Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g96 12/22 kur. 13-15
  • Kwa Nini Rafiki Yangu Bora Zaidi Alihama?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Rafiki Yangu Bora Zaidi Alihama?
  • Amkeni!—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kukabili Uhalisi
  • Wasiliana
  • Kuziba Pengo
  • Dumisha Mtazamo Unaofaa
  • Kwa Nini Siwezi Kudumisha Marafiki?
    Amkeni!—1996
  • Unaweza Kuwa Rafiki ya Yehova
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
  • Marafiki Wangu wa Kweli ni Nani?
    Amkeni!—2011
  • Biblia Inasema Nini Kuhusu Urafiki?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1996
g96 12/22 kur. 13-15

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Rafiki Yangu Bora Zaidi Alihama?

‘WAONEKANA kama umepoteza rafiki yako bora zaidi.’ Watu watasema hivi mtu fulani aonekanapo ana huzuni kidogo au kushuka moyo. Lakini kama kweli umepoteza rafiki yako bora zaidi, usemi huo unakuwa na maana zaidi.

Kwani, urafiki wa kweli ni kitu cha kipekee na cha thamani. Biblia husema: “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.” (Mithali 17:17) Marafiki wa kweli hutuandalia uandamani na utegemezo. Wao hutusaidia kukua kihisia-moyo na kiroho. Ingawa marafiki wa kawaida au watu unaojuana nao waweza kuwa wengi, watu mmoja mmoja ambao unaweza kuwatumaini kabisa na kuwa na usiri nao kwa kawaida ni wachache.

Hivyo ikiwa rafiki yako bora zaidi amehama, inaeleweka kwamba waweza kusikia vibaya sana. Kijana fulani aitwaye Bryan alikumbuka jinsi alivyohisi rafiki yake bora zaidi alipohama. “Niliogopa, nikawa mpweke, na kuumia,” alisema. Labda wahisi hivyo.

Kukabili Uhalisi

Kufikiria sababu iliyofanya rafiki yako ahame kwaweza kusaidia. Kwa hakika, haikuwa kwa sababu ya kukosa kuthamini urafiki wenu. Kuhama kumekuwa sehemu ya kudumu ya maisha ya kisasa. Kila mwaka katika Marekani pekee, zaidi ya watu milioni 36 huhama! Kulingana na Ofisi ya Idadi ya Watu ya Marekani, Mmarekani wa kawaida atahama mara 12 katika maisha yake.

Kwa nini kuhama kote huku? Sababu hutofautiana. Familia nyingi huhama ili kupata kazi nzuri zaidi na makao mazuri zaidi. Katika nchi zinazoendelea, vita na umaskini umewalazimisha mamilioni ya familia kuhama. Na vijana wakuapo watu wazima wachanga, wengi huamua kuhama na kujitegemea wenyewe. Wengine huhama ili kufunga ndoa. (Mwanzo 2:24) Na wengine waweza kuhama ili kufuatia mapendezi ya kiroho. (Mathayo 19:29) Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, wengi huacha mazingira waliyoyazoea ili kutumikia katika maeneo—labda hata katika nchi za kigeni—ambapo kuna uhitaji mkubwa zaidi wa wahudumu wa Kikristo. Wengine huhama katika nchi zao ili kutumikia katika Betheli, kama ambavyo ofisi zinazosimamia kazi za Mashahidi wa Yehova zinavyoitwa. Ndiyo, ingawa twawapenda marafiki wetu, twapaswa kuona ukweli huu wa maisha kwamba kadiri wakati upitavyo, yaelekea watahama.

Hata sababu iwe ni nini iliyomfanya rafiki yako ahame, waweza kujiuliza jinsi utakavyokabili hali ya kuhama kwake. Lakini ingawa ni jambo la asili kuhisi mpweke kidogo na kushuka moyo kwa muda fulani, labda waweza kutambua kwamba kujitenga na kujikalia bila furaha hakutaboresha mambo hata kidogo. (Mithali 18:1) Hivyo basi acha tuchunguze mambo fulani ambayo yaweza kusaidia.

Wasiliana

“Tambua kwamba urafiki wenu haujakoma,” alishauri kijana Bryan. Ndiyo, kwa hakika kuhama kwa rafiki yako kutabadili uhusiano wenu, lakini hiyo haimaanishi kwamba uhusiano wenu wapaswa kukoma. Mshauri wa matineja Dakt. Rosemarie White alisema: “Ni vigumu kukabili upotezo katika hali yoyote ya maisha, lakini njia ya kuishughulikia kwa mafanikio ni kuuchukulia kama badiliko na si kama mwisho wa jambo.”

Waweza kufanya nini kuuendeleza urafiki? Fikiria habari ya Biblia ya Daudi na Yonathani. Ingawa walitofautiana sana kwa umri, wao walikuwa marafiki wa karibu zaidi. Wakati hali ilipomlazimisha Daudi kukimbilia uhamishoni, hawakuachana bila ya kusema neno. Kinyume cha hivyo, waliuthibitisha urafiki wao usiokoma, hata kufanya agano, au mapatano ya kudumisha urafiki wao.—1 Samweli 20:42.

Vivyo hivyo, waweza kuongea na rafiki yako kabla hajaondoka. Mweleze rafiki yako jinsi unavyothamini urafiki huo na jinsi unavyotaka kuendeleza mawasiliano. Patty na Melina, ambao walikuwa marafiki sana na ambao sasa wametenganishwa na maili 5,000 za bara na bahari walifanya hivyo hasa. “Sisi hupanga kuwasiliana,” alieleza Patty. Hata hivyo, mipango kama hiyo yaweza kutetereka, isipokuwa mwafanya mipango fulani dhahiri.—Linganisha Amosi 3:3.

Biblia yatuambia kwamba mtume Yohana aliposhindwa kumwona rafiki yake Gayo, aliwasiliana kwa ‘kumwandikia kwa wino na kalamu.’ (3 Yohana 13) Nanyi pia mwaweza kukubaliana kutumiana barua au kadi kwa ukawaida, labda mara moja kwa juma au kwa mwezi. Na ikiwa wazazi wako hawakatazi simu za mbali kwa sababu ya gharama, labda mwaweza kupigiana simu pindi kwa pindi na kuarifiana mambo ya karibuni katika maisha yenu. Au mwaweza kukubaliana kutumiana ujumbe ambao umerekodiwa katika kaseti au kanda ya vidio. Baadaye, yawezekana hata kupanga ziara ya mwisho-juma au likizo pamoja. Hivyo urafiki huo waweza kuendelea kusitawi.

Kuziba Pengo

Hata hivyo, kuondoka kwa rafiki mpendwa kutaacha pengo katika maisha yako. Tokeo laweza kuwa kwamba una wakati mwingi. Usiuruhusu wakati huo kupotea bure. (Waefeso 5:16) Uutumie kufanya jambo fulani lenye manufaa—labda waweza kujifunza kupiga ala fulani ya muziki, kujifunza lugha mpya, au kufuatia upendezi fulani ili kupitisha wakati. Kutumwa na wengine wenye uhitaji ni namna nyingine ya kufaa ya kutumia wakati. Ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, waweza kuongeza wakati wako katika kazi ya kuhubiri peupe. (Mathayo 24:14) Au waweza kuanzisha mradi wa funzo la Biblia la kupendeza.

Zaidi, mtume Paulo aliwashauri Wakristo katika Korintho ‘kukunjuka’—yaani, kuwahusisha wengine kuwa marafiki wao. (2 Wakorintho 6:13) Labda umetumia wakati mwingi sana na rafiki mmoja tu hivi kwamba umesahau wengine wawezao kuwa marafiki. Vijana miongoni mwa Mashahidi wa Yehova wapata kwamba mara nyingi nafasi za kuanzisha urafiki zipo nyingi pale pale katika makutaniko yao. Hivyo jaribu kufika katika mikutano ya kutaniko mapema na ukae kidogo baadaye. Hili litakupa wakati zaidi kuwajua watu. Makusanyiko ya Kikristo na vikusanyiko vidogo vya kirafiki huandaa nafasi za kufanya urafiki.

Hata hivyo, ni vizuri kutahadhari: Usiwe mwenye haraka wa kufanya urafiki na vijana ambao unaanza kushirikiana nao kwa ukaribu sana na ambao hushiriki miradi ya kiroho na maadili nao. Vijana kama hao waweza kukushawishi vibaya na waweza kukufanyia mabaya zaidi kuliko mema. (Mithali 13:20; 1 Wakorintho 15:33) Shirikiana tu na vijana wenye akili ya kiroho ambao wana sifa za mwenendo mwema.

Upatapo mtu kama huyo, sitawisha urafiki kwa kupanga kufanya kitu fulani pamoja. Shirikini mlo. Tembeleeni jumba la kuhifadhi vitu vya kale. Tembeeni pamoja. Pangeni kutumia siku katika huduma ya Kikristo pamoja, mkiwazuru watu mkiwa na habari njema za Ufalme wa Mungu. Kwa kupita kwa wakati na jitihada, urafiki mpya waweza kukua. Kwa sababu upendo wa Kikristo ni wenye kuenea—huo ‘hukunjuka’ kuwatia ndani wengine—ufanyapo marafiki wapya, hupaswi kuhisi umekosa uaminifu-mshikamanifu kwa rafiki yako aliyehama.

Pia waweza kutumia wakati kuwa karibu na wale wakupendao zaidi—wazazi wako. Wao waweza kuwa msaada mkubwa, hata hivyo kwanza waweza kuona kuwa jambo gumu kutafuta uandamani wao. Kijana aitwaye Josh alisema: “Nilijilazimisha kutumia wakati pamoja nao, kwani wakati huo sikuwa na uhusiano wa karibu na mama au baba. Lakini sasa wao ni marafiki wangu bora zaidi!”

Kumbuka pia kwamba bado una rafiki mbinguni. Kama Dan mwenye umri wa miaka 13 asemavyo, “kwa kweli huko peke yako kwa sababu bado una Yehova.” Kupitia sala Baba yetu wa kimbingu anapatikana kwetu wakati wowote. Atakusaidia ukabiliane na hali hii ngumu ikiwa wamtumaini.—Zaburi 55:22.

Dumisha Mtazamo Unaofaa

Mfalme Sulemani mwenye hekima alitoa shauri hili: “Usiseme: Kwani siku za kale kupita siku hizi?” (Mhubiri 7:10) Yaani, usiendelee kufikiria yaliyopita; jinufaishe na wakati uliopo pamoja na nafasi zao zote. Bill, ambaye sasa yumo katika miaka ya mapema ya 20, alifanya hivyo hasa alipopoteza rafiki yake bora zaidi. Alikumbuka: “Baada ya muda mfupi nilianza kufanya urafiki na sikuendelea kufikiria sana yaliyopita. Nilijitahidi kujitayarisha kwa ajili ya wakati ujao na kuishi wakati uliopo.”

Madokezo hayo yaweza kusaidia, lakini bado ni huzuni rafiki yako bora zaidi ahamapo. Muda waweza kupita kabla ya kumbukumbu za nyakati nzuri mlizokuwa nazo pamoja hazijaacha kuumiza. Kumbuka kwamba badiliko ni sehemu ya maisha na kwamba hukuandalia nafasi ya kukomaa na kukua. Ingawa yaweza kuonekana kama haiwezekani kuziba kikamili nafasi ya rafiki wa pekee, waweza kukuza sifa ambazo zitakufanya upate “kibali kwa BWANA, na kwa watu pia.” (1 Samweli 2:26) Ufanyapo hivyo, wakati wote utakuwa na mtu fulani wa kumwita rafiki yako!

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kuaga rafiki yako bora zaidi ni ono lenye maumivu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki