Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g93 10/8 kur. 5-9
  • Twaweza Kuwalindaje Watoto Wetu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Twaweza Kuwalindaje Watoto Wetu?
  • Amkeni!—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Elimisha Mtoto Wako!
  • Zoeza kwa Ukamili Kabisa
  • Wenye Hadhari Kama Nyoka
  • Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako
    Amkeni!—2007
  • Kuzuia Nyumbani
    Amkeni!—1993
  • Wazazi Wanawezaje Kuwafundisha Watoto Wao Kuhusu Ngono?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Kulea Watoto tangu Uchanga
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1993
g93 10/8 kur. 5-9

Twaweza Kuwalindaje Watoto Wetu?

“Usiwaambie kamwe. Hiyo itakuwa siri yetu.”

“Hakuna mtu ambaye angeweza kukuamini.”

“Ukiwaambia, wazazi wako watakuchukia wee. Watajua kwamba lilikuwa kosa lako.”

“Je! hutaki tena kuwa rafiki yangu wa pekee?”

“Hutaki nifungwe jela, sivyo?”

“Nitawaua wazazi wako ikiwa utawaambia.”

BAADA ya kuwatumia watoto ili kutosheleza tamaa zilizopotoka, baada ya kuwaondolea usalama wao na hisi yao ya kutokuwa na hatia, bado wale wanaowatenda vibaya wataka jambo moja zaidi kutoka kwa watendwa vibaya wao—UKIMYA. Ili kupata ukimya huo, wao hutumia aibu, usiri, hata hofu kuu. Hivyo, watoto hunyang’anywa silaha yao bora zaidi dhidi ya kutendwa vibaya—nia ya kusema, kulalamika na kumwomba mtu mzima awalinde.

Kwa kusikitisha, mara nyingi jamii iliyopevuka hushirikiana na wale wanaowatenda vibaya watoto. Jinsi gani hivyo? Kwa kukataa kuwa macho kuona hatari hiyo, kwa kusitawisha mtazamo wa ukimya kuihusu, kwa kuamini ngano zinazorudiwa-rudiwa mara nyingi. Kukosa maarifa, kuarifiwa kimakosa, na ukimya huwalinda watenda vibaya, si watendwa vibaya.

Kwa kielelezo, Baraza la Maaskofu Wakatoliki la Kanada hivi karibuni lilikata maneno kwamba ni “hila ya ukimya iliyo ya kawaida” iliyoruhusu kutenda watoto vibaya kuendelee miongoni mwa makasisi Wakatoliki kwa miongo mingi. Katika kuripoti juu ya mweneo wa tatizo la ngono za kiukoo, gazeti Time pia lilitaja “hila ya ukimya” kuwa jambo “linalosaidia tu kuchochea msiba huo” katika familia.

Hata hivyo, Time lilionyesha kwamba hila hiyo inaporomoka hatimaye. Kwa nini? Kwa ufupi, ni kwa sababu ya elimu. Ni kama vile gazeti Asiaweek lilivyosema: “Wastadi wote wanakubali kwamba ulinzi bora zaidi dhidi ya kutenda watoto vibaya ni kuelimishwa kwa umma.” Ili kulinda watoto wao, ni lazima wazazi waelewe mambo halisi ya tisho hilo. Usitiwe kiwi na ngano zinazowalinda wale wanaotenda vibaya watoto na wala hazilindi watoto.—Ona sanduku ukurasa 6.

Elimisha Mtoto Wako!

Mfalme Sulemani mwenye hekima alimwambia mwanae kwamba elimu, hekima, na uwezo wa kufikiri vingeweza kumlinda “na njia ya uovu, na watu wanenao yaliyopotoka.” (Mithali 2:10-12) Watoto wanahitaji mambo hayo, sivyo? Kijitabu cha FBI kiitwacho Child Molesters: A Behavioral Analysis chasema hivi chini ya kichwa “Mtendwa Vibaya Kirahisi”: “Kwa watoto wengi ngono ni mada iliyo mwiko ambayo hawapokei habari zilizo sahihi juu yayo, hasa kutoka kwa wazazi wao.” Usiache watoto wako wawe “watendwa vibaya kirahisi.” Waelimishe juu ya ngono.a Kwa kielelezo, hakuna mtoto anayepaswa kufikia ubalehe ilihali hajui jinsi mwili utakavyobadilika wakati huo. Kukosa maarifa kutawafanya wavurugike, waone haya—na wawe rahisi kushambuliwa.

Mwanamke tutakayemwita Janet alitendwa vibaya kingono akiwa mtoto, na miaka mingi baadaye watoto wake wawili walitendwa vibaya kingono. Yeye akumbuka hivi: “Jinsi tulivyolelewa, hatukuzungumzia ngono kamwe. Kwa hiyo nilikua nikiionea haya. Lilikuwa jambo la kuaibisha. Na nilipo-zaa watoto, ilikuwa vivyo hivyo. Ningeweza kuzungumza na watoto wa watu wengine lakini si wangu. Nafikiri hiyo haifai kwa sababu watoto ni rahisi kushambuliwa ikiwa huzungumzi nao juu ya mambo hayo.”

Mafunzo juu ya kuzuia kutendwa vibaya yaweza kutolewa mapema. Unapowafunza watoto wako kutaja majina ya viungo vya mwili kama vile kuma, matiti, mkundu, mboo, waambie kwamba sehemu hizo ni nzuri, ni za pekee—lakini ni za kifaragha. “Watu wengine hawaruhusiwi kuzishika—hata mama wala baba—na hata sio daktari isipokuwa kama mama au baba yupo hapo au amesema ni sawa.”b Inafaa kwamba taarifa hizo zitolewe na wazazi wote wawili au kila mtunzi aliye mtu mzima.

Katika kitabu The Safe Child Book, Sherryll Kraizer aandika kwamba ingawa watoto wapaswa wajihisi huru kupuuza, kupigia yowe, au kutoroka kutoka kwa yule anayewatenda vibaya, watoto wengi wanaotendwa vibaya hueleza baadaye kwamba hawakutaka waonekane wafidhuli. Hivyo watoto wanahitaji kujua kwamba watu fulani wazima hufanya mambo mabaya na kwamba hata mtoto hapaswi kutii kila mtu anayemwambia afanye jambo baya. Nyakati hizo mtoto ana haki kamili ya kusema la, kama vile Danieli na wenzake walivyowaambia watu wazima Wababuloni waliowataka wale chakula kisicho safi.—Danieli 1:4, 8; 3:16-18.

Ufundishaji mmoja unaopendekezwa na wengi ni ule mchezo wa “Namna gani ikiwa . . . ?” Huenda kwa kielelezo ukauliza hivi: “Namna gani ikiwa mwalimu wako anakuambia umpige mtoto mwingine? Wewe ungefanya nini?” Au: “Namna gani ikiwa (mama, baba, mhubiri, polisi) angekuambia uruke kutoka jengo refu?” Huenda jibu la mtoto likawa halitoshi au si sahihi kabisa, lakini usimsahihishe kwa ukali. Mchezo huo haupaswi kutia ndani mambo ya kushtua au ya kuogofya; kwa kweli wastadi wanapendekeza kwamba uchezwe kwa njia ya upole, yenye upendo, hata ya mchezo-mchezo.

Halafu, wafundishe watoto wakinze maonyesho ya shauku ambayo hayafai au yanayowafanya wakose kustarehe. Kwa kielelezo, muulize hivi, “Namna gani ikiwa rafiki fulani ya mama na baba angetaka kukubusu kwa njia inayokufanya uone isivyo kawaida?”c Mara nyingi ni bora kumtia moyo mtoto atende kihalisi yale ambayo angefanya, ukiufanya uwe mchezo wa “Ebu tujifanye.”

Kwa njia iyo hiyo, watoto wanaweza kujifunza kukinza njia nyingine zenye hila za wanaowatenda vibaya. Kwa kielelezo, huenda ukauliza hivi: “Namna gani ikiwa mtu fulani anasema, ‘Unajua, nakupenda sana. Je! hutaki uwe rafiki yangu?’” Mtoto anapojifunza kukinza njia hizo, zungumzieni njia nyinginezo. Huenda ukauliza hivi: “Mtu fulani akisema, ‘Hutaki kunihuzunisha, sivyo?’ Wewe utasema nini?” Mwonyeshe mtoto jinsi ya kusema la kwa maneno na kwa ishara za mwili zilizo thabiti na za waziwazi. Kumbuka, mara nyingi watenda vibaya hujaribu kuona jinsi mtoto anavyoitikia kwa maneno fulani yenye hila. Kwa hiyo ni lazima mtoto afunzwe kukinza kwa uthabiti na kusema, “Nitakushtaki.”

Zoeza kwa Ukamili Kabisa

Katika kuzoeza, usizungumze kwenye kikao kimoja tu na basi. Watoto wanahitaji kukaririwa sana. Tumia uamuzi wako mwenyewe kujua mazoezi yanapaswa kuwa ya bidii kiasi gani. Lakini uzoeze kwa ukamili kabisa.

Kwa kielelezo, hakikisha kwamba unapinga jaribio lolote la mtenda vibaya kufanyiza masikilizano ya kisiri na mtoto. Watoto wapaswa wajue kwamba haifai kamwe kwa mtu mzima kuwaomba wasiwaambie wazazi siri fulani. Wahakikishie kwamba sikuzote inafaa kwao kusema—hata ikiwa walikuwa wameahidi kutokusema. (Linganisha Hesabu 30:12, 16.) Baadhi ya watenda vibaya humlaghai mtoto wakijua kwamba mtoto huyo amekosa kutii sheria fulani ya familia. “Sitakushtaki ikiwa hutanishtaki” ndio ujumbe. Kwa hiyo watoto wapaswa wajue kwamba hawataingia katika shida kamwe kwa kushtaki—hata katika hali hizo. Ni salama kusema.

Mazoezi yako yapaswa pia yamwezeshe mtoto akinze matisho. Baadhi ya watenda vibaya wameua wanyama wadogo mbele ya mtoto na kutisha kufanya vivyo hivyo kwa wazazi wa mtoto huyo. Wengine wamemwonya mtendwa vibaya wao kwamba watawatenda vibaya ndugu zake wachanga. Kwa hiyo wafunze watoto kwamba wanapaswa sikuzote kumshtaki yule aliyewatenda vibaya, hata iwe ni matisho gani aliyotoa.

Kwa habari hiyo, Biblia yaweza kuwa kifaa chenye kusaidia katika kufundisha. Kwa sababu hiyo hukazia waziwazi nguvu kuu kupita zote ya Yehova, hiyo yaweza kufanya matisho ya mtenda vibaya yasitishe sana. Watoto wanahitaji kujua kwamba hata iwe ni matisho gani yanayotolewa, Yehova aweza kusaidia watu wake. (Danieli 3:8-30) Hata wakati watu wabaya wanapowadhuru wale ambao Yehova huwapenda, yeye aweza sikuzote kurekebisha mambo baadaye na kufanya mambo yawe bora tena. (Ayubu, sura 1, 2; 42:10-17; Isaya 65:17) Wahakikishie kwamba Yehova huona kila jambo, kutia na watu wanaofanya mabaya na watu wema wanaofanya kila wawezalo ili kuwakinza.—Linganisha Waebrania 4:13.

Wenye Hadhari Kama Nyoka

Si wengi wanaovutiwa na watoto kingono wanaotumia nguvu kumtenda mtoto vibaya kingono. Kwa kawaida wao hupendelea kufanya urafiki na watoto kwanza. Hivyo, shauri la Yesu kuwa ‘hadhari kama nyoka’ lafaa. (Mathayo 10:16, NW) Uangalizi wa karibu wa wazazi wenye upendo ni mojawapo ulinzi salama ulio bora zaidi dhidi ya kutendwa vibaya. Baadhi ya watenda vibaya hutafuta mtoto aliye peke yake katika mahali pa umma na kuanzisha mazungumzo ili kuamsha udadisi wa mtoto. (“Je! unapenda pikipiki?” “Kuja uone watoto wa mbwa katika gari langu.”) Ni kweli, huwezi kuwa na watoto wako nyakati zote. Na wastadi wa utunzi wa watoto watambua kwamba watoto wahitaji uhuru fulani wa kufanya mambo yao. Lakini wazazi wenye hekima wanatahadhari juu ya kuwapa watoto uhuru mwingi sana kabla ya wakati ufaao.

Hakikisha kwamba unawafahamu vema watu wazima au vijana wowote wenye umri mkubwa wenye uhusiano na watoto wako, ukitumia hadhari zaidi unapoamua ni nani anayepaswa kuwatunza watoto wako wakati wewe haupo. Uwe macho kuona watunzi-watoto wanaofanya watoto wako wahisi isivyo kawaida au wasistarehe. Vivyo hivyo, uwe macho kuona matineja wanaoonekana kuwa wenye kupendezwa zaidi na watoto wachanga na hawana marafiki wa rika lao wenyewe. Chunguza kikamili makao na shule za kuwatunza watoto. Zuru mahali hapo pote na kuwahoji wafanyakazi, ukitazama kwa uangalifu jinsi wanavyoshughulika na watoto. Waulize kama wataona vibaya ikiwa utakuja kuona watoto wako katika nyakati wasizotazamia; ikiwa hilo haliruhusiwi, tafuta mahali pengine.—Ona Amkeni! la Desemba 8, 1988, kurasa 3-9, au Desemba 8, 1987, kurasa 3-11, (Kiingereza).

Hata hivyo, ukweli wenye kusikitisha ni kwamba, hata wazazi walio bora kabisa hawawezi kudhibiti kila jambo linalowapata watoto wao.—Mhubiri 9:11.

Ikiwa wazazi wanashirikiana pamoja, kuna jambo moja wanaloweza kudhibiti: mazingira ya nyumbani. Na kwa kuwa nyumbani ndiko kunakotokea visa vingi vya watoto kutendwa vibaya, huko ndiko tutakazia akili katika makala yetu inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

a Ona Amkeni! la Oktoba 8, 1992, kurasa 16-25 (Kiswahili), na la Julai 8, 1992, ukurasa 30 (Kiingereza).

b Bila shaka, ni lazima wazazi wawaoshe na kuwabadili mavazi watoto wadogo sana, na katika nyakati hizo wazazi huosha viungo vya faragha. Lakini wafunze watoto wako waoge wenyewe mapema; wastadi fulani wa utunzaji wa watoto hupendekeza kwamba wajifunze kuosha viungo vyao vya uzazi wakifikia umri wa miaka mitatu ikiwezekana.

c Wastadi fulani waonya kwamba ukimlazimisha mtoto wako abusu au akumbatie kila mtu anayeomba maonyesho hayo ya shauku, huenda usifanikishe mazoezi hayo. Hivyo, wazazi fulani huwafunza watoto waombe radhi kwa heshima au watumie njia nyingine wanapoombwa mambo wasiyotaka.

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

Alilia kwa Sauti Ili Apate Msaada

“KILIO cha Kijana kwa Yehova Chakomesha Mashambulizi ya Mtenda Vibaya,” kikasema kichwa kikuu cha gazeti la U.S. The Arizona Republic, mnamo Mei 5, 1993. Mtenda vibaya huyo alimtwaa kwa nguvu kijana wa miaka 13 akitumia bastola, akamchukua hadi kwenye nyumba yake. Wakati kijana huyo alipolia kwa sauti, “Yehova, nisaidie!” mtenda vibaya huyo alishtuka na akamwacha mvulana huyo aende zake. Baadaye polisi walimtia nguvuni mtu huyo.

Ingawa kwa kweli kuitia jina la Yehova kwafaa chini ya hali kama hizo, haimaanishi kwamba watumishi wa Mungu hawatashambuliwa katika hizi “siku za mwisho” zenye hatari. (2 Timotheo 3:1-5, 13) Kwa hiyo ni lazima wazazi Wakristo wawazoeze watoto wao watahadhari na watu wote wasiowajua, hata wawe ni wenye mamlaka gani.

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

Wafunze watoto watumie maneno na ishara za mwili zilizo thabiti na za waziwazi ili kukinza matongozi yasiyofaa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki