Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 3/22 kur. 19-22
  • Kutoka Kuwa Hipi Mwomba-Lifti Hadi Kuwa Mishonari wa Amerika Kusini

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutoka Kuwa Hipi Mwomba-Lifti Hadi Kuwa Mishonari wa Amerika Kusini
  • Amkeni!—1994
  • Habari Zinazolingana
  • Pigano Langu Gumu na Lililo Refu la Kutafuta Dini ya Kweli
    Amkeni!—1995
  • Sababu kwa Nini Watu wa Namna Zote Wanakuwa Mashahidi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Je! Ilifaa Nijitahidi Kushinda Watu Wote?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Kumkaribia Mungu Kulinisaidia Niwezane na Hali
    Amkeni!—1993
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 3/22 kur. 19-22

Kutoka Kuwa Hipi Mwomba-Lifti Hadi Kuwa Mishonari wa Amerika Kusini

NILIKUWA nikiomba lifti (kubebwa na gari) nipelekwe Birmingham, Uingereza, nikiwa na msichana-rafiki yangu Mfaransa katika 1974. Mashahidi wa Yehova wawili walitupita kwa gari lao wakitoka kazini, na wakati mmoja wao, John Hyatt, alipogeuka kututazama, alimwambia mwenzake hivi kwa sauti kubwa ya mshangao, “Sasa watu wa jinsi ile watakujaje kuijua kweli juu ya Mungu?” Bila shaka, sikujua hilo mpaka baadaye. Hata hivyo, hawakusimama watubebe; hata wewe usingalisimama. Sura yangu ilikuwa ya hipi asilia (jamaa asiyechunga nywele wala mavazi).

Lakini acha nianzie mwanzo. Mimi nilizaliwa Richmond, Virginia, U.S.A., katika 1948. Jambo la kwanza kabisa nikumbukalo ni wakati nilipokuwa na miaka mitano bila kuweza kutembea. Nilikuwa na ugonjwa wa kupooza. Mama yangu aliniosha nikiwa juu ya machela katika hamamu (bafu). Kwa tukio zuri, baada ya majuma manne au matano, kwa msaada wa wazazi wangu na madaktari, nilipona. Niliweza kutembea tena.

Familia yetu ilikuwa ya namna ya asili ya Kusini hasa—ya kujikalia na mambo yetu wenyewe, Wabaptisti wa Kusini. Wazazi wetu walitaka kwamba sisi watoto—ndugu wawili, dada yangu, na mimi—tuhudhurie kanisa mpaka tuwe na miaka 18. Tukiwa na miaka 18 tuliacha kanisa. Mimi nilikuwa nimebatizwa nilipokuwa na miaka saba, kwenye krusedi fulani ya Billy Graham. Nilichukua ubatizo wangu kwa uzito; haukufanywa kwa msisimko mwingi wa hisiamoyo. Nakumbuka wazi kwamba niliweka maisha yangu wakfu kwa Mungu, ingawa kwa kweli sikujua yeye ni nani.

Wazazi wetu walitufundisha maadili mazuri, staha kwa mamlaka, na staha kwa Biblia. Mawazo hayo ya mapema yaliongoza maamuzi ambayo ningefanya muda wote uliobaki wa maisha yangu. Hadi leo hiihii, mimi hushukuru kwa mazoezi hayo ya wazazi.

Katika darasa la sita, nakumbuka nikiifikiria hali ya ulimwengu na kuwaza hivi: ‘Haiwezi kuendelea hivi.’ Hata wakati huo, mimi sikufikiri kwamba mifumo ya kisiasa ingeweza kuendelea.

Katika miaka yangu ya utineja, nilianza kupatwa na ugonjwa wa kujikunja uti wa mgongo, kasoro ambayo yawezekana kuwa ililetwa na ule ugonjwa wa kupooza uliotangulia. Nikawa kitu tu cha kufanyiwa uchunguzi na majaribio mbalimbali ya kitiba huku kiwiliwili changu kikiwa ndani ya kitegemeza-mwili cha ubuni wa Risser, cha kufunika mwili kama vile mifupa ya gofu la mnyama ifunikwavyo na ngozi yake ya juu.

Sikujichagulia kuwa na sura hiyo. Nilionekana kama sanamu-binadamu. Watoto wale wengine shuleni walikuwa wenye fadhili, lakini somo nililojifunza nilipokuwa nikivaa lile fuko la kutegemeza mwili katika shule ya sekondari ni hili: Kubali hali yoyote tusiyoweza kuibadili.

Nilitarajiwa kuhudhuria chuo, basi nilienda. Nilikuwa katika darasa lile lililohitimu 1970. Katika miaka ya ’60 ile harakati ya mahipi ilikuwa imechacha kwelikweli, na ukosefu wa adili na dawa za kulevya yalikuwa mambo ya kawaida ya siku hizo. Nilipokuwa chuoni nilikula jasho langu mwenyewe, na kazi yangu ofisini ilitaka niwe na nywele fupi na kuvaa suti. Lakini ile roho ya kujitegemea na ya kutokukubali kwa rafiki zangu kufuata mitindo ya watu wale wengine ilinivutia. Wao walichukizwa sana na mfumo sawasawa na mimi. Nilivaa suruali za dangarizi chini ya vazi langu la kuhitimu.

Elimu haikuwa imeridhisha. Kwa kumtazama ami yangu tajiri nilikuwa nimesadiki kwamba fedha hazikuwa utatuzi. Yeye hakuwazidi maskini kwa furaha. Faida gani basi? Kwa hiyo niling’oka, nikaacha nywele zangu zikue, nikaingilia kutafuta kusudi la kweli maishani.

Nilisafiri katika Ulaya kwa tiketi ya gari-moshi na kwa kuinulia magari kidole-gumba. Lengo langu lilikuwa kuomba-lifti nifike kotekote ulimwenguni. Labda ningepata matatuzi mahali fulani. Katika mfuko wangu wa mgongoni nilibeba suruali mbili za dangarizi, shati tatu, na Biblia.

Nikiwa nimeketi katika vyumba vya pombe, nikinywa bia na kuisoma Biblia, nikawa nikiwauliza maswali wale walionizunguka, huku nikipata borongo la majibu. Nilikuwa nikitafuta, nikitazama, nikipapasa—kitu gani? Sikujua hasa.

Katika London kikundi cha “Watoto wa Mungu” kilinivutia. Lakini hali moja na ujumbe uliotolewa na mahipi wote walio vijana, ujumbe wao ulikuwa wa kitoto—upendo wa kupenda chochote tu. Kumbe hapa sina cha kujiambulia majibu.

Nikiwa katika ziara ya kanisa maridadi sana la Kianglikana, lililokuwa kathedro la Katoliki hapo kwanza, nilipigwa na butwaa. Nilimwuliza vikari aliyekuwa ameongoza ziara hiyo kwa nini yeye alipata kuwa padri. Yeye aliinua mkono na kufikicha kidole-gumba pamoja na vidole vingine kwa ishara ya mtu mwenye kugusa fedha! Nilitamauka kabisa. Lo! unafiki gani! Kwa kukata tamaa, nikakusanya vitabu vyangu vyote vya kidini nikaviwasha kiberiti.

Septemba 1973, nilianza mwendo tena, kidole-gumba nje kuomba lifti—safari ya Liverpool niwaone waimbaji Beatles na kusikia muziki wao. Gordon Marler alinibeba ndani ya gari lake. Biblia ikawa mazungumzo yetu kwa sababu wote wawili tuliisoma, kwa hiyo tukatajiana maandiko tuliyofahamu.

Baada ya hapo, Gordon akawa ndiye kiunzi changu cha kuipata “kweli.” Tulikuwa tukipashana habari kwa barua na katika masika ya 1974, aliniandikia kwamba alikuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Sikuingiwa na jina Mashahidi wa Yehova, kwa maana sikuwa nimepata kamwe kufikiwa nao katika Richmond. Miezi kadhaa baadaye barua ilifika ikiwa na mwaliko huu: “Njoo unitembelee ujifunze Biblia.” Alisema funzo lake lilikuwa jioni ya Jumatano. Kwa hiyo asubuhi moja ya Jumatano nikanyoosha tena kidole-gumba changu. Ilikuwa rahisi zaidi kupata mtu wa kunibeba kwa sababu msichana-rafiki yangu Mfaransa alikuwapo.

Tulienda pamoja na Gordon kwenye funzo lake la Biblia. Kumbe mwenye nyumba alikuwa ni John Hyatt, yule aliyekuwa ametupita njiani mapema kidogo akiwa ameuliza kwa kushangaa, ‘Sasa watu wa jinsi ile watakujaje kuijua kweli juu ya Mungu?’ Tulipojulishwa kwake, alipaaza sauti ya mshangao: “Oh, wale mahipi wawili wa ile barabara, wale Mayankii (Waamerika)!”

Mambo yalianzia hapo. Nilikuwa na maswali mengi kutokana na usomaji wangu wa Biblia. Hakukuwa na wakati wa kutosha kuyapata majibu, kwa kuwa mkusanyiko mkubwa wa Mashahidi ungeanza mapema asubuhi kesho yake. John alinipa kitabu, Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, akaniambia nichague sura fulani, nilete maswali yangu yote, na kurudi Jumatano ifuatayo. Alinialika kwenye mkusanyiko Jumapili. Wale watu safi, waungwana walinivutia. Msichana-rafiki yangu hakupendezwa. Nilipomwambia kwamba nilimpenda Mungu kuliko vile nilivyompenda, alienda zake.

Jumatano, nilirudi kwenye nyumba ya John, nikiwa nimechagua ile sura juu ya Yesu Kristo. Nilikuwa na maswali hususa juu ya mwenendo wa ngono na unabii wa Danieli wa majuma 70 ya miaka. John alikuwa mweneza-evanjeli wa wakati wote, aliyeijua Biblia kwelikweli. Aliniambia maoni ya Biblia ni kwamba ngono ni ya watu waliofunga ndoa peke yao, akanielewesha wazi yale majuma 70 ya Danieli. Sasa vile vijambo vya usomaji wangu wa Biblia vikawa vikielezwa kwa mwingiano mzuri. Saa nane ya usiku, nikasema: “Hii ndiyo kweli.” Nilikuwa nimekusudia kulala katika bustani ya mji, kama nilivyokuwa nimefanya mara nyingi wakati uliopita, lakini John akakataa na kunitandikia katika sakafu ya sebule ya nyumba.

Ilionekana alifanya hivyo kwa maongozi ya kimungu, kwa maana usiku huo genge la vipara-ngoto lilikuwa likifanya fujo katika mtambo wa kubeba watu ghorofani. Hakika sura yangu ingalifanya nitandikwe vibaya.

Mafunzo yalipoendelea, nilijifunza kwamba nilikuwa nimewaza kweli nikiwa mtoto. Mfumo hauwezi kuendelea. Unapepesuka ukatokomee. Mungu mwenyewe atasawazisha mambo kwa njia ya serikali yake, ule Ufalme niliokuwa nimesali upatikane lakini nisiuelewe kamwe. (Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10) Kuchukia kwangu unafiki kulionyeshwa kuwa sawa. Hata Yesu hakuupenda. (Mathayo, sura 23) Nilikuwa nimepapasa kumtafuta Mungu, naye akawa amejiacha apatikane nami.—Matendo 17:27.

Nilimwambia kweli hiyo kila mtu niliyekutana naye. Papohapo nikataka kwenda nyumbani nikashiriki huo ujuzi pamoja na familia yetu. Niliporudi Richmond, nilifanya hivyo hasa.

Nilipiga simu pia kwenye Jumba la Ufalme. Ndugu Herbert Lohwasser akaijibu simu. Alikuwa akifanya kazi katika hilo jumba jipya, akilitayarisha kwa wakfu walo. Nikamwambia nilitaka funzo la Biblia. Yeye akanieleza juu ya mkutano mkubwa kesho yake ambapo jiji lote lilialikwa kusikia hotuba ya Biblia. Nilienda.

Nilionekana waziwazi kama kuku mweupe, sura yangu ikinitangaza kuwa mgeni mwenye kuzuru. Huko painia mseja-kijana aitwaye Mike Bowles alijijulisha kwangu na kunialika niketi kando yake mbele kwenyewe. Baadaye, ule umati ulinong’ona-nong’ona kwa kuulizana, “Ni nani msichana yule mwenye nywele ndefu maridadi mwenye kuketi kando ya Mike Bowles?” Huyo alikuwa mimi!

Baada ya funzo langu la tatu, nilinyoa nywele zangu na kubadili namna yangu ya kuvalia. Sura yangu ya nje ilianza kupatana na hisia zangu za ndani. Nilijiunga na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika Oktoba na kuanza kazi ya kuhubiri peupe Novemba. Punde si punde nikawa nikiongoza mafunzo ya Biblia pamoja na wengine. Katika Machi 1975, nilibatizwa tena, safari hii kwa kufananisha wakfu wangu kwa Yehova, yule Mungu niliyepata kumjua hatimaye.

Nilianza huduma ya wakati wote, kama wale waliokuwa wamenisaidia sana. Nilianza kukaa Betheli ya Brooklyn, makao makuu ya Mashahidi wa Yehova, katika Mei 1976. Nilikuwa na kazi mbili, kuendesha mtambo wa kupandisha na kushusha watu ghorofani na kupeleka barua. Kazi zote mbili ziliniwezesha kuwa na pendeleo la kuongea na ndugu wa kiroho kila siku.

Baada ya miaka miwili, nilirudi nyumbani Virginia nikawa mhubiri wa wakati wote kwa muda fulani. Hatimaye nikawa mzee katika kutaniko. Kazi hiyo ilifurahisha, lakini ndani yangu mlikuwa na hangaiko fulani. Niliwazawaza hivi: ‘Lazima iwe kuna jambo zaidi niwezalo kufanya katika utumishi wa Mungu.’ Je! ni utumishi wa mishonari? Hilo lingeweza kuwa ndilo jambo lenyewe? Nilijaza ombi la Watchtower Bible School of Gilead nikakubaliwa kupata mazoezi ya wamishonari katika lile darasa la Oktoba 1983 hadi Machi 1984.

Kabla ya kuhitimu, mgawo wangu wa mishonari ulitangazwa: Kolombia, Amerika Kusini. Nikawa barabarani tena lakini si kidole-gumba juu kuomba lifti za magari safari hii.

Kituo changu cha kwanza kilikuwa kwenye ofisi ya tawi ya Watch Tower katika Santa Fe de Bogotá, ambako nilijifunza Kihispania kwa dhati muda wa miezi mitatu. Halafu nikagawiwa kwenda makao ya mishonari katika Medellín, ambako kulikuwa na mafunzo ya Kihispania muda wa saa nne kwa siku, siku sita kwa juma.

Kuanza kuhubiri katika lugha mpya kulikuwa na mambo. Mwanzoni-mwanzoni nilienda nikibisha hodi mlangoni nikiwa peke yangu kabisa huku dada mwenye kusema Kihispania akiniangalia kwa umbali ambao angeweza kunisikia. Nilitolea mwanamke mmoja magazeti yetu ya Kikristo kwa peso 30. Huyo mwanamke alionekana mwenye ghadhabu akafunga mlango! Nilipomrudia dada, nilielezwa kwa nini. “Chunga matamshi yako,” dada akasema. “Ulisema besos, si pesos.” Lo, nilikuwa nimeomba huyo mwanamke anipe busu 30!

Kolombia ni mahali maridadi. Uvutio mkuu ni watu wenyewe. Wao ni wachangamfu, wenye kujishusha na wasiojifanya sana kama watu katika nchi zenye usitawi mkubwa zaidi wa viwanda. Kwa hiyo, kufundisha Biblia ni tofauti. Watu wa Kolombia huitikia hadithi, vielezi, kusimuliwa maono ya maisha ya kweli bila kuelezwa mambo magumu. Wamezoea zaidi maisha halisi. Watu huishi karibu na watu hapa. Wana hisia za kujali sana mambo na huitikia. Wasikilizaji wangu ni kama wasikilizaji ambao Yesu alisema nao, watu wa hali ya chini; hiyo husababisha nijaribu kumwiga Yesu kwa ukaribu ninapofundisha. Hawa watu hunikumbusha Waefeso 3:19, ambapo Paulo alisema juu ya “upendo wake Kristo, upitao ufahamu kwa jinsi ulivyo mwingi.”

Katika 1989, nilipewa mgawo mpya, mwangalizi wa mzunguko. Hiyo yamaanisha kwamba mimi husafiri kwenye kutaniko tofauti la Mashahidi wa Yehova kila juma na kukaa pamoja nayo, tukienda pamoja kutafuta mlango kwa mlango wale watakao kumjua Mungu, nikitoa hotuba katika Jumba la Ufalme, na kuambatana na akina ndugu na dada wa hapo kwenye mafunzo ya Biblia.

Yehova huendelea kunitia nidhamu na kunitakasa kwa njia nyingi. Nakumbuka tukio moja hususa. Mosquera, nje ya Bogotá, ndilo kutaniko nililopaswa kutumikia, na kama kawaida akina ndugu walikuwa wamenipangia kukaa pamoja na familia fulani—dada, mume wake asiyeamini, na watoto wawili.

Niliwasili nikakuta nyumba ya chumba kimoja hasa, iliyosongamana vitu ikiwa na vitanda vya ghorofa, ikiwa imetenganishwa na sehemu nyingineyo ya nyumba na kipazia tu. Mimi nikaelekezwa kwenye nafasi hiyo, na baada ya kuambiwa nichague kitanda changu, nikachagua ile sehemu ya chini. Hiyo ilikuwa Jumanne. Nilipolala nikisoma Biblia karibu saa 3:30 usiku, wale watoto wawili waliingia, na kukuru-kakara wakawa wamepanda katika ile sehemu ya juu.

Nilifikiri-fikiri. ‘Mambo gani haya! Mimi nahitaji faragha zaidi ya hii. Mtu kama mimi, mtu aliyezoea kuwa na chumba chake mwenyewe (au angalau nafasi yake mwenyewe ya faragha katika bustani ya jijini), afanya nini hapa?’ Nilipiga moyo konde kwamba hakika ningetafuta malazi mengine ziara ifuatayo kisha nikalala. Kila usiku mambo yalikuwa yaleyale. Lakini Alhamisi nilipokuwa nikisoma, kichwa kidogo kilichungulia chini kutoka kile kitanda cha juu. Ilikuwa ni Andrés, mwenye umri wa miaka tisa. “Ndugu Fleet,” yeye akauliza, “je! umelala?” Nikajibu sivyo kwa haraka ya kukosa adabu. Swali likafuata tena. “Ndugu Fleet,” yeye kauliza, “je! umesali?” Sivyo kwa mara nyingine.

Halafu Andrés akauliza, “Wewe usalipo, je, naweza kuja chini, halafu unitolee sala mimi pia?” Niliguswa moyo. Mtazamo wangu ulibadilika. Kwa uhakika, mtazamo wangu juu ya ziara yote ulibadilika. “Yatima” alikuwa ni huyu hapa akitaka mtu asali pamoja naye. Mimi nilikuwa mtu huyo. Nilisali pamoja naye. Na nilikaa pamoja na familia hiyo ziara fulani ya baadaye. Andrés mdogo alinisaidia nipunguze kukaza fikira juu ya mahitaji yangu mwenyewe nizikaze zaidi juu ya mahitaji ya kibinafsi ya akina ndugu. Nilianza kuwatafuta ‘mayatima’—wale wanaopapasa wakimtafuta Mungu, sawa na vile mimi nilivyofanya nikiwa mtoto. (Zaburi 10:14) Baba ya Andrés sasa anahudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme na amejiunga nasi katika kazi ya kuhubiri peupe.

Tangu nilipowasili Kolombia, idadi ya wale wanaomwabudu Yehova imeongezeka kutoka 22,000 hadi 55,000. Sasa mimi sishindani tena na lile hangaiko la kwamba kuna jambo fulani zaidi ninalopaswa kuwa nikilifanya. Naridhika kuwa katika mahali pema hapa. Nitamshukuru milele Mungu mwenye rehema ambaye macho yake yalipenya ndani ya sura yangu ya juujuu tu ya uhipi na kuona mtu mwenye kujitahidi kumpata Mungu wa kweli, ambaye jina lake ni Yehova.—Kama ilivyosimuliwa na Richard Fleet.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Richard katika 1973

[Picha katika ukurasa wa 21]

Richard Fleet, mishonari wa Amerika Kusini

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki