Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 3/22 kur. 16-18
  • Naweza Kuepukaje Kuchezea Ukosefu wa Adili?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Naweza Kuepukaje Kuchezea Ukosefu wa Adili?
  • Amkeni!—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Kufuliza Kujihadhari”
  • Kuweka Mipaka
  • ‘Kama Wanipenda, Ungekubali Tufanye’
  • Wakati Ambapo Umesisimuka Kupita Kiasi
  • Ni Wakati Gani Ambapo Mtu Anakuwa Amepita Mipaka?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Ukosefu wa Adili—Kuna Madhara Gani?
    Amkeni!—1994
  • Jinsi ya Kuwa na Uchumba Wenye Mafanikio
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • “Kupita Kiasi” Kwafikia Wapi?
    Amkeni!—1993
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 3/22 kur. 16-18

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kuepukaje Kuchezea Ukosefu wa Adili?

“Mimi nilikuwa nikiona ni sawa kupigana pambaja za kubusiana na kupapasana, kwamba ilikuwa tu njia ya kuonyesha shauku zangu za ndani na upendo. Nilifikiri ningeweza kuacha kabla ya kufanya jambo lolote zito kama uasherati. Lakini nilikosea sana.” Ndivyo alivyoandika msichana mmoja aitwaye Valerie aliyetumbukia katika ukosefu wa adili.a

VIJANA Wakristo wajua kwamba Biblia hulaumu vikali ngono kabla ya ndoa. (1 Wakorintho 6:9, 10) Hata hivyo, huenda wengine wasing’amue kwamba Biblia hulaumu vikali pia kuchezea ukosefu wa adili—kujitia katika shauku za kindani ambazo ni wazi zimewekwa akiba kwa wenzi waliofunga ndoa peke yao. (Wagalatia 5:19)b Je! hiyo yamaanisha kwamba ni kosa kuonyesha shauku? Sivyo hata kidogo.

Biblia husimulia hadithi ya msichana Mshulami na mvulana mchungaji waliokuwa wamechumbiana. Mafahamiano yao ya kirafiki yalikuwa safi na ya adili kabisa. Hata hivyo, kwa wazi walionyeshana shauku fulani-fulani kabla ya kufunga ndoa. (Wimbo Ulio Bora 1:2; 2:6; 8:5) Leo, wenzi fulani wenye kufanya mafahamiano ya kirafiki huenda vilevile wakaona kwamba kushikana mikono na kukumbatiana, ni maonyesho yafaayo ya upenzi ndoa ionekanapo kuwa yakaribia sana.c

Ni rahisi sana hata kwa wenzi wawili wenye makusudio ya kuheshimika kusisimuka kupita kiasi na kuanza kuchezea ukosefu wa adili. Wao waweza kuepukaje kufanya hivyo?

“Kufuliza Kujihadhari”

Kwenye Zaburi 119:9, mtunga-zaburi aliuliza: “Jinsi gani kijana aisafishe njia yake?” Jibu? “Kwa kutii [kufuliza kujihadhari, NW], akilifuata neno lako.” Njia moja ya kufuliza kujihadhari ni kuchunga ni akina nani walio rafiki zako. “Sikuzote rafiki zangu wananisonga tufanye kitu chenyewe,” asema mvulana Mwamerika mmoja aitwaye Nakia. Biblia huonya hivi: “Rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) Gazeti moja la habari za vijana lilitoa ushauri mwema liliposema: “Jitahidi kutafuta rafiki wapya wenye kanuni kama zako.”Njia nyingine ya kufuliza kujihadhari ni kuepuka hali za kufanya uache msimamo wako. Fikiria lililotendeka wakati mpenzi mchungaji wa yule msichana Mshulami alipomwalika katika matembezi ya kimahaba. Makusudio yake yalikuwa safi vya kutosha; alichotaka tu ni kufurahia mazuri ya masika pamoja naye. Hata hivyo, kaka za huyo msichana Mshulami ‘walimkasirikia.’ Si kwamba hawakuwatumaini wenzi wawili hao. Lakini walijua vema vishawishi ambavyo vingeweza kutokea kama wangeruhusiwa kuwa peke yao katika mazingira ya kimahaba. Utatuzi? Wale kaka walivunja mipango ya kimahaba ya wenzi hao na kumpa dada yao kazi ya kumshughulisha.—Wimbo Ulio Bora 1:6; 2:8-15.

Kuwa peke yako katika mazingira ya kimahaba huendelea kutokeza hatari leo. Akumbuka hivi tineja mmoja tutakayemwita Mary: “Tulipoenda sehemu za kufanya mafahamiano, kwa kawaida tulikuwa na msindikizaji.” Ingawa hivyo, wakati mmoja walijikuta katika chumba wakiwa peke yao. “Tulisisimuka kupita kiasi. Ni upumbavu wetu tu ulioruhusu hilo litendeke. Tulikuwa na mtazamo wa kwamba ‘Hilo halitatupata sisi.’ Sasa najua lazima uwe na msindikizaji wakati wote, vyovyote vile. Fanya mipango mingine ikiwa huwezi kupata mtu yeyote wa kwenda nawe. Sisi tuliacha kinga yetu ikalegea.”

Usilegeze kinga yako! Ikiwa unafanya mafahamiano ya kirafiki na mtu fulani, panga sehemu zenu za mafahamiano kwa uangalifu. Ikiwezekana, nendeni sehemu hizo za mafahamiano mkiwa vikundi, au ukazie kuwa na msindikizaji. Epuka mazingira hatari, kama kuwa peke yenu katika gari lililoegeshwa au katika chumba fulani. Kwa kawaida, kufurahia ushirika katika ziara za majumba ya hifadhi, mikahawa, na kadhalika ni salama zaidi. Kwa namna moja, ungeweza pia kukumbuka maneno ya Hosea 4:11: “Divai na divai mpya huondoa fahamu za wanadamu.” Kwa kuwa kileo huelekea kupunguza kinga za mtu, yafaa kuwa mwangalifu sana kuhusu kukitumia hata ikiwa kulingana na sheria umetimiza umri wa kunywa.

Kuweka Mipaka

Mithali 13:10 hutoa ushauri mwingine wa maana isemapo hivi: “Hekima hukaa nao wanaoshauriana.” Usingoje mpaka uingie katika mazingira ya kimahaba yenye lindi la msisimuko wa hisiamoyo ndipo uanze kujiwekea kanuni za kufuata. Wenzi wawili wanaofanya mafahamiano ya kirafiki ni wenye hekima kuweka mipaka kimbele, kuzungumza wazi ni shauku gani zifaazo waonyeshane. Hata hivyo, ni lazima wote wawili wafuate ile kanuni kwenye Waefeso 4:25: “Mkaseme kweli kila mtu na jirani yake.”

Kwa kielelezo, tuseme kwamba msichana ahisi kwamba uhusiano wake na kijana mwanamume umefikia hatua ya kupigana busu la kwa-heri ya usiku. Hata hivyo, yule kijana mwanamume aona kwamba kwa sababu ya hali yake ya hisiamoyo, busu lingekuwa kishawishi cha kupita kiasi. Kwa kuhofu kukataliwa au labda kuhisi ana wajibu wa kupendeza huyo msichana, huenda huyo kijana mwanamume akatenda dhidi ya uamuzi wake bora. Lakini hata liwe ni jambo la kumtia haya kama nini, ahitaji kusema kweli na kueleza hisia zake za kweli katika jambo hilo. Kwa kuwa upendo wa Kikristo “hautafuti mambo yake,” kila mmoja apaswa kustahi hisia za mwenzake—na dhamiri yake—katika jambo hilo. (1 Wakorintho 13:5; 1 Petro 3:16) Ni kweli, kuongea juu ya habari hiyo yenye kuamsha hisia kwa urahisi kwaweza kuwa jambo gumu na la kuonea haya, hasa katika zile hatua za mapema za mafahamiano ya kirafiki. Lakini kufanya hivyo kwaweza kusaidia sana kuzuia matatizo mazito yasisitawi baadaye. Jambo la kupendeza ni kwamba, uwezo wenu wa kuwasiliana na kusikilizana katika mambo hayo huenda pia ukaonyesha uhusiano wenu unaweza kadiri gani kutokeza ndoa thabiti.

‘Kama Wanipenda, Ungekubali Tufanye’

Ingawa hivyo, nyakati fulani hali huanza kupamba moto mno hata makusudi yawe ni mazuri kadiri gani. Huo sasa ndio wakati upaswapo kusema kijasiri! Funga breki kwa fadhili lakini kwa imara. Nenda zako ikiwa lazima. (Linganisha Mithali 23:2.) Namna gani ikiwa mtu unayeenda naye sehemu za mafahamiano akataa kustahi mipaka ya kiasi na aendelea kukusonga uruke mipaka? Kwa kuhuzunisha, vijana fulani wamenaswa na madokezo yenye maana ya wazi kama vile, ‘Kama wanipenda, ungekubali tufanye’ au, ‘Kila mtu hufanya’ au hata, ‘Si karibuni tu tutaoana, sasa shida iko wapi?’ Kama katika nyakati za Biblia, kuna wale ambao hujaribu kutongoza ‘kwa ubembelezi wa midomo yao.’ (Mithali 7:21; linganisha Zaburi 5:9.) Usijiachilie ushindwe na vitisho vya maneno!

Kwanza, mtu akupendaye kwelikweli hatakusonga kamwe ufanye jambo lichafualo dhamiri yako ya Kikristo au likufanyalo uhisi ukikosa starehe. (1 Wakorintho 13:5) Pili, si kweli hata kidogo kwamba ‘kila mtu anafanya.’ Na hata kama kila mtu angekuwa akifanya, hiyo haingemaanisha kamwe kwamba wewe wapaswa kufanya. Kumbuka kanuni iliyo kwenye Kutoka 23:2: “Usiandamane na mkutano kutenda uovu.”

Kwa habari ya ahadi za kufunga ndoa, hakuna popote ambapo Maandiko huwapa wenzi waliochumbiana ruhusa ya kujiendesha kama watu waliofunga ndoa. Zaidi ya hilo, angalia takwimu za kuhuzunisha zilizoripotiwa katika kitabu The Compleat Courtship, cha Nancy Van Pelt: “Zaidi ya asilimia 33 ya wasichana wenye ujuzi wa ngono walikuwa wakiamini kwamba mara ya kwanza walipofanya ngono wangefunga ndoa na yule jamaa lakini ni wachache kati yao waliofanya hivyo. Hata hivyo, kati ya jamaa walio watendaji wa ngono walioombwa maoni ni asilimia 7 tu waliowaza kwamba wangeoa yule msichana. Moja la mambo mawili lilikuwa likitendeka—ama yule msichana alikuwa akijidanganya ama yule jamaa hakuwa akisema kweli. Uamuzi ni wako.” Mithali yenye hekima husema: “Mjinga huamini kila neno; bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.”—Mithali 14:15.

Wakati Ambapo Umesisimuka Kupita Kiasi

Kijana Mjerumani aitwaye Thomas aungama hivi: “Mimi nilikuwa na rafiki-msichana wa daima, nasi tulikaribia kufanya makubwa. Lakini yaonekana sikuzote tuliacha kabla ya kuvuka mipaka. Hiyo ikanipa hisia ya kwamba ningeweza kujidhibiti.” Kujipumbaza hivyo kulimwongoza afanye ukosefu wa adili katika ngono. Kumbuka onyo hili la Biblia: “Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.”—1 Wakorintho 10:12.

Namna gani ikiwa wenzi wawili watumbukia hasa ndani ya mwenendo usiofaa? Kijana mwanamume aitwaye John asema hivi: “Mimi na mchumba wangu tulipoanza mafahamiano ya kirafiki pale mwanzoni, mwenendo wetu ulikuwa safi na ulikaa katika kiwango cha juu. Lakini safari moja tulianza kubusiana na kupigana pambaja za kupapasana—karibu kufikia kufanya uasherati. Hapo ndipo nilipoamua kusema na mmoja wa wazee katika kutaniko langu.” Ndiyo, wakati wenzi wawili waruhusupo mambo yafike hapo, wote wawili wahitaji msaada! Usijidanganye kufikiri kwamba mwaweza kutatua tatizo peke yenu. “Nilikuwa nikisali hivi, ‘Tusaidie tusirudie,’” aungama kijana mmoja. “Nyakati fulani hiyo ilisaidia, lakini mara chache haikusaidia.” Hivyo Biblia hutoa ushauri mwema isemapo hivi: ‘Waite wazee wa kutaniko.’ (Yakobo 5:14, NW) Waangalizi hao wa Kikristo waweza kutoa shauri, mawaidha, au karipio lolote lililo la lazima kufanya uhusiano wenu—na, la maana zaidi, uhusiano wenu na Mungu—urudie njia ifaayo.

Ingawa hivyo, ni vizuri zaidi kuweka kinga zifaazo, kuweka mipaka mapema, na kupiga moyo konde kubaki safi machoni pa Mungu. Kwa njia hiyo mwaweza kuepuka msiba.

[Maelezo ya Chini]

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

b Ona makala “Vijana Huuliza . . ‘Kupita Kiasi’ Kwafikia Wapi?” katika toleo la Oktoba 22, 1993.

c Katika sehemu fulani za ulimwengu, maonyesho ya shauku kati ya watu wasiofunga ndoa huonwa kuwa ya kuchukiza na ya kuudhi. Wakristo hujiangalia wasijiendeshe kwa njia yoyote ambayo ingeweza kukwaza wengine.—2 Wakorintho 6:3.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Wenzi wenye hekima watakataa maonyesho yasiyofaa ya shauku

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki