Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g93 9/22 kur. 6-11
  • Upweke-Je! Umeazimia Kupambana Nao na Kuushinda?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Upweke-Je! Umeazimia Kupambana Nao na Kuushinda?
  • Amkeni!—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ni Juu Yako
  • Tenda Utakavyo
  • Uhusiano Bora Kabisa Unaohitaji
  • Mahali Unapokuza Mwaridi, Mbaruti Hauwezi Kumea
  • Ni Nini Kinachoweza Kufanya Maisha Yajawe na Umaana Kwelikweli
  • Mungu Akiwa Pamoja Nawe, Hauko Peke Yako Kamwe
  • Usiache upweke uathiri vibaya maisha yako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Kuushinda Upweke
    Amkeni!—2004
  • Kwa Nini Watu Wengi Huhisi Upweke?
    Amkeni!—2004
  • Upweke-Teso Kubwa Lililofichika
    Amkeni!—1993
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1993
g93 9/22 kur. 6-11

Upweke-Je! Umeazimia Kupambana Nao na Kuushinda?

JE! WEWE ni mpweke? Kuna pindi katika maisha ambapo ni kawaida kuhisi upweke, uwe umefunga ndoa au uwe mseja, uwe mwanamume au mwanamke, uwe mzee-mzee au kijana. Ujue pia kwamba kuwa peke yako hakumaanishi kwamba ni lazima utapatwa na upweke. Msomi aliye peke yake ambaye amejiingiza katika utafiti wake hahisi upweke. Mchoraji aliye peke yake anayechora picha hana wakati wa kuhisi upweke. Wao hufurahia wakati wa faragha, na faragha yawa rafiki yao mkubwa zaidi.

Hisia ya upweke wa kweli huanzia ndani yetu kabisa badala ya kuanzia nje. Upweke waweza kuanzishwa na tukio lenye kuhuzunisha—kifo, talaka, kupoteza kazi, msiba fulani. Tunapowasha ulimwengu wetu wa ndani kwa uangavu, upweke huo waweza kupunguzwa, labda hata upotee baada ya muda fulani, na ule msiba tuliopata waweza kuvumiliwa, kumalizwa.

Hisia hutokana na mawazo yako. Baada ya msiba kumalizwa na hisia ulizotoa kupunguzwa kabisa, basi ni wakati wa kuzingatia mawazo yanayojenga yanayokuwezesha uendelee na maisha yako ya kawaida.

Uwe mwenye utendaji. Jidhibiti. Kuna mambo mazuri ya kufanywa. Kwa hiyo uwe mwenye urafiki. Pigia mtu simu. Andika barua. Soma kitabu. Alika watu nyumbani mwako. Shauriana na wengine. Ili uwe na marafiki, ni lazima uwe mwenye urafiki. Jichunguze mwenyewe kindani ili uwafikie wengine. Onyesha vitendo vidogo vya fadhili. Shiriki mambo fulani madogo-madogo ya kiroho yenye kufariji pamoja nao. Utapata maneno haya ya Yesu kuwa ya kweli: “Heri [kuna furaha zaidi katika, New World Translation] kutoa kuliko kupokea.” Utatambua kweli nyingine ya mithali: “Anyweshaye atanyweshwa mwenyewe.”—Matendo 20:35; Mithali 11:25.

Ni Juu Yako

Ni vigumu? Je! ni rahisi kusema kuliko kufanya? Ni rahisi kusema kuliko kufanya kitu chochote kifaacho. Hilo ndilo jambo linalofanya kukifanya kuridhishe. Ni lazima ujitahidi kabisa. Sehemu fulani yako yaenda kwenye kutoa, na shangwe yako yaongezeka zaidi na zaidi. Ni juu yako kutia jitihada ili uondoe upweke unaotaka kukudhibiti. Mwandikaji mmoja katika gazeti Modern Maturity alisema: “Hakuna mtu mwingine anayesababisha upweke wako, lakini wewe waweza kufanya jambo fulani juu ya upweke huo. Waweza kupanua maisha yako kwa urafiki mmoja tu. Waweza kumsamehe mtu unayehisi alikuumiza. Waweza kuandika barua. Waweza kupigia mtu simu. Ni wewe tu unayeweza kugeuza maisha yako. Hakuna mtu yeyote awezaye kukufanyia hilo.” Alinukuu barua moja aliyopokea yenye “kutaja kimahususi jambo hilo: ‘Naambia watu ni juu yao kufanya maisha yao yasiwe ya upweke au yasiyoridhisha. Basi fanya hivyo!’”

Si lazima marafiki wako wenye kukusaidia wawe binadamu pekee. Daktari mmoja wa dawa za kutibu wanyama alisema hivi: “Matatizo makubwa zaidi yanayokabili wazee-wazee si magonjwa ya kimwili, bali upweke na kupuuzwa wanakopata. Kwa kuandaa . . . uenzi, wanyama vipenzi (kutia ndani mbwa) huandaa kusudi na uradhi wakati ambapo wazee-wazee mara nyingi wanakuwa wamejitenga na jamii.” Gazeti Better Homes and Gardens lilisema hivi: “Wanyama vipenzi husaidia kutibu watu wenye masumbufu ya kihisia-moyo; huwatia moyo wagonjwa wa kimwili, walemavu, na wasiojiweza; na kupatia wapweke na wazee-wazee nguvu tena.” Makala nyingine katika gazeti moja ilisema hivi juu ya watu wanaoanza kusitawisha kupendezwa katika wanyama vipenzi: “Mahangaiko ya wagonjwa yalipungua na walikuwa wakionyesha upendo wao kwa wanyama vipenzi wao bila woga wa kukataliwa. Baadaye walianza kuwasiliana na watu, wakizungumzia kwanza utunzaji wa wanyama vipenzi wao. Walianza kuhisi wakiwa na daraka. Walihisi walihitajiwa, kwamba jambo fulani liliwategemea.”

Mara nyingi mno mtu anayepata upweke hawezi kujiimarisha vya kutosha kujisaidia mwenyewe, ili ajitoe mwenyewe katika hali ya kutamauka sana. Kuna msukumo fulani, hali fulani ya kukataa kujikakamua kwa kadiri hiyo, lakini ikiwa ataka kumaliza upweke wake, ni lazima afanye hivyo. Dakt. James Lynch aliandika hivi juu ya kukataa kwa watu kukubali shauri ambalo hawapendi: “Hali ya kibinadamu ni kwamba kwa ujumla sisi hukataa kusikia, au angalau kukataa kutumia katika tabia yetu, habari tusiyoipenda.” Huenda mtu akataka kushinda upweke wake, lakini huenda asitake kujikakamua ili aushinde.

Tenda Utakavyo

Ili kushinda mshuko mkubwa wa moyo, mtu ahitaji kudumu katika kufuatia uchangamfu na fadhili halisi. (Linganisha Matendo 20:35.) Hilo lahitaji mtu aache hali hiyo ya upweke wa ndani kwa kufanya mambo ambayo ni kinyume cha ulegevu wao ulio hatari. Tenda kwa furaha, cheza dansi, imba wimbo wenye kufurahisha. Fanya jambo lolote linaloonyesha furaha. Litie chumvi, ulifanye kupita kiasi, ondoa hali hiyo ya huzuni kwa kujaza mawazo yenye furaha. Kama yapi?

Kama yale yapatikanayo katika Wafilipi 4:8: “Hatimaye, ndugu zangu, mambo yo yote yaliyo ya kweli, yo yote yaliyo ya staha, yo yote yaliyo ya haki, yo yote yaliyo safi, yo yote yenye kupendeza, yo yote yenye sifa njema; ukiwapo wema wo wote, ikiwapo sifa nzuri yo yote, yatafakarini hayo.”

Uhitaji ni kufanya maisha yako yawe na umaana fulani. Ukihisi kwamba maisha yako yana umaana fulani, utapata nguvu ya kuuitikia umaana huo na kutafuta kuridhisha maisha yako. Hutaelekea kuangukia upweke wenye kukatisha tamaa. Kwa kupendeza, jambo hilo laonyeshwa katika kitabu cha Viktor Frankl, Man’s Search for Meaning. Ajadili kitabu hicho kuhusu wafungwa katika kambi za mateso za Hitler. Wale ambao hawakuwa na hisi ya kuwa na umaana katika maisha yao walitumbukia katika upweke na kukosa moyo wa kuendelea kuishi. Lakini “kule kutambua thamani ya ndani ya mtu kwategemea mambo ya kiroho ya juu zaidi, na hakuwezi kutikiswa na maisha ya kambi.” Aliendelea kusema hivi: “Mateso hukosa kuwa mateso kwa njia fulani wakati kusudi layo linapojulikana, kama vile kusudi la dhabihu. . . . Hangaiko kubwa la binadamu si kupata raha wala kuepuka maumivu, bali kuona umaana maishani mwake. Hiyo ndiyo sababu mtu huwa tayari hata kuteseka, mradi tu ajue, awe na uhakika kwamba kuna kusudi fulani katika kuteseka kwake.”

Uhusiano Bora Kabisa Unaohitaji

Njia ya kupata mtazamo wa kiroho kwelikweli ni kumwendea Mungu moja kwa moja na Neno lake, Biblia. Imani katika Mungu na sala yenye bidii kwake yaweza kuyapa maisha yetu kusudi. Basi, hata mahusiano ya kibinadamu yaporomoke, hatuko peke yetu, hatutapatwa na upweke. Kama Frankl alivyosema, kuteseka kwa kusudi fulani kwaweza kuvumilika, hata kuwa chanzo cha shangwe. Mchunguzaji mmoja wa tabia ya kibinadamu alisema hivi: “Mfia-imani katika mti aweza kuwa na furaha ambayo mfalme katika kiti chake cha enzi aweza kutamani.”

Mitume wa Kristo walihisi shangwe kutoka kwa Yehova waliponyanyaswa na wanadamu; mateso hayo yalikuwa na kusudi kubwa sana kwao. “Heri [wenye furaha ni, NW] wenye kuudhiwa kwa ajili ya haki; maana ufalme wa mbinguni ni wao. Heri [wenye furaha ni, NW] ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu.” (Mathayo 5:10-12) Itikio kama hilo limerekodiwa katika Matendo 5:40, 41: ‘Nao waliwaita mitume, wakawapiga, wakawaamuru wasinene kwa jina lake Yesu; kisha wakawaacha waende zao. Nao wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo.’

Mahali Unapokuza Mwaridi, Mbaruti Hauwezi Kumea

Jaza udongo wa akili yako na mbegu zenye uzuri na zenye kusudi zuri; usiachie nafasi mbegu za kutamauka kusikofaa na upweke wenye utupu. (Linganisha Wakolosai 3:2; 4:2.) Je! ni vigumu kufanya hivyo? Chini ya hali fulani, ni kama haiwezekani. Mwanashairi mmoja alisema hivi: “Mahali unapokuza mwaridi, . . . mbaruti hauwezi kumea,” jambo ambalo tena lahitaji jitihada zinazofaa na kuwa na moyo wenye bidii. Lakini laweza kufanywa, laendelea kufanywa.

Chukua kielelezo cha Laurel Nisbet. Alipatwa na ugonjwa wa kupooza na akiwa na umri wa miaka 36 aliwekwa katika pafu la chuma, ambamo alilala chali kabisa kwa miaka 37. Akipooza kabisa kuanzia shingo kwenda chini, hakuna jambo jingine ambalo angeweza kufanya ila tu kusogeza kichwa chake. Mwanzoni alihuzunika sana kiasi cha kuhisi kwamba hafai kitu. Kisha baada ya kujihurumia kwa karibu siku moja, aliamua, ‘Hayo Yatosha!’ Alikuwa na watoto wawili wa kulea na mume wa kutunza. Alianza kujenga maisha yake; alijifunza kusimamia nyumba yake akiwa ndani ya pafu la chuma.

Laurel alikuwa akipata usingizi kidogo sana. Alitumiaje muda wa saa nyingi za usiku? Kwa kutumbukia katika upweke? La. Alisali kwa Baba yake wa kimbingu, Yehova. Alikuwa akisali apate nguvu, akisali kwa ajili ya akina ndugu na dada zake wa Kikristo, na kwa ajili ya fursa za kutoa ushahidi kwa wengine juu ya Ufalme wa Mungu. Alibuni njia za kuhubiri na alivutia watu wengi kwa kutoa ushahidi kwa jina la Yehova. Hakuruhusu mibaruti ya upweke imee; alikuwa mwenye shughuli mno akikuza miwaridi.

Hali iyo hiyo ilimpata mishonari wa Watch Tower, Harold King. Akiwa amefungwa kifungo cha miaka mitano akiwa peke yake katika gereza la Uchina, alikuwa shabaha rahisi sana ya kupatwa na upweke wa muda mrefu. Hata hivyo, alikataa kuwa na mtazamo huo usiofaa, na kwa tendo alilopanga lenye moyo, aliweka akili yake katika mwendo tofauti. Baadaye alisimulia jambo hilo hivi:

“Nilipangia programu ya utendaji wa ‘kuhubiri.’ Lakini mtu atahubiria nani akifungwa peke yake? Niliamua kwamba ningetayarisha hotuba za Biblia zinazofaa kutokana na mambo ambayo ningeweza kukumbuka na kisha nihubirie watu wa kuwaziwa tu. Basi nikaanza kazi ya mwigizo wa kuhubiri, nikibisha mlango wa kuwaziwa tu na kutoa ushahidi kwa mwenye nyumba wa kuwaziwa tu, nikizuru milango kadhaa wakati wa asubuhi. Baada ya muda nilikutana na Bi. Carter wa kuwaziwa tu, aliyeonyesha kupendezwa kadiri fulani, na baada ya ziara kadhaa za kurudia tulipanga tuwe na funzo la Biblia la kawaida. Katika funzo hilo tulizungumzia vichwa vikuu kutoka kitabu ‘Let God Be True,’ kama nilivyokuwa nikivikumbuka. Nilifanya mambo hayo yote kwa sauti, ili kwamba kusikika kwa mambo hayo kuyakazie hata zaidi akilini mwangu.”

Maelfu ya Mashahidi wa Yehova waliofungwa katika kambi za mateso za Hitler wangepata uhuru wao kama tu wangekana imani yao. Ni wachache sana waliofanya hivyo. Maelfu walikufa wakiwa waaminifu—baadhi yao kwa kuuawa, baadhi yao kwa magonjwa na utapiamlo. Shahidi mmoja aliyefungwa—aliyeitwa Josef—alikuwa na ndugu wawili katika kambi nyinginezo. Mmoja wao alilazimishwa kulala chali ili aone upanga ukiteremka kukatilia mbali kichwa chake. Josef alieleza hivi: “Wengine kambini waliposikia kisa hicho walinipongeza. Mtazamo wao unaofaa ulinigusa moyo sana. Kuendelea kuwa mwaminifu-mshikamanifu kulimaanisha mengi zaidi kuliko kuokoka.”

Ndugu yake mwingine, alipokuwa akikabili kikosi cha wanajeshi wenye kufyatua risasi, aliulizwa kama angependa kusema jambo lolote. Aliomba ruhusa ya kusali, nayo ilikubaliwa. Sala hiyo ilijawa na maneno yenye kugusa moyo na shangwe ya moyoni hivi kwamba amri ilipotolewa ya kufyatua risasi, hakuna hata mtu mmoja katika kikosi hicho aliyetii. Amri hiyo ilirudiwa, ambapo risasi moja ilifyatuliwa, ikimpiga mwilini. Akighadhabika kwa tukio hilo, ofisa mwenye kuwaongoza kisha alitoa bastola yake mwenyewe na kumaliza uuaji huo.

Ni Nini Kinachoweza Kufanya Maisha Yajawe na Umaana Kwelikweli

Hali hizo zote zilitia ndani imani thabiti kwa Mungu. Wakati kila kitu kingine kimejaribiwa na kukosa kufaulu, nyakati zote imani thabiti huwapo ili kuleta ushindi juu ya upweke na kufanya maisha yaliyokuwa matupu wakati mmoja yajawe na umaana. Maisha mengi yanayoonwa kuwa yenye kujaa maana kilimwengu kwa hakika hayana maana. Ni kwa nini iko hivyo? Kwa sababu matokeo huwa kifo, hurudi mavumbini, na kupotea kabisa, bila kuacha alama duniani. Ni kama vile Mhubiri 9:5 lisemavyo: “Kwa sababu walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote, wala hawana ijara tena; maana kumbukumbu lao limesahauliwa.” Umaana wowote unaoshikamanishwa na maisha yaliyo mbali na makusudi ya Yehova ni ubatili.

Ebu tazama mbingu zilizojaa nyota, hisi ukubwa wa anga hiyo iliyo juu yenye giza, na hisi yako ya umaana yawa ni kama si kitu. Unaelewa hisia za mtunga-zaburi alipoandika hivi: “Nikiziangalia mbingu zako, kazi ya vidole vyako, mwezi na nyota ulizoziratibisha; mtu ni kitu gani hata umkumbuke, na binadamu hata umwangalie?” Mwana wa Daudi Sulemani alitupilia mbali kazi za binadamu, akisema, “Mambo yote ni ubatili,” na akamalizia hivi: “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.”—Zaburi 8:3, 4; Mhubiri 12:8, 13.

Basi, kwa uchanganuzi wa mwisho, mtu mwenye upweke, au mtu mwingine yeyote, atatiaje umaana katika maisha yake? Kwa kuishi maisha yake katika kumhofu Mungu, akitii sheria za Mungu. Ni wakati huo tu ndipo awezapo kujipatanisha na makusudi ya Mungu, Muumba wa ulimwengu wote mzima ulio mkubwa, na kuwa sehemu ya mpango huo wa milele wa kimungu.

Mungu Akiwa Pamoja Nawe, Hauko Peke Yako Kamwe

Shahidi mmoja wa Yehova Mwafrika aliye mwaminifu alisema kwamba hata ikiwa mahusiano yake ya kibinadamu yalikwisha, bado hakuwa peke yake baada ya kuvumilia mnyanyaso mkatili na kuhisi ameachwa. Alinukuu Zaburi 27:10: “Baba yangu na mama yangu wameniacha, bali BWANA, [Yehova, NW] atanikaribisha kwake.” Yesu alihisi vivyo hivyo. “Tazama, saa yaja, naam, imekwisha kuja, ambapo mtatawanyika kila mmoja kwao kwao, na kuniacha mimi peke yangu; walakini mimi si peke yangu, kwa kuwa Baba yupo pamoja nami.”—Yohana 16:32.

Yesu hakuogopa kubaki peke yake. Mara nyingi alitafuta ufaragha kimakusudi. Alipokuwa peke yake, hakuwa mpweke. Alijifunua kwa mtiririko wa roho ya Mungu na kuhisi ukaribu Naye alipozungukwa na vitu Vyake alivyoumba. Nyakati nyingine aliepuka ushirika wa watu ili awe na ushirika na Mungu peke yake. ‘Alimkaribia Mungu, naye Mungu akamkaribia.’ (Yakobo 4:8) Bila shaka alikuwa rafiki ya Mungu wa karibu zaidi.

Rafiki kama yule anayefafanuliwa katika Maandiko ni kitu chenye thamani sana. (Mithali 17:17; 18:24) Abrahamu “aliitwa rafiki wa Mungu” kwa sababu ya imani yake thabiti katika Yehova Mungu na utii wake usio na shaka kwake. (Yakobo 2:23) Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake: “Ninyi mmekuwa rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo. Siwaiti tena watumwa; kwa maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini nyinyi nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu.”—Yohana 15:14, 15.

Wakiwa na marafiki kama Yehova Mungu na Kristo Yesu, wale wenye imani wanaweza kushindwaje na pambano lao dhidi ya upweke?

[Picha katika ukurasa wa 8]

Sala na utendaji mwingine mbalimbali yaweza kukusaidia uepuke upweke

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mambo yaliyopata Harold King na maelfu ya Mashahidi wa Yehova wengine katika kambi za mateso yaonyesha kwamba imani katika Mungu yaweza kushinda upweke chini ya hali ngumu zaidi

[Hisani]

Picha ya U.S. National Archives

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki