Kutofanya Mazoezi ya Kimwili Kwaweza Kukuua
HUO ndio ujumbe unaotolewa na Shirika la Moyo la Amerika na Shirika la Moyo na Maradhi ya Ghafula la Kanada. Kwa miongo mingi, uvutaji wa sigareti, msongo wa damu, na kuwa na kolesteroli nyingi katika damu ndizo zilizotajwa kuwa matatizo makubwa ambayo yangesababisha maradhi ya moyo yaliyoonwa kwamba yangeweza kudhibitiwa. Lakini katika 1992 jambo jingine liliongezwa kwenye orodha hiyo—kutofanya mazoezi ya kimwili. Labda ndilo tatizo rahisi zaidi kudhibiti.[1][2]
“Jizoeze tu na kwa ukawaida,” akasema Dakt. John Duncan wa Dallas, Texas.[3] Kwa kusikitisha watu wengi hawafanyi mazoezi kwa ukawaida. “Kuna maoni yasiyofaa katika Amerika kwamba Waamerika wengi wanafanya mazoezi ya kimwili kwa kufuata ule mtindo wa kujizoeza wa miaka mitatu au minne ambayo imepita,” akasema Tom McMillen, msimamizi-msaidizi wa Baraza la Rais la Kujizoeza na Michezo. “Hiyo si kweli. Vifo vipatavyo 250,000 kila mwaka husababishwa na kutofanya mazoezi.”[4]
“Ni asilimia 22 pekee ya Waamerika wanaofanya mazoezi ya kimwili leo kwa kiwango kinachopendekezwa kwa afya nzuri,” kulingana na Dakt. Walter R. Dowdle, anayeshikilia wadhifa wa mkurugenzi wa Vituo vya Kudhibiti Maradhi vya U.S. “Jitihada ya nchini pote inahitajika ili kukabiliana na kiwango cha juu cha kutofanya mazoezi ya kimwili katika United States.”[5]
Utendaji wenye nguvu kupita kiasi hauhitajiki, kama ilivyoripotiwa na gazeti la Kanada Medical Post: “Utafiti mpya umethibitisha kwamba hata matembezi ya polepole yaweza kunufaisha afya.”[6] Dakt. Anthony Graham, mkuu wa maradhi ya moyo katika Hospitali ya Wellesley jijini Toronto, Kanada, alieleza hivi: “Tunazungumzia utendaji wa kimwili wenye kiasi, aina fulani ya utendaji wa kawaida unaoweza kuwa wenye kiasi kama kufanya kazi kwa ukawaida katika bustani yako mara kadhaa kwa juma, au kutembea miendo mifupi. . . . Sasa tunajifunza kwamba hata kiasi hicho cha utendaji unaofanywa kwa ukawaida utapunguza hatari zinazoweza kukabili mtu. Ni mtazamo wa kwamba mazoezi ni ‘kitu cha kufanywa na wote.’”[7]
Dakt. Russell Pate wa Chuo Kikuu cha South Carolina alikubaliana na jambo hilo, akisema hivi: “Nina hakika kwamba mamilioni kwa mamilioni ya watu wanaamini kwamba kama hawawezi kujiunga na vilabu vya mazoezi ya kimwili na kutumia muda wa saa tano kwa juma huko, basi hawana tumaini la kufanya mazoezi. Nafikiri twapaswa kutangaza rasmi kwamba ni muhimu sana kutembea polepole kuzunguka jengo baada ya mlo mkuu.”[8]
Kwa kuwa hata utendaji wa kimwili unaofanywa kwa kiasi wafaa afya yako, je, waweza kutembea au kupanda na kushuka orofa kwa ukawaida badala ya kupanda lifti? Mbona usiegeshe gari lako mbali kidogo na mahali uendapo, labda dukani, na kutembea mwendo unaobaki? “Ni bora kufanya chochote kile kuliko kutofanya chochote,” akasema Dakt. Robert E. Leach, msimamizi wa tiba ya mifupa katika Kituo cha Afya cha Chuo Kikuu cha Boston.[9]