Kutoa Utunzi—Kukabili Mikazo ya Siku kwa Siku
IKIWA kutoa utunzi hukuletea mikazo fulani, hasa ile ambayo hukuwa umetazamia, huenda ukaelekea kuhisi mwenye hatia. Huenda ukajiuliza: ‘Je! kuna jambo lisilofaa katika uhusiano wangu na wazazi wangu? Je! watu wazima katika tamaduni nyingi hawaishi kwa furaha pamoja na wazazi wao maisha yao yote?’
Huenda hali yako ikawa tofauti. Huenda wazazi wako walihamia nyumbani mwako baada ya miaka 20, 30, 40, au zaidi ya kuishi kivyao. Hilo lamaanisha kwamba wewe na wazazi wako mlifanyiza mitindo-maisha na tabia bila kutegemeana kwa sehemu kubwa ya maisha zenu. Katika muda wa miongo kadhaa, huenda mitindo-maisha hiyo na tabia hizo zimekuwa tofauti sana. Lakini sasa, ukiwa mtoa-utunzi wakabiliwa na uhitaji wa kupatanisha maisha yako kwa upatano na wale walio chini ya utunzi wako. Hilo laweza kuwa jambo gumu sana kuliko ikiwa mlikuwa mkiishi pamoja kwa kipindi kirefu cha wakati.[1]
Pia, huenda wazazi fulani wakawa wagonjwa sana au katika njia nyinginezo wakahitaji utunzi zaidi wa kipekee. Ingawa, kwa kufaa, huenda ukawa unatoa yale yanayohitajiwa na huoni uhitaji wa sasa wa kuwaweka wazazi wako katika nyumba ya utunzi, hali hiyo kwa kueleweka huweka mikazo ya siku kwa siku kwenu nyote. Kutunza wazazi wako ni jambo la asili. Kuwa wazee na kuwa wagonjwa si jambo la asili. Muumba hakukusudia kamwe kwamba watu wapoteze nguvu zao na afya yao kwa kuzeeka. Kwa hiyo, usifikiri una kasoro fulani kwa sababu hali hiyo yahitaji mengi zaidi, kihisiamoyo na kimwili, kuliko vile ulivyokuwa umetarajia.—Mwanzo 1:26-31; Zaburi 90:10.
Mikazo inayohusiana na kutoa utunzi haionyeshi uhusiano mbaya kati yako na wazazi wako. Hasa ikiwa ulifurahia uhusiano mzuri pamoja nao kabla ya wao kuhitaji msaada wako, yaelekea kwamba magumu yoyote upatayo ni tokeo la matatizo ambayo yaweza kutokana na kutoa utunzi. Waweza kushughulikaje kwa matokeo na mikazo ya siku kwa siku?
Kushughulika na Hisia za Hatia
Hata watu wanaofanya yote wawezayo na wapaswayo kufanya kwa wazazi wao huhisi wenye hatia nyakati nyingine juu ya kutofanya mengi zaidi. Hata hivyo, hisia ya hatia isiyofaa yaweza kuwa tatizo. Waweza kujipata ukifanya maamuzi yaliyokusudiwa kuondoa hatia yako lakini hayakunufaishi ama wewe ama wazazi wako. Kwa kielelezo, ni nini kingetukia ikiwa mwanamke angejiingiza mno katika kutoa utunzi na kupuuza mume na watoto wake mwenyewe? Yeye, mume wake, na watoto wake wangepatwa na matokeo mabaya. Kwa hiyo usiache hisia ya hatia isiyofaa ithibiti maisha yako.
Je! wakati mwingine wewe huhisi mwenye hatia kwa sababu yaonekana kwamba huwezi kamwe kuwafanyia wazazi wako mambo ya kutosha? Basi, yawezekana kwamba mahitaji ya wazazi wako yapita yale uwezayo kuandaa. Hali yaweza kuwa kwamba, hata ufanye nini, sikuzote kuna mengi zaidi ambayo yangaliweza kufanywa. Isitoshe, ukiwa na maoni ya kwamba kutoa utunzi ni njia ya kuwalipa wazazi wako kwa yote waliyokufanyia ulipokuwa ukikua katika utunzi wao, sikuzote utahisi mwenye hatia, kwa sababu huwezi kuwalipa kikamili.
Kitabu You and Your Aging Parents chaonyesha uhitaji wa kuamua utawafanyia wazazi wako mambo kiasi gani. Hicho chasema: “Utajiokoa mwenyewe usichoke sana kihisiamoyo hasa ukitegemeza [maamuzi yako] si juu ya yale ungependa kufanya au hata yale upaswayo kufanya, bali juu ya yale uwezayo kufanya.”[4]
Naam, amua kihalisi yale unayoweza kutazamia kutoka kwako mwenyewe. Huenda ikasaidia ukipata msaada wa rafiki unayetumaini anayejua uwezo wako, mapungukio yako, na hali ya familia yako. Je! waweza kuhamishia wazazi wako nyumbani mwako? Je! una nafasi ya kutosha? Je! watakubali kuhamia humo? Ikiwa wazazi wako hawaishi pamoja nawe, unaweza kuwazuru mara nyingi kadiri gani, na wakati gani? Ukifanya yale uwezayo, hupaswi kuhisi mwenye hatia. Ukihisi mwenye hatia bado, ona hisia hiyo kuwa isiyofaa na usiruhusu iongoze maamuzi yako.
Gawanya Mzigo Huo
Kitabu cha Biblia cha Mhubiri chaonyesha jinsi isivyofaa kuwa “mwovu kupita kiasi” au mwenye “haki kupita kiasi” na kwamba kuwa mwenye haki kupita kiasi kwaweza kufanya ‘ujiangamize.’ (Mhubiri 7:16-18) Hilo laweza kutukia ikiwa wajaribu kufanya mengi zaidi ya yale unayotaka kufanya, unayoweza kufanya, na hata unayopaswa kufanya.
Ikiwa tayari ulikuwa na ratiba yenye mambo mengi kabla ya kuanza kutunza wazazi wako, ni lazima uondoe utendaji fulani mwingineo au upate msaada. Lakini, wengi wanaohitaji msaada husita kuuliza. Huenda wakahisi wenye haya mno au wakadai kwamba wengine hawataki kusaidia. Hata hivyo, ikiwa wajichosha, wewe hujinufaishi wala hunufaishi mtu yeyote aliye karibu nawe. Katika kitabu chake juu ya kutoa utunzi, mwandikaji-vitabu E. Jane Mall aita kazi hiyo ya kupita kiasi kuwa “dalili za mfia-kazi.” Yeye ashauri hivi: “Wapaswa kuwa na orodha ya mambo ya kutangulizwa, na matatu kati ya mambo hayo ya kutangulizwa yapaswa kuwa, kuwa na wakati pamoja na [mwenzi] wako, kuwa na wakati pamoja na watoto wako na marafiki, na kuwa na wakati kwa ajili yako mwenyewe.”[7]
Ndiyo, huenda ukahitaji kugawanya mzigo. Kwa hiyo waweza kuenda wapi upate msaada? Familia, marafiki, majirani, na wataalamu waweza kusaidia. Lakini ni lazima uombe msaada huo. Na ni lazima uuombe moja kwa moja. Madokezo hayafanyi kazi sikuzote. Huenda ukashangaa ni nani na ni watu wangapi wanaotaka kusaidia ukifanya mahitaji yako yaeleweke wazi na maombi yako yawe dhahiri. Kwa kielelezo, huenda ukamwomba mtu fulani akusafishie nyumba. Ikiwa hilo lingekuondolea mzigo, basi huo si wakati wa kusisitiza juu ya kuisafisha nyumba wewe mwenyewe eti kwa sababu ‘hakuna mwingine anayeweza kuisafisha vile itakwavyo.’
Ikiwa una ndugu au dada, wao pia washiriki daraka la kuwatunza wazazi wao. Labda umetoa utunzaji wote au sehemu kubwa yao kufikia sasa, ukiamini kwamba ndugu na dada zako hawawezi au hawataki. Hata hivyo, je, umewaomba msaada moja kwa moja? Watu fulani wataitikia ifaavyo—ikiwa inafanywa iwe wazi kwao kwamba msaada wahitajiwa.
Wengine hufanya kazi ya kutunza mzazi kuwa yao peke yao katika kujaribu kupata au kudumisha kibali cha wazazi. Au huenda wakapata hisia ya kuwa watu wenye kumcha Mungu kwa kufanya kazi yote wao wenyewe. Huenda wakalalamika kwamba wengine hawasaidii na utunzi huo, lakini pia huenda wakaonyesha dalili kwamba wanapendelea iwe hivyo. Hiyo yaweza kuwa namna ya kuwa mwenye haki kupita kiasi. Lakini kwa nini ujiletee magumu yasiyotakwa? Ikiwa msaada wapatikana, omba uupate, halafu uutumie.
Tahadhari: Usitazamie kwamba ndugu na dada zako watashiriki madaraka hayo kwa usawa pamoja nawe. Ingawa nyakati nyingine huenda ikawezekana kwao kufanya hivyo, mara nyingi hali zao wenyewe hufanya hilo liwe gumu, ama lisiwezekane. Katika visa vingi ni jambo lifaalo zaidi kwa mshiriki mmoja wa familia kuwa mtoa-utunzi wa kipekee, huku washiriki wengine wa familia, hasa ndugu na dada, wakichangia kifedha na kwa kupiga simu, kuzuru, au mara kwa mara kuwapeleka wazazi wao nyumbani au katika safari za miisho-juma.
Kuishi Karibu-Karibu
Kuishi karibu-karibu sana kwaweza kutokeza udhia mdogo-mdogo. Tabia ambazo hazingekuudhi kutoka kwa rafiki zaweza kuonekana kuwa zisizovumilika katika mshiriki wa karibu wa familia.[14]
Isitoshe, huenda wazazi wako wakasema jambo kama, ‘Natamani ungetumia wakati mwingi zaidi pamoja nami, lakini najua una shughuli nyingi zaidi usiweze kufanya hivyo.’ Maoni hayo yaweza kuficha itikadi ya mzazi kwamba kwa kweli hujali sana juu ya mzazi wako. Huenda ukaitikia maneno kama hayo kwa kukasirika. Badala ya kukasirika, je, haingefaa kutatua tatizo halisi la wazazi wako lililofichika, lile la kutumia wakati mwingi zaidi pamoja nawe? Hata ikiwa huwezi kukubali ombi hilo, kueleza mambo kwa fadhili kutatokeza matokeo bora zaidi kuliko jibu lenye kuumiza.—Mithali 12:18.
Jitihada nyingi za kusitawisha sifa zinazotiwa moyo katika Biblia zitakuwezesha kubaki ukiwa mwenye fadhili lakini mwenye uthabiti ihitajiwapo. Kitabu cha Biblia cha Wakolosai chakiri kihalisi kwamba nyakati nyingine tuna ‘sababu ya kumlaumu mwenzetu.’ Hicho hutuelekeza ‘tuchukuliane na kusameheana.’ Pia hicho hutuhimiza tujivike “moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu.” (Wakolosai 3:12-14) Kwa kweli sifa kama hizo zitasaidia sana kupunguza udhia wa kuishi karibu-karibu.
Hata iwapo hivyo, ikiwa mara kwa mara wakosea, wakosa subira, na kusema jambo ambalo hukupaswa kusema, ‘jua lisichwe na uchungu wako bado haujakutoka.’ Omba msamaha upesi, na usahau jambo hilo. Usiruhusu liwe chanzo kingine cha hisia za hatia.[15]—Waefeso 4:26, 27.
Kudumisha Faragha
Ikiwa wewe na wazazi wako waishi katika nyumba ileile, huenda mkakosa faragha. Lakini wewe na wazazi wako mwahitaji kiasi fulani cha faragha. Huenda mkazungumzia tatizo hilo pamoja nao na kufikia uelewano kwamba nyakati fulani na mahali fulani ni pa faragha kwako na kwa familia yako ya karibu. Mathalani, kwa familia fulani, lakini si zote, mlango uliofungwa wenye ishara inayosema usisumbue, waweza kueleweka na wote kuwa ukionyesha sehemu au wakati wa faragha kwa mtu aliye ndani.
Ikiwa chumba hicho hakina mlango, kisetiri chenye kuchukulika au kitu cha kugawanya chaweza kutumiwa kwa makusudi ayo hayo. Kikumbusha chenye busara chaweza kufaa ikiwa faragha ihitajiwayo inavunjwa kwa ghafula. Jambo kuu ni, uhitaji wa kila mtu wa kuwa na faragha wapaswa kustahiwa na wote katika familia.
Pendeleo
Kumbuka kwamba ingawa kuzorota kokote kwa afya ya wazazi wako hukuletea maumivu, Muumba wetu, Yehova, ataka tupate kiasi fulani cha shangwe hata tupatapo hali zenye kujaribu. Kazi hii yaweza pia kukusaidia kumkaribia Yehova zaidi ukimtegemea yeye kwa sala. Mmoja atoaye utunzi alieleza jambo hilo hivi: “Sikuzote nilikuwa karibu na Yehova, lakini kutoa utunzi kulinifunza kumtegemea yeye kabisa. Ilikuwa kama tofauti kati ya simu ya mbali sana na kuwa na mtu huyo hapo pamoja nawe. Yehova alikuwa papo hapo pamoja nami.”[17]
Kutoa utunzi ni pendeleo pamoja na kazi. Wasiliana na wazazi wako ili ujue mahitaji yao ni nini. Waandalie mahitaji hayo, na udumishe shangwe katika kufanya hivyo.—Wafilipi 4:4-7; 1 Petro 5:7.
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
Kufanya Kutoa Utunzi Kufurahishe
1. Kile ambacho wazazi wataka kutoka kwa watoto wao walio watu wazima ni uwasiliano bora. Hilo lataka kuwakaribia wazazi wako na kufunua mambo muhimu juu yako. Hilo laweza kuwa jambo gumu katika uhusiano wa mzazi na mtoto aliye mtu mzima. Mitazamo yoyote ya kuhukumu katika pande zote mbili itakuwa kizuizi. Mitazamo hiyo yahitaji kuondolewa ili kupata uhusiano wa karibu.[18]
2. Ikiwa mmoja wa wazazi wako anakuambia juu ya tatizo au hangaiko fulani, sikiliza kwa hisiamwenzi. Majibu yanayopuuza hisia zao yaweza kuongeza hisia zisizofaa kama vile: ‘Oh, mambo si mabaya sana hivyo’ au, ‘Najua, mambo ayo hayo hunipata mimi.’ Utakuwa mwenye matokeo zaidi ukijaribu kutambua hisia za wazazi wako zilizofichika, halafu ukubali na kushiriki hili (‘Yaonekana una wakati mgumu sasa hivi, lakini tutaukabili pamoja’).—Mithali 20:5.
3. Ikiwa wewe ni mwenzi wa yule anayetoa utunzi hasa, uwe mwenye kutegemeza kimwili na kihisiamoyo. Wasiliana na mwenzi wako; ama sivyo hali ya kutoelewana itatokea.[21] Utegemevu wa mwenzi hufanyiza tofauti kubwa. Mwanamke mmoja aliomboleza kwamba kukosa utegemezo kutoka kwa familia yake kulikuwa “kugumu zaidi kushughulikia kuliko kutunza mama [yake].” Kwa upande mwingine, yeye alithamini sana msaada wa rafiki mmoja aliyemsaidia pindi kwa pindi. Yeye alisema hivi: “Ilinigusa moyo alipotoa msaada. Hilo lilikuwa jambo la kunijali sana, na lilinivuta karibu zaidi naye.”[22]
[Sanduku katika ukurasa wa 10]
Ikiwa Unapokea Msaada
Huenda ikawa kwamba wewe ndiye unayetunzwa. Unaweza kufanya nini ili kusaidia kudumisha uhusiano uliosawazika na wenye amani na watoto wako?
Wazazi fulani hufanya kosa la kujaribu kudhibiti mambo kwa kusumbua-sumbua, kuhoji-hoji, au kuonyesha hatia. Yaelekea wajua kwamba hilo hutokeza uthibiti mdogo zaidi na mkazo mwingi zaidi. Matokeo ni bora zaidi unapojaribu kuwaonyesha watoto wako walio watu wazima kwamba unawastahi wao, faragha yao, na maoni yao, hata wakati usipokubali. Kuwapongeza watoto wako mara kwa mara ni kwenye matokeo. Mtoto mmoja aliye mtu mzima alisema: “Mtoto ataka kibali cha wazazi wake hata awe ana umri gani.”[23]
Katika hali hiyo ya upendo na staha, wasiliana na watoto wako juu ya mahitaji yako. Madokezo na mambo yasiyo wazi mara nyingi huleta madhara mengi kuliko mazuri, kwa hiyo sema kwa njia ya moja kwa moja, lakini kwa fadhili.[24] Hata ikiwa wewe na watoto wako hamkubaliani juu ya jambo fulani, busara yako itachangia kuwa na uhusiano wa karibu ulio wa haki usio na kutoelewana.
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Katika kutunza wazazi wako, pia uwe na wakati pamoja na mwenzi wako, watoto wako, na wewe mwenyewe