Wakati Ulimwengu Mpya Utakapokuja
ULIMWENGU mpya wa Mungu utakuja wakati ulimwengu wa sasa unapopitilia mbali. Lakini waweza kuuliza, ‘Je! twaweza kuamini kikweli kwamba ulimwengu huu utakwisha?’ Naam, ebu fikiria, je, kuna ulimwengu uliopata kwisha wakati uliopita?
Ndiyo, kulingana na uthibitisho kamili, ulimwengu mmoja ulipata kwisha. “Dunia ile ya wakati ule [siku za Noa] iligharikishwa na maji, ikaangamia,” Biblia yasema. Mungu “hakuuachilia ulimwengu wa kale, bali alimhifadhi Nuhu, mjumbe wa haki, na watu wengine saba, hapo alipoleta gharika juu ya ulimwengu wa wasiomcha Mungu.”—2 Petro 2:5; 3:6.
Ona kwamba huo ulikuwa “ulimwengu wa wasiomcha Mungu,” au mfumo mwovu wa mambo, ulioangamia. Haikuwa Dunia-Sayari, wala mbingu zenye nyota, wala familia ya kibinadamu iliyokwisha. Waokokaji wa Furiko walipoongezeka kwa idadi, ulimwengu mwingine (wetu wa sasa) ukaja kuwapo. Ni nini kitakachoupata?
Baada ya kusema kwamba ulimwengu wa Noa uliangamizwa, Biblia yaendelea kusema hivi: “Mbingu za sasa na nchi zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo.” (2 Petro 3:7) Moto waonyesha uharibifu wa ulimwengu. Kwa kweli, “dunia [hii iliyopo leo] inapita.” (1 Yohana 2:17) Lakini lini?
Mitume wa Yesu walitaka kujua, kwa hiyo waliuliza hivi: “Tuambie, mambo hayo yatakuwa lini? Nayo ni nini dalili ya kuja kwako, na ya mwisho wa dunia?” (Mathayo 24:3) Akijibu Yesu alitoa ishara ambayo ingewezesha watu waliokuwa wakiishi wakati wa utimizo wayo kujua kwamba ulimwengu mmoja ungekwisha upesi karibuni; na ulimwengu mpya ungechukua mahali pao. Ishara hiyo ilikuwa nini?
Ile Ishara
Ishara hiyo ilitia ndani sehemu nyingi, naam, matukio mengi yalitabiriwa. Ili ishara hiyo itimizwe, matukio hayo yote yalipaswa yatukie kwa njia moja ya pekee katika wakati mmoja hasa, katika kizazi kimoja. (Mathayo 24:34) Matukio hayo ni gani?
Baadhi ya matukio yaliyotajwa na Yesu yalikuwa: “Taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi; na njaa na tauni mahali mahali.” “Wakati huo watawasaliti ninyi mpate dhiki, nao watawaua; nanyi mtakuwa watu wa kuchukiwa na mataifa yote kwa ajili ya jina langu. . . . Kwa sababu ya kuongezeka maasi, upendo wa wengi utapoa.”—Luka 21:10, 11; Mathayo 24:7-9, 12.
Mtume Paulo alitaja hali nyingine ambazo zingetambulisha “siku za mwisho” za ulimwengu huu. Aliandika hivi: “Siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, . . . wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, . . . wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu, wenye mfano wa utauwa lakini wakikana nguvu zake.”—2 Timotheo 3:1-5.
Kwa kweli, umepata kuona au kusikia mambo hayo yote—mapigano ya kimataifa yakishinda vita vya zamani, matetemeko makubwa ya nchi, tauni zenye kuenea kote na upungufu wa chakula, chuki na mnyanyaso dhidi ya wafuasi wa Kristo, ongezeko la uhalifu, na nyakati zilizo ngumu zaidi ya nyingine zote. Mbali na mambo hayo, Biblia yatabiri kwamba Mungu ‘atawaharibu hao waiharibuo nchi.’ (Ufunuo 11:18) Na wanadamu wanaiharibu dunia hivi sasa!
Mwezi wa Novemba uliopita, magazeti yalikuwa na vichwa vikuu vifuatavyo: “Wanasayansi Mashuhuri Zaidi Watahadharisha Juu ya Uharibifu wa Dunia.” Dakt. Henry Kendall, aliyetunukiwa tuzo la Nobel na ambaye ni mwenyekiti wa Chama cha Wanasayansi Wenye Kuhangaika, alisema hivi: “Onyo hilo halijatiwa chumvi, wala si kilio cha bure.” Makala moja ya gazeti iliripoti hivi: “Orodha ya wanasayansi 1,575 walioandika onyo hilo ni orodha ya wanasayansi mashuhuri katika jumuiya ya kimataifa ya wanasayansi.” Onyo lao la kuharibiwa kabisa kwa dunia yetu halipasi kupuuzwa!
Hakuna shaka juu yalo. Ishara hiyo inatimizwa kwa sehemu zayo zote, kutia ndani utabiri huu mkuu wa Yesu: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja,” naam, mwisho wa ulimwengu huu. (Mathayo 24:14) Yesu alisema kwamba utakuja wakati habari njema ya Ufalme wa Mungu itakuwa imehubiriwa ulimwenguni pote. Na kuhubiri huko kunafanywa sasa na Mashahidi wa Yehova kwa kiwango hicho kilichotabiriwa!
Jambo Unalohitaji Kufanya
Kwa hiyo, uthibitisho wote waonyesha uhakika wa kwamba ulimwengu mpya wa Mungu u karibu sana. Lakini, ili uokoke mwisho wa ulimwengu huu na kufurahia maisha katika ulimwengu mpya, wahitaji kufanya jambo fulani. Baada ya kusema kwamba “dunia inapita,” Biblia yaonyesha jambo unalotakwa kufanya, ikieleza hivi: “Yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.”—1 Yohana 2:17.
Basi wahitaji kujifunza mapenzi ya Mungu na kuyafanya. Mashahidi wa Yehova watafurahia kukusaidia ujue mapenzi hayo. Kisha waweza kuokoka mwisho wa ulimwengu huu na kufurahia milele baraka za ulimwengu mpya wa Mungu.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]
Picha ya NASA
[Picha katika ukurasa wa 10]
Wakati wenye matatizo makubwa watangulia kwa ukaribu sana ulimwengu mpya