Sababu Iliyonifanya Niache Ukasisi kwa Ajili ya Huduma Bora Zaidi
NILIWEKELEWA mikono kuwa kasisi wa Katoliki katika Julai 31, 1955, nikiwa na umri wa miaka 24. Kilikuwa kilele cha miaka 12 niliyotumia katika seminari ya dayosisi ya askofu, Rachol, Goa, India. Na ni nini kilichochochea tamaa yangu ya kuwa kasisi?
Nilizaliwa katika Bombay, India, Septemba 3, 1930. Mwaka uliofuata, baba yangu alistaafu, na familia ikatulia katika Salvador do Mundo, Bardez, Goa, katika pwani ya kusini-magharibi ya India. Nilikuwa mdogo zaidi kati ya watoto wanne. Kuanzia utoto nililelewa katika desturi na mapokeo ya Kireno ya Kikatoliki, ambayo yamekuwako katika Goa tangu 1510, wakati ilipotawalwa na Ureno.
Wazazi wangu, wakiwa waaminifu katika imani zao, walikuwa Wakatoliki wenye bidii ambao kila mwaka walisherehekea Krismasi, Kufunga, Ista, na karamu za kumheshimu Bikira Mariamu na “watakatifu” kadhaa. Makasisi walioshiriki katika sherehe hizo mara nyingi walikuwa wanakaa nyumbani mwetu, nyakati nyingine zaidi ya siku kumi kwa wakati mmoja. Hivyo, tulikuwa na uhusiano wenye kuendelea pamoja nao, na nikiwa kijana nilivutiwa nao.
Utumishi Wangu Katika Goa, Salamanka, na Roma
Nilianza huduma ya kikasisi nikiwa na idili nyingi sana, na sikuwa na mashaka yoyote kuhusu kweli ya mafundisho na mazoea ya Kanisa Katoliki. Katika miaka saba ya kwanza ya huduma katika Goa, nilifanya wajibu wa kijamii na upadre katika St. Thomas Chapel katika Panaji, jiji kuu la Goa. Wakati uleule, katika kile kilichokuwa Chuo cha Ufundi cha Ureno cha serikali, nilikuwa na mgawo wa kiserikali ambao ulikuwa na madaraka mawili—profesa na pia mkurugenzi wa majengo ya chuo.
Katika 1962, nilipelekwa kwenye Chuo Kikuu cha Salamanka, katika Hispania, ambapo nilipata digrii ya kuwa profesa wa Falsafa ya Sheria na Sheria ya Kanoni. Katika mafunzo yangu ya kisheria, baadhi ya masomo niliyojifunza, hasa Sheria ya Roma na Historia ya Sheria ya Kanoni, zilinichochea kuchunguza jinsi sheria za Kanisa Katoliki zilitokea na kuibuka kufikia kumtambua papa kuwa mwandamizi wa Petro na ‘mwenye mamlaka kuu juu ya kanisa.’
Nilifurahi kwamba mipango ilikuwa ikifanywa kwa ajili ya masomo yangu ya kidini katika Roma, Italia, ambako ningekuwa na fursa ya kujifunza mengi kuhusu uongozi wa kanisa. Nilihamia Roma katika kiangazi cha 1965.
Wakati huo baraza kuu la Vatikani ya Pili lilikuwa limefikia kilele chalo. Nilipokuwa nikifuatia masomo yangu ya kidini, nilikuwa na mazungumzo yenye kupendeza pamoja na wanadini kadhaa na “Mababa wa Baraza” ambao walipinga washikilia desturi mno katika baraza. Papa aliyekuwa akitawala alikuwa Paul wa 4, ambaye niliwasiliana naye kibinafsi kwa cheo changu nikiwa kaimu msimamizi wa Shirika la Makasisi wa India katika Roma.
Mahitilafiano na Mashaka ya Mapema
Katika kipindi chote cha kukutana huku na masomo yangu na utafiti wa digrii yangu, nilipata fursa ya kupata mwono zaidi wa historia na maendeleo ya umbo la msingi wa Kanisa Katoliki.a Kinyume cha maoni ya washikilia desturi katika baraza hilo, ambao walizoea aina ya utawala kamili wa Pius wa 12 (1939-58), wenye akili iliyofunguka hatimaye waliweza kupata kibali cha baraza la Sheria ya Kisharti kwa Kanisa (Kichwa kikuu cha Kilatini, Lumen Gentium, Nuru ya Mataifa). Miongoni mwa mambo mengineyo, katika sura ya 3 ilishughulika na haki ya maaskofu kushiriki wakiwa baraza katika mamlaka kamili na kuu ya papa juu ya kanisa. Kina cha fundisho hilo kilikuwa ni mapokeo lakini lilionwa na wenye kushikilia desturi kuwa la kizushi na la kimapinduzi.
Niliona maoni hayo yote mawili kuwa yasiyokubalika, kwa kuwa yalikosa kweli ya Gospeli. Hayo yanapotoa Mathayo 16:18, 19 na yanaruhusu mafundisho yote yasiyo ya kimaandiko ya wakati uliopita na wakati ujao na masharti ya kanisa.b Niliona kwamba maneno ya Kigiriki yanayotumiwa katika andiko hili, peʹtra (namna ya kike), kumaanisha “mwamba,” na peʹtros (namna ya kiume), kumaanisha “kipande cha mwamba,” hayakutumiwa na Yesu kuwa ya maana sawa. Zaidi ya hilo, ikiwa Petro alikuwa amepewa uwezo wa kuwa mwamba, kama jiwe la pembeni, hakungelikuwa na mabishano miongoni mwa mitume baadaye juu ya ni nani aliyekuwa mkuu zaidi kati yao. (Linganisha Marko 9:33-35; Luka 22:24-26.) Pia, Paulo hangethubutu kumkemea Petro hadharani kwa ‘kutoenda sawasawa na ile kweli ya Injili.’ (Wagalatia 2:11-14) Niliamua kwamba wafuasi wote wa Kristo wapakwa kwa roho ni kama jiwe sawasawa, Yesu akiwa jiwe kuu la pembeni.—1 Wakorintho 10:4; Waefeso 2:19-22; Ufunuo 21:2, 9-14.
Kadiri nilivyofikia kiwango cha juu cha elimu na cheo cha kipadri na mbadilishano wa maoni niliyokuwa nayo, ndivyo nilivyojitenga katika akili na moyo kutokana na masharti mbalimbali ya Kanisa Katoliki, hasa yale yanayohusu kuwekelewa mikono kwa makasisi katika maana ya “Sadaka Takatifu ya Misa” na “Sakramenti Iliyobarikiwa Zaidi ya Ekaristi.”—inayoitwa badiliko la mkate na divai kuwa mwili na damu halisi.
Katika maana ya Kikatoliki, “Sadaka Takatifu ya Misa” ni ukumbusho wa daima na kufanywa upya kwa dhabihu ya Yesu bila damu kwenye “msalaba.” Lakini Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kwa ujumla na hasa barua ya Paulo kwa Waebrania ilikuwa dhahiri kwangu kung’amua kwamba dhabihu ya Yesu ilikuwa kamilifu. Kazi yake ilikuwa kamili. Na haikuhitaji au kuwa nyepesi kupata maongezeo yoyote, marudio, au marekebisho. Dhabihu hiyo ilitolewa “mara moja [kwa wakati wote, NW].”—Waebrania 7:27, 28.
Utafutaji Wangu wa Kweli Waendelea
Ili kujitahini mwenyewe, niliendelea kufanyia kazi dayosisi na dayosisi za askofu mkuu, katika Magharibi mwa Ulaya, kwa dayosisi ya askofu mkuu ya New York, na kwa dayosisi ya Fairbanks, Alaska. Ulikuwa mtihani mgumu sana wa miaka tisa la kutafuta kwangu kweli. Nilijihusisha hasa katika mambo ya usimamizi, sheria za kidini, na utekelezaji wa sheria. Nilijitenga mbali kadiri nilivyoweza na desturi za ushirika wa kidini na sherehe. Jambo lililokuwa gumu zaidi lilikuwa kule kusema Misa ya kila siku. Lilitokeza hitilafu ya hisia na hisia-moyo kwa sababu sikuamini katika dhabihu ya Kristo isiyo ya damu au katika badiliko la mkate na divai kuwa mwili na damu halisi au katika ukasisi mtakatifu wa kidunia unaohitajiwa ili kufanya kihalali na kisheira ule “mzungu” wa badiliko la mkate na divai kuwa mwili na damu halisi.
Wakati wa Baraza la Pili la Vatikani, kulikuwa na mabishano kuhusu “mzungu” huu. Wasioshikilia sana desturi wakiongozwa na jamii ya maaskofu Wakatoliki Waholanzi waliunga mkono “ufananisho wa mifano,” yaani, mkate na divai inamaanisha tu au kuwakilisha mwili na damu ya Kristo. Kwa upande ule mwingine, washikilia desturi mno, wakiongozwa na jamii ya maaskofu Wakatoliki Waitalia, walitetea vikali “badiliko la mkate na divai kuwa mwili na damu halisi,” yaani, kubadilishwa kwa mkate na divai kuwa kweli namna halisi ya mwili na damu ya Kristo kwa “maneno matakatifu” yaliyosemwa wakati wa Misa. Hivyo, msemo ulikuwa: ‘Katika Uholanzi vitu vyote hubadilika isipokuwa mkate na divai, ilhali katika Italia, hakuna kitu kinachobadilika isipokuwa mkate na divai.’
Najitenga na Kanisa
Kwa sababu ya kuelezwa vibaya huko kwa Kristo na gospeli yake, nilihisi kutamaushwa sana na kuvurugika hivi kwamba mradi wangu wa kumtukuza Mungu na kuokoa nafsi ulikuwa ukiharibiwa na mafundisho bandia. Hivyo, katika Julai 1974, nilijiuzulu shughuli za huduma nikiomba pumziko la wakati usiojulikana. Halingekuwa jambo la akili na linalokubalika kwangu kuomba niondolewe kwenye orodha ya ukasisi ambao haukuwa na msingi wa Kibiblia. Kwa sababu hiyo, kuanzia Julai 1974 hadi Desemba 1984, niliendelea kujitenga kabisa na dini yoyote. Sikushirikiana na dini yoyote ile ya Jumuiya ya Wakristo kwa sababu hakukuwa na yoyote kati yazo iliyoshiriki maamuzi yangu ya dhidi ya Utatu, kutokufa kwa nafsi, fu-ndisho la watu wote waadilifu kupata uhai wa milele mbinguni, na adhabu isiyokoma ya moto wa helo. Niliyaona mafundisho hayo kuwa yaliyotokana na upagani.
Amani na Furaha ya Ndani
Kujitenga kwangu na dini kulikoma katika Desemba 1984. Katika cheo changu nikiwa meneja wa Idara ya Akiba na Malipo ya biashara ya Anchorage, Alaska, ilinipasa nizungumze invoisi kadhaa na mteja mmoja, Barbara Lerma. Alikuwa na haraka na akasema kwamba alipaswa kuhudhuria “funzo la Biblia.” Ule msemo “funzo la Biblia” ulivuta uangalifu wangu, na nikamuuliza maswali machache ya Kibiblia. Bila kukawia na kwa njia fulani alinipa majibu yafaayo na ya Kimaandiko ambayo yalifaana na maamuzi yangu mwenyewe ya mafundisho. Alipoona kwamba nilikuwa na maswali mengi, Barbara alinifanya niwasiliane na Gerald Ronco, aliyekuwa katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Alaska.
Mazungumzo yenye kujenga yanayohusiana na Biblia yaliyofuata yaliniletea amani na furaha ya ndani. Hawa ndio watu niliokuwa nikitafuta—watu wa Mungu. Nilimwomba Mungu anipe mwongozo na kwa wakati unaofaa nikaanza kushirikiana na Mashahidi wa Yehova nikiwa mhubiri asiyebatizwa wa habari njema. Nilishangaa kwelikweli kujua kwamba makao makuu ya tengenezo hili yalikuwa katika Brooklyn, New York, kilometa chache tu kutoka Holy Family Church katika Manhattan, ambapo nilitumikia (katika 1969, 1971, na 1974) nikiwa pasta mshirika wa Parish Church of the United Nations.
Kusaidia Familia Yangu Kuona Kweli
Baada ya miezi sita ya kushirikiana na Mashahidi wa Yehova katika Anchorage, nilihamia Pennsylvania katika Julai 31, 1985. Nikiwa huko nilikuwa na pendeleo la kushiriki habari njema za Ufalme wa Yehova na mpwa wangu Mylene Mendanha, ambaye alikuwa akifuatia masomo ya juu ya biokemia katika Chuo kikuu cha Scranton. Mylene alipojua kwamba nilikuwa nikiwatafuta Mashahidi wa Yehova, alifadhaika, kwa kuwa mwanzoni alikuwa ameelezwa vibaya kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa dhehebu. Mwanzoni hakuniambia jambo lolote kwa kuwa aliniheshimu nikiwa mjombake na kasisi aliyaheshimu matimizo yangu ya elimu ya kikasisi.
Jumapili iliyofuata, Mylene alienda kwenye Kanisa Katoliki kwa ajili ya Misa, na mimi nilienda kwenye Jumba la Ufalme kwa ajili ya hotuba ya Biblia na Funzo la Mnara wa Mlinzi. Jioni hiyohiyo tuliketi pamoja, yeye akiwa na Jerusalem Bible ya Katoliki nami nikiwa na New World Translation of the Holy Scriptures. Nilimwonyesha jina Yahweh katika Biblia yake na lile linalolingana na hilo Yehova, katika New World Translation. Alipendezwa sana kujua kwamba Mungu ana jina na kwamba anataka tumwite kwa jina lake. Pia nilimwambia jinsi mafundisho yasiyo ya Kimaandiko ya Utatu, badiliko la mkate na divai kuwa mwili na damu halisi, na kutokufa kwa nafsi na nikamwonyesha maandiko yaliyolingana. Alishangaa kabisa!
Kupendezwa kwa Mylene kuliamshwa zaidi nilipomwambia juu ya tumaini la uhai wa milele katika Paradiso duniani. Kabla ya hapo alikuwa na wasiwasi ni nini kingetokea kwake akifa. Alifikiri hakuwa mtakatifu vya kutosha kwenda moja kwa moja mbinguni, lakini hakufikiri alikuwa mwovu kiasi cha kuhukumiwa adhabu ya mto wa milele katika helo. Hivyo, jambo alilokuwa nalo tu akilini lilikuwa purgatori, ambamo angepaswa kungojea kwa subira sala za watu na Misa ili kumpeleka mbinguni. Hata hivyo, baada ya kumwonyesha na kumwelezea maandiko machache kuhusu tumaini la uhai wa milele katika Paradiso duniani, alikuwa na hamu ya kujifunza zaidi juu ya hizi habari njema za ajabu. Mylene alihudhuria mikutano ya Jumba la Ufalme pamoja nami. Tulianza funzo la Biblia rasmi na Mashahidi wa mahali hapa. Baada ya muda mfupi, tulijiweka wakfu kwa Yehova Mungu na tukabatizwa katika Mei 31, 1986.
Familia yangu, hasa ndugu yangu mkubwa, Orlando, walikasirika sana kwa habari ya kuacha kwangu ukasisi. Alimjulisha dada yangu Myra Lobo Mendanha, ambaye alimtuliza, akisema: “Acha tusisumbuliwe na jambo hili, kwa kuwa Alinio hangeacha miaka yake yote 43 ya kazi ngumu bila sababu nzuri sana.” Katika Septemba 1987, Myra na familia yake walijiunga nami katika Wisconsin, U.S.A. Sikupata ugumu wa kuwafanya waone jinsi mafundisho na mazoea mengi ya Katoliki yasivyo ya kimaandiko. Walikuwa na hamu ya kujifunza kweli za Biblia. Upesi, Mylene nami tukaanzisha funzo la Biblia pamoja nao. Walipohamia Orlando, Florida, waliendelea na funzo lao.
Amani na shangwe tuliyofurahia sote ilitufanya tushiriki habari njema za Ufalme wa Yehova na dada yangu mkubwa, Jessie Lobo, anayeishi Toronto, Kanada. Alikuwa ametolewa ushahidi katika 1983. Hata hivyo, akiwa na ndugu aliye kasisi, aliamini kwamba hakuna kitu ambacho kingebadilisha imani yake. Miaka minne baada ya mazungumzo ya kwanza na Mashahidi wa Yehova, alipojua kwamba nilikuwa Shahidi wa Yehova na kwamba Myra na familia yake walikuwa wahubiri wa habari njema, alimfikia Shahidi ambaye alianzisha funzo la Biblia bila kukawia. Jessie alibatizwa katika Aprili 14, 1990; Myra, shemeji yangu Oswald, na mpwa wangu Glynis walibatizwa Februari 2, 1991. Walikuwa na furaha sana kumtumikia Yehova, Aliye Juu Zaidi.
Washikilia desturi wasiobadilika na wenye akili iliyofunguka katika Kanisa Katoliki kwa kweli ni watu welekevu. Wanaamini wanafanya mapenzi ya Mungu. Hata hivyo, hatupaswi kusahau uhakika wa kwamba “mungu wa dunia hii amepofusha fikira zao wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo aliye sura yake Mungu.” (2 Wakorintho 4:4) Basi, ni dhahiri, kwamba hekima ya mfumo huu wa mambo ni upumbavu kwa Mungu. (1 Wakorintho 3:18, 19) Nina shukrani na furaha kama nini kwamba Yehova “humtia mjinga hekima” kupitia ujuzi sahihi wa Neno lake.—Zaburi 19:7.
Miaka yangu 19 ya utumishi nikiwa kasisi Mkatoliki ni jambo lililopita. Mimi sasa ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ni tamaa yangu kutembea katika njia za Yehova na kufuata Mwanaye, Yesu Kristo, Mfalme na Mwokozi wetu. Ningependa kusaidia wengine wamjue Yehova ili kwamba wao pia wastahili zawadi ya uhai wa milele katika paradiso duniani, kwa utukufu wa Mungu wa kweli, Yehova.—Kama ilivyosimuliwa na Alinio de Santa Rita Lobo.
[Maelezo ya Chini]
a Nilitoka Salamanka nilipokuwa bado nafanya utafiti wa insha yangu ya Sheria ya Kanoni, ambayo nilitoa katika 1968.
b Andiko hili kwa sehemu lasema hivi, kulingana na New American Bible ya Katoliki: “Nami nakuambia wewe, wewe ni ‘Mwamba,’ na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu . . . Lolote utakalotangaza kuwa limefungwa duniani litafungwa mbinguni; lolote utakalotangaza kuwa limeachiliwa duniani litafunguliwa mbinguni.”—Ona sanduku, ukurasa 23.
[Sanduku katika ukurasa wa 23]
Funguo za Ufalme
Kwa habari ya “funguo za ufalme wa mbinguni,” maana yayo yawa dhahiri wakati tunapofikiria lawama ambayo Yesu alitolea viongozi wa kidini: “Mmeuondoa ufunguo wa maarifa; wenyewe hamkuingia, na wale waliokuwa wakiingia mmewazuia.” (Luka 11:52) Zaidi ya hayo Mathayo 23:13 huonyesha “kuingia” kuwa kukielekeza kuingia katika “ufalme wa mbinguni.”
Funguo ambazo Yesu aliahidi Petro zilianzisha daraka la kipekee la kielimu ambalo lingefungua fursa za pekee kwa watu mmoja-mmoja kuingia katika ufalme wa mbinguni. Petro alitumia pendeleo hilo katika pindi tatu, kusaidia Wayahudi, Wasamaria, na Wasio Wayahudi.—Matendo 2:1-41; 8:14-17; 10:1-48; 15:7-9.
Kusudi la ahadi hiyo lilikuwa, si juu ya Petro kuamuru mbingu juu ya nini kingefungwa au kufunguliwa, bali Petro kutumiwa kuwa chombo cha mbingu kwa ajili ya migawo hiyo mitatu hususa. Hilo ni kweli kwa sababu Yesu aliendelea kuwa Kichwa cha kweli cha kutaniko.—Linganisha 1 Wakorintho 11:3; Waefeso 4:15, 16; 5:23; Wakolosai 2:8-10; Waebrania 8:6-13.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Alinio de Santa Rita Lobo sasa ni Shahidi