Kiu Yangu ya Mungu Yaridhishwa
NILIKUWA nimejifunza katika seminari za Amerika Kusini kwa miaka kumi, nikitumia miaka mitatu ya mwisho kuzingatia theolojia na falsafa. Lakini sasa mkulima wa hali ya chini alikuwa akiniambia kwamba angeweza kunisaidia nielewe Biblia. Kukata tamaa kwangu juu ya mafundisho ya seminari kulinifanya nisikilize.
Ni nini kilichokuwa kimenichochea nitake kuwa kasisi? Lakini ni kwa nini miaka mingi katika seminari iliniacha nikiwa na kiu ya Mungu isiyoridhishwa?
Maisha ya Hali ya Chini
Wazazi wangu walitulea sisi wavulana saba katika Vallegrande katika Bolivia. Tuliishi katika bonde lenye rutuba, tukifuga ng’ombe na kukuza mimea kama mahindi, njugu, na viazi. Kijiji chetu cha Naranjal kilikuwa mbali peke yacho, kwa hiyo sikuwa na fursa sana ya kwenda shuleni. Hata hivyo, nilijifunza kusoma na kuandika.
Kila mwaka kasisi wa Roma Katoliki alikuwa akitembelea kijiji chetu kwa ajili ya sherehe ya kidini ya mahali petu. Nilikuwa nikivutiwa sana na jinsi alivyokuwa akizungumza kuhusu Mungu. Katika ziara yake moja, alitangaza kwamba seminari moja ilikuwa imefunguliwa katika Bolivia izoeze vijana wanaume wawe makasisi. Nilipomwambia kwamba nilitaka kujifunza juu ya Mungu, alianza kupendezwa nami. Alisema: “Unaweza kuwa kama ngazi, ukisaidia watu wafike mbinguni.”
Nilitamani sana kwenda kwenye seminari hiyo na kupata ujuzi juu ya Mungu. Nilitumaini kwamba nikiwa huko ningeondolewa kidogo mvurugo niliohisi. Kwa kielelezo, ingawa mama yangu alinifundisha kwamba milima, maua, na miti ilikuwa zawadi kutoka kwa Mungu, pia alisema kwamba Mungu hupeleka watu wengine kwenye helo wapatwe na mateso yenye ukatili. ‘Mungu awezaje kuwa hivyo?’ nikajiuliza.
Mazoezi ya Seminari
Hiyo seminari mpya ilikuwa katika Tupiza, mji uliokuwa katika bonde lenye kupendeza. Nilifika huko katika 1958. Nilipokuwa mchanga kidogo, nilikuwa nikifurahia kupanda kilima ambako ningetafakari juu ya Muumba wetu mpendwa. Hata hivyo, nilikata tamaa kwa kutojifunza mengi juu ya Mungu katika seminari hiyo. Hata hawakuwa na Biblia nzima huko, kulikuwa na “Agano Jipya” tu. Nilipouliza nipewe moja, wafunzi waliniambia kwamba niwe na saburi.
Baada ya mwaka wa kwanza, ni watatu kati yetu peke yao waliofaulu kuendelea na mtaala huo. Wengine wote walirudishwa nyumbani. Kwa sababu tulikuwa wachache sana, tulipelekwa Buenos Aires, Argentina, kuendelea na masomo yetu. Nilipofika Seminari ya San Miguel, nilihisi staha kubwa sana. Ilionekana kuwa mahali pakubwa sana. ‘Kwa kweli nitaweza kumkaribia Mungu hapa,’ nikawaza. Tulijifunza Kilatini, Kigiriki, Kiingereza, na Kifaransa, na tulijifunza juu ya maisha ya wale ambao Kanisa Katoliki liliheshimu kuwa “watakatifu.” Lakini masomo hayo yaliniacha nikihisi utupu. Maswali yangu yalibaki bila kujibiwa.
“Inakuwaje kwamba Mungu ni Utatu?” nikauliza mmoja kati ya wafunzi. Alijibu kwamba hata wanatheolojia mashuhuri kama yule Mwitaliano wa karne ya 13 Thomas Aquinas walishindwa kueleza mambo kama hayo. Bado sikuwa nimepata kuona Biblia nzima, kwa hiyo nikauliza mmoja wa maprofesa kuhusu “Agano la Kale.”
“Hilo ni la Waprotestanti tu,” yeye akajibu.
Nilijiuliza hiyo ingewezekanaje kwa sababu nilijua kwamba mara nyingi Yesu alinukuu kutoka ndani yalo. Nikafadhaika na kushuka moyo.
Baada ya muda, sita kati yetu tulichaguliwa kuwa wanafunzi wa kidini, nasi tukaweka nadhiri za kudumisha usafi wa kiadili, umaskini, na utii. Baada ya funzo la mwaka mmoja tukiwa wanafunzi wa kidini, tulienda kwenye seminari ya Córdoba, Argentina. Tungeweza tu kuvaa mavazi ya kidini pekee huko, ambayo yalikuwa joho refu jeusi na ukosi mweupe, pamoja na tasbihi na msalaba mkubwa. Nilijawa na matarajio mengi; sasa kwa mara ya kwanza kabisa, ningejifunza theolojia.
Kukata Tamaa Zaidi
Mtaala wa theolojia ulifundisha uhakiki wa Biblia, ambao unaona Biblia kuwa kitabu cha fasihi kama kitabu kingine chochote. Nilikata tamaa kwamba maswali yangu mengi bado hayakuwa yakijibiwa. Nikawa rafiki wa karibu wa askofu mmoja. “Inakuwaje kwamba Biblia inasema Yesu alikuwa katika helo?” nikauliza. (Matendo 2:31) Lakini aliepa swali langu tu.
Pia kulikuwa na maswali mengi ya kiadili yaliyonisumbua. Niliuliza mwanatheolojia mmoja kuhusu kupiga punyeto na ngono kati ya waseja. Badala ya kurejezea mambo ambayo Neno la Mungu husema kuhusu vitendo hivyo, alichangamkia mawazo ya karibuni zaidi ya wanatheolojia mashuhuri katika Paris. Akanionyesha kimoja kati ya vitabu vyao. “Wanasema kwamba mambo hayo si dhambi,” akasema. “Usiwe na wasiwasi.” Lakini jibu hilo halikuniridhisha.
Siku moja nilikuwa nikipitia vitabu katika maktaba ya seminari nilipotukia kufungua kitabu kilichoandikwa katika Kifaransa. Kilinukuu Zaburi 42:2, kinachosema hivi: “Nafsi yangu inamwonea kiu Mungu.” Nikajiwazia, ‘He, hivyo ndivyo ninavyohisi hasa.’ Upesi baadaye, nikiwa ninazuru nyumbani, nilitembelea nyumba ya watawa katika mji wa karibu wa Vallegrande. Huko katika duka la vitabu, nikaona nakala ya Biblia nzima—tafsiri ya Nácar-Colunga. Hiyo ilikuwa mara ya kwanza kabisa kwangu kuona Biblia nzima. Nikauliza kama ningeweza kuinunua, nikiwa siamini kabisa kama ingewezekana. Jinsi nilivyofurahi kutoka kwenye duka hilo nikiwa na Biblia yangu mwenyewe kwapani mwangu!
Nilienda nyumbani nikiimba na kupiga mbinja. Nilipofika, nikaanza kusoma Zaburi 42, inayoanza hivi: “Kama ayala aioneavyo shauku mito ya maji. Vivyo hivyo nafsi yangu inakuonea shauku, Ee Mungu. Nafsi yangu inamwonea kiu Mungu, Mungu aliye hai.” ‘Labda sasa,’ nikawaza, ‘kiu yangu ya Mungu itaridhishwa.’ Lakini upesi nikatambua kwamba ningehitaji msaada kupata majibu ya Biblia kwa maswali yangu. Masomo yangu ya seminari yalishindwa kuandaa msaada huo.
Katika 1966, niliambiwa kwamba seminari ya juu yenye kufundisha hasa theolojia na falsafa ilikuwa imefunguliwa karibu na Cochabamba katika nchi niliyozaliwa ya Bolivia na kwamba ningehamishwa huko. Wafanyakazi wa seminari hiyo walikuwa makasisi wachanga Wahispania, wanatheolojia wa kisasa, na ilikuwa na maktaba nzuri sana. ‘Labda sasa nitapata majibu kwa maswali yangu,’ nikafikiri.
Mara nyingi niliuliza maswali kama haya: “Inawezekanaje kwamba Mariamu awe mama ya Mungu?” Lakini, wafunzi hawakupendezwa sana na maswali kama hayo. Badala ya hivyo, walihangaikia zaidi falsafa ya Kikomunisti. Wakati mmoja nilikutana na kardinali mmoja, lakini yeye alipendelea zaidi kunieleza juu ya maono yake katika Vita ya Ulimwengu 2 kuliko kujibu maswali yangu.
Baada ya miaka kumi ya mazoezi ya seminari, niliomba likizo ya mwaka mmoja ili niweze kuondoka nje na kukutana na watu. Nilitaka nipate ono la kuongea na watu kuhusu gospeli. Upesi nikang’amua kwamba singeweza kuridhika kamwe na nyumba za watawa, kwa hiyo nikaamua kuomba niondolewe nadhiri zangu. Baadaye nikamwoa mwanamke aliyekuwa hapo awali mtawa, Porfiria. Tukaanza kukaa katika jiji la Santa Cruz, Bolivia.
Mgeni Mwenye Kushangaza
Siku moja katika mwaka uliofuata, nilikuwa nimeketi barazani ambapo mwanamke mwenyeji wa nyumba alikuwa akioka mkate katika jiko la kutumia moto wa kuni. Mtu mmoja alifika langoni. Nilidhani kwamba alikuwa na shughuli na mwanamke huyo, kwa hiyo nikasema: “Karibu!” Akaingia, na kuketi kando yangu. Ingawa alikuwa amevalia kinadhifu, ningeweza kuona kwa sura yake kwamba alikuwa mtu wa hali ya chini. Kwa mshangao wangu alianza kusema juu ya Biblia.
Baadaye nilikuja kujua kwamba jina la mtu huyo lilikuwa Adrian Guerra na kwamba alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Haikunichukua muda mrefu kutambua kwamba hakujua kusoma vizuri. Nilijitayarisha kwa ajili yake, lakini sikuogopa. ‘Haidhuru,’ nikafikiri, ‘najua Kilatini na Kigiriki. Nimesoma theolojia na nimetumia miaka mingi nikizungumza juu ya falsafa na wanatheolojia na maaskofu.’ Sikuwa na kiburi wala sikumdharau, lakini sikutarajia kamwe kujifunza jambo lolote kutoka kwake.
Aliomba maoni yangu juu ya swali alilouliza, Ni kwa nini ubaya umeongezeka sana katika ulimwengu? Tukazungumzia hilo, kisha akaniomba nimwonyeshe Biblia yangu. Kufikia wakati huu nilikuwa nimenunua Jerusalem Bible ya Katoliki iliyokuwa imetoka kuchapishwa tu. Aliniuliza nisome Ufunuo 12:12, linalosema hivi: “Lakini kwa habari yenu, dunia na bahari, taabu inakuja—kwa sababu yule ibilisi ameshuka kwenu kwa ghadhabu, akijua kwamba siku zake zimehesabiwa.”
“Hili kwa kweli larejezea wakati dhambi ilipoanza,” nikajibu. Akaniuliza nisome muktadha yenye kuzunguka, mistari 7-10, inayosema kwamba vita katika mbingu ilianza wakati Kristo alipopata kuwa Mfalme, na matokeo yakawa kwamba Shetani na malaika zake wakatupwa duniani. “Hali mbaya sana tunazoona sasa ni tokeo la hasira iliyoongezeka ya Ibilisi,” Adrian akaeleza. “Lakini tunaweza kufurahi kwamba sasa Kristo ni Mfalme na kwamba siku za Ibilisi zimehesabiwa.”
Kujifunza jambo hilo kutoka katika Biblia kulinisisimua sana. Lakini nilishangazwa sana pia kwamba mtu huyu wa maisha ya hali ya chini, mwenye tabasamu nzuri, angeweza kuketi hapo tu na kunifafanulia Maandiko kwa utulivu.
Kiu Yangu ya Mungu Yaridhishwa
Adrian aliniachia fasihi fulani na kuahidi kwamba atarudi. Nilifurahi aliporudi tena, nami nikaanza kumwuliza maswali haya ambayo yalikuwa yamenitatanisha kwa muda mrefu: “Mungu anawezaje kuwa Utatu?” na, “Kwa nini Yesu alikuwa katika helo?” Alitumia kiongozi chenye kuelekeza katika Biblia kinachoitwa Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, naye akaniomba nisome kutoka katika Biblia yangu mwenyewe maandiko yaliyotajwa hapo ambayo yalijibu maswali yangu. Nilijihisi nikiwa mjinga kama burro (punda au fala). Nikajifunza kwamba jina la Mungu ni Yahweh, au Yehova, na kwamba yeye si Utatu, kwamba helo ni kaburi na kwamba Yesu hakuwa na fahamu alipokuwa huko kwa sehemu za siku tatu.—Zaburi 16:10; Mhubiri 9:10; Isaya 42:8.
Mara nyingi nilikuwa nimeuliza katika seminari kuhusu yale maisha ya baadaye na niliambiwa kwamba mbinguni ni kama kanisa kubwa ambako wote watasimama mbele ya Mungu na kuomba. ‘Ni lenye uchovu kama nini!’ nikawaza. Lakini sasa, kwa sababu ya kufafanuliwa ahadi ya Biblia ya uhai wa milele katika dunia-paradiso, imani yangu kwa upendo wa Mungu kwa ainabinadamu iliamshwa tena.—Zaburi 37:9-11, 39; Ufunuo 21:3, 4.
Baada ya ziara chache, siku moja Adrian alifika na mtu wa nchi ya kigeni, aliyenitajia kuwa mwangalizi wa kutaniko. “Unauliza maswali mengi sana,” akasema, “niliamua kwamba mishonari huyu ataweza kukusaidia vizuri zaidi.” Lakini nilikuwa nampenda Adrian, na kuwapo kwa mishonari huyo kulinifanya niwe na wasiwasi. Kwa hiyo niliendelea kujifunza Biblia na Adrian. Nilianza kuhudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme na kukuta kwamba hotuba za Biblia zilikuwa zenye kufundisha sana.
Kuushinda Woga Wangu
Baada ya muda Adrian akaanza kunitia moyo nishiriki pamoja na wengine mambo niliyokuwa nimejifunza. Kwenye mikutano yao Mashahidi wa Yehova hutiwa moyo wafundishe watu nyumba kwa nyumba. Kwa kweli, nikaja kung’amua kwamba kichwa cha Biblia ambacho Adrian alizungumza nami mara ya kwanza, kuhusu kisababishi cha ubaya unaoongezeka, kilikuwa kichwa cha mazungumzo kilichopendekezwa kwa Mashahidi wa Yehova katika Bolivia mwezi huo katika 1970. Niliweza kuona kwamba mazoezi aliyopokea Adrian yalimtayarisha amtumikie Mungu kwa njia bora zaidi kuliko vile miaka yangu kumi ya mazoezi ilivyokuwa imenitayarisha! Lakini, wazo la kuzuru watu nyumbani kwao lilinitia woga. Lilikuwa tofauti sana na kuhubiria watu ambao huja kanisani.
Wakati uliofuata Adrian alipokuja kusoma na mimi, nilijificha ndani ya nyumba na kujifanya kwamba siko nyumbani. Ni lazima iwe alishuku hilo kwa sababu alingojea nje kwa saburi kwa muda wa saa nzima kabla ya kuondoka. Lakini hakuchoka na kuniacha; kwa mshangao wangu alirudi juma lililofuata. Polepole, upendo wangu kwa Yehova ukawa wenye nguvu zaidi, na nikaushinda woga wangu. Katika 1973 mke wangu nami tulibatizwa. Porfiria akawa painia, akitumikia wakati wote katika kazi ya kuhubiri na kuongoza mafunzo ya Biblia. Aliendelea hivyo mpaka kufikia na kutia ndani siku ya kifo chake mapema katika 1992.
Adrian akawa msomaji mwenye ufasaha, na kwa miaka mingi sasa, nimetumikia nikiwa mzee katika kutaniko. Sote wawili twaendelea kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu nyumba kwa nyumba. Hivi karibuni nilikutana na mwanamke mmoja aliyesema hivi: “Ungalibaki na kanisa. Ungalifanya mambo mengi mazuri ukiwa humo.”
Nilimwomba alete Biblia yake. Alipoileta, nilimwonyesha Yeremia 2:13, linaloeleza jinsi Israeli walivyokataa Neno la Mungu. Lasema hivi: “Wameniacha mimi, niliye chemchemi ya maji ya uzima, wamejichimbia mabirika, mabirika yavujayo, yasiyoweza kuweka maji.”
“Jambo fulani kama hilo limepata kanisa,” nikamwambia. “Kujaribu kuridhisha kiu ya Mungu waliyo nayo watu kwa mafundisho ya Kikatoliki yasiyo ya Kibiblia ni kama kujaribu kujaza birika linalovuja.” Kwa kweli, ni wakati tu nilipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova kwamba kiu yangu ya Mungu ikaridhishwa.—Kama ilivyosimuliwa na Hugo Durán.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Adrian na mimi tukitangaza ujumbe wa ufalme pamoja