Je! Ulimwengu Huu Utaokoka?
Hakuna kizazi kingine [kama hiki] ambacho kimepata kusikia mengi yakisemwa kuhusu mwisho wa ulimwengu. Wengi wana hofu kwamba ulimwengu utakwisha katika mteketezo wa kinyukilia. Wengine wanafikiri kwamba uchafuzi huenda ukaharibu ulimwengu. Na bado wengine wana wasiwasi wa kwamba mvurugiko wa kiuchumi utafanya matungamo-matungamo ya wanadamu yakabiliane yenyewe kwa yenyewe.
Je! kweli ulimwengu huu ungeweza kwisha? Ikiwa ungekwisha, hilo lingemaanisha nini? Je! ulimwengu umepata kwisha wakati wowote uliotangulia?
Ulimwengu Waisha—Mwingine Wachukua Mahali Pao
Ndiyo, ulimwengu ulipata kwisha. Fikiria ulimwengu uliokuwa mwovu sana katika siku za Noa. Biblia hueleza: “Dunia [ulimwengu, New World Translation] ile ya wakati ule iligharikishwa na maji, ikaangamia.” Biblia pia husema: “Wala [Mungu] hakuuachilia ulimwengu wa kale, bali alimhifadhi Nuhu (Noa), mjumbe wa haki, na watu wengine saba, hapo alipoleta Gharika juu ya ulimwengu wa wasiomcha Mungu.”—2 Petro 2:5; 3:6.
Angalia kile kilichomaanishwa na mwisho wa ulimwengu huo na kile ambacho hakikumaanishwa. Haikumaanisha mwisho wa ainakibinadamu. Noa na familia yake waliokoka Furiko la tufeni pote. Pia Dunia sayari na mbingu zenye nyota na uzuri ziliokoka. Ni “ulimwengu wa wasiomcha Mungu” ndio ulioharibiwa, mfumo wa mambo ulio mwovu.
Hatimaye, wazao wa Noa walipoongezeka, ulimwengu mwingine ukatokea. Ulimwengu huo wa pili, au mfumo wa mambo, umedumu hadi siku yetu. Historia yao imejawa na vita, uhalifu, na jeuri. Ni nini kitakachoupata ulimwengu huu? Je! utaokoka?
Wakati Ujao wa Ulimwengu Huu
Baada ya kusema ulimwengu wa siku ya Noa ulipatwa na uharibifu, masimulizi ya Biblia huendelea kusema: “Mbingu za sasa na nchi zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo.” (2 Petro 3:7) Kwa kweli, kama vile mwandikaji mwingine wa Biblia anavyoeleza: “Ulimwengu [uliopo leo] unapitilia mbali.”—1 Yohana 2:17, NW.
Biblia haimaanishi kwamba dunia halisi au mbingu zenye nyota zitapitilia mbali, kama vile hizo hazikupitilia mbali katika siku ya Noa. (Zaburi 104:5) Badala yake, ulimwengu huu, pamoja na “mbingu” zao au watawala wa kiserikali chini ya uvutano wa Shetani, na “dunia” yao, au jamii ya kibinadamu, utaharibiwa kama kwa moto. (Yohana 14:30; 2 Wakorintho 4:4) Ulimwengu huu, au mfumo wa mambo, utaharibiwa kama vile hasa ulimwengu wa kabla ya Furiko ulivyoharibiwa. Hata Yesu Kristo alisema kuhusu hali iliyokuwa katika “siku za Nuhu (Noa)” kuwa mfano wa yale ambayo yatatokea kabla tu ya mwisho wa ulimwengu huu—Mathayo 24:37-39.
Kwa kutokeza, Yesu aliposema kuhusu siku za Noa, ilikuwa ni kwa kujibu swali la mitume wake: “Ni nini dalili [ishara, NW] ya kuja kwako, na ya mwisho wa dunia” [ulimwengu]? (Mathayo 24:3) Wafuasi wa Yesu walijua kwamba ulimwengu huu ungekwisha. Je! taraja hilo liliwaogopesha?
Kinyume cha hivyo, Yesu aliposimulia mambo ambayo yangetukia kabla ya mwisho wa ulimwengu, yeye aliwatia moyo washangilie ‘kwa kuwa ukombozi wao ulikuwa unakaribia.’ (Luka 21:28) Naam, kukombolewa kutoka Shetani na mfumo wake wa mambo ulio mwovu kuingia katika ulimwengu mpya wenye amani!—2 Petro 3:13.
Lakini ulimwengu huu utakwisha lini? Ni “dalili [ishara, NW]” gani ambayo Yesu alitoa ya ‘kuja kwake, na ya mwisho wa dunia’ [ulimwengu]?
Ile “Ishara”
Neno la Kigiriki linalotafsiriwa hapa “kuja” ni pa·rou·siʹa (paruusia), na humaanisha “kuwapo,” yaani, hasa mtu kuwa tayari yupo. Kwa hiyo wakati ile “ishara” ionwapo, haingemaanisha Kristo alikuwa karibu aje bali kwamba tayari alikuwa amerudi na alikuwapo. Ingemaanisha kwamba alikuwa ameanza kutawala bila kuonekana akiwa mfalme wa kimbingu na kwamba karibuni angekomesha maadui wake.—Ufunuo 12:7-12; Zaburi 110:1, 2.
Yesu hakusimulia tukio moja tu kuwa ndilo ile “ishara.” Yeye alisimulia matukio mengi na hali za ulimwengu. Yote hayo yangetukia katika wakati ambao waandikaji wa Biblia waliuita “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5; 2 Petro 3:3, 4) Fikiria baadhi ya mambo ambayo Yesu alitabiri yangetia alama ya “siku za mwisho.”
“Taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme.” (Mathayo 24:7) Vita katika nyakati za kisasa imekuwa ya kadiri kubwa kuliko wakati wowote uliotangulia. Mwanahistoria mmoja alisema: “Vita ya Ulimwengu ya Kwanza [kuanzia 1914] ilikuwa ndiyo vita ya kwanza ‘ya ujumla.’” Na bado, vita ya ulimwengu ya pili ilikuwa yenye uharibifu mkubwa zaidi ya hiyo. Na vita vyaendelea kuikumba dunia. Naam, maneno ya Yesu yamepata utimizo kwa njia ya kutazamisha!
“Kutakuwa na njaa.” (Mathayo 24:7) Kufuatia Vita ya Ulimwengu 1 kukaja labda ile iliyopata kuwa njaa kubwa zaidi ya zote katika historia yote. Njaa kuu pia ilifuata Vita ya Ulimwengu 2. Pigo la utapiamlo huathiri sehemu moja kwa tano ya watu wote duniani, ikiua watoto wapatao milioni 14 kila mwaka. Kwa kweli, kumekuwako “njaa.”!
“Kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi.” (Luka 21:11) Kwa wastani, tangu 1914 watu zaidi ya mara kumi kupita karne zilizopita wamekufa kila mwaka kutokana na matetemeko ya nchi. Fikiria machache kati yayo yaliyo makubwa: 1920, Uchina, 200,000 waliuawa; 1923, Japani, 99,300 waliuawa; 1939, Uturuki, 32,700 waliuawa; 1970, Peru, 66,800 waliuawa; na 1976, Uchina, karibu 240,000 (au, kulingana na vyanzo fulani, 800,000) waliuawa. Hakika, ni “matetemeko makubwa ya nchi”!
“Tauni mahali mahali.” (Luka 21:11) Punde tu baada ya Vita ya Ulimwengu 1, watu wapatao milioni 21 walikufa kwa homa ya Hispania. Science Digest liliripoti: “Katika historia yote kifo hakijapata kamwe kushambulia kwa uangamivu mwingi na kwa haraka zaidi kadiri hiyo.” Tangu wakati huo, ugonjwa wa moyo, kansa, UKIMWI, na mapigo mengine mengi yameua mamia ya mamilioni.
“Kuongezeka maasi.” (Mathayo 24:12) Ulimwengu wetu tangu 1914 umejulikana kuwa wenye uhalifu na jeuri. Katika sehemu nyingi hakuna yeyote anayehisi kuwa salama katika barabara za mjini hata wakati wa mchana. Usiku watu hukaa nyumbani mwao wakiwa wamefunga milango yenye vyuma, wakiogopa kwenda nje.
Mambo mengine mengi yalitabiriwa kutukia katika siku za mwisho, na hayo yote yanatimizwa. Hilo lamaanisha kwamba mwisho wa ulimwengu ni karibu. Lakini, kwa furaha, kutakuwako na waokokaji. Baada ya kusema “ulimwengu unapitilia mbali,” Biblia inaahidi kwamba: “Yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hubaki milele.”—1 Yohana 2:17, NW.
Kwa hiyo tunahitaji kujifunza mapenzi ya Mungu na kuyafanya. Ndipo tunapoweza kuokoka mwisho wa ulimwengu huu tufurahie kwa umilele baraka za ulimwengu mpya wa Mungu. Biblia inaahidi kwamba wakati huo: “Mungu . . . atafuta kila chozi katika macho [ya watu], wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:3, 4.
Isipokuwa iwe imeonyeshwa vingine, manukuu yote ya Biblia yametoka kwenye Union Version ya Kiswahili.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 6]
Sifa kwa Foto: Ndege: Foto ya USAF. Mtoto: Foto ya WHO imepigwa na W. Cutting. Tetemeko la ardhi: Y. Ishiyama, Chuo Kikuu cha Hokkaido, Japani.