Vijana Huuliza...
Kwa Nini Wazazi Wangu Huwa na Hali ya Moyo Ibadilikayo Upesi?
“NI VIGUMU sana kushughulika na mama,” asema Jeanette mchanga.a “Ikiwa amechoka, yeye hunikasirikia sana. Hakuna jambo lolote nisemalo linalokuwa sawa.”[1] Jim ana tatizo kama hilo. “Kitu kibaya kikitendeka,” yeye adai, “[wazazi] watakukasirikia bila sababu yoyote. Kwa kielelezo, gari likikataa kuanza. Baba yangu atanipigia kelele—kana kwamba ni kosa langu!”[2]
Hilo ni lalamiko kubwa sana miongoni mwa matineja: Kwamba wazazi wao wana hali ya moyo ibadilikayo upesi, wenye kasirani, na wenye itikio lisilojulikana. Siku moja, wao ni wenye furaha, ni wachangamfu, na wenye kutumaini. Siku ifuatayo, wameshuka moyo sana na kuwa wenye kuchambua kila kitu unachosema au kufanya. “Wao hunipigia makelele bila sababu yoyote,” alalamika kijana mmoja.[3]
Hata hivyo, jambo lenye kushangaza nyakati nyingine ni kwamba karibu kila mtu—kutia ndani wazazi—hupitia hali tofauti-tofauti za moyo pindi kwa pindi.[4] Ni sehemu ya kuwa binadamu. Hivyo, Biblia yasimulia watu tofauti-tofauti kuwa “wamefurahiwa moyo,” “moyo mpole,” au hata kuwa katika “moyo wa kutaka kupigana.” (Esta 1:10; Ayubu 11:19, NW; Matendo 12:20, NW) Mabadiliko fulani ya hali ya moyo huonekana kuhusika na pindi fulani za kibiolojia. Kwa kielelezo, wanawake hupatwa mara nyingi na mabadiliko ya hali ya moyo wakati wa vipindi vya hedhi. Na ni jambo la kawaida kwa watu wa jinsia zote mbili kupatwa na hali nzito ya kimwili au kihisiamoyo katika kipindi cha katikati ya alasiri na cha jioni.[5]
Mikazo na Uchovu wa Akili
Makala moja katika American Health yasema hivi: “Nyakati nyingi hali mbaya za moyo husababishwa na mambo ya kimwili. Ingawa ugonjwa na lishe isiyofaa yaweza kuwa mambo ya kwanza ya kusababisha hali hiyo, mara nyingi uchovu ndio huwa kisababishi kikuu.”[6] Hizi ni “nyakati zilizo ngumu kushughulika nazo,” na katika familia nyingi kama si familia zote, ni lazima mama na baba waajiriwe kazi. (2 Timotheo 3:1, NW) Uchovu na unyong’onyevu huwa matokeo ya kawaida. Wakiwa na mikazo ya akili isababishwayo na misongo yenye kuzidi, baadhi ya wazazi huenda wakahisi kama Ayubu mwadilifu, aliyejieleza kuwa “nimejawa na mapigo.”—Ayubu 10:15, NW; 14:1.
Wazazi wanapojishughulisha sana na magumu yao wenyewe, mawasiliano yaweza kukosa kuwapo. Alalamika Jason mchanga: “Wao wakuambia ufanye jambo fulani, na unalifanya. Lakini wadai kwamba walikuambia ufanye jambo jingine tofauti, nao wakasirika. Unakasirika, na wanakuadhibu kwa sababu unakasirika!”[7]
Nyakati nyingine mibano ya maisha huenda ikamaliza nguvu za kihisia-moyo za wazazi wanazohitaji ili kuitikia mahitaji yako. Mithali 24:10 lasema hivi: “Ukizimia siku ya taabu, nguvu zako ni chache.” Mzazi mmoja aliungama hivi: “Mara nyingi mimi humchukua Diana kutoka shuleni ninaporudi nyumbani kutoka kazini. Yeye huingia ndani ya gari na kuanza kunieleza juu ya mambo yote yaliyotendeka shuleni siku hiyo—na kuna siku ambazo huwa sina nguvu ya kusikiliza. Mimi huwa mchovu na mwenye kufikiria matukio ya siku yangu nisiwe na subira ya kumsikiliza.”[8] Waweza kuhisi umekataliwa binafsi wazazi wanapotenda hivyo, lakini mara nyingi hiyo huwa ni uchovu tu.
“Inawezekana pia kwamba,” asema mwandikaji Clayton Barbeau, “wazazi wako wana matatizo ambayo huyajui. Vijana wengi huwa hawajui ukubwa wa matatizo ya kiuchumi ya maisha ya familia. Ukifikiria makao na gharama ya chakula na hali ya wasiwasi ya kazi ya kisasa, huenda wazazi wako wanahangaikia mambo ambayo hawajakueleza lakini wanajadiliana kati yao.”[9] Au huenda wanashughulikia mambo ya siri. Baba mmoja Mkristo atumika akiwa mwangalizi katika kutaniko moja la Mashahidi wa Yehova. Binti yake asema hivi: “Nyakati nyingine anapokuwa na matatizo mengi ya kutaniko akilini mwake, yeye huwa mwenye kunung’unika sana. Ajaribu asitulaumu-laumu, lakini yeye huwa na mikazo mikubwa sana ya akili kiasi cha kwamba hawezi kushughulikia mambo mengine.”[10] Mithali 12:25 hutaja jambo hilo vizuri: “Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha.”
Huenda wazazi wako wakajitahidi sana wafiche msononeko wao kwa bidii ili usiuone. Lakini mambo ni kama vile mithali moja isemavyo: “Kwa huzuni ya moyo roho hupondeka.” (Mithali 15:13) Nyakati nyingine uchungu wao wa ndani waweza kuwashinda, na udhia kidogo tu waweza kutokeza mfyatuko wa mfadhaiko wote waliokuwa wameweka. “Nyakati nyingine baba yangu anaporudi kutoka kazini,” asema msichana mmoja tineja, “yeye huwa ni kama amekasirika kwa sababu ya jambo lililotendeka kazini. Na kama nilisahau kufanya jambo fulani, baba yangu hunikumbusha juu ya hilo. Kisha ajaribu kutafuta jambo jingine ambalo aweza kunipigia kelele juu yalo.”[11]
Sasa, bila shaka misemo michafu yapaswa kuepukwa. (Wakolosai 3:8) Wazazi wanaamriwa na Mungu wasiwachokoze watoto wao. (Waefeso 6:4) Lakini hata yule mtu mwadilifu Ayubu, alipokuwa chini ya msongo wa hali zenye kusononesha, alijikuta akisema ‘maneno ya haraka.’ (Ayubu 6:3) Kwa hiyo kabla ya kuanza kuhukumu vikali wazazi wako, jiulize hivi: ‘Mimi huitikiaje wakati nimekuwa na siku mbaya au ninapohisi msongo mkubwa sana? Je! nyakati nyingine mimi huwa mwenye hasira au mwenye kuchokozeka upesi?’ Kama ni hivyo, labda waweza kuwa mwenye kusamehe zaidi kwa wazazi wako.—Linganisha Mathayo 6:12-15.
Kijana mmoja tineja aitwaye Chad alijionea mwenyewe jinsi maisha ya baba yake yalivyokuwa na mikazo mingi ya akili.[12] “Mimi hufanya kazi pamoja na baba yangu katika kazi yake ya kupaka magari rangi na kuyarekebisha,” yeye asema, “na sasa naweza kuona kiasi cha msongo anaopata. Yeye huwa na pilikapilika siku nzima!”
Tatizo Katika Maisha ya Makamo
Katika 2 Wakorintho 7:5, mtume Paulo alikiri kwamba alikuwa amekuwa na ‘hofu ndani.’ Baadhi ya hali tofauti-tofauti za moyo za wazazi wako zaweza kusababishwa na mahangaiko ya kindani. Kitabu The Healthy Adolescent chasema hivi: “Kama vile kijana anayebalehe hupambana na matatizo ya ujana, ndivyo wazazi vilevile hupambana na matatizo ya umri. Wazazi huwa wanakaribia umri wa makamo, ambao, kama ilivyo na miaka ya utineja, ni kipindi kigumu chenye kujaa matatizo yacho.”[13]
Kwa wazazi fulani kule kutambua kwamba wanakuwa wazee zaidi hufadhaisha sana. “Nilianza kuhisi kwamba maisha yangu yalikuwa yakikwisha,” baba mmoja akasema. “Kazi yangu haikunifurahisha tena, watoto wangu walikuwa wakijitayarisha kuondoka nyumbani, nilihisi kuwa mzee sana kiumri, na sikuona jambo la kutazamia ila tu ustaafu.”[14] Ingawa wewe wafurahia kuwa katika “upeo wa maisha,” huenda wao wanavumilia matatizo ya kimwili ambayo yametokana na kuongezeka kwa umri wao. (Mhubiri 11:10) Kwa kielelezo, huenda mama yako anapatwa na mabadiliko ya hormoni ya kukoma kwa hedhi na dalili zayo zenye kuudhi—uchovu, maumivu ya mgongo, vipindi vya ghafula vya joto ya mwili, na kubadilika-badilika kwa hali ya moyo, tukitaja machache tu.b[15]
Kadiri ukaribiavyo utu mzima, ndivyo kadiri wazazi wako wapaswa kukabili ukweli wa maneno ya Biblia katika Mwanzo 2:24: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake.” Kwani, huenda ikawa kwamba tayari unachukua hatua kubwa za kuwa huru kutokana nao! Kitabu Talking With Your Teenager chasema hivi: “Jambo hilo laweza kuhuzunisha sana. . . . Huenda sisi [wazazi] tukahisi kwamba hatupendwi kama tulivyopendwa zamani . . . Mara nyingi vijana wetu huwa mbali sana nasi, hawaonyeshi hisia zao sana, wenye kujitetea sana. Tamaa yao ya kutotaka kuwa nasi, ya kujionea mengi nje ya familia, ya kufanya maamuzi au kufanya mipango bila uvutano wetu yaonyesha kwamba sisi si sehemu ya maana katika maisha yao kama tulivyokuwa zamani.”[16]
Kwa hiyo inakuwa rahisi kuona sababu inayofanya wazazi wako nyakati nyingine wawe hasa wenye hali ya moyo ibadilikayo upesi wakati masuala yahusuyo kujitegemea kwako kunakoongezeka yanapotokea. Steve mchanga asema hivi: “Wazazi wangu husahau sana. Unawaeleza unaenda nje, na baadaye wanakuuliza, ‘Unaenda wapi?’ Unasema, ‘Niliwaeleza ninaenda kucheza voliboli.’ Wao wasema, ‘Hukutueleza,’ kisha wanaanza kukupigia makelele. Hiyo hutendeka kila wakati.”[17] Lakini hali ambayo huenda ukaona kuwa ni kukasirika upesi au kunung’unika juu ya mambo madogo-madogo huenda tu ikafunua upendo wao wa ndani na hangaiko lao juu yako. Wao wajua jinsi ulimwengu ulivyo mbaya, na ingawa wao watambua uhitaji wako wa kujitegemea, nyakati nyingine wao waweza kuhofia hali njema yako. (Linganisha 2 Wakorintho 11:3.) Huenda wakaitikia mambo kupita kiasi au huenda wasiwe wenye kupatanisha mambo. Je! uwapende kwa kiasi kidogo zaidi?
Kuwaona Wazazi kwa Njia Ifaayo
Ulipokuwa mchanga zaidi, huenda ikawa ulikuwa ukiwaona wazazi wako kuwa wenye kujua mambo yote na wenye uwezo wote. Unapozidi kuwa mtu mkubwa zaidi na mwenye hekima zaidi, labda kasoro zao zaja kuonekana zaidi. Na mara kwa mara wazazi wanapokuwa wenye hali ya moyo ibadilikayo upesi au wenye kunung’unika, laweza kuwa jambo rahisi kuanza kuwadharau. Lakini Biblia yaonya dhidi ya ‘kudhihaki mzazi.’ (Mithali 30:17) Isitoshe, huenda hata ikawa kwamba si wao pekee hupatwa na hali ya moyo ibadilikayo upesi katika nyumba yenu. “Nyakati fulani mimi vilevile huwa na hali ya moyo ibadilikayo upesi,” akakiri msichana mmoja.[18] Labda wewe ni mwenye kukasirika upesi, mwenye uzito wa moyo, au asiyetaka kuwasiliana zaidi ya kadiri utambuavyo.
Hata hali iweje, badala ya kuwaona wazazi wako kwa njia ya kuchambua, jaribu kusitawisha ‘huruma’ na hisia-mwenzi kwao. (1 Petro 3:8) Kama ambavyo makala itakayofuata katika mfululizo huu itakavyoonyesha, jambo hilo laweza kukusaidia ushughulikie hali zao za moyo.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
b Kwa habari zaidi juu ya umri wa makamo na magumu yao, ona matoleo ya Amkeni! ya Februari 22, 1983, Kiingereza, na Julai 8, 1984.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Wazazi wengi huwa tu na mikazo mingi ya akili kwa sababu ya matakwa ya maisha