Maoni ya Biblia
Je! Ni Vibaya Kuhuzunika?
“MIMI NAAMINI TUMAINI LA UFUFUO KWA UTHABITI, NA NILIFIKIRI KWAMBA NI KOSA KUONYESHA KIHORO CHANGU MBELE YA WENGINE NA KWAMBA KWA NJIA HIYO NINGEKUWA NIKIWAPA SABABU YA KUTIA SHAKA KWAMBA NINA TUMAINI THABITI HIVYO. NILIFIKIRI KWAMBA KAMA NAAMINI UFUFUO KIKWELI, SINGEHISI POTEZO LANGU KWA KINA KIREFU HIVYO.”—CHARLENE, MKRISTO ALIYEBATIZWA KWA ZAIDI YA MIAKA 21.[1][2]
WAKATI mtu umpendaye afapo, huenda kukatokea hisia na mitazamo ambayo hukutarajia—hofu, hasira, hatia, na mshuko wa moyo. Ile ahadi ya Biblia yenye kuchangamsha moyo juu ya ufufuo wa wafu kwenye uhai katika dunia ya kiparadiso chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu yaweza kusaidia kupunguzia Mkristo kishindo cha kifo. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15; Ufunuo 21:1-4) Lakini kama vile maneno ya Charlene yaonyeshavyo, wakati mpendwa afapo, Wakristo fulani hubeba mzigo usio wa lazima—ile hisia ya kwamba ni kosa kuomboleza, kwamba kihoro hufunua kwa kadiri fulani ukosefu wa imani katika ahadi ya Biblia ya ufufuo.
Ingawa hivyo, Biblia husema nini juu ya kuonyesha kihoro? Je! ni kosa kuomboleza wakati mpendwa afapo?
Walionyesha Huzuni
Imani ya Abrahamu yajulikana sana. Alipotahiniwa, Abrahamu ‘ni kana kwamba alimtoa Isaka mwana wake.’ (Waebrania 11:17, NW; Mwanzo 22:9-13) Kulingana na ithibati, hakuna mtu aliyekuwa amepata kufufuliwa kabla ya wakati wake, lakini Abrahamu alikuwa na imani kwamba, ikihitajika, ‘Mungu angeweza kumwinua mwana wake hata kutoka kwa wafu.’ (Waebrania 11:19) Karibu miaka 12 baada ya imani ya Abrahamu kutahiniwa, mke wake, Sara, alikufa.[3] Mtu huyo mwenye imani aliitikiaje? Biblia yaeleza kwamba ‘alifika kuomboleza Sara na kumulilia.’a (Mwanzo 23:2, Zaire Swahili Bible) Ndiyo, mtu huyo aliyekuwa na imani kwamba Mungu angeweza kuwafufua wafu alionyesha kihoro peupe. Na bado, Abrahamu hutajwa kuwa kielelezo cha kutokeza cha imani.—Waebrania 11:8-10.
Kimoja cha vielelezo vyenye kugusa zaidi cha kuonyesha peupe kihoro cha kupoteza mpendwa kilikuwa Yesu Kristo mwenyewe. Kwa habari ya kifo cha Lazaro, rafiki wa karibu wa Yesu, twasoma hivi: “Mariamu alipofika pale alipokuwapo Yesu, na kumwona, alianguka miguuni pake, akamwambia, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. Basi Yesu alipomwona analia, na wale Wayahudi waliofuatana naye wanalia, aliugua rohoni, akafadhaika roho yake, akasema, Mmemweka wapi? Wakamwambia, Bwana, njoo utazame. Yesu akalia machozi.”—Yohana 11:32-35.
Inachangamsha moyo kwelikweli kuona kwamba Mwana mkamilifu wa Mungu hakuwa na aibu kuonyesha kihoro peupe. Neno la lugha ya awali lililofasiriwa “akalia machozi” (da·kryʹo) humaanisha “kumwaga machozi kwa unyamavu.”[6] Ajabu kubwa ni kwamba hapo kwanza Yesu alikuwa amefufua watu wawili—mwana wa mjane wa Naini na binti ya Yairo—na alikusudia kabisa kumfufua Lazaro. (Luka 7:11-15; 8:41, 42, 49-55; linganisha Yohana 11:11.) Muda fulani mapema alikuwa amemwambia Martha hivi: “Mimi ndimi ufufuko na uzima. Anayeniamini mimi hata kama anakufa ataishi.” (Yohana 11:25, HNWW) Hata hivyo, hisiamoyo nyingi sana zilimkaba Yesu mpaka macho yake yakafurika machozi.
Kuna jambo fulani lililo la maana yenye kina kirefu zaidi. Yesu ndiye “mfano kamili wa hali ya Mungu mwenyewe.” (Waebrania 1:3, HNWW) Hisia nyororo na nzito za Yesu alipopoteza mpendwa katika kifo zaonyesha mfano wenye kugusa moyo wa Baba yetu wa kimbingu, Yehova. Zaonyesha Mungu ambaye moyo wake huumwa na maumivu makali kutokana na kihoro cha watumishi wake.—Linganisha Zaburi 56:8.
Kwa wazi, basi, si kosa kuonyesha kihoro wakati mtu umpendaye afapo. Abrahamu aliombolezea kifo cha Sara. Yesu alihuzunika kwa kina kirefu Lazaro alipokufa. Yehova Mungu huelewa maumivu yetu kwa sababu “hujishughulisha sana” kwa ajili yetu.—1 Petro 5:7.
Ingawa hivyo, namna gani lile tumaini la Kikristo? Je! lafanyiza tofauti?
‘Kutohuzunika Kama na Wengine’
Wakati watu fulani katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza Thesalonike walipoonyesha kihoro juu ya kupoteza waamini wenzao, mtume Paulo alijaribu kuwafariji. Aliandika hivi: “Lakini, ndugu, hatutaki msijue habari zao waliolala mauti, msije mkahuzunika kama na wengine wasio na matumaini.” (1 Wathesalonike 4:13) Ndiyo, wale walio na uhakika katika ahadi ya Mungu ya kuwainua wafu ni afadhali kuliko wale wasio na tumaini la ufufuo.b Jinsi gani hivyo?
Wale wasio na tumaini la ufufuo huwa na hali ya kukata tamaa wakabiliwapo na kifo. Hata ikiwa wao hudai kuamini maisha ya namna fulani baada ya kifo, ni wachache ambao hupata faraja halisi kutokana na hilo. Kwa wengine wengi, huzuni yao haisababishwi tu na uhakika wa kwamba wapendwa wao wametenganishwa nao na kifo bali pia na uhakika wa kwamba huo ni utenganisho wa daima kwao. Kwa kukosa uelewevu wa wazi juu ya ufufuo, matumaini yao huzikwa pamoja na wapendwa wao; kwa kadiri wanavyohusika, wao hawatawaona tena kamwe.—Linganisha 1 Wakorintho 15:12-19, 32.
Hata hivyo, mambo ni tofauti kwa Wakristo wa kweli. Paulo alieleza kwamba kifo ni kama usingizi—si kwa sababu tu ni hali isiyo na ufahamu ambayo yafanana na usingizi mzito bali pia kwa sababu yawezekana kuamshwa kutokana nao kwa njia ya ufufuo. (Zaburi 13:3; Mhubiri 9:5, 10) Tumaini hilo lenye msingi wa Biblia hufanyiza tofauti.
Wakati Mkristo apotezapo mpendwa katika kifo, yeye huhisi potezo hilo kwa kadiri ileile wasioamini wahisivyo kupoteza mwenzi aliyetokomea, potezo la uso waliofahamiana nao, kutokuwapo kwa sauti iliyopendwa. Tumaini la ufufuo haligandishi hisia ya moyo. Hata hivyo, hilo husawazisha kule kuomboleza. Tumaini hilo haliondoi uhitaji wa kuonyesha kihoro, hapana, lakini laweza kufanya yale maumivu yawe mepesi zaidi kuvumiliwa.
[Maelezo ya Chini]
a Kuhusu neno la Kiebrania lililofasiriwa “kuomboleza,” Theological Wordbook of the Old Testament hutaarifu hivi: “Wote waliohisi potezo la aliyeondoka walikuwa wakija kushiriki kihoro chao pamoja na washirika wa ile familia. . . . Vikelele vyembamba au mayowe mara nyingi viliandamana na kule kuomboleza.”[4] Kwa habari ya neno la Kiebrania la ‘lia,’ kitabu hichohicho chaeleza hivi: “Ijapokuwa machozi hushirikishwa na macho, kulia hushirikishwa na sauti; Washemu hawalii kwa unyamavu, bali kwa sauti. . . . Katika A[gano la] [K]ale lote kulia ndiyo njia ya kiasili na ya hiari ya kuonyesha hisia chungu.”[5]
b Wakristo wa karne ya kwanza ambao Paulo aliwaandikia walikuwa na tumaini la ufufuo wa kwenda mbinguni ambako wangetumikia wakiwa watawala-wenzi pamoja na Kristo. (1 Wathesalonike 4:14-17; linganisha Luka 22:29, 30.) Hivyo Paulo aliwatia moyo wafarijiane kwa tumaini la kwamba kwenye kuwapo kwa Kristo waaminifu miongoni mwao waliokuwa wamekufa wangefufuliwa na wangeunganishwa pamoja na Kristo na pamoja na mtu na mwenzake. Hata hivyo, kwa walio wengi sana kati ya wale waliokufa, Biblia hutoa tumaini la ufufuo wa kuingia katika paradiso ya kidunia iliyorudishwa.—Yohana 5:28, 29; Ufunuo 21:1-4.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]
Jean-Baptiste Greuze, elezo kutoka Le fils puni, Louvre; © Photo R.M.N.y