Wahamia Puerto Riko
KATIKA Mei 9, 1993, Idara ya Tafsiri ya Kihispania, ikiwa na washiriki 20, ilihama kutoka makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York, kwenda kwenye ofisi mpya ya tawi ya Watch Tower Society katika Guaynabo, Puerto Riko. Kwa nini ilihama? Mshiriki mwenye daraka wa waandishi wa makao makuu ya Mashahidi wa Yehova aeleza hivi: “Tumepata kuwa watafsiri hufanya kazi nzuri wanapoishi mahali ambapo lugha wanayotafsiri inasemwa kila siku. Zaidi ya hilo, wao huwa macho kwa mambo yoyote mapya ya lugha hiyo. Puerto Riko imeteuliwa kwa kufaa kuwa kitovu cha ulimwengu wenye kusema Kihispania.”
Idara ya Tafsiri ya Kihispania imekuwa Brooklyn, New York, tangu 1928 na imetimiza daraka la maana katika kueneza ujumbe wa Ufalme kwa kusaidia kufanya fasihi ya Biblia ipatikane kwa watu wenye kusema Kihispania wapatao 350,000,000 ulimwenguni pote. Mnara wa Mlinzi lilichapishwa kwa mara ya kwanza kwa Kihispania katika 1917. Leo, zaidi ya nakala 3,000,000 za Mnara wa Mlinzi na zaidi ya nakala 2,000,000 za Amkeni! huchapwa katika Kihispania kila mwezi. Katika miaka ya karibuni ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Uhispania imetoa msaada wenye thamani katika kazi hii pia, hasa katika kutafsiri gazeti Amkeni! Kuna Mashahidi wa Yehova zaidi ya 1,100,000 wanaosema Kihispania ulimwenguni, karibu asilimia 25 ya jumla ya Mashahidi ulimwenguni pote. Hesabu hii inatia ndani makumi ya maelfu ya wahamiaji wanaotumikia katika nchi zisizosema Kihispania, kama vile Australia, Ujerumani, Sweden, na United States.
Uhamiaji kwenye majengo makubwa na mapya zaidi katika Puerto Riko una manufaa nyingine. Unaruhusu watafsiri na wasomaji kutoka nchi tofauti, kama vile, Kolombia, Meksiko, Puerto Riko, Uhispania na Venezuela, waunganishwe kwenye kitovu kimoja ili kwamba ladha ya kimataifa ya vichapo vya sosaiti katika Kihispania iweze kuchochewa zaidi. Hili litasaidia kueleza ujumbe wa Ufalme katika njia iliyo wazi na sahihi kwa watu wenye kusema Kihispania ulimwenguni pote. Tunatazamia baraka za Yehova juu ya maendeleo hayo mapya.