Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • hp sura 15 kur. 140-150
  • Je! “Mwisho wa Ulimwengu” Ni Karibu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! “Mwisho wa Ulimwengu” Ni Karibu?
  • Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MWISHO—WA KITU GANI, NA WAKATI GANI?
  • UTIMIZO MWINGINE WA UNABII WA YESU
  • ILE “ISHARA” KATIKA WAKATI WETU
  • HAYO YANA MAANA GANI KWAKO?
  • Uharibifu wa Ulimwengu Uliotabiriwa Utakuja Lini?
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • “Mwisho wa Ulimwengu” Ni Karibu!
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Je! Inaweza Kuwa Mwisho wa Ulimwengu Ni Karibu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Siku za Mwisho
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
Pata Habari Zaidi
Furaha​—Namna ya Kuipata
hp sura 15 kur. 140-150

Sura ya 15

Je! “Mwisho wa Ulimwengu” Ni Karibu?

“JE! WEWE Uko Tayari kwa Ajili ya Mwisho wa Ulimwengu?” likauliza gazeti Star la Toronto. Ulizo hilo lingefanya watu wengine wafikirie habari kama hii:

“Sydney, Australia—Huko porini katika Australia, kikundi cha wanajiji 100 ambao wamekimbia wakayaacha makao yao na anasa za maisha ya ki-siku-hizi wanajitayarisha kwa ajili ya kile wanachokiamini kuwa ‘mwisho wa ulimwengu’ unaoelekea kuja karibuni.”

2 Lakini watu wengi leo wana wasiwasi wa kwamba “mwisho” huo ungeweza kuletwa na vita ya kutumia makombora ya nyukilia, uchafuaji wa hewa, maji na ardhi au mambo mengine yaliyo hatari kweli kweli. Kwa mfano:

“Isaac Asimov mwandikaji wa mambo ya kisayansi amehesabu njia zipatazo 20 ambazo kwazo uhai unaweza kupotea usionekane tena duniani, tangu kufa kwa jua mpaka njaa kubwa.”—Gazeti Star la Toronto.

3 Ingawa hivyo, tuna sababu nzito zaidi ya kuhangaika. Sababu hiyo inategemea Neno la Mungu lenye kuaminika. Watu wengi wamesoma katika Biblia juu ya “mwisho wa ulimwengu.” (Mathayo 13:39, 40; 24:3, Authorized Version, New American Bible) Kwa kuwa tunajua kwamba ahadi yo yote ya Mungu itatimia, inatupasa tutake kuona Biblia inasema nini juu ya mwisho huo na utakuwa na matokeo gani juu ya maisha zetu sasa na wakati ujao.

MWISHO—WA KITU GANI, NA WAKATI GANI?

4 Maandiko yanatuhakikishia kwamba Mungu ataangamiza wale wanaoendeleza maovu na taabu. (Zaburi 37:28; 145:20) Yesu Kristo na hata mtume Petro walilinganisha utekelezaji huu unaokuja wa hukumu na ule uharibifu wenye kuchagua ambao Mungu alitimiza wakati wa Noa. Dunia yenyewe haikuharibiwa. Lakini waovu waliuawa kwa gharika ya dunia nzima. Mungu alihifadhi Noa na jamaa yake; wakawa jamii ya kidunia yenye uadilifu juu ya dunia iliyosafishwa. Baada ya Petro kutaja tukio hilo, aliongozwa na Mungu atabiri kuja kwa “ile siku ya hukumu na ya kuharibiwa watu wasiomwogopa Mungu.” Ndipo zitakapoingia “mbingu mpya na dunia mpya” ambamo “uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:5-7, 13, NW; Mhubiri 1:4; Isaya 45:18.

5 Ni wazi kwamba tunataka kujua mwisho huo utakaoleta uharibifu wa taratibu (mfumo) ya mambo ya sasa utakuja wakati gani. Yesu alisema kwamba Baba tu ndiye anayeijua “siku ile na saa ile.” (Mathayo 24:36) Lakini jambo hilo halituachi tukiwa bila habari? Hapana, kwa maana kwa fadhili Mungu alitia ndani ya Neno lake habari za kujulisha waabudu wake wakati huo ukikaribia.—Linganisha Amosi 3:7.

6 Biblia inatupa sababu ya kuwa na hakika kwamba Mungu ana uwezo wa kutabiri matukio yatakayokuja. Kwa mfano, katika Danieli 9:24-27 aliandikisha unabii ukionyesha wakati Masihi, au Kristo, angefika. Luka aliyekuwa tabibu (mganga) wa karne ya kwanza anasimulia kwamba mwaka wa 29 W.K. Wayahudi walikuwa wakingoja Masihi aje kwa maana waliujua unabii wa Danieli. (Luka 3:1, 2, 15) Abba Hillel Silver, mwanachuo Myahudi, anakubaliana na hilo kwa kuandika hivi: “Masihi alitazamiwa karibu na ile robo ya pili ya karne ya kwanza W.K.” Yesu alibatizwa akawa Kristo mwaka wa 29 W.K., na ndio mwaka barabara ulioonyeshwa na unabii wa Danieli.

7 Unabii uo huo ulio katika Danieli ulitabiri kwamba baada ya Masihi kufa, ‘mji na patakatifu vingeangamizwa.’ Ndiyo, Mungu alisema mapema kwamba Yerusalemu na hekalu takatifu la mji huo vingeharibiwa, na hapo ikome taratibu (mfumo) ya mambo ya Kiyahudi iliyokuwako.—Danieli 9:26.

8 Muda mfupi kabla Yesu hajafa mwaka wa 33 W.K., yeye alitoa maelezo zaidi juu ya jambo hilo. Alisema kwamba wakati huo Mungu alikuwa akiuacha ukiwa mji wa Yerusalemu na hekalu lake. Pia, alisema anakwenda zake, arudi baadaye. (Mathayo 23:37-24:2) Lakini wanafunzi wake wakauliza:

“Tuambie, mambo haya yatakuwa wakati gani, ni rani itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa taratibu ya mambo [au, ‘mwisho wa ulimwengu’]?”—Mathayo 24:3, NW.

9 Jibu lake lingekuwa lenye maana sana kwa Wakristo wa karne ya kwanza. Kama lilivyokuwa la maana wakati huo ndivyo lilivyo la maana kwetu, kwa kuwa kama tutakavyoona, Yesu alitoa jibu lenye kueleza mambo mengi zaidi ya yale waliyouliza mitume au ambayo wangeweza kufahamu.—Yohana 16:4, 12, 13.

10 Yesu aliutaja unabii wa Danieli. (Mathayo 24:15) Unabii huo haukuwa umetaja mwaka fulani ulio wazi wa kuachwa utupu kwa Yerusalemu, basi hata Yesu asingeutaja. Lakini alieleza matukio ambayo yote pamoja yangekuwa “ishara” ya kwamba taratibu (mfumo) ya Kiyahudi ilikuwa katika siku za mwisho. Unaweza kusoma maneno yake katika Mathayo 24:4-21 na Luka 21:10-24. Alitabiri kungekuwa na Masihi (Makristo wa uongo), vita, upungufu mwingi wa chakula, matetemeko ya ardhi, magonjwa ya kipuku, kuteswa kwa Wakristo na shughuli ya kuhubiri yenye kuenea mbali. Historia inaonyesha wazi kwamba mambo hayo yalitukia muda wa kizazi kilichokuwa hai mpaka Warumi walipouharibu Yerusalemu mwaka wa 70 W.K.

MAKRISTO WA UONGO: Yosefo, mwanahistoria wa karne ya kwanza, anataja majina ya watu watatu wenye kujiita Masihi

VITA: Kulikuwako vita vya Waparthia katika magharibi ya kusini ya Asia; fujo za uasi katika Gauli na Spania; maasi ya Wayahudi katika sehemu fulani-fulani za Milki hiyo; maasi ya Washamu na Wasamaria juu ya Wayahudi

NJAA KUU: Njaa kuu zilitukia Rumi, Ugiriki na Yudea, na moja imetajwa katika Matendo 11:28

MATETEMEKO YA ARDHI: Yalitukia Krete, katika Smirna, Hierapoli, Kolosai, Kio, Mileto, Samo, Rumi na Yudea

WAKRISTO WALITESWA lakini WAKAHUBIRI MAHALI PENGI SANA: Angalia maandishi yaliyo katika Matendo 8:1, 14; 9:1, 2; 24:5; 28:22

11 Wakristo wangeweza kujiokolea uhai wao kwa sababu waliuamini unabii wa Yesu. Kristo alikuwa ameonya hivi: ‘Mtakapoona mji wa Yerusalemu umezungukwa na majeshi, kimbieni.’ (Luka 21:20-24) Kama ilivyotabiriwa, Warumi waliuzunguka mji wa Yerusalemu katika Oktoba wa mwaka wa 66 W.K. wakiongozwa na Jemadari Gallo. Wakristo wangeweza kukimbia namna gani? Bila ya kutazamiwa iwe hivyo, yale majeshi yakajiondosha. Wakristo walifuata onyo la Yesu wakaukimbia mji. Mwaka wa 70 W.K., Warumi walirudi wakiongozwa na Jemadari Tito. Waliuacha mji huo ukiwa, wakaua Wayahudi zaidi ya milioni moja. Wewe ukitembelea Rumi, utaweza kuona picha ya kumbukumbu la tukio hilo ikiwa imechongwa juu ya Tao la Tito.

12 Yaliyotukia wakati wa siku za mwisho wa taratibu (mfumo) ya Kiyahudi yanathibitisha kwamba “ishara” aliyoitoa Yesu ilikuwa yenye kuaminika kabisa. Hilo ni jambo la maana kwetu kwa sababu leo unabii wa Yesu juu ya “umalizio wa taratibu ya mambo” una maana kubwa hata zaidi.

UTIMIZO MWINGINE WA UNABII WA YESU

13 Matabiri ya Yesu juu ya Makristo wa uongo, vita, njaa kubwa na matetemeko ya ardhi, na kuteswa kwa Wakristo, yalitimizwa kabla ya mwaka wa 70 W.K. Walakini, yeye alitabiri mambo zaidi ambayo ni wazi yangetukia baadaye. Alisema kwamba “mataifa yote ya ulimwengu” yangelazimika kukubali kuwapo kwake katika utukufu wa kimbingu. (Mathayo 24:30) Pia, alitabiri kwamba watu wangetenganishwa kama “kondoo na mbuzi,” na watu wenye mfano wa kondoo wangeingia katika uzima wa milele. (Mathayo 25:32, 46) Mambo hayo hayakutukia kabla ya mwaka wa 70 W.K. wala katika mwaka huo wenyewe.

14 Miaka zaidi ya 25 baada ya anguko la Yerusalemu, Mungu alimwongoza mtume Yohana aandike katika Ufunuo matukio ya wakati ujao. Katika sura ya sita, Yohana alitangulia kuona ‘wapanda farasi’ ambao wangeleta misiba ya namna-namna duniani. Ukisoma Ufunuo 6:3-8, NW, utaona kwamba Yohana alitabiri (1) vita, (2) “upungufu wa chakula” na (3) “tauni yenye kuleta kifo.” Hayo ni baadhi ya mambo yale yale ambayo Yesu alikuwa ametabiri katika ile “ishara.” Basi tunapata uthibitisho zaidi kwamba kungekuwako utimizo wa pili au mkubwa zaidi wa matabiri ya Yesu. Juu ya jambo hilo Profesa A. T. Robertson anasema hivi:

“Kusudi letu linatimizwa tunapomfikiria Yesu kuwa alitumia uharibifu wa hekalu na mji wa Yerusalemu uliotukia katika kizazi hicho mwaka wa A.D. 70 kuwa mfano pia wa kuja kwake mwenyewe kwa pili na wa mwisho wa ulimwengu au umaliziko wa kizazi.”—Kitabu Word Pictures in the New Testament, Volume 1, ukurasa 188.

15 Wengine wanasema, ‘Lakini nyakati zote kumekuwako vita, vipindi vya njaa kubwa na magonjwa ya kipuku. Sasa basi mtu ataujuaje utimizo wa pili wa ile “ishara”?’

16 Ni wazi kwamba utimizo huo lazima uwe wenye kutokeza, uwe tofauti na vita fulani ya mahali fulani tu, usiwe ni ugonjwa wa kipuku au tetemeko la ardhi la kisehemu fulani tu. Angalia kwamba Ufunuo 6:4 unasema vita hiyo ingeondoa “amani [si katika taifa au mkoa mmoja, bali] duniani.” (HNWW) Tena, Yesu alionyesha kwamba ingekuwa ishara yenye mambo mengi. Kwa hiyo, zaidi ya kuwako vita vyenye kuenea mahali pengi, kungekuwako njaa kubwa zenye kutokeza sana, matetemeko ya ardhi makubwa na tauni kubwa sana, na mambo mengine mengi. Yote hayo yangetokea pamoja muda wa kizazi kimoja. (Mathayo 24:32-34) Kwa kufahamu hivyo, na kwa kuikumbuka historia ya kibinadamu, watu wengi wanafahamu waziwazi kwamba sasa ile ‘ishara ya umalizio wa taratibu ya mambo’ imekwisha kuonekana.

ILE “ISHARA” KATIKA WAKATI WETU

17 Ufunuo 6:4 ulionyesha kungekuwa na vita ya duniani pote. Je! imekuwako? Ndiyo, tangu vita ya miaka 1914-1918. Sydney J. Harris, mwandikaji wa habari za magazeti, anaandika kwamba ‘Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilihusu nchi zenye watu ambao jumla yao inazidi asilimia 90 ya idadi ya watu wa ulimwengu.’ Kulingana na kitabu Encyclopedia Americana, askari zaidi ya 8,000,000 waliuawa katika Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na raia zaidi ya 12,000,000 wakafa kwa kuchinjwa-chinjwa ovyo, kwa kukosa chakula au kuachwa katika hatari.

18 Watu wengine wanajaribu kupuza jambo hilo kwa kusema kwamba hapo zamani wanadamu hawakuwa na njia za usafirishaji wala tekinolojia (ufundi) ya kuweza kutokeza vita ya ulimwengu. Lakini hayo yanatia mkazo kwamba Vita ya Ulimwengu ya Kwanza haikuwa na mfano wayo.

“Wakati ulipoendelea kupita tangu siku za Agosti, 1914, imeonekana wazi zaidi na zaidi kwamba kutokea kwa ghafula kwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza kulileta mwisho wa kizazi.”—Kitabu The Norton History of Modern Europe.

“Vita ya Ulimwengu ya Kwanza—inayoitwa kwa ufupi Ile Vita Kuu na walioiokoka—inakumbukwa mpaka sasa kuwa ndilo tukio lililotenganisha kipindi cha historia ya zamani na cha historia ya kisasa. . . . Kuna ukweli fulani katika imani ambayo watu wengi wanafuata bila kujua, ya kwamba nyakati za Kisasa zilianza na Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Huo ndio wakati tulipopoteza hali yetu ya kuwa bila hatia.”—Gazette la Montreal.

“Mwaka elfu-moja-mia-tisa-kumi-na-nane haukuileta mileani, bali ulileta nusu-karne ya mahitilafiano—ghasia-ghasia, vita, mapinduzi makubwa, maangamizi, na uharibifu wa kipimo kilichokuwa hakijaonekana wala kuwaziwa hapo kwanza.”—Profesa H. S. Commager.

19 Ndiyo, ‘vita ilitokezwa kwa kipimo kisichopata kuwaziwa hapo kwanza,’ sawa na vile Biblia ilivyokuwa imeonyesha. Punde si punde ikatokea vita ya pili ya ulimwengu. Iliua kati ya watu “35,000,000 na 60,000,000.”

“Vita ya Ulimwengu ya Pili ilieneza kifo na maangamizi makubwa karibu sehemu zote za ulimwengu kwa kipimo kisichopata kuonekana hapo kwanza. . . . kujaribu kueleza bei ya mali na uhai ulioharibiwa ni kazi bure: jumla ya bei ya vitu hivyo ni kubwa sana isiweze kuhesabiwa.”—Encyclopedia Americana.

Tena unajua kwamba zaidi ya kuwako kwa vita vingi ambavyo vimetokea tangu mwaka wa 1945, sasa kuna hatari ya uwezekano wa kutokea vita ya kutumia makombora ya nyukilia.

20 Magonjwa yasiyopata kuwa na mfano hapo kwanza ni ushuhuda mwingine wa kuonyesha kwamba utimizo ulio mkubwa wa ile “ishara” ulianza na Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. (Luka 21:11) Baada ya kukubali kwamba tauni za hapo kwanza ziliua watu wengi kwa muda wa miongo (makumi) mingi ya miaka, gazeti Science Digest lilionyesha kwamba homa-mafua ya Kispania ya mwaka wa 1918 ilikuwa kubwa sana zaidi ya hapo, kwa kusema:

“Vita hiyo ilikuwa imeua watu zaidi ya milioni 21 muda wa miaka minne ya kutifua kivumbi cha vita kali kweli kweli; ile homa-mafua yenye kuenea sana iliua hesabu ya watu inayokaribia iyo hiyo kwa muda wa miezi yapata minne. Katika historia yote iliyotangulia, kifo hakikuwa kimepata watu kwa ukatili mwingi hivyo, kwa haraka nyingi kama hiyo. . . . Daktari mmoja aliuita msiba mkubwa wa kitiba upitao misiba ya nyakati zote.”

“Jumla ya waliokufa katika ulimwengu inaonyeshwa kwa ukawaida kuwa milioni 21, lakini ‘labda hesabu hiyo imekadiriwa vibaya kwa sababu inaweza kuwa ilikuwa kubwa sana zaidi ya hiyo.’ Huenda ikawa hesabu hiyo ya watu ndio waliokufa katika sehemu ndogo ya Bara Hindi tu; waliokufa huko katika Oktoba wa mwaka 1918 walikuwa ‘hawana ulinganifu katika historia ya tangu magonjwa kutokea huko kale.’ ”—Scientific American.

Isitoshe. Wanasayansi wameshindwa kukomesha kifo kiache kufagia watu kwa magonjwa. Ugonjwa mmoja ukionekana kama kwamba ‘umemalizwa kabisa,’ mwingine unajitokeza na kuua watu. Wanadamu wanapeleka maroketi kwenye mwezi, lakini wameshindwa kukomesha kabisa maleria, kansa na ugonjwa wa moyo.

21 Yesu alisema kwamba “matetemeko ya ardhi mahali hapa na hapa” yangekuwa pia sehemu ya ile “ishara.” (Mathayo 24:7, NW; Luka 21:11) Katika historia yote kumekuwako matetemeko ya ardhi. Lakini kipindi cha tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza kinaonekana kuwaje kikilinganishwa na matukio ya historia yote? Katika kitabu Il Piccolo, Geo Malagoli anatoa maoni haya:

“Kizazi chetu kinaishi katika kipindi hatari chenye kujawa na mitetemeko ya ardhi, kama hesabu zinavyoonyesha. Kwa kweli, kwa muda wa miaka 1,059 (tangu mwaka 856 mpaka 1914) vyanzo vyenye kuaminika vinataja matetemeko makubwa ya ardhi 24 tu kuwa yameua watu 1,973,000. Walakini, [katika] maafa ya hivi majuzi, tunaona kwamba watu 1,600,000 wamekufa kwa muda wa miaka 63 tu, kwa sababu ya matetemeko 43 yaliyotukia kuanzia mwaka 1915 mpaka 1978. Ongezeko hilo la kustaajabisha sana linazidi kukazia ukweli mwingine ulio wazi—kizazi chetu ni chenye balaa kwa njia nyingi.”

22 Huenda watu wakasema kwamba idadi ya watu wa ulimwengu inayozidi kuongezeka na ukubwa wa majiji ndiyo mambo ambayo yamesababisha vifo vingi zaidi kutokana na matetemeko ya ardhi tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Hata kama hiyo ndiyo sababu, bado haiyabadili mambo yaliyotukia yawe hayakutukia. Hali moja na njaa kubwa. Ijapokuwa jitihada nyingi zimefanywa chakula kiwe kingi, kama ule mpango wa kutumia Ukulima wa Nafaka Bora, bado tunasoma habari kama hizi:

“Mtu asiyepungua mmoja kati ya kila watu wanane walio duniani angali akitaabishwa na namna fulani ya ugonjwa wa kukosa chakula kinachojenga mwili.”

“Baraza ya Chakula cha Ulimwenguni ya Umoja wa Mataifa ilikutana katika Ottawa majira ya vuli iliyopita kisha wakahakikisha ni kweli kwamba watu milioni 50 wanakufa njaa kila mwaka.”

“Mashirika ya ulimwengu yanayoshughulika na chakula yanakadiri kwamba watu zaidi ya bilioni moja hawatapata chakula cha kuwatosha mwaka huu.”

23 “Kuongezeka kwa kutokutii sheria” na kupunguka kwa upendo yalipasa pia yawe mashuhuda ya kuonyesha “umalizio wa taratibu ya mambo.” (Mathayo 24:3, 12, NW) Labda si lazima wewe uelezwe hesabu za uhalifu au uharamia uliotendwa ili usadiki kwamba mambo hayo yanatimizwa leo. Lakini, kuhusu jambo hilo, soma maelezo ya kiunabii juu ya “siku za mwisho” katika 2 Timotheo 3:1-5. Angalia yanavyotaja kwa usahihi sana mambo tunayoyaona sasa.

HAYO YANA MAANA GANI KWAKO?

24 Yesu alitabiri kwamba watu wengi wangesumbuliwa sana moyoni na utimizo wa ile “ishara.” “Watu watazirai kwa sababu ya woga, wakitazamia mambo yatakayoupata ulimwengu.” Walakini, wafuasi wake hawangefanya hivyo. Kristo aliwaambia: “Wakati mambo kayo yatakapoanza kutendeka, simameni na kuinua vichwa vyenu juu, kwa maana ukombozi wenu umekaribia.” (Luka 21:26, 28, HNWW) Haitupasi kamwe kuyapuza yanayotendeka sasa, wala tusikose kuyafikiria kwa kudhani yanatokea hivi hivi tu. Wale waliokuwa Yerusalemu wakaupuza utimizo wa unabii wa Yesu katika siku zao walikufa. Yesu anatuambia sisi: “Endeleeni kuwa mmeamka . . . ili ninyi mpate kufaulu kutoroka.”—Luka 21:34-36, NW.

25 Ndiyo, inawezekana kuuokoka mwisho wa taratibu (mfumo) mbovu ya mambo ya sasa. Hakuna mwanadamu anayeijua barabara ‘siku na saa’ ya mwisho unaokuja, lakini mambo ambayo yametukia duniani muda wa maisha yetu yanathibitisha kwamba ni karibu sana. Walakini, tunatakwa tufanye mambo mengi zaidi ya ‘kuendelea kulinda’ tu. (Mathayo 24:36-42, NW) Mawazo na mwenendo wetu yanapasa yabadilike. Petro anaandika hivi: “Maisha zenu zinapasa ziwe takatifu na zilizowekwa wakf kwa Mungu, wakati ninyi mnapoingojea ile Siku ya Mungu. . . . Fanyeni yote mwezayo mwe safi na wasio na kikosa.”—2 Petro 3:11-14, Good News Bible.

26 Yesu alisema yanayofuata kuwa sehemu ya Ile “ishara”: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14, NW) Ili tushiriki fungu letu vizuri katika utendaji wetu, tunahitaji kujua “ufalme” huo ni nini na sababu gani sasa ni wa maana sana kwa kuwa mwisho ni karibu. Acha sasa tulichunguze jambo hilo.

Mambo ya Kuzungumziwa]

Sababu gani tupendezwe na habari za “mwisho wa ulimwengu”? (1-3)

Kulingana na Biblia, ni nini kitakachokwisha? (4)

Sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kwamba ule “mwisho” utakuja? (5, 6)

Yesu alitabiri nini juu ya taratibu (mfumo) ya mambo ya Kiyahudi?

Na ni mambo gani yaliyotukia? (7-10)

Lilikuwa jambo la maana namna gani kuielewa ile “ishara” wakati huo? (11, 12)

Sababu gani inatupasa tutazamie utimizo mwingine wa ile “ishara,” na utimizo huu ungekuwaje tofauti na ule wa kwanza? (13-16)

Vita vilivyotabiriwa vimetimiaje katika wakati wetu? (17-19)

Kumekuwa na utimizo gani wa magonjwa ya kipuku? (20)

Ni ushuhuda gani mwingine ambao wewe ungeweza kutumia kuonyesha kwamba ile “ishara” inaendelea kutimizwa? (21-23)

Utimizo wa sasa wa ile “ishara” unahusuje maisha yako? (24-26)

[Sanduku katika ukurasa wa 140]

“Matabiri juu ya mwisho wa ulimwengu yametolewa tangu nyakati za kale. . . . Hata hivyo, leo kuna dalili zisizobadilika za mambo ya kuogopesha yatakayotukia; ‘matatizo yenye kuletwa na watu’ yanayoelekea kutokutatuliwa hata na wanasiasa walio na busara nyingi zaidi; watu wenye maoni ya kupita kiasi katika ulimwengu wa makombora ya nyukilia na wanadamu wenyewe kujiharibia sana mazingira yasiyoweza kupatikana tena.”—“The Spectator,” Ontario, Canada.

[Sanduku katika ukurasa wa 147]

“Nyakati zote vita imekuwa neno gumu kueleza na labda Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ndiyo ngumu kuliko vita vyote. Chinichini ya yale masimulizi yaliyo wazi juu ya mashindano na miungano ya mapatano ambayo wanahistoria wanatumia ili waeleze habari za vita, kuna jambo fulani lililo kubwa zaidi, hali ya wasiwasi unaosumbua ulimwengu. . . . Ile vita hata haikuwa imekwisha wakati ulimwengu ulipoanza kujitayarishia ile nyingine iliyoifuata.”—Barry Renfrew wa Associated Press.

“Matukio yaliyoanzishwa Agosti 4, 1914 . . . yaliharibu utaratibu wa kiadili na wa kisiasa, yakaondoa usawaziko wa mamlaka kati ya mataifa, yakakomesha Ulaya isiwe tena yenye kuongoza matukio ya ulimwengu mzima, kisha yakaua watu mamilioni kadha. . . . mwaka wa 1914 ulimwengu ulipoteza utegemeano ambao umeshindwa kuupata tena tangu wakati huo.”—“The Economist,” London.

[Sanduku katika ukurasa wa 149]

VIFO KUTOKANA NA TETEMEKO

(Kadirio la miaka 1,122)

Hadi mwaka wa 1914​—1,800 kila mwaka

Tangu mwaka 1914​—25,300 kila mwaka

[Sanduku katika ukurasa wa 144]

Wakristo walifuata onyo la Yesu wakaukimbia Yerusalemu kabla haujaharibiwa na Warumi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki