Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 2/8 kur. 4-6
  • Kukadiria Mahitaji ya Wazazi Wako

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kukadiria Mahitaji ya Wazazi Wako
  • Amkeni!—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wao Wataka Nini Hasa?
  • Uwe Mwepesi Kuitikia
  • Unawaonaje Wazazi Wako?
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Kuwaheshimu Wazazi Wetu Wazee-Wazee
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Kufurahisha Mioyo ya Wazazi Wako
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Ninawezaje Kuwafahamu Wazazi Wangu Vizuri Zaidi?
    Amkeni!—2009
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 2/8 kur. 4-6

Kukadiria Mahitaji ya Wazazi Wako

ILI kuwa mwenye msaada wa kweli kwa wazazi wako wanaozeeka, ni lazima ujue mahitaji yao na mapendeleo yao. Ama sivyo huenda—ukiwa na makusudi mazuri—ukatoa maandalizi na utumishi ambao wazazi wako hawahitaji na hawataki, ingawa huenda wakasita kukuambia hilo. Kisha uhusiano wako, unaotegemea kutoelewana, ungekuwa wenye mkazo usiohitajiwa si kwako tu bali pia kwa wazazi wako.

Wao Wataka Nini Hasa?

Akifikiri kwamba siku fulani itakuwa lazima kuwahamisha wazazi wake waishi naye, mwanamke fulani apanga kuwahamisha mara hiyo. Baadaye yeye agundua kwamba wazazi wake waweza kuishi vizuri katika nyumba yao wenyewe—na wangefurahi zaidi kuishi hivyo!

Baada ya kuleta wazazi wake waje kuishi naye, mwana fulani asema: “Hamtalipa fedha kuishi katika nyumba yangu! Si baada ya yote mliyonifanyia!” Hata hivyo, hilo hufanya wazazi wake wahisi kuwa wenye kutegemea mno. Hatimaye wamwambia kwamba wangependelea adhama ya kuchangia kwa njia fulani.

Familia yaandaa kila utumishi mdogo kwa wazazi wao wanaozeeka ili kuhakikisha kwamba wanastarehe na hawalemewi kwa kujikaza kimwili. Baadaye wagundua kwamba wazazi wao wataka kujifanyia mambo mengi wao wenyewe.

Katika kila moja ya vielelezo vilivyo juu, utumishi uliotolewa haukuhitajiwa na pia haukutakwa na wazazi. Hilo laweza kutukia kwa urahisi ikiwa mwana au binti mwenye makusudi mazuri asukumwa na hisi ya kuwa na daraka inayopita kiasi au ikiwa kuna ukosefu wa kuelewa juu ya mahitaji halisi ya wazazi. Fikiria juu ya mkazo usiohitajiwa ambao hilo hutokeza kwa wote wanaohusika. Bila shaka, suluhisho ni kukadiria uhitaji na matakwa halisi ya wazazi wako.

Je! kwa kweli wazazi wako wahitaji kuhamia kwenye nyumba yako wakati huu? Je! wao hata wataka kuhama? Huenda ikakushangaza kujua kwamba baadhi ya watu wazee-wazee hutamani kuishi kwa kujitegemea kadiri iwezekanavyo. Kwa kuogopa kudhaniwa kuwa wasio na shukrani, huenda wakasita kueleza watoto wao kwamba wangependelea kuishi peke yao katika nyumba yao wenyewe, kujapokuwa matatizo fulani. Huenda wakawapenda watoto wao na wakatamani kutumia wakati pamoja nao. Lakini eti wawategemee watoto wao? La, huenda wakapendelea kujifanyia mambo wao wenyewe.

Labda siku fulani itakuwa lazima kuwahamisha wazazi wako katika nyumba yako. Hata hivyo, ikiwa wakati huo haujafika bado, na ikiwa wanapendelea kwa haki kuishi kivyao, kwa nini uwakataze miaka hiyo ya kujitegemea? Je! mabadiliko fulani ya nyumbani au kupiga simu kwa ukawaida ulioratibiwa au kuzuru kungewawezesha waendelee kuishi katika nyumba yao wenyewe? Huenda wakahisi kuwa wenye furaha zaidi nyumbani mwao wenyewe, wakifanya maamuzi yao wenyewe ya kila siku.

Mmoja aliyetoa utunzi alieleza juu ya haraka yake mwenyewe katika kumhamisha mama yake kwake: “Baba yangu alipokufa, tulimhamisha mama yetu kwetu, tukimhurumia. Vile mambo yalivyokuja kuwa, yeye aliishi kwa miaka 22 zaidi. Badala ya kuuza nyumba yake, yeye angaliendelea kuishi ndani yayo. Usiwe mwenye haraka katika kuamua ni hatua zipi zipaswazo kuchukuliwa. Uamuzi huo, ukiisha kufanywa, si rahisi kubadilishwa.”—Linganisha Mathayo 6:34.[3]

‘Lakini,’ huenda ukapinga, ‘vipi ikiwa jambo fulani lingempata mmoja wa wazazi wangu huku wakiishi katika nyumba yao wenyewe? Ikiwa mama au baba angeanguka na kujiumiza, ningejihisi mwenye hatia sana!’ Hilo ni hangaiko lifaalo, hasa ikiwa nguvu au afya ya wazazi wako imezorota kiasi cha kwamba kuna hatari halisi ya kuwa na aksidenti. Hata hivyo, ikiwa hali si hiyo, jiulize mwenyewe kama hangaiko lako ni juu ya wazazi wako au juu yako, yaani, kujilinda mwenyewe usipatwe na hatia isiyofaa.[4]

Fikiria pia uwezekano wa kwamba wazazi wako wangekuwa afadhali zaidi katika nyumba yao wenyewe. Katika kitabu You and Your Aging Parents, Edith M. Stern na Dakt. Mabel Ross wasema: “Uchunguzi umeonyesha kwamba watu wazee-wazee huendelea bila kuzeeka sana na kuwa wenye shauku kikweli katika nyumba zao wenyewe kuliko kwingineko. Kwa ufupi, majaribio mengi yasiyofaa ya kufanya miaka yao ya mwisho-mwisho iwe rahisi hufanikiwa kufanya tu miaka hiyo iishe upesi zaidi.” Kwa hiyo, saidia wazazi wako waishi kwa kujitegemea kadiri iwezekanavyo, huku ukiandaa utunzi na utumishi ambao wao wahitaji kikweli.[5] Pia mara kwa mara wapaswa kukadiria tena na kufanya marekebisho kadiri mahitaji ya wazazi wako yaongezekavyo au hata kupungua.[6]

Uwe Mwepesi Kuitikia

Kwa kufikiria afya na hali za wazazi wako, huenda ikawa kwamba kuwahamisha katika nyumba yako ndio chaguo bora. Ikiwa ndivyo, uwe mwepesi kuitikia uwezekano wa kwamba huenda wakapendelea kujifanyia mambo mengi wenyewe kadiri iwezekanavyo. Kama vile watu wa umri wowote, yaelekea kwamba wanataka kutambuliwa wao wenyewe, wawe na ratiba yao wenyewe ya utendaji, na marafiki wao wenyewe. Hilo laweza kufaa. Ingawa itafurahisha kufanya mambo fulani pamoja mkiwa familia iliyopanuka, huenda ikawa vema kwako kuweka utendaji fulani kwa ajili ya familia yako ya karibu tu na kuwaruhusu wazazi wako wafanye utendaji wao wenyewe pia. Mmoja anayetoa utunzi alitaja hivi kwa hekima: “Hakikisha wazazi wako wana fanicha na picha wanazozifahamu ambazo ni za kipekee kwao.”

Katika kujaribu kutambua mahitaji halisi ya wazazi wako, zungumza nao. Sikiliza mahangaiko yao na uwe mwepesi kuitikia yale wanayoweza kuwa wanajaribu kukuambia. Waeleze yale ambayo unaweza na usiyoweza kuwafanyia ili wasiumizwe na matazamio yasiyo ya kweli. “Uwe na uelewevu wa wazi juu ya yale yatakayotazamiwa kutoka kwa wote katika familia,” akapendekeza mtoa utunzi mmoja. “Mwe na mazungumzo ya mara kwa mara ili kuepuka kukasirika na uchungu.”[9] Ukitoa ahadi za muda mrefu (“Nitawapigia simu kila Jumatatu alasiri”; “Nitawatembeza nje kila mwisho-juma”), huenda ukataka ueleweshe wazi kwamba ungependa kujaribu kufanya hivyo kwa kipindi fulani cha wakati na kuona jinsi mambo yanavyokuwa. Kwa njia hiyo, usipofanikiwa, tayari una fursa ya kukadiria tena hali yao.

Hakuna mojawapo mambo yaliyo juu yapaswayo kuchukuliwa kuwa sababu za kuwanyima wazazi wako heshima na msaada wanaohitaji. Msimamo wa Muumba juu ya jambo hilo ni dhahiri. Watoto walio watu wazima wawia wazazi wao staha, utunzi, na utegemezo. Yesu alishutumu Mafarisayo wenye kujiona kuwa wenye haki kwa kuyapinda maandiko ili kutoa udhuru wa kuwapuuza wazazi. Maneno ya wazi kwenye Mithali 30:17 yafunua karaha ambayo Mungu huhisi kuelekea wale wasiostahi wazazi wao: “Jicho la mtu amdhihakiye babaye, na kudharau kumtii mamaye; kunguru wa bondeni wataling’oa, na vifaranga vya tai watalila.”—Ona Marko 7:9-13; 1 Timotheo 5:4, 8.

Utoapo msaada unaohitajiwa kwa wazazi wako, huenda pia ukakabili mikazo mipya. Waweza kuikabilije? Makala ifuatayo itatoa madokezo fulani.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Mzazi aweza kufurahia utendaji wa kujitegemea pamoja na marafiki na pia familia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki