Mtoto Wako Akitendwa Vibaya
ILI kukomesha kutenda vibaya, ni lazima ukutambue unapokuona. Katika vitabu vingi vyenye habari hiyo, wastadi wameorodhesha ishara nyingi za kufunua visa vya kutendwa vibaya ambazo wazazi waweza kuwa macho kuona. Hizo zinatia ndani: malalamiko ya kuhisi uchungu wakati wa haja ndogo au kubwa, maambukizo ya viungo vya uzazi, mikwaruzo au majeraha kwenye sehemu za uzazi, kuanza ghafula kukojoa kitandani, kukosa hamu ya kula au matatizo mengine ya kula, tabia za kingono kama za watu wazima, hofu ya ghafula ya mahali kama shule au sehemu za nyumba, vipindi vya kuona wasiwasi mwingi, hofu kuu ya kuvua nguo, hofu ya kuwa pekee na mtu anayejulikana, na kujikata-kata.
Hata hivyo, uwe mwangalifu usikate maneno mapema mno. Nyingi kati ya dalili hizo zikiwa peke yazo hazimaanishi kwamba mtoto hasa ametendwa vibaya kingono. Kila moja yaweza kuonyesha tatizo fulani jingine. Lakini, ukiona ishara zenye kutia wasiwasi, anzisha mazungumzo hayo kwa upole, labda kwa maneno kama vile: “Ikiwa mtu yeyote akugusa kwa njia yoyote inayokufanya ukose kustarehe, ninataka ujue kwamba sikuzote unaweza kuniambia, na nitafanya yote niwezayo ili kukulinda. Je! jambo lolote la aina hiyo limekupata wakati wowote?”—Mithali 20:5.
Ikiwa mtoto wako afunua juu ya kutendwa vibaya kingono, hapana shaka utahisi umepondeka moyo. Lakini kumbuka: Itikio lako litakuwa na sehemu kubwa katika kupona kwa mtoto wako. Mtoto wako amekuwa akichukua mzigo wenye kulemea na anakuhitaji, pamoja na nguvu zako za mtu mzima, umwondolee mzigo huo mabegani pake. Msifu mtoto kwa kuwa mwenye ujasiri na kuweza kukuambia yale yaliyotukia. Mhakikishie mtoto tena na tena kwamba utafanya kila uwezalo ili kumwandalia ulinzi; kwamba kutendwa vibaya huko kulikuwa kosa la mtenda vibaya, si la mtoto huyo; kwamba mtoto huyo si “mbaya”; kwamba unampenda mtoto huyo.
Wastadi fulani wa kisheria hushauri kuripoti kutendwa vibaya huko kwa wenye mamlaka haraka iwezekanavyo. Katika mabara fulani huenda mfumo wa sheria ukataka hilo lifanywe. Lakini katika mahali pengine mfumo wa sheria huenda usitoe tumaini la kufanya mashtaka yenye kufanikiwa.
Hata hivyo, namna gani ikiwa mtenda vibaya ni mwenzi wako unayempenda? Inasikitisha kwamba wanawake wengi hushindwa kuchukua hatua ya maana. Bila shaka, si rahisi kamwe kukabili uhalisi wenye kukirihisha wa mwenzi ambaye ni mtenda watoto vibaya. Vifungo vya kihisiamoyo, na hata utegemeo wa kifedha, waweza kuwa wenye nguvu sana. Mke aliyekosewa anaweza pia kung’amua kwamba kuchukua hatua kwaweza kumgharimu mume wake familia yake, kazi yake, sifa yake.a Hata hivyo, ukweli hasa ni kwamba huenda anavuna yale aliyopanda. (Wagalatia 6:7) Kwa upande ule mwingine, watoto wasio na hatia watapatwa na hasara zaidi ikiwa hawaaminiwi au hawalindwi. Wakati ujao wao umo hatarini. Wao hawana uwezo ambao watu wazima wanao. Mshtuko waweza kuwajeruhi na kuwadhuru vibaya kwa maisha yote. Wao ndio wanaohitaji na wastahili kushughulikiwa kwa wororo.—Linganisha Mwanzo 33:13, 14.
Kwa hiyo ni lazima wazazi wafanye kila jitihada iwezekanayo ili kuwalinda watoto wao! Wazazi wengi wenye kuchukua daraka huchagua kutafuta msaada wa wataalamu kwa ajili ya mtoto aliyetendwa vibaya. Kama vile ungalifanya na daktari wa tiba, hakikisha kwamba mtaalamu yeyote kama huyo ataheshimu maoni yako ya kidini.b Msaidie mtoto arudie kujistahi kwa upendo wa mzazi unaoendelea kuonyeshwa.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa uhalisi, tayari mtenda vibaya yumo mashakani na ahitaji sana msaada. Hata mtenda kosa akidai kwamba anasikitika, huenda mwenzi aliyekosewa akafikiri hivi: Mbona yeye hakuungama makosa kabla ya kufunuliwa na mtendwa vibaya?
b Mathalani, wakati Mashahidi wa Yehova wanapokabiliwa na masuala yanayohusu kutiwa damu mishipani, wao huhakikisha kwamba daktari anaheshimu itikadi zao za kidini.