Vijana Huuliza. . .
Naweza Kujipatanishaje na Kuhama Kwetu?
JE! FAMILIA yenu imehama hivi majuzi? Basi labda wewe wakubali kwamba ni matukio machache maishani yaliyo ya kutaabisha—au ya kuleta mikazo kama hilo.[1] Na baada ya virago kuondolewa katika sanduku la mwisho na fanicha ya mwisho kuwekwa ifaapo, huenda bado ukahisi umeshuka moyo, mwenye huzuni, au mwenye wasiwasi. Si kitu kama makao yenu mapya ni bora au ya hali ya chini kuliko yale ya kwanza. Bado unasikitika uliacha nyumba yenu ya zamani, shule yako ya zamani, na hasa marafiki zako wa zamani.
Bila shaka, ni kawaida mtu kuhisi akitamani makao yake ya kwanza. Lakini Biblia hushauri hivi: “Usiseme, Kwani siku za kale kupita siku hizi? Maana si kwa hekima uulizavyo neno hilo.” (Mhubiri 7:10) Hekima hukusaidia uone mambo kihalisi. Kwa kweli, ‘siku za zamani’ katika makao yenu ya kwanza hazikuwa kamilifu kwa kweli—hata labda hazikukaribia kuwa hivyo. Badala ya kuharibu maisha yako, kuhama huenda kukakupa fursa na faida mpya. Hata hivyo, kujipatanisha na hali za kuhama si rahisi. Basi, ni nini kiwezacho kukusaidia kufanya hivyo?
Jistareheshe
Mna kweli nyingi katika maneno ya wimbo mmoja wa zamani uliosema: “Popote pale niwezapo kujipumzisha ndiyo makao ya starehe yangu.”[1a] Ndiyo, badala ya kujisumbua juu ya mahali ambapo umeacha nyuma, kwa nini usijitahidi kufanya mahali penu papya pawe kwenu? Kichapo The Teenager’s Survival Guide to Moving chadokeza hivi: “Mara tu ukiisha kuhamia mahali, jaribu kufanya chumba chako kipya kistareheshe na chenye hali ulizozoea.”[2] Kwa kielelezo, ungeweza kupamba chumba chako kwa vitu na picha ulizozoea. Ikiwa wewe hushirikiana chumba kimoja na ndugu yako, jaribu kuufanya uwe mradi wa pamoja.
Katika nyakati za Biblia mtunga-zaburi aliwatia moyo watu wa Mungu wafahamu jiji lao kuu, akisema: “Tembeeni katika Sayuni, uzungukeni mji, ihesabuni minara yake . . . yafikirini [yakagueni, NW] majumba yake.” (Zaburi 48:12, 13) Vivyo hivyo, pata kuujua ujirani wako. Pata kujua mahali duka zilipo, shule yako mpya, maktaba ya hapo, na mahali penginepo. Hiyo itakusaidia uhisi umestareheka zaidi.[3]
Bila shaka ulikuwa umepanga kaida fulani, au njia ya kufanya mambo, katika makao yenu ya zamani. Kwa kadiri urudiavyo kawaida hiyo ya zamani upesi zaidi, ndivyo utakavyostareheka upesi zaidi.[3a] Hasa wapaswa ‘kuenenda katika lilo hilo’ kuhusu mambo ya kiroho kama mikutano ya Kikristo na funzo la Biblia.—Wafilipi 3:16.
Siku za Shule
Kujipatanisha na hali za shule mpya ni jambo gumu lenyewe, hasa ikiwa umehama katikati ya mwaka wa shule. Katika mabara fulani taratibu ya masomo ya shule hupangwa kulingana na hali za mahali, na huenda ikatofautiana sana na masomo uliyokuwa nayo katika shule yenu ya zamani. Huenda ukajikuta ukiwa nyuma sana ya wanafunzi wa shule yenu mpya; huenda hata ukalazimika kurudishwa darasa la chini zaidi.[4]
Ingawa huenda wakati huo likaonekana kuwa jambo la kukuvunjia heshima, usivunjike moyo; kubaki nyuma kimasomo ni hasara ya ziada ambayo hutokea kwa kawaida kutokana na kuhama. Isitoshe, ingawa huenda shule zilizo katika eneo lenu zikawa zina taratibu ya masomo ya kiwango kisichobadilika, ule mkazo wa kuhama na kujipatanisha na watu tofauti, hali, na desturi tofauti, na pia ule msongo wa kujaribu kukumbuka majina mapya mengi—yote hayo yaweza kujumlika kuchosha nguvu zako za kuweka fikira mahali pamoja.[4a] Suluhisho ni nini? Jaribu kujipa wakati wa ziada kwa ajili ya masomo yako ya kufanyia nyumbani, na uache kutazama televisheni sana. Baada ya muda yaelekea utafanya maendeleo katika masomo yako.
Kufanya Marafiki Wapya
“Kufanya marafiki wapya kulikuwa kwa kweli ndio ufunguo [wa kujipatanisha na hali],” asema kijana jina lake Brian ambaye familia yao ilihamia sehemu ya kusini ya United States. “Baada ya mimi kupata marafiki kadhaa wa umri wangu ambao mapendezi yetu mengi yalifanana, mambo yalilainika. Jambo moja tu la makao yetu ya zamani ambalo nasikitika kutokuwa nalo ni kucheza mpira wa magongo wa barafuni.”[5] Akiwa ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, kwa hekima Brian alitafuta marafiki miongoni mwa vijana wenye kuhofu Mungu wanaohudhuria Jumba la Ufalme la kwao. Ikiwa wewe nawe wataka marafiki walio na viwango vya juu vya kiadili na ambao kwa kweli hukujali wewe kama mtu, mahali bora zaidi pa kuwatafuta ni Jumba la Ufalme la kwenu.—Mithali 13:20.
Bila shaka, hutapata kamwe marafiki kwa kukaa ukinuna au kujitenga peke yako. (Linganisha Mithali 18:1.) “Nilivyopata marafiki wapya,” asema Anita, “ilikuwa ni kwa kutimiza sehemu yangu na kujijulisha. Pia nimeona kwamba kwa kuwa na mtazamo ufaao—kutabasamu tu na kuonekana mwenye furaha—watu watakuja na kujijulisha kwako.” Ndiyo, watu watavutwa kwako ukiwatolea upendezi—tabasamu ya kirafiki na mwelekeo wa uchangamfu! Na uwe mwenye subira. Urafiki huchukua muda kusitawika.
Ingawa hivyo, nyakati fulani waweza kupata mwanzo mzuri wa kusitawisha urafiki kwa kuzuru yale yatazamiwayo kuwa makao yenu mapya kabla ya kuhama. Laura mwenye umri wa miaka 13 asema hivi: “Niliudhika kweli kweli mara ya kwanza nilipojua kwamba tungelazimika kuhama karibuni. Lakini nimeweza kutumia wakati nikipata kuwajua baadhi ya watoto wa mahali tunakokwenda na hiyo imenisaidia nihisi nafuu zaidi kuhusu kuhama.”[7]
Urafiki Ufaao Dhidi ya Usiofaa
Je! wewe wasema ni ushirika mchache wa kufaa upatikanao miongoni mwa vijana katika mji wenu mpya? Basi ‘kunjuka’ katika urafiki wako. (2 Wakorintho 6:11-13) Ingawaje, baadhi ya urafiki ulio mchangamfu zaidi ulioandikwa katika Biblia ulikuwa kati ya watu waliotofautiana sana umri—kama vile Daudi na Yonathani, na Paulo na Timotheo. (1 Samweli 18:1; 1 Wakorintho 4:17) Kwa hiyo mbona ufanye urafiki na marika wako tu? Katika kutaniko la Kikristo mna watu wa umri mkubwa zaidi ambao wewe ungeweza kufurahia ushirika wao kweli kweli.
Ni kweli, huenda watu wa jinsi hiyo wasiweze kukimbia sana bila kujikokota unapocheza nao mchezo wa mpira. Wala huenda wasielekee kupendezwa sana kusikiliza muziki uupendao sana. Na bado, huenda wakawa washirika wenye kujenga sana. Kwa kuwa njia bora zaidi ya kupata rafiki ni kuwa mmoja wewe mwenyewe, ungeweza kuanza kwa kujitolea kumsaidia jambo fulani mmoja wa hao wenye umri mkubwa zaidi. Au kwa nini usiwaulize tu kama ingekuwa sawa kuwapitia dakika chache? Huenda urafiki wa kuridhisha ukasitawi.
Kwa upande mwingine, ukijikalia peke yako tu chumbani na kujisikitikia, ungeweza kuwa mpweke kwa urahisi na kushuka moyo. Hiyo ingeweza kufanya watu wa aina isiyofaa wajitolee kuwa marafiki zako. Kwa kielelezo, magenge ya matineja ni tatizo zito katika maeneo mengi. Wao huwaahidi vijana wapweke kuwapa ushirika na hisia ya kukubaliwa. Lakini kama ilivyokuwa katika nyakati za Biblia, vijana wa jinsi hiyo huenda pia wakajaribu kukuhusisha katika kutenda makosa, wakisema: “Haya! . . . Tumwotee asiye na hatia, bila sababu [kwa kujifurahisha tu, NW].” Lakini Mfalme Sulemani mwenye hekima alionya hivi: “Mwanangu, usiende njiani pamoja nao; uzuie mguu wako usiende katika mapito yao. Maana miguu yao huenda mbio maovuni.”—Mithali 1:10-16.a[8]
Kaza Fikira Juu ya Wengine
Njia moja hakika ya kuacha kufikiria upweke wako ni kutafuta njia za kuwatia wengine moyo—hasa washiriki wa familia yenu wenyewe. “Kuhama si mboga hata kwa wazazi,” lakumbusha gazeti Current Health, “nao huthamini msaada wote wawezao kupata.”[9] Huenda ikawa mama au baba pia anaendelea kujipatanisha na hali za kazi mpya. Huenda ile nyumba mpya ikawa haifai sana au isiyo ya kupendeza kama ile ya zamani. Na ikiwa wewe una akina ndugu na dada, labda hata wao wanapatwa na upweke na kuvunjika moyo. Mbona usitafute njia ya kuwasaidia? Uliza wazazi wako kama kuna vikazi vya ziada ambavyo ungeweza kufanya. Ikiwa ndugu zako waonekana wapweke, jitolee kukaa kidogo pamoja nao. Kumbuka “upendo hujenga” wenye kuupokea na wenye kuuonyesha pia.—1 Wakorintho 8:1.
Basi, kwa kumalizia, kama utapendezwa au hutapendezwa na makao yenu mapya itakutegemea sana wewe. Twakumbushwa hadithi ya mwanamume mmoja mzee mwenye hekima aliyefikiwa na magari mawili yaliyojaa wageni. “Sisi twafikiria kuhamia hapa,” ikasema familia katika gari la kwanza. “Watu wa huku wakoje?” Yule mwanamume mzee naye akauliza: “Watu wa kule mtokako wakoje?” Ile familia ikajibu: “Sisi twatoka mji wenye urafiki sana. Watu ni wakarimu na wafadhili nao hujali sana wageni.” Huyo mwanamume mzee akatabasamu. “Mimi nafikiri mngependezwa na mahali hapa,” akasema. “Watu hapa ndivyo walivyo haswa.”
Yule mwanamume mzee akauliza familia katika gari la pili swali hilohilo. Wakajibu: “Sisi twatoka mji mdogo wa wachoyo. Watu huko ni wavivu na vimbelembele sana, tena vidomodomo wee.” Yule mwanamume mzee akakunja uso. “Mimi sidhani mngefurahi kuwa hapa,” akasema. “Watu hapa ndivyo walivyo haswa.”[10]
Ni nini maana ya hadithi? Watu kila mahali ni kama wanafanana. Na kama wewe wafurahi au waudharau ushirika wao yategemea sana mitazamo yako mwenyewe, hali za kuhisi mambo, na njia za kushughulika na wengine. Kwa hiyo endeleza mtazamo ufaao! Amua ya kwamba utajitahidi kufaidika kwa kadiri uwezavyo kutokana na kuhama kwako. Hapana, huenda mambo yasiwe yaleyale kamwe. Lakini kwa jitihada na subira, wewe waweza kufanya mambo yawe mazuri zaidi ya hapo kwanza. Mradi wewe upo pamoja na wale wakupendao kweli kweli, mahali popote paweza kuwa nyumbani kikweli.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Vijana Huuliza . . . Je! Nijiunge na Genge?” iliyotokea katika toleo la Novemba 8, 1992 la Amkeni!
[Picha katika ukurasa wa 13]
Chukua hatua ya kwanza kufanya marafiki wapya