Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 2/22 kur. 25-27
  • Kwa Nini Ni Lazima Tuhame?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Ni Lazima Tuhame?
  • Amkeni!—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Familia Zenye Kuhama
  • Hisi Zenye Kuchanganyikana
  • Sababu Inayofanya Kuhama Kutokeze Mkazo
  • Kukabiliana na Hali ya Kuhama
  • Naweza Kujipatanishaje na Kuhama Kwetu?
    Amkeni!—1994
  • “Toka Katika Bara Lako na Kutoka kwa Watu wa Ukoo Wako”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Kwa Nini Rafiki Yangu Bora Zaidi Alihama?
    Amkeni!—1996
  • Je, Niko Tayari Kuondoka Nyumbani?
    Amkeni!—2010
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 2/22 kur. 25-27

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Ni Lazima Tuhame?

Unatoka shuleni ukiwa na mipango mingi ya mwisho-juma—kuwa ufuoni siku nzima, kucheza mpira, kutumia jioni yenye ukimya kusoma mambo fulani. Lakini mama anaporudi kutoka kazini, uso wake waonyesha kwamba kuna jambo baya. ‘Leo kampuni iliniambia nichague kati ya kuhamishwa nifanye kazi mahali pengine ama kufukuzwa kazini,’ mama asema. ‘Inaonekana kwamba ni lazima tuhame.’ Kwa ghafula unahisi kuvunjika moyo sana.

KAMA familia yenu inataka kuhama, basi si nyinyi peke yenu. Katika nchi fulani zilizoendelea, kuhamahama kumekuwa maisha ya kawaida kwa familia nyingi. Kwa kielelezo, katika United States, Idara ya Kuhesabu Watu yakadiria kwamba Mwamerika wa kawaida atahamahama mara 12 katika maisha yake.[1] Kwani, kila mwaka milioni 12 ya vijana wa Amerika hupatwa na mikazo ya kuhama![2] Hata hivyo, huenda tarakimu kama hizo zisikutie moyo kama ni familia yenu inahama. Huenda ukashindwa kabisa na tazamio hilo la kuhama. ‘Kwa nini ni lazima tuhame?’ huenda ukauliza kwa uchungu.

Familia Zenye Kuhama

Mara nyingi familia haina la kufanya ila kuhama tu. Katika nyakati za Biblia familia ya Elimeleki na Naomi ililazimishwa kuhamia bara la ujirani la Moabu wakati njaa kali ilipokumba Israeli. (Ruthu 1:1, 2) Wazazi wengi leo hujipata katika hali kama hizo. Katika nchi zinazoendelea, ukame na kupuuzwa kwa mazingira kumelazimisha mamilioni ya watu wahamie majiji yenye watu wengi na vituo vya kutoa usaidizi—ama kuhamia nchi nyinginezo.[3] Katika nchi za Magharibi, mshuko wa mambo ya kiuchumi umefanya viwanda vingi na biashara nyingi kufungwa. Mashamba ambayo hapo awali yalikuwa yenye ufanisi sasa hayaleti faida. Kazi zimekuwa chache. Kwa hiyo huenda wazazi wako wasiwe na la kufanya ila tu kuhamia eneo lenye utajiri zaidi.[4]

Hata hivyo, si familia zote huhama ili kutoroka umaskini. Kupandishwa cheo kazini, kuhamishwa kwa mahali ambapo mzazi anafanya kazi, mvunjiko wa ndoa, afya mbaya, hali ya anga isiyo nzuri—zote ni sababu za kawaida ambazo hufanya baadhi ya familia zihame.[5] Msosholojia John D. Kasarda ataja sababu nyingine kubwa: “Kuna maoni ya kwamba majiji ni hatari zaidi siku hizi. Hasa dawa za kulevya zimesababisha ongezeko kubwa la uhalifu kwa watu mmoja-mmoja na mali.”[6] Wengine wanahisi kwamba ni salama zaidi kuishi katika viunga vya jiji au katika mji mdogo.

Katika nyakati za Biblia, Abrahamu alihama kutoka makao yake yenye ustarehe katika Uru ili kutumikia mapendezi ya Mungu. (Mwanzo 12:1; Waebrania 11:8) Ndivyo ilivyo leo, familia fulani miongoni mwa Mashahidi wa Yehova wamehamia maeneo ambayo yana uhitaji wa wahubiri wengi zaidi wa ujumbe wa Ufalme. (Mathayo 24:14) Wengine wameanza kuhudhuria kutaniko la ujirani ambalo lina uhitaji zaidi wa waangalizi au watumishi wa huduma. Ingawa kuhama kwa njia hiyo huenda kusiwe kuhamisha makao, kunamaanisha kujaribu kujipatanisha na watu wapya na hali mpya.

Hata sababu za kuhama kwa familia yenu ziwe gani, labda haikuhama kwa mapendekezo yako. Na inaeleweka kwamba huenda usifurahi sana juu ya jambo hilo.

Hisi Zenye Kuchanganyikana

Si kwamba kuhama kwote ni kubaya. Justin mwenye umri wa miaka 12 huudhika akumbukapo makao yao ya zamani katika jiji kubwa. “Yalikuwa mabaya sana,” yeye asema.[7] “Kulikuwa na jeuri nyingi katika ujirani wetu. Hungeweza kwenda meta 50 kutoka nyumbani bila kuhofu magenge ya wakora. Watu walikuwa wakijifungia ndani ya nyumba zao. Nilichukia sana hali hiyo. Nilipojua kwamba tulikuwa tunahamia mashambani, nilifurahi sana.”

Lakini, wazo la kuacha marafiki wako na hali unazozijua vizuri huenda zikafanya uwe na wasiwasi. Anita mchanga alikuwa na hisia kama hizo alipojua kwamba familia yao ilikuwa ikihama. “Nilikuwa nimeishi kwa muda mrefu zaidi wa maisha yangu katika kituo cha kijeshi cha U. S. nchini Uingereza,” yeye akumbuka. “Nilijiona mwenyewe kuwa Mwingereza kuliko kuwa Mwamerika. Nilipokuwa na umri wa miaka kumi, nilipata kujua kwamba baba yangu alikuwa akihamishwa kikazi kurudi United States, New Mexico—lile jangwa! Kwanza nilishindwa jambo la kuwaza. Nilikuwa na msisimko lakini mwenye hofu kidogo. Sikutaka kuacha marafiki wangu. Hilo lilikuwa ndilo jambo gumu zaidi kwa habari ya kuhama.”[8]

Sababu Inayofanya Kuhama Kutokeze Mkazo

Siku hizi, inaonekana kama vijana hasa wanapatwa na mikazo ya kuhama. Gazeti Reader’s Digest lasema hivi: “Wastadi wa akili watuambia kwamba hata kuhama kuzuri ni tukio lenye kufadhaisha, na lenye kuleta mikazo mingi ya kihisia.”[9]

Sababu moja ni kwamba ule msisimko na tazamio la kuhama zenyewe ni hali za kutokeza mkazo. Maahirisho na mambo yanayozuia kuhama yasiyoepukika yaweza kuongeza mikazo. Biblia yasema hivi: “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua.” (Mithali 13:12) Hata kama kila mtu anakutazamia kwa hamu, “kuhama kwaweza kutokeza huzuni nyingi na wasiwasi mwingi katika washiriki wa familia,” lasema gazeti Parents. “Hilo hutukia kwa sababu kule kuagana huamsha hisia za upotezo na wasiwasi juu ya kuhama.”[11] Kwa hiyo ni jambo la kawaida kupatwa na hisia hizo—mshtuko, hasira, mfadhaiko, na kushuka moyo vilevile.[12]

Kitabu The Teenager’s Survival Guide to Moving chasema hivi: “Kuhama kunamaanisha zaidi ya kuhamisha tu makao. Kwamaanisha kubadili mambo mengi ya maisha yako—shule yako, walimu wako, utendaji wako, marafiki wako. Na badiliko huwa gumu nyakati zote, hata kama ni badiliko zuri.”[13] Mfanyakazi wa kijamii Myra Herbert adai kwamba kuhamahama sana kwaweza kutokeza “hali za kushindwa na huzuni.” Kwanza, watoto wanaohamahama “hubadilibadili programu za shule nyakati zote na hasa ikiwa wanapata ugumu wa kusoma, wao huacha masomo kabla ya kumaliza.” Kuacha marafiki, yeye asema, “ni jambo gumu hasa” kwa vijana.[14]

Kukabiliana na Hali ya Kuhama

Basi ni rahisi kuona sababu inayofanya tarajio la kuhama likufanye uwe na wasiwasi, ukose furaha na hata kukasirika. Lakini kufikiria sana juu ya hisia zisizofaa kutafanya tu mambo yawe magumu zaidi. Ni afadhali zaidi ikiwa unajaribu kusitawisha maoni yafaayo. Hisia zisizofaa, kama vile wasiwasi, au huzuni, ni mambo ya kawaida sana chini ya hali hizo. Mara nyingi hisia hizo huisha baada ya muda fulani. Wakati uo huo, jaribu kukazia akili mafaa ya kuhama kwenu.

Anita, aliyetajwa hapo awali, sasa ana umri wa miaka 15 na wamehama tena tangu wakati ule. “Tulipohama, nilihuzunika,” yeye akumbuka. “Lakini nilifikiria mambo yafaayo—kwamba ningekutana na watu wapya na kwenda sehemu zenye kupendeza.” Yeye ni mwenye furaha na amejipatanisha vizuri na kao lao jipya.[15]

Nyakati nyingine hata ukijitahidi kadiri gani, wewe bado huhisi hisia zisizofaa. Ikiwa hivyo, basi usizipuuze. Kwani, “roho iliyopondeka” yaweza kukudhuru kimwili. (Mithali 17:22) Labda wahitaji kutoa uangalifu zaidi kwa uhitaji wako wa kupumzika, kufanya mazoezi, au lishe ifaayo. Unahitaji vilevile kusema juu ya hisia zako, hasa na wazazi wako. (Mithali 23:26) Uwajulishe hofu zako na mahangaiko yako.[16]

Kwa kielelezo, je, unaugua kwa sababu utalazimika kuacha baadhi ya vitu vyako uvipendavyo sana kwa sababu ‘hakuna nafasi ya kutosha’? Au unahisi kwamba pindi hiyo ya kuhama ni karibu sana na wakati wa mitihani ya shule na kwamba una mkazo mwingi mno? Hata lalamiko lako liwe gani, Mithali 13:10 yatukumbusha hivi: “Kiburi huleta mashindano tu, bali hekima hukaa nao wanaoshauriana.” Wazazi wako wanaweza kukubali kufanya mambo fulani. Kama sivyo, angalau wanaweza kukuhurumia, kukutegemeza, na kukufariji.

Usiruhusu porojo na maneno yenye kuogofya juu ya kao lenu jipya yadhoofishe jitihada zako za kudumisha mtazamo ufaao. Mithali 14:15 yasema hivi: “Mjinga huamini kila neno, bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.” Tafuta mambo ya hakika wewe mwenyewe. Anita asema hivi: “Nilienda kwenye maktaba na kufanya utafiti juu ya historia na tamaduni ya sehemu tulizohamia.”[17] Labda waweza kuzuru kao lenu jipya kimbele kama hamhami mbali. Kufanya hivyo kwaweza kukusaidia sana kuondolea mbali shaka zako na kukutayarisha kiakili kuhama.

Ni kweli kwamba si rahisi kuondoka. “Kabla uhame,” chadokeza kitabu The Teenager’s Survival Guide to Moving, “zuru mara ya mwisho sehemu uzipendazo zaidi. . . , na kuziaga.”[18] Huenda ukataka kutengeneza kitabu cha picha au kitabu kitupu chenye kubandikwa picha ili uwe ukikumbuka sehemu hizo.[19] Jambo la maana zaidi, chukua wakati wa kuaga marafiki wako. Uwahakikishie kwamba uhusiano wako nao haujakwisha. Mtume Yohana alitumia “karatasi na wino” katika kuwasiliana na wale aliowapenda, na wewe vilevile unaweza kufanya hivyo! (2 Yohana 12) Ukiazimia na kutia jitihada, hata urafiki wa mbali waweza kusitawi.

Hatimaye machozi yako ya kuagana yatakauka, na utakabili ugumu wa kujipatanisha na kao lenu jipya—ambao utakuwa habari itakayozungumzwa katika toleo letu linalokuja.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mbona usifanye utafiti mapema na kujifunza juu ya kao lenu jipya?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki