“Wakati Bora” Watumiwa Kidogo-Kidogo
NI WAZAZI wachache hutumia wakati wa kutosha pamoja na watoto wao siku hizi. Wengi ni waseja na wanajitahidi kuandalia watoto wao mahitaji yao bila usaidizi wa mwenzi wa ndoa. Na kwa sababu ya hali ya kiuchumi inayoendelea kuharibika, wazazi wengi waliofunga ndoa wanapata kwamba ni lazima baba na mama wafanye kazi nje ili familia iweze kujiendeleza kifedha. Basi, haishangazi kwamba wazo la wakati bora limeenea.
Kama inavyoeleweka kwa kawaida, wakati bora mara nyingi huhusisha kuratibu kutumia wakati fulani na mtoto, hasa kukiwa na utendaji fulani hususa akilini—kwa mfano, safari ya pekee kama kuzuru makao ya wanyama. Kwa wazi, wazo hilo linafaa. Watoto wanahitaji uangalifu wowote wa pekee wanaoweza kupata. Hata hivyo, wazo linalopendwa sana la wakati bora lina madhara yanayoendelea kuwa wazi zaidi kwa wataalamu wa malezi ya watoto.
Kwa wazi, wazazi wengi wenye shughuli, wanaofikiria tu kazi yao wamechukua wazo linalodanganya la kwamba kutumia wakati mfupi uliopangwa na kuratibiwa pamoja na mtoto kutaandaa mahitaji yote ya mtoto kwa habari ya utunzaji wa mzazi. Hivyo, gazeti Daily News lamnukuu Dkt. Lee Salk, profesa katika Shule ya Kitiba ya Chuo Kikuu cha Cornell katika United States, akisema: “Wazo la wakati bora ni bure.” Yeye aeleza: “Maneno hayo yametokea kwa sababu ya hisi ya hatia ya wazazi. Watu walikuwa wanajipatia ruhusa ya kutumia wakati mchache zaidi na watoto wao.”
Lakini, je, ubora wa wakati, uangalifu wa mzazi ukiwa umekazwa tu kwa mtoto bila kukengeuka hautalipia ukosefu wa wingi wa wakati? La, kwa sababu rahisi—wazazi hufundisha watoto wao kwa mafanikio sana kupitia mfano. Sehemu ya kuhuzunisha ya kweli hiyo ilionyeshwa kwa huzuni na uchunguzi mmoja wa hivi karibuni wa vijana wa jijini. Wale waliokuwa na washiriki wa familia katika jela wakati walipokuwa wakilelewa walikuwa na uwezekano wa mara mbili wa kufungwa gerezani pia. Kwa njia iyo hiyo, wale wanaolelewa na walevi au watumiaji wa dawa za kulevya walikaribia mara mbili kuiga tabia hizo zenye kudhuru.
Mfano mzuri wa mzazi unaweza kuwa na nguvu vilevile. Tatizo ni kwamba kuweka mfano mzuri huchukua wakati, vipindi virefu vya wakati mwingi, si wakati mfupi-mfupi tu ulio bora. Kama gazeti Daily News la New York linavyotaja: “Tatizo la wazo la wakati bora ni kwamba wakati muhimu sana kati ya mzazi na mtoto—yale mazungumzo na maamuzi yanayoleta usalama, sifa bora na kujistahi—hujitokeza wenyewe.” Hakuna mtu anayeweza kuratibu wakati unaojitokeza wenyewe. Mzazi anaweza kuweka kando dakika 15 za wakati bora atumie na mtoto, lakini mtu anaweza kujuaje kama mzazi na mtoto watasikilizana wakati huo? Na mtoto atajifunzaje kupitia mfano ikiwa hizo ndizo dakika za pekee katika siku anazotumia pamoja na mzazi?
Lakini kwa sababu wazazi wana wakati mchache sana wa kutumia, suluhisho ni nini? Hakuna majibu rahisi. Hakuna kitu kinachoweza kubadili ukweli wa kwamba ulimwengu huu umefanya kulea watoto kuwe jambo gumu sana. Huenda wazazi wengine wakaweza kuacha kuzingatia sana kazi zao. Mwandikaji mmoja wa kitabu cha karibuni juu ya utunzaji wa watoto anahimiza mzazi yeyote anayeweza asizingatie sana kazi yake—akae nyumbani na watoto. Lakini kwa wazazi wengi, hakuna chaguo kama hilo. Na hata wale wenye ratiba ya kazi inayoweza kubadilika au wale wasio na kazi yenye mshahara bado wanaona ni vigumu kutumia wakati mwingi wa kutosha na watoto wao.
Wataalamu wengine huhimiza wazazi wachunguze kazi wanazofanya nyumbani, kama kusafisha, kupika, kurekebisha vitu, kutunza gari, kufua, na kununua vitu madukani, waone kama wanaweza kufanya baadhi ya kazi hizo pamoja na watoto wao. Kufanya kazi pamoja hata kwa kazi za kawaida, au kupumzika tu pamoja, kwaweza kupatia wazazi wakati wanaohitaji wa kuwasiliana na kuandaa mfano mzuri. Wazazi Wakristo wana kazi nyingine ambayo wangetaka wafanye wakiwa na watoto wao. Mikutano ya Kikristo, huduma, funzo la Biblia la familia, ushirika na waamini wenzi—hayo yote yaandalia wazazi wakati muhimu wa kuwa na watoto wao.
Kwa kupendeza, Sheria iliyotolewa kwa taifa la Israeli ilitaja jambo kama hilo miaka 3,000 hivi iliyopita. Katika Kumbukumbu la Torati 6:6, 7, twasoma hivi: “Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.” Maisha hayakuwa rahisi hivyo katika nyakati za kale. Fikiria wakati wote uliohitajiwa wa kushughulikia mahitaji ya kila siku—kadiri ya kazi iliyohitajiwa ili baba aandalie familia yake, au jitihada iliyotumiwa katika kazi kama kupika au kufua! Lakini wazazi waliompenda Yehova walifanya kazi nyingi kadiri walivyoweza wakiwa na watoto wao na hivyo wakapata fursa nyingi katika siku za kukaza Sheria ya Mungu ndani ya mioyo michanga ya watoto wao.
Wazazi Wakristo wanahitaji kufanya hivyo leo. Wakati ukifika wa kutumia wakati na watoto wao, ni lazima waepuke kufanya mambo wanayoona kuwa rahisi tu kufanya. Ule msemo wa kale, “Si wingi, bali ni ubora,” hautumiki katika kulea watoto. Hasa wakati wa miaka yao ya ukuzi, watoto hawahitaji tu wakati wa pekee bali pia wakati wa kuwa tu “pamoja.”
[Picha katika ukurasa wa 17]
Familia ikiwa yenye shughuli nyumbani, watoto wahusika
[Picha katika ukurasa wa 17]
Kutumikia Yehova pamoja