata kidogo kwa daraka la umama? Je! aruhusiwe kuleta mtoto katika ulimwengu? Hisia za Mungu kumwelekea mtoto huyo hazikubadilika eti kwa sababu tu mama yake alitenda kipumbavu na kwa njia inayokosa adili. Kuzaliwa kwa mtoto kwaweza sana kumsaidia mama yake ang’amue matokeo ya asili ya ukosefu wake wa adili na kwa hiyo kumkazia hekima ya sheria za Mungu. Kuondoa uthibitisho wa ngono yake haramu kwaweza kumwacha akiwa na uchungu wa hatia, au kwaweza kumfanya ajiingize hata zaidi katika vitendo vingine vya ukosefu wa adili.
Ikiwa hakuna baba anayeshiriki mzigo huo, itakuwa vigumu kumlea mtoto huyo. Lakini uhusiano wenye nguvu pamoja na Baba yetu wa kimbingu waweza kumwandalia mama nguvu za adili na hisiamoyo, utegemezo, na mwongozo ili afaulu. Pia ameandaa kundi la Kikristo lisaidie kupunguza mzigo wa wazazi wasio na wenzi.