Kuwaandalia Watoto Mahitaji Yao
KWA kweli, watoto wanahitaji uangalifu mwingi, na inaonekana wengi hawapati mahitaji yao. Hali ya vijana wengi leo huthibitisha jambo hilo. Mtafiti mmoja aliyenukuliwa katika gazeti The Globe and Mail la Toronto, Kanada, alisema: “Vijana wetu wamejitenga sana na familia zao na hivyo wamekosa uzoefu na hekima.”
Tatizo limetokea wapi? Je, inawezekana tatizo limesababishwa kwa kadiri fulani na kukosa kuona umuhimu wa kuwapa watoto uangalifu? Mwanasaikolojia anayewasaidia wanawake wanaochuma mapato ya chini kujua jinsi ya kuwatunza watoto wao anasema: “Sote tunahitaji kujifunza kuwa wazazi. Na tunapaswa kutambua kwamba tutapata thawabu kubwa sana baadaye tukitumia wakati na watoto wetu sasa.”
Hata watoto wanahitaji kufundishwa kwa ukawaida. Si mara mojamoja tu bali kwa ukawaida, naam, siku nzima. Kutumia wakati pamoja na watoto tangu wakiwa wachanga ni muhimu kwa ukuzi wao.
Wazazi Wanahitaji Kujitayarisha
Wazazi wanahitaji kujitayarisha kabla mtoto hajazaliwa ili watimize wajibu wao mzito. Wanaweza kujifunza kutokana na kanuni ambayo Yesu Kristo alitoa kuhusu umuhimu wa kupangia mambo. Alisema: “Ni nani kati yenu anayetaka kujenga mnara ambaye haketi kwanza na kuhesabu gharama?” (Luka 14:28) Kulea watoto, ambako mara nyingi huitwa mradi wa miaka 20, ni kazi ngumu zaidi kuliko kujenga mnara. Kwa hiyo ili ufanikiwe kumlea mtoto, unahitaji kuupangia mradi huo.
Kwanza, ni muhimu wazazi wajitayarishe kiakili na kiroho. Uchunguzi uliohusisha wanawake 2,000 wajawazito huko Ujerumani ulionyesha kwamba watoto wa akina mama waliotaka kuwa na familia walikuwa na hali nzuri, kihisia na kimwili, kuliko watoto wa akina mama ambao hawakutaka kuwa na watoto. Kwa upande mwingine, mchunguzi mmoja alikadiria kwamba kuna uwezekano wa asilimia 237 kwamba mwanamke aliye katika ndoa yenye matatizo atapata mtoto aliye na matatizo ya kihisia na kimwili kuliko mwanamke aliye katika ndoa isiyo na matatizo.
Basi, ni wazi kwamba akina baba wanachangia sana ukuzi wa mtoto. Dakt. Thomas Verny alisema: “Baba anayempiga na kumpuuza mke wake mjamzito anasababisha hatari kubwa ya kihisia na kimwili kwa mtoto.” Ama kwa hakika, inasemekana kwamba zawadi bora zaidi ambayo mtoto anaweza kupata ni kuwa na baba anayempenda mama yake.
Homoni zinazosababishwa na wasiwasi na mfadhaiko, ambazo hutokezwa katika damu ya mama, zinaweza kumwathiri mtoto akiwa tumboni. Hata hivyo, inadhaniwa kwamba mtoto huwa hatarini mama anapofadhaika sana au kuwa na wasiwasi kwa muda mrefu kuliko anapovunjika moyo au kupatwa na matatizo mara kwa mara. Jambo muhimu zaidi ni jinsi mama anavyohisi kumhusu mtoto wake aliye tumboni.a
Vipi ikiwa u mjamzito na mume wako hakusaidii ama hutaki kuwa na mtoto? Si ajabu kwamba hali fulani zinaweza kumfanya mwanamke ashuke moyo anapokuwa mjamzito. Lakini, sikuzote kumbuka kwamba mtoto wako hana makosa. Basi, unawezaje kuendelea kuwa mtulivu licha ya hali hizo ngumu?
Mamilioni ya watu wamesaidiwa na mwongozo wa hekima unaopatikana katika Neno la Mungu, Biblia. Inasema: “Katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” Maneno hayo yanaweza kukusaidia kufuata shauri hili: “Msihangaike juu ya kitu chochote.” (Wafilipi 4:6, 7) Utapata msaada kutoka kwa Muumba anayekujali.—1 Petro 5:7.
Ni Jambo la Kawaida
Akina mama fulani vijana huhuzunika na kuhisi uchovu majuma machache ya kwanza baada ya kupata mtoto. Hata wanawake ambao walitaka sana kuwa na mtoto wanaweza kusononeka. Hilo ni jambo la kawaida. Hiyo ni kwa sababu viwango vya homoni hubadilika-badilika akina mama wanapojifungua. Pia wanawake wanapojifungua kwa mara ya kwanza, wanakuwa na majukumu mbalimbali kama vile kumlisha mtoto, kumbadilisha nepi na kumtunza kila wakati.
Mama mmoja alihisi kwamba mtoto wake analia ili kumkasirisha tu. Si ajabu kwamba mtaalamu wa masuala ya kulea watoto huko Japan alisema: “Akina mama wote hupata mfadhaiko unaotokana na kulea watoto.” Kulingana na mtaalamu huyo, “ni muhimu mama asijitenge kamwe.”
Hata mama akishuka moyo wakati fulani, anaweza kumlinda mtoto wake asiathiriwe na hisia zake zinazobadilika-badilika. Gazeti Time linasema: “Akina mama waliojitahidi kuwatunza watoto wao na kucheza nao licha ya kushuka moyo, waliwasaidia watoto wao kuwa wachangamfu.”b
Jinsi Baba Anavyoweza Kusaidia
Baba anaweza kumsaidia na kumtegemeza mtoto wake. Mtoto anapolia usiku wa manane, mara nyingi baba anaweza kumshughulikia mtoto ili mwenzi wake alale. Biblia inasema: “Ninyi waume, mwishi vizuri pamoja na wake zenu.”—1 Petro 3:7, Verbum Bible.
Yesu Kristo aliwawekea waume mfano bora. Hata alikufa kwa ajili ya wafuasi wake. (Waefeso 5:28-30; 1 Petro 2:21-24) Hivyo, waume wanaojinyima starehe ili kuwatunza watoto wao wanamwiga Kristo. Ama kweli, kulea watoto ni mradi ambao wazazi wote wawili wanapaswa kushiriki.
Ushirikiano
Yoichiro, baba wa msichana wa miaka miwili anasema: “Mimi na mke wangu tumejadiliana kinaganaga jinsi tunavyopaswa kumlea binti yetu. Kila wakati tatizo linapotokea tunajadiliana jinsi ya kulitatua.” Yoichiro anatambua kwamba mke wake anahitaji kupumzika, hivyo yeye huandamana na binti yake katika shughuli mbalimbali.
Zamani, familia zilipokuwa kubwa na zenye umoja, watoto wakubwa na watu wa ukoo waliwasaidia wazazi kuwatunza watoto. Hivyo, mfanyakazi katika Kituo cha Utunzaji wa Watoto huko Kawasaki, Japan, anasema: “Mara nyingi, akina mama hufaidika wanapozungumza na wengine kuhusu jambo hilo. Akina mama wengi wameweza kukabiliana na matatizo waliposaidiwa.”
Gazeti Parents linasema kwamba wazazi “wanahitaji watu wanaoweza kuzungumza nao kuhusu mahangaiko yao.” Watazungumza na nani? Akina mama na baba waliopata mtoto wa kwanza wanaweza kufaidika wakiwa tayari kukubali maoni na kuwasikiliza wazazi wao wenyewe au wakwe zao. Babu na nyanya wanapaswa kutambua kwamba wenzi hao vijana wana haki ya kujiamulia mambo.c
Wazazi vijana wanaweza pia kupata msaada kutoka kwa waamini wenzao. Unaweza kupata watu wenye uzoefu wa miaka mingi katika kulea watoto ambao wako tayari kukusikiliza katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova la kwenu. Wanaweza kukupa madokezo yanayofaa. Hata unaweza kuzungumza na “wanawake wenye umri mkubwa,” kama vile Biblia inavyowaita wanawake ambao wamefuata kanuni za Kikristo kwa muda mrefu ambao wako tayari kuwasaidia wanawake vijana.—Tito 2:3-5.
Bila shaka, wazazi wanapaswa kuamua maoni watakayofuata. Yoichiro anasema: “Kila mtu alitushauri.” Mke wake, Takako, anakiri hivi: “Mwanzoni, sikufurahia madokezo ya watu wengine kwa sababu nilihisi wananichambua kwa kuwa sina ujuzi wa kulea watoto.” Hata hivyo, kwa kujifunza kutoka kwa wengine, waume na wake wengi wamesaidiwa kuwa na maoni yanayofaa kuhusu jinsi wanavyoweza kuwatunza watoto wao.
Msaada Bora
Hata ikiwa hakuna mtu aliye tayari kukusaidia, kuna mtu mwenye kutegemeka anayeweza kukuimarisha. Huyo ni Yehova Mungu, aliyetuumba, ambaye macho yake yanaweza kuona hata “kiini-tete” cha watu wote duniani. (Zaburi 139:16) Wakati mmoja Yehova aliwaambia hivi watu wake wa zamani, kama ilivyoandikwa katika Neno lake Biblia: “Je, mke anaweza kumsahau mtoto wake anayenyonya hivi kwamba asimhurumie mwana wa tumbo lake? Hata hawa wanawake wanaweza kusahau, lakini mimi mwenyewe sitakusahau wewe.”—Isaya 49:15; Zaburi 27:10.
Yehova hawasahau wazazi. Amewaandalia maagizo mazuri ya kulea watoto katika Biblia. Kwa mfano, miaka 3,500 hivi iliyopita, Musa nabii wa Mungu aliandika hivi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa nguvu zako zote.” Kisha Musa akasema: “Maneno haya [kutia ndani shauri la kumpenda na kumtumikia Yehova] ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako; nawe uyakazie kwa mwana wako na kuyasema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.”—Kumbukumbu la Torati 6:5-7.
Unafikiri wazo kuu ni nini katika agizo hilo la Neno la Mungu? Ni kwamba unapaswa kuwafundisha watoto wako kila siku kwa ukawaida. Haitoshi tu kuwa na watoto wako mara mojamoja. Kwa kuwa mawasiliano mazuri hutokea bila kupangwa, unahitaji kutenga wakati ili uwe na watoto wako kwa ukawaida. Kufanya hivyo kutakuwezesha kutii amri hii ya Biblia: “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa.”—Methali 22:6.
Kuwazoeza watoto wako inavyofaa kunatia ndani kuwasomea kwa sauti. Biblia inasema kwamba mwanafunzi wa karne ya kwanza Timotheo, ‘aliyajua maandishi matakatifu tangu utoto mchanga.’ Kwa hiyo, mama yake, Eunike, na nyanya yake Loisi walimsomea kwa sauti alipokuwa angali mtoto. (2 Timotheo 1:5; 3:14, 15) Ni vizuri kuanza kufanya hivyo mara tu unapoanza kuongea na mtoto wako. Lakini utasoma nini, na unawezaje kumfundisha mtoto?
Mtoto wako anapaswa kusikia ukisoma Biblia. Inaonekana Timotheo alisomewa Biblia. Pia kuna vitabu vingine vyenye picha za kupendeza vinavyoweza kumsaidia mtoto kuijua Biblia. Vitabu hivyo humsaidia mtoto kuwazia mambo ambayo Biblia inafundisha. Kwa mfano, kuna Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia na Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi. Vitabu hivyo vimewasaidia mamilioni ya watoto kuingiza mafundisho ya Biblia akilini na moyoni.
Kama Biblia inavyosema, “wana [na mabinti] ni urithi kutoka kwa Yehova; uzao wa tumbo ni thawabu.” (Zaburi 127:3) Muumba wako amekupa “urithi,” mtoto mzuri, anayeweza kukuchangamsha na kukufurahisha. Kulea watoto, hasa wamsifu Muumba wao, ni kazi yenye kufurahisha!
[Maelezo ya Chini]
a Mbali na homoni za mfadhaiko, nikotini, kileo, na dawa nyingine za kulevya zinaweza pia kumwathiri mtoto sana. Akina mama wajawazito wanapaswa kujiepusha kabisa na vitu vyovyote hatari. Isitoshe, ni muhimu kumwuliza daktari kuhusu jinsi dawa zinavyoweza kumwathiri mtoto aliye tumboni.
b Iwapo mama ana huzuni nyingi sana, amevunjika moyo, havutiwi na mtoto wake, na hapendezwi na chochote, huenda anaugua ugonjwa wa kushuka moyo baada ya kujifungua. Ikiwa ndivyo, anapaswa kumwona daktari. Tafadhali ona matoleo ya Amkeni! ya Julai 22, 2002, ukurasa 19-23 na Juni 8, 2003, ukurasa wa 21-23.
c Tafadhali soma makala “Babu na Nyanya—Shangwe Yao, Magumu Yao,” katika toleo la Amkeni! la Machi 22, 1999.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Maoni ya mama kuhusu mtoto wake aliye tumboni ni muhimu sana
[Picha katika ukurasa wa 9]
Ingawa mama aliyejifungua karibuni anaweza kuwa na hisia zinazobadilika- badilika, bado anaweza kumsaidia mtoto wake ahisi anapendwa na yuko salama
[Picha katika ukurasa wa 10]
Akina baba wana daraka la kusaidia kuwatunza watoto
[Picha katika ukurasa wa 10]
Unapaswa kumsomea mtoto tangu utotoni