Sura ya 7
Kuwa na Watoto— Daraka na Thawabu
1-4. (a) Kuna mambo gani machache yenye kustaajabisha juu ya ukuzi wa kitoto kichanga ndani ya tumbo la uzazi? (b) Kujua mambo hayo kunakusaidiaje uthamini maneno ya Zaburi 127:3?
KUZAA WATOTO ni taraja lenye kufurahisha na linalotaka kufikiriwa kwa uzito vilevile. Ni kweli kwamba ni jambo linalotukia kila siku kati ya wanadamu. Hata hivyo kila uzazi ni matokeo ya utaratibu wa ajabu na ulio mgumu. Tunapofahamu jambo fulani juu ya hayo, tunaweza kuona vizuri zaidi sababu gani mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu alisema hivi: “Tazama, wana ndio urithi wa [Yehova ] , uzao wa tumbo ni thawabu.” (Zaburi 127:3) Ebu angalia yanayotukia.
2 Chembe moja ya mbegu kutoka kwa mwanamume inaungana na yai lililo ndani ya mwanamke. Chembe hizo mbili zinakuwa kitu kimoja, na moja hiyo inaanza kugawanyika. Inakuwa chembe mbili, hizo mbili zinakuwa nne, na nne zinakuwa nane, mpaka mwishowe chembe hiyo moja inapokuwa mtu mzima, kadiri ya chembe 60,000,000,000,000! Kwanza chembe hizo mpya zilikuwa namna moja, kisha zikaanza kugeuka kuwa namna mbalimbali—chembe za mifupa, chembe za minofu, chembe za mishipa ya fahamu, chembe za ini, chembe za macho, chembe za ngozi, na kuendelea vivyo hivyo.
3 Siri fulani za kuzaana na za kuonyesha aina ya chembe hii na chembe hii na kazi zao, zimefunuliwa, lakini nyingi zimebaki bila kufunuliwa. Ni nini kinachoifanya chembe ya kwanza ianze kugawanyika? Wakati kugawanyika huko kunapoendelea, ni nini kinachozifanya chembe zianze kugeuka kuwa namna nyingi zilizo tofauti? Ni nini kinachozifanya namna hizo mbalimbali ziungane pamoja katika maumbo ya pekee, ukubwa na kazi za pekee, kuwa ini, pua, kidole kidogo cha miguu? Mageuzo hayo yanaanza kutokea wakati uliotangulia kuwekwa. Ni nini kinachoongoza mipango hiyo ya wakati uliowekwa? Vilevile, mimba hiyo inayoanza kukua ndani ya tumbo la uzazi la mama ni mwili na umbo la kurithi ambalo ni tofauti na lake. Kwa kawaida mwili wake unakataa vitu vya kigeni, kama vile ngozi au viungo vinavyotiwa katika mwili wa mtu kutoka kwa watu wengine. Kwa sababu gani mwili wake haukatai mimba hiyo ya uzazi ambayo ni kitu kigeni, badala ya kuilisha muda wa siku kama 280?
4 Kazi hizo zote za ajabu zinatokea kwa wakati uliopangwa kwa sababu Yehova Mungu alizipangia utendaji katika chembe moja inayofanyizwa na shahawa na yai la mwanamke. Mtunga zaburi anaonyesha hilo anapomwambia Muumba hivi: “Macho yako yaliona hata mwanzo wa mimba yangu, na sehemu zake zote ziliandikwa katika kitabu chako, kwa habari za siku zile wakati zilipofanywa na wakati huo mojawapo ya hizo ilikuwa bado kuwapo.”—Zaburi 139:16, NW.
UKUZI NA KUZALIWA
5-8. Kati ya juma ya nne ya kuwa na mimba na kuzaliwa kwa kitoto kichanga, ni mambo gani machache yanayotukia ndani ya tumbo la uzazi?
5 Mimba inakua haraka. Muda wa juma ya nne inakuwa na ubongo, mishipa ya fahamu, na mishipa ya damu pamoja na moyo ukivuta damu na kupitisha katika mishipa iliyokwisha kuwekwa tayari. Damu inafanyizwa na kifuko cha kiini cha yai muda wa juma sita; kisha ini nalo linachukua kazi hiyo, ambayo mwishowe inafanywa na mafuta yaliyo katika mifupa. Katika juma ya tano mikono na miguu inaanza kutokea; katika muda wa juma nyingine tatu, vidole vya mikono na vya miguu vinatokea. Juma ya saba minofu mikubwa inakuwa imefanyizwa pamoja na macho, masikio, pua na mdomo.
6 “Mifupa yangu,” mtunga zaburi anaendelea, akimwambia Yehova, “hukufichwa wewe wakati nilipofanywa kwa siri.” (Zaburi 139:15, NW) Katika juma ya tisa kiungo fulani kilicho laini kinaanza kugeuka kuwa mfupa wakati boma la mifupa linapofanyizwa, na kile kitoto kinachokua kinaitwa sasa kijusu (mimba ya miezi minne) badala ya mimba. “Wewe mwenyewe ulifanyiza figo zangu.” (Zaburi 139:13 NW) Taratibu zilizowekwa na Mungu ili ziongoze mambo hayo zinatokea katika mwezi wa nne, nazo figo sasa zinachuja damu.
7 Wakati huo kile kitoto kinachokua kinajongeza na kujipotapota, kinasokota vidole vyake vya mikono au vya miguu wakati kiganja cha mkono wake au wayo wa mguu wake unaposikia msisimuko. Kinashika vitu kwa chanda na kwa kidole gumba, na kunyonya kidole gumba chake na kwa njia hiyo kuzoeza mishipa itakayotumiwa baadaye kujinyonyesha maziwa ya mama yake. Kinapiga kitefutefu (hiccup), na mama anasikia kikiruka. Wakati wa mwezi wa sita viungo vingi karibu vimekamilika. Vitundu vya pua vimefunguka, kope zimetokea, upesi macho yatafunguka, nayo masikio yatatenda kazi hivi kwamba hata katika tumbo la uzazi kitoto kichanga kinaweza kushtushwa na makelele makubwa.
8 Juma zinapotimia 40, utungu (uchungu) wa kuzaa unaanza. Mishipa ya mji wa mimba ya mama inafinyana na kuwa mifupi na kitoto sasa kinaelekea kuzaliwa. Wakati wa kuzaliwa, mara nyingi kichwa chake kinafinywa kisiwe na umbo la kawaida, lakini, kwa kuwa mifupa yake ya kichwa haijaungana pamoja, baada ya kuzaliwa kichwa kinakuwa na umbo lake la kawaida. Mpaka sasa mama amekifanyia kitoto kichanga kila jambo: amekipa hewa safi inayotakiwa (oksijeni), chakula, ulinzi, umotomoto na vilevile kuondolewa kwa takataka (uchafu). Sasa yakipasa kitoto kichanga kijifanyie kazi upesi, ama sivyo kitakufa.
9. Ili kitoto kichanga kiishi nje ya tumbo la uzazi, ni mageuzo gani yanayopaswa kutukia upesi?
9 Ni lazima kianze kupumua ili mapafu yatie oksijeni katika damu. Lakini ili jambo hilo lifanywe, ni lazima geuzo jingine kubwa litukie mara moja: ni lazima njia ya kupitishia damu igeuke! Wakati kijusu kilipokuwa katika tumbo la uzazi, kulikuwako na tundu katika ukuta wa moyo wacho. Ukuta huo ulitenga chumba cha upande wa kulia na chumba cha upande wa kushoto cha moyo na kuizuia damu nyingi ya kitoto kichanga isiende kwenye mapafu wakati wo wote. Kwa habari ya damu iliyofanya hivyo, mshipa mkubwa ulipeleka sehemu kubwa ya damu kwa kupita kando ya mapafu. Humo tumboni mwa uzazi, kiasi cha kumi (10%) kwa mia cha damu tu ndicho kilichopitia njia ya mapafu; baada ya kuzaliwa damu yote inapaswa ifanye hivyo, tena bila kukawia! Ili kutimiza jambo hilo, kwa muda wa nukta chache baada ya kuzaa, ule mshipa mkubwa wa damu uliopita kando ya mapafu unafinyana, na ile damu iliyopitia humo, inakwenda sasa kwenye mapafu. Wakati huu lile tundu lililo katika ukuta wa moyo linaziba, na damu yote ile inayovutwa kutoka upande wa kulia wa moyo inakwenda sasa kwenye mapafu ikatiwe oksijeni. Kitoto kichanga kinapumua, damu hiyo imetiwa oksijeni, mageuzo makubwa yamekwisha fanyika na kitoto kinaishi! Kama mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu alivyojumlisha mambo yote kwa uzuri sana: “Uliendelea kunificha katika tumbo la mama yangu. Nitakusifu wewe kwa sababu kwa njia yenye kutia hofu nimeumbwa kiajabu.”—Zaburi 139:13, 14, NW.
10. Kwa kufikiria ukuzi wa ajabu wa kitoto kichanga ndani ya tumbo la uzazi, imewapasa wazazi wawaoneje watoto wao?
10 Lo! jinsi inavyowapasa watu waliooana waione kwa shukrani zawadi hii kutoka kwa Yehova! Ule uwezo wa kuzaa kiumbe cha kibinadamu, mtoto ambaye ni sehemu yao wawili lakini aliye tofauti na kila mmoja wao! Kweli kweli, “ndio urithi wa [Yehova]”!
KUUTUNZA “URITHI” HUO
11. Ni maulizo gani ambayo wale wanaofikiria kuanza jamaa wamepaswa wajiulize wenyewe, na kwa sababu gani?
11 Kulikuwako sababu nyingine kuliko ile ya uadilifu (inayopasa wema na ubaya) iliyomfanya Yehova Mungu aweke sheria iliyoamuru ngono zifanywe kati ya watu waliooana tu. Alikuwa akifikiria vilevile kuzaliwa kwa watoto. Mtoto anahitaji baba na mama wanaopendana na watakaopenda na kuutunza uzao wao. Mtoto anayezaliwa sasa hivi anahitaji upendo na usalama wa nyumbani, akiwa na baba na mama wanaomtaka na watakaompatia mazingira (hali) yanayotakiwa ili apate kukua na kusitawisha utu wake. Mume na mke wanaofikiria kuzaa mtoto wamepaswa wajiulize hivi: Je! tunataka mtoto? Je! tunaweza kumpatia mambo ambayo anataka—si yale ya kimwili tu, bali ya kimoyoni na ya kiroho vilevile? Je! tutamlea vya kufaa, tumwekee mifano mizuri ya kufuata? Je! tuna nia ya kuyakubali madaraka yanayoletwa na uzazi, na kukubali kujinyima mambo fulani? Labda tulipokuwa watoto ilionekana kwamba wazazi wetu walituzuia tusiwe na uhuru, lakini tunapokuwa wazazi tunaona namna kulea watoto kulivyo kazi yenye kutumia wakati mwingi sana. Lakini daraka la kuwa mzazi laweza kuleta furaha nyingi vilevile.
12-14. Mwanamke akiisha kupata mimba, anaweza kusaidiaje kitoto kichanga kipate kukua na afya nzuri kwa (a) chakula anachokula? (b) anavyofanya na vileo, tumbako, dawa za kulevya? (c) kuzuia mahangaiko yake ya moyo?
12 Uamuzi umekwisha kufanywa—kwamba na wazazi ama na hali za uzazi. Wewe, mke, umepata mimba. Utunzaji wa huu “urithi wa [Yehova]” unaanza. Inakupasa ule vyakula fulani, inakupasa uepuke kula vingine au kula kwa kiasi. Vyakula vilivyo na madini nyingi za chumaa ni vya maana sana, kwa kuwa katika tumbo la uzazi kile kitoto kichanga kinaweka akiba ya chuma cha kutosha kuendelea muda wa miezi sita kikiisha kuzaliwa. Unahitaji kunywa maziwa mengi zaidi (vilevile jibini au fromage inafaa) ili utoe calcium ambayo kitoto chako kichanga kinahitaji ili mifupa ikue. Na chakula sawa kilicho na carbohydrate au hydrate de carboneb (sukari na wanga au amidon) kitakusaidia uepuke kunenepa mno. Ni kweli kwamba mnakula watu wawili, lakini mmoja ni mdogo sana sana!
13 Labda mambo mengine yanahitaji au hayahitaji kufikiriwa, ikitegemea namna mnavyoishi. Vinywaji vyenye kileo vinapeleka kileo kwenye kijusu, kwa hiyo ni lazima kuangalia, kwa vile kiasi kinachozidi kingeweza kuzuia maendeleo ya akili na ya mwili. Vitoto vingine vimezaliwa vikiwa vimelewa kwa sababu mama zao walikuwa wanywaji sana wa pombe. Kuvuta tumbako kunatia sumu yake katika damu ya kijusu (kitoto au mimba ya miezi minne), na vilevile inafanya hewa chafu ikae katika damu yake badala ya hewa safi (oksijeni). Kwa njia hiyo, matazamio ya kitoto kichanga kupata afya ya kawaida yanaweza kuharibiwa hata kabla hakijazaliwa, kusiwe na dawa. Kuharibika kwa mimba ghafula na vitoto vinavyozaliwa vikiwa vimekufa ni mambo yanayotukia kwa kawaida katika wanawake wanaovuta tumbako. Dawa za kulevya zinazotumiwa na mama zaweza kufanya kitoto kizaliwe kikiwa na mazoea ya kutumia dawa hizo za kulevya, vilevile dawa fulani zisizo za kulevya zinazotumiwa ili kuponya magonjwa fulani zaweza kuwa za hatari, labda hata kukilemaza kitoto. Hata kunywa kahawa kupita kiasi kunadhaniwa kuwa kunaweza kufanyiza madhara (maumizo) fulani.
14 Tena, hangaiko la moyo katika mama laweza kugeuza mtoko wa umajimaji unaochochea viungo vingine ndani ya mwili wake na kukichochea mno kijusu, na hivyo kufanya kitoto kichanga kilichozaliwa sasa hivi kiwe kitukutu na chepesi kukasirika. Kitoto kichanga kinachokua chaweza ‘kufichwa katika tumbo la mama yake,’ lakini kungekuwa kukosea kudhani kwamba kimezuiwa kabisa kisipatwe na hali zinazokizunguka. Kinaweza kupatwa nazo kupitia kwa mama; yeye ndiye njia yake pekee ya kupokelea hali zilizo nje yake, na hilo linampa hasa uwezo wa kuamua kama matokeo hayo ni mema au mabaya. Namna anavyojitunza mwenyewe na namna anavyoitikia hali hizo itaonyesha tofauti kati ya hayo. Ni wazi kwamba inampasa ashirikiane na wale walio karibu yake katika jambo hilo, na sana sana anahitaji upendo na utunzaji wa mume wake.—Linganisha 1 Samweli 4:19.
MAAMUZI YANAYOKUPASA KUFANYA
15, 16. Ni maamuzi gani yanayopaswa kufanywa juu ya mahali na namna mtoto atakavyozaliwa?
15 Je! utazalia mtoto wako katika hospitali au nyumbani? Huenda mara nyingine ukalazimika kufanya moja la hayo. Huenda katika maeneo mengi kusiweko hata mahospitali. Katika maeneo mengine huenda lisiwe jambo la kawaida kuzaa mtoto nyumbani, na huenda kukatokeza hatari kwa sababu ya kukosa msaada wa mzalishi aliye na ujuzi. Wakati wo wote inapowezekana, inafaa nyakati zote kuchunguzwa na daktari wakati wa kuwa mjamzito (mimba), upate kujua kama unaweza kutazamia kuzaa kama ilivyo kawaida au utazaa kwa taabu.
16 Je! utakubali mtoto wako azaliwe kwa njia inayotumiwa kumpa mama dawa za kupoteza fahamu na maumivu au atazaliwa kwa njia ya asili? Yakupasa wewe na mume wako mwamue, mkiisha kuyachunguza mambo yenye kuleta faida na yenye kuleta hasara. Huenda kuzaa katika njia ya asili kukampasa mume wakati wa tukio la maana. Kwa kutumia njia hiyo, mtoto mchanga anawekwa pamoja na mama yake bila kukawia. Ikiwa uchunguzi wa daktari unaonyesha kwamba kuzaa huko hakutakuwa na magumu ye yote, wengine wanaamini kwamba hizo ni faida zinazopaswa kufikiriwa sana. Wachunguzi wengine wanasisitiza kwamba watoto wanaozaliwa katika hali zilizo tulivu zaidi za uzazi wa kutumia njia ya asili, hawana mahangaiko mengi ya moyoni na magonjwa ya akili.
17-19. Uchunguzi umefunua nini juu ya kufaa kwa mtoto kuwa pamoja na mama yake upesi iwezekanavyo akiisha kuzaliwa?
17 Gazeti linaloitwa Psychology Today, toleo la Desemba 1977, linaeleza hivi:
“Kwa miaka mingi wachunguzi wamepata kujua ya kwamba mwaka wa kwanza wa maisha ya mtoto unaweza kuwa na matokeo yenye kuendelea juu ya ukuzi wake wa baadaye wa akili na wa mwili. Kwa sasa inaonekana kwamba siku ya kwanza kuzaliwa mtoto—labda hata dakika zake za kwanza 80—ni za maana sana vilevile. Kile kifungo cha upendo na huruma anachofanyiza mama juu ya mtoto, na utunzaji anaoanza kumpatia, ni mambo ya maana sana baada ya kuzaliwa mtoto. Vilevile, uchunguzi wa karibuni sana unaonyesha kwamba zile saa za kwanza zinaweza kupasa sana kusitawishwa kwa maoni ya mama kuelekea mtoto wake, nguvu ya daraka la kumtimizia mahitaji yake, na uwezo wake wa kumlea.”
18 Ikiwa mama hapewi zile dawa za kawaida za kupoteza fahamu na za kutuliza maumivu wakati wa kuzaa, mtoto atakuwa macho, akitazama huku na huku, akifuata miendo ya watu, akigeuka anaposikia sauti za watu, na sana sana aweze kuijua sauti nyembamba ya kike. Upesi mama na mtoto wanaweza kutupiana macho. Jambo hilo laonekana kuwa la maana, na katika uchunguzi fulani akina mama wametoa taarifa kwamba wakati mtoto wao alipowatazama walijiona kuwa karibu zaidi sana naye. Kugusana kwa mwili wa mama na wa mtoto mara baada ya kuzaliwa, kunaonwa kuwa faida kwa wote wawili.
19 Wachunguzi wanadai kwamba magumu yanayowapata watoto wachanga wanaotunzwa na vituo vya afya yanaanza saa chache za kwanza za maisha. Ulinganifu uliofanywa kati ya watoto wanaopewa utunzaji bora katika hospitali wakati wa kuzaliwa na wale wengine wanaopewa kwa mama zao mara hiyo, unaonyesha kwamba baada ya mwezi mmoja watoto wachanga waliozaliwa kwa njia ya asili walikuwa bora. “Hata kwa kustaajabisha zaidi,” Psychology Today laeleza, “katika umri wa miaka mitano, watoto wenye kutunzwa na mama zao walionyesha uwezo mkubwa wa kuwa na akili nyingi nao walishinda mtihani wa lugha kuliko watoto waliotunzwa kulingana na kawaida ya utaratibu wa hospitali.”
20. Ili kuamua kwa hekima juu ya mambo hayo, ni jambo gani jinginelo linalopaswa kukumbukwa?
20 Walakini, katika yote hayo ni lazima hali zichunguzwe kwa uangalifu. Tusisahau kwamba wazazi wetu wa kwanza wa kibinadamu walituachia urithi wa kutokamilika. Kwa lazima urithi huo unanyang’anya leo “uzazi wa asili” sehemu fulani ya hali yake ya asili, na makosa tuliyorithi yanaweza kuleta magumu. (Mwanzo 3:16; 35:16-19; 38:27-29) Acha uamuzi wenu uongozwe na hali zenu wenyewe na jambo mnalosadiki kuwa la hekima zaidi katika hali yenu, kwamba hilo linapatana na uzazi “bora” ambao wengine wanakusudia kuwa nao au sivyo.
21, 22. Kuna faida gani za kunyonyesha mtoto maziwa ya mama?
21 Je! utamnyonyesha mtoto wako maziwa yako mwenyewe? Kuna faida nyingi kwako na mtoto wako vilevile. Maziwa ya mama ndicho chakula bora cha watoto wachanga. Ni chepesi kuyeyuka tumboni, na kinatoa ulinzi juu ya magonjwa, machafuko ya tumboni na magumu yanayokamatana na kupumua. Siku chache za kwanza matiti yanatoa maziwa ya manjano yanayovifaa sana vitoto vichanga kwa sababu (1) hayana mafuta na sukari nyingi na wanga (amidon), nayo yanayeyuka vyepesi zaidi tumboni, (2) yana nguvu sana ya kuzuia magonjwa kuliko maziwa ya mama yatakayotokea siku chache baada ya hapo, na (3) hayamfanyi mtoto mchanga apate kuendesha (kuhara) sana kunakosaidia kuondoa chembe, ute na nyongo zilizolundamana katika matumbo ya kitoto kichanga kabla ya kuzaliwa.
22 Kunyonyesha mtoto maziwa ya mama kunamfaidi mama. Kunapunguza kutokwa kwa damu ya mama kwa sababu kule kunyonya kwa mtoto kunaamsha mji wa mimba ili upate kurudi mahali pake. Vilevile kunyonya kunaamsha matiti yapate kutoa maziwa mengi zaidi, na akina mama waliokuwa wakiogopa kwamba hawangeweza kutoa maziwa ya kutosha, sasa wanaona kwamba hakuna upungufu wa maziwa. Mara nyingine kunyonyesha mtoto maziwa ya mama kwa kawaida kunaahirisha (kunakawiza) muda yai la kike linapoanza safari ya kwenda kukutana na mbegu ya kiume na vilevile kipindi cha kuingia mwezini (hedhi), na kwa kadiri hiyo kunaelekea kuwa njia ya asili ya kuzuia kupata mimba nyingine. Chama kinachoitwa American Cancer Society kinasema kwamba “akina mama wanaonyonyesha watoto wao maziwa ya mama hawapatwi sana na ugonjwa wa donda la matiti.” Vilevile, kunyonyesha mtoto maziwa ya mama kunapunguza gharama za jamaa!
UKUZI WA MTOTO—UTAULENGA MSHALE NAMNA GANI?
23. Ni kanuni gani juu ya kulea watoto zinazoonyeshwa katika Zaburi 127:4, 5?
23 “Kama mishale mkononi mwa shujaa, ndivyo walivyo wana wa ujanani. Heri mtu yule aliyelijaza podo lake hivyo.” (Zaburi 127:4, 5) Ubora wa mshale unajulikana kwa namna unavyolengwa vizuri wakati unapouacha upinde. Mshale unapaswa ulengwe kwa uangalifu na kwa ufundi ili upige shabaha. Kwa njia iyo hiyo, inawafaa ninyi kama wazazi, mwufikirie kwa, hekima na kwa sala mwanzo wa maisha mtakaompa mtoto wenu. Je! atakapoacha kuwa chini ya ulinzi wenu, atakuwa mtu mzima aliyesawazika na aliyekomaa, mwenye kuheshimiwa na wengine na kuwa heshima kwa Mungu?
24. (a) Ni mazingira (hali) gani ya nyumbani ambayo wazazi wamepaswa kujitahidi kufanyia watoto wao? (b) Sababu gani hilo ni jambo la maana?
24 Maamuzi juu ya atakavyotunzwa na kupewa malezi yamepaswa yafanywe kabla mtoto hajazaliwa. Kwanza, wazazi ndio mazingira (hali) yote ya kwanza ya mtoto mchanga. Mazingira hayo yatakuwa ya namna gani? Je! yataonyesha kwamba wazazi wanathamini shauri hili linalotoka katika Neno la Mungu: “Uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano yaondoke kwenu, pamoja na kila namna ya ubaya; Lena iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi”? (Waefeso 4:31, 32) Vyo vyote maisha ya nyumbani yalivyo, yataonekana katika mtoto mchanga. Jaribuni kuyafanya mazingira ya mtoto wenu kuwa ya amani na usalama, ya uchangamshi na upendo. Mtoto anayependwa sana atafuata sifa hizo nazo zitageuza maoni yake ya moyoni kuwa hivyo. Maoni yenu yatajulikana, mifano yenu itafuatwa. Sheria za uzazi za Muumba wetu zilifanya mipango ya ajabu ili mtoto apate ukuzi ndani ya tumbo la uzazi: mtauendeleza namna gani nje ya tumbo la uzazi? Mambo mengi sana yanategemea hali za nyumbani mnazotoa. Hali hizo, pamoja na sheria za uzazi, zinaamua namna ya mtu mzima atakavyokuwa mtoto wenu. “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.”—Mithali 22:6.
25, 26. Sababu gani ni jambo la busara kwa wazazi kutumia wakati mwingi na uangalifu wao kwa watoto wao?
25 Wala mwanamume wala mwanamke hawezi kufanyiza kipande kimoja cha jani, lakini wakiwa pamoja wanaweza kuzaa mwanadamu, aliye na mambo magumu kufahamika yasiyo na mwisho, na aliye tofauti na mtu mwingine ye yote duniani! Ni tendo la ajabu, lenye kustaajabisha sana hivi kwamba ni vigumu kusadiki sababu gani watu wengi leo wanakosa kuthamini ubora wa daraka linalofuatana na tendo hilo! Watu wanapanda maua, wanayamwagilia maji, kuyawekea mbolea, wakiyapalilia—yote hayo wanafanya ili wawe na bustani nzuri. Je! tusitumie wakati mwingi zaidi na jitihada nyingi zaidi tuwafanye watoto wetu wawe wazuri?
26 Mume na mke waliofunga ndoa wana haki ya kuzaa watoto. Watoto wao wana haki inayolingana ya kuwa na wazazi kwa hakika, si katika jina tu. Huenda Mkristo aliyejiweka wakfu kwa Mungu akatumia wakati na juhudi nyingi akishiriki maarifa ya Biblia pamoja na mtu mwingine kwa kutumaini kumfanya awe mwanafunzi, hata hivyo asifanikiwe sikuzote. Je! wazazi ambao ni Wakristo wasitumie wakati mwingi hata zaidi ya huo ili ‘wawalee watoto wao wenyewe katika adabu na rekebisho la moyoni la Yehova’? (Waefeso 6:4, NW) Wakimlea mtoto mmoja awe mtumishi mwema wa Yehova Mungu, Mpaji wa uzima, je! hilo si jambo la kuwafanya wafurahi sana? Ndipo, kweli kuzaa kwao mwana au binti huyo kutakapokuwa kumethawabishwa sana.—Mithali 23:24, 25.
27. Sababu gani utu wa mtoto mwenyewe umepaswa ufikiriwe katika kuongoza ukuzi wake?
27 Zaburi 128:3 inawafananisha watoto na mizeituni: “Mkeo atakuwa kama mzabibu uzaao, vyumbani mwa nyumba yako. Wanao kama miche ya mizeituni.” Miti inaweza kugeuzwa katika njia nyingi kwa kuizoeza. Mingine inakuzwa ikiwa imelala juu ya ukuta. Mingine inatambaa ikining’inia chini kidogo. Mingine hata inafanywa iwe midogo na mifupi kwa kukata mashina yao na kuisongamanisha pamoja, kama mimea inayopandwa katika vyungu. Mithali moja inakazia namna malezi ya mapema yatakavyomfanya mtoto awe baadaye vilevile: “Mtoto alewavyo ndivyo akuavyo.” Hapa panahitaji usawa. Kwa upande mmoja, mtoto anahitaji kuongozwa ili afuate kawaida za haki. Wakati uo huo mtoto asitazamiwe kufuata fikira fulani za wazazi ambazo wametangulia kuwazia juu ya utu hasa anaopaswa kuonyesha. Huwezi kufanya mzeituni uzae tini. Mlee mtoto wako katika njia zinazofaa lakini usimlazimishe kufuata mfano fulani uliotangulia kukusudiwa, ambao hautamruhusu aonyeshe utu wake mwenyewe na vipawa alivyorithi apate kuona njia ya kawaida ya kuvionyeshea. Jipe mwenyewe wakati wa kutosha ili upate kumjua mtoto huyo ambaye umezaa. Halafu, kama mti mchanga mwororo (laini), mpe mtoto wako uongozi wenye nguvu sana ili umlinde na kumtegemeza katika njia inayofaa, lakini uwe uongozi wa upole sana ili usije ukamzuia akose kukua awe mzuri kama anavyotakiwa.
NI THAWABU KUTOKA KWA YEHOVA
28. Tunaweza kufaidikaje na yanayosemwa na Mwanzo 33:5, 13, 14 juu ya namna Yakobo alivyohangaikia watoto wake?
28 Yakobo wa kale alitamani sana kutunza watoto wake. Wakati safari ilipopangwa, ambayo bila shaka ilikuwa ya mwendo mrefu mno kwao, Yakobo alimwambia aliyekuwa akipanga safari hiyo hivi “Bwana wangu anajua ya kuwa watoto ni wachanga, tena kondoo na ng’ombe nilio nao wanyonyesha. Hao wanyama wakiharakishwa siku moja, watakufa wote. Tafadhali bwana wangu na apite mbele ya mtumwa wake; nami nitawaongoza polepole kwa kadiri ya mwendo wa wanyama walio mbele yangu, na kwa kadiri ya mwendo wa watoto.” Alipokuwa akikutana mapema na Esau ndugu yake, aliulizwa hivi, “Ni nani hawa walia pamoja nawe?” Jibu la Yakobo lilikuwa hivi, “Ni watoto Mungu aliompa mtumwa wako kwa neema yake.” (Mwanzo 33:5, 13, 14) Haiwapasi wazazi leo wawaonyeshe watoto wao huruma tu, bali wawaone vilevile kama Yakobo alivyowaona—kuwa neema kutoka kwa Yehova. Bila shaka, kabla ya kuoa, imempasa mwanamume afikirie kwa uzito kama anaweza kulisha na kutunza mke na watoto wake. Biblia inashauri hivi: “Tengeneza kazi yako huko nje, jifanyizie kazi yako tayari shambani, ukiisha, jenga nyumba yako.” (Mithali 24:27) Kupatana na shauri hilo linalofaa, imempasa mwanamume afanye mapema matayarisho ya ndoa na ya maisha ya jamaa. Kisha, hata ikitokea mimba isiyo na mpango, itashangiliwa kwa furaha wala haitaogopwa kuwa gharama.
