Vijana Wanauliza...
Kwa Nini Niteseke kwa Ulemavu?
“NILIKUWA na miaka mitano,” Becky akumbuka. “Rafiki yangu alikuwa amenibeba katika baiskeli yake wakati gari moja lilipotokea kwenye kona na kutugonga.” Matokeo yalikuwa nini? “Nilivunjika mguu na kupata majeraha mabaya sana ya kichwa. Madaktari hawakutarajia kwamba ningeishi.” Hata hivyo, kwa kweli Becky aliishi, na sasa ni msichana mchangamfu wa miaka 16. Lakini aksidenti hiyo iliacha alama yayo. “Iliniacha nikiwa dhaifu sana,” yeye asema.
Kijana mmoja anayeitwa Craig pia ni mlemavu, hilo likiwa tokeo la ugonjwa wa kupooza kwa ubongo. “Ugonjwa wa kupooza kwa ubongo huathiri misuli yangu na mfumo wangu wa neva,” aeleza Craig. “Misuli yangu haiitikii inavyotakikana kwa ujumbe mbalimbali ambao ubongo wangu unaipelekea. Kwa hiyo, nina tatizo la kutembea, kuongea, na kudumisha usawaziko wangu wa kusimama. Naweza kufanya mambo hayo yote lakini si vizuri sana.”
Je! wewe pia una aina fulani ya ulemavu wa kimwili? Takwimu zaonyesha kwamba kufikia mwaka 2000, idadi ya vijana wenye ulemavu mbalimbali itafikia karibu milioni 59 ulimwenguni pote. (World Health, Januari/Februari 1985) Hata hivyo, hakika ya kwamba wengi sana wana tatizo kama lako haifariji sana wakati unapotaka kukimbia, kuruka, na kucheza kama vijana wengine lakini huwezi.
Matatizo ya Walemavu
Ulemavu wa kimwili si jambo jipya. Katika nyakati za Biblia wengine walilazimika kuwa vilema (2 Samweli 4:4; 9:13), vipofu (Marko 8:22), na kupooza (Mathayo 12:10). Vilema kama hao mara nyingi hupata shida katika kutekeleza mambo ya msingi sana ya maisha.—Linganisha Kumbukumbu la Torati 28:29; Mithali 26:7.
Huenda wewe pia ukawa na vita iyo hiyo dhidi ya vizuizi vyako. Kuvaa nguo, kula, au kwenda shule kunaweza kuhitaji jitihada nyingi sana—na msaada mwingi kutoka kwa wengine. “Siwezi kufanya chochote kwa usahihi kwa upande wangu wa kulia,” asema Becky. “Hivyo ilinibidi nijifunze kuandika kwa mkono wangu wa kushoto. Kutembea kumekuwa kugumu pia. Wakati huu ninatembea kikawaida, lakini siku nyingine mimi huchechema vibaya.” Au fikiria tatizo la kijana mwingine mbilikimo. Yeye asema, na kwa kuchekesha: “Kufikia swichi za taa zilizo katika ukuta ni tatizo jingine kubwa sana . . . Kwa hakika nyumba zimebuniwa kwa watu warefu.”—How it Feels to Live With a Physical Disability, cha Jill Krementz.
Ingawa hivyo, huenda ukapata kwamba matatizo yanayokufadhaisha zaidi si ya kimwili. Gazeti Parents laeleza hivi: “Vijana huwa wepesi sana kuona maitikio ya wengine, jambo linalofanya maisha yawe magumu hasa kwa vijana wenye uhitaji wa pekee. . . . Wanajiuliza wengine wanawaonaje jinsi walivyo na mara nyingi hawaamini maonyesho ya kirafiki, wakiona maonyesho hayo yenye makusudi mema kuwa maonyesho ya huruma wasiopenda.” Ni kawaida kutaka kupendwa na kukubaliwa na wengine. Na bado, unaweza kuhisi umetengwa kando. Kama vile Michelle mchanga anavyosema: “Nimekuwa tofauti na mtu yeyote yule katika maisha yangu yote. Sababu ni kwamba sina mkono wangu wa kushoto.”
Kuwa tofauti pia kwaweza kufanya ufanyiwe mizaha sana. “Nilisomea shule ya walemavu mpaka darasa la tano,” akumbuka Craig. “Lakini katika darasa la tano, nikaanza kwenda katika shule ya kawaida. Sikupata matatizo mengi sana mpaka siku moja ambapo wavulana wengine walianza kunicheka. Ilikuwa ni kwa sababu ya jinsi nilivyotembea.” Becky pia ana kumbukumbu zenye kuumiza za matendo ya kikatili aliyofanyiwa na wanashule wenzake. Kwa sababu upasuaji wa mapema ulikuwa umeharibu sauti yake, sauti yake inakwaruza kidogo. “Watoto shuleni walikuwa wakiniita sauti-dubwana,” yeye asema.
Watu wazima pia wanaweza kuonyesha ubaguzi usiofaa. Wengine wanaweza kuepuka kukutazama machoni. Wengine wanaweza kuepuka kabisa kukuzungumzia, wakielekeza maneno yao kwa wazazi wako au waandamani wako—kana kwamba huonekani au umelemaa kiakili. Jambo la kuchukiza zaidi linaweza kuwa ni watakia-mema wanaokuhurumia nyakati zote, wakiongezea hisia yako kwamba wewe ni kama bidhaa zinazoharibika.
Maoni ya Mungu Juu ya Jambo Hilo
Hata hivyo, Mungu anahisije juu yako? Je! ulemavu wako ni ishara fulani ya kwamba hakupendi? Ona yale ambayo Yesu alisema alipokutana na “mtu, kipofu tangu kuzaliwa.” Wanafunzi wake waliuliza: “Ni yupi aliyetenda dhambi, mtu huyu au wazazi wake, hata azaliwe kipofu?” Yesu akajibu: “Huyu hakutenda dhambi, wala wazazi wake.” (Yohana 9:1-3) La, upofu huo haukutokana na dhambi fulani hususa kwa upande wa huyo kipofu au wazazi wake. Badala ya hivyo, ilikuwa ni tokeo la kutokukamilika ambako sisi sote tumerithi kutoka kwa Adamu. Mtume Paulo aeleza hivi: “Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.”—Warumi 5:12.
Basi, ulemavu wa kimwili si tokeo la tendo au adhabu ya kimungu. Mengine ni matokeo ya kutokujali. Na bado mengine ni kwa sababu tu ya “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11, NW) Na kuna vijana wanaolemaa kwa sababu ya kutendwa vibaya au kutokujali kwa upande wa wazazi wao.
Hata chanzo cha matatizo yako kiwe ni nini, hupasi kuhisi kwamba Mungu anakuona kama kitu kilichoharibika. Tofauti na hilo, anakuona kuwa mwenye thamani sana, hasa ikiwa wewe ni mcha Mungu. (Luka 12:7) Yeye ‘hujishughulisha sana na mambo yako’ kwa njia ya binafsi sana na anafurahi kukutumia katika utumishi wake. (1 Petro 5:7) Kwani, hata mmoja wa watumishi wa Mungu wenye kutokeza sana wa wakati wote, mtume Paulo, inaonekana alitaabishwa na ulemavu fulani wa kimwili—“mwiba katika mwili.” (2 Wakorintho 12:7) Inafariji kama nini kujua kwamba “wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA [Yehova, NW] huutazama moyo.” (1 Samweli 16:7) Yeye anafahamu sana mambo unayoweza kutimiza na ajua yale utakayoweza kufanya utakaporudishwa kwenye ukamilifu katika ulimwengu wake mpya.—Ufunuo 21:3, 4.
Kukabiliana na Wengine
Kwa tukio baya, wanafunzi wenzako na wengine huenda wasishiriki maoni ya juu ya Mungu. Kwa kweli, nyakati nyingine watu ni wakatili tu. Basi, usishangae ikiwa marika wako wengine ni wakatili ivyo hivyo kwa habari ya taabu zako. Ingawa hivyo, mara nyingi watu hawakusudii kukuumiza au kukuaibisha; nyakati nyingine huwa ni wadadisi tu. Wakiwa hawajihisi huru juu ya taabu yako au labda kwa kutokuwa na hisia, wanaweza kusema jambo la kipumbavu au lenye kuumiza.
Unaweza kufanya nini? Nyakati nyingine unaweza kuzuia hali zenye kuaibisha. Kwa mfano, unaweza kujaribu kustarehesha wengine ukitambua kwamba hawajihisi huru au hawajui la kusema. Tambua kwamba sisi sote huelekea kuwa na woga kwa jambo tusilolifahamu. Saidia wengine wasione tu ulemavu wako ili wakujue kihalisi. Hali ikifaa, unaweza kujaribu kusema kitu kama: “Je! unajiuliza ni kwa nini ni lazima nitumie kigari cha kusukumwa?” Kulingana na gazeti Parents, mwalimu mmoja aliyekatwa kiungo fulani, huridhisha udadisi wa wanafunzi wake kwa kuanzisha mazungumzo kwa maneno haya: “Nadhani mwajiuliza ni nini kilichotukia. Je! mngependa kujua?”
Hata ujitahidi jinsi gani, huenda bado ukaudhiwa mara kwa mara. Becky mchanga asema hivi: “Nilipokuwa mchanga sana, nilikuwa naudhika sana wengine waliponifanyia mzaha; nimekuwa mwenye kuudhika upesi muda wote wa maisha yangu. Lakini sasa siachi jambo hilo liniudhi. Nyakati nyingine mimi hata naweza kuchekelea hali hiyo.” Ndiyo, kuwa mcheshi kunaweza sana kuzuia maneno yenye kuudhi. Kuna “wakati wa kucheka.” (Mhubiri 3:4) Mfalme Sulemani alitoa shauri hili pia: “Usitie moyoni mwako maneno yote yaliyosemwa.” (Mhubiri 7:21) Nyakati nyingine njia bora ya kushughulikia maneno ya upumbavu ni kuyapuuza. “Usijali wanayosema watu,” asema Becky.
Tumaini Lakusaidia Ukabiliane
Kwa kweli, jamii yote ya kibinadamu imepungukiwa. “Viumbe vyote pia vinaugua pamoja, navyo vina utungu pamoja hata sasa,” yasema Biblia. (Warumi 8:22) Lakini unaweza kuwa na tumaini la wakati ujao. Kwa mfano, chukua msichana mchanga ambaye tutamwita Carol. Alizaliwa akiwa karibu kiziwi. Kisha aksidenti ya baiskeli ilimfanya akatwe mguu. Carol alitaka kufa. Lakini alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na akajifunza juu ya ulimwengu mpya wenye uadilifu unaokuja ambamo “hapana mwenyeji atakayesema, mimi mgonjwa.” (Isaya 33:24) Kwa kweli, alipata tumaini kwamba siku moja ulemavu wake mbalimbali utaponywa—kimwujiza!—Isaya 35:5, 6.
Kujifunza juu ya Mungu kumekuwa na uvutano gani juu ya mwelekeo wa Carol? Rafiki zake wa karibu Wakristo wasema hivi juu yake: “Yeye ni mchangamfu nyakati zote na hafikirii sana ulemavu wake.” Lakini, kwa kupendeza wao wasema pia hivi: “Wengi wa rafiki zake hawatambui kwamba ana mguu bandia na kwamba hawezi kusikia vizuri sana.” Kwa nini? “Anategemea kusoma midomo na vitu vya kusaidia kusikia.” Kwa wazi, Carol amefanya mengi kuliko tu kuwa na tumaini kwa wakati ujao. Amejitahidi kufikia uwezo wake wote sasa. Jinsi unavyoweza kufanya ivyo hivyo itazungumziwa katika makala itakayofuata katika mfululizo huu.
[Picha katika ukurasa wa 19]
Wengine huona ikifaa kueleza hali yao kwa watu wanaoonekana kuwa wana udadisi