29. Sababu gani shauri la kuzaa watoto limepaswa lifikiriwe kwa uzito mapema?
29 Kwa wazi, shauri hilo la kuzaa watoto lastahili kufikiriwa kwa uzito sana, si kwa habari ya mzaliwa wa kwanza tu bali vilevile na wo wote wanaoweza kuzaliwa baadaye. Je wazazi wanaona ni vigumu kulisha, kutunza na kulea watoto ambao tayari wamekwisha kuwa nao? Basi, kuheshimu Muumba wao na vilevile ubora wa upendo umepaswa bila shaka kuwaongoza wafikirie sana namna ya kutumia kujiweza ili wapunguze kuongezeka kwa watoto katika jamaa.
30. (a) Sababu gani tunaweza kusema kwamba, kweli mtoto ni mall ya, Mungu (b) Jambo hilo limepaswa liwafanye wazazi wawe na maoni gani?
30 Hasa, mtoto ni wa nani? Ni mtoto wako, katika maana moja. Lakini, katika maana nyingine, mtoto huyo ni mali ya. Muumba. Umekabidhiwa (umepewa) naye upate kumtunza, kama vile wazazi wako walivyokabidhiwa (walipewa) naye wakutunze wewe kama mtoto. Lakini kwa hakika hukuwa mali ya wazazi wako utendewe katika njia yo yote ambayo wangependa; wala mtoto wako si mali yako katika maana hiyo. Wazazi hawawezi kuongoza wala kuzuia muda wa mtungo wa mimba wala kukua kwa mtoto ndani ya tumbo la uzazi. Hawawezi hata kuona wala kufahamu sana taratibu za ajabu zinazohusiana na uzazi. (Zaburi 139: 13, 15; Mhubiri 11:5) Ikiwa kasoro (kosa) fulani ya mwili inaharibu mimba au mtoto anazaliwa akiwa amekufa, hawawezi kumfufua mtoto huyo. Hivyo, inatupasa tukubali kwa unyenyekevu kwamba Mungu ndiye Mpaji-Uzima wetu sote, nasi sote tu mali yake: “Dunia ni mali ya Yehova na vyote vinavyoijaa, nchi inayozaa na wale wanaokaa ndani yake.”—Zaburi 24:1, NW.
31, 32. (a) Wazazi wana daraka gani mbele za Mungu? (b) Ni mini linalotokana na kutimiza daraka hilo kwa kufaa?
31 Una daraka juu ya watoto unaotokeza katika ulimwengu na vilevile utatoa hesabu kwa Muumba juu ya namna unavyowalea, Yeye aliiumba dunia, akakusudia ikaliwe na watu, tena akawapa wazazi wetu wa kwanza wa kibinadamu uwezo wa kuzaa ili watimize kusudi hilo. Uasi wao juu yake uliwaweka upande wa Adui aliyepinga matumizi ya halali ya Mungu ya enzi yake kuu juu ya jamaa yake ya viumbe vilivyo mbinguni na duniani. Kwa kuwalea watoto wako mpaka wakue wawe watu wenye kushika ukamilifu kwa Muumba wao, wewe na jamaa yako mwaweza kumwonyesha Adui huyo huwa mwongo na Yehova Mungu kuwa wa kweli. Kama Mithali 27:11 inavyoeleza: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.”
32 Kutimiza wajibu ulio nao juu ya watoto, pamoja na daraka lako kwa Mungu, kunaweza kukuletea faida ya kutimiza jambo la kweli maishani. Utakuwa na uwezo wa kuitikia maneno ya Zaburi 127:3 kwa kuthamini na moyo wote, ukisema: “Uzao wa tumbo ni. thawabu.”
[Maelezo ya Chini]
a Kama nyama, na mboga za majani, maboga, mizizi kama viazi, karati, mihogo, maharagwe, mbaazi na dengu.
b Kutia na vyakula vyenye wanga na vile vilivyo na sukari nyingi.
[Picha katika ukurasa wa 93]
Kuwa karibu sana sasa kunaepuka kutengana baadaye