Vijana Huuliza . . .
Namna Gani Nikishikwa na Mahaba kwa Mtu Asiye Mwamini?
“Mimi nina tatizo,” akakiri msichana mmoja Mkristo. “Mimi nina upendo wa kupumbazwa juu ya jirani yangu. Yeye ni mfadhili, mwungwana, na mwenye ufikirio, lakini amekosa kuwa jambo moja—mpenda Yehova. Najua ni kosa kwangu kupendezwa naye, lakini sina hakika juu ya jinsi ya kushughulikia hisia zangu kwake.”[1]
Mark alikuwa na miaka 14 alipojipata katika hali kama hiyo.a Akawa na fikira za kupumbazika kimahaba kwa msichana asiyeshiriki imani zake za kidini. “Mara nyingi nilikuwa nikiota ndoto za mchana juu ya vile mambo yangekuwa tukiwa pamoja, tukifunga ndoa,” asema. “Lakini nilijua lilikuwa kosa.”[2]
MAPENZI na fikira za kupumbazika kimahaba ni mambo ya kawaida wakati wa miaka ya utineja, ambapo misisimko ya kuvutwa kimahaba huwa yenye nguvu. (Linganisha 1 Wakorintho 7:36.) Kwa kukosa njia ya kufungulia hisia hizo, vijana wana elekeo la kusitawisha fikira za kupumbazika kimahaba kwa walimu wawapendao zaidi, watumbuizi, na kadhalika. Kwa kuwa kwa kadiri kubwa mahusiano ya kibinafsi na watu wazima wa jinsi hiyo hayawezi kufikiwa, kwa kawaida mapenzi hayo ya kupumbazika huwa ya muda mfupi na yasiyo na madhara sana.b Ingawa hivyo, namna gani ikiwa umesitawisha hisia zenye nguvu kwa mtu wa rika lako—mtu fulani aliye na nia na uwezo wa kuwa na uhusiano—lakini mtu huyo hashiriki imani zako za kidini hata kidogo?
Huenda baadhi wasiweze kuona jambo hili kuwa tatizo. Kwanza, vijana wengi hawapendezwi sana na dini. Na hata miongoni mwa wale wapendezwao, kutafuta mapenzi ya mtu wa imani tofauti huenda kukawa si jambo la kuudhi sikuzote.[3] Huenda hata watu wenye akili za kukubali mambo sana wakalikubali. Ingawa hivyo, watu wazima wengi huona matatizo yawezayo kuwapo katika mahusiano ya jinsi hiyo, hasa kwa kuwa mara nyingi tokeo layo huwa ni ndoa. Hivyo mwandikaji Andrea Eagan aliwashauri vijana hivi: “Kuwa na malezi mamoja ya kidini si jambo la maana ikiwa hakuna yeyote kati yenu aliye wa kidini. Lakini ikiwa zoea la kidini ni la maana kwa mmoja wenu au nyote wawili, basi tofauti juu ya dini ni lazima zifikiriwe. . . . Si lazima mwe wamoja kwa habari ya dini . . . , lakini ni lazima mweze kuishi pamoja.”[4]
Ushauri huo huenda ukasikika kuwa wafaa. Lakini kwa kweli waonyesha “hekima ya dunia hii.” (1 Wakorintho 3:19) Biblia huonyesha kwamba mahaba kati ya mwamini na mtu asiye mwamini hutokeza masuala yenye maana kubwa kuliko upatano wa ndoa. Vijana miongoni mwa Mashahidi wa Yehova wajua kwamba jambo hilo lahusisha utii kwa Neno la Mungu, ambalo huhimiza Wakristo wafunge ndoa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Kwa kuwa kutafuta mapenzi si tafrija tu bali ni utangulizi wa ndoa, ingemchukiza Mungu ikiwa mmoja wa watumishi wake angehusika kimahaba pamoja na mtu ambaye hajaweka maisha yake wakfu kwa Yehova.
Hata hivyo, vijana fulani Mashahidi wamejipata wakivutiwa na watu wasio waamini. Hilo hutendekaje? Wewe wapaswa kufanya nini ukijipata katika hali ya jinsi hiyo?
Jinsi Litendekavyo
Kwanza, ng’amua kwamba wanadamu wote wana elekeo la kufanya makosa. “Ni nani awezaye kuyatambua makosa yake?” akauliza mtunga-zaburi. (Zaburi 19:12) Vijana hasa ndio wenye kuelekea kufanya makosa ya mahaba. Kwa nini? Kwa sababu sahili ya kwamba wao hawana busara itokanayo na maarifa na umri. (Mithali 1:4) Kwa kuwa kijana Mkristo hajawa na maarifa mengi ya kushughulika na watu wa jinsia tofauti, huenda asijue kabisa jinsi ya kushughulikia uvutio—au uelekezeo fikira—wa kimahaba.
Ndivyo ilivyokuwa kwa Sheila alipong’amua kwamba mvulana mwanashule mwenzake alikuwa na upendo wa kupumbazwa kwake. “Nilitambua kwamba alipendezwa nami,” akasema Sheila. “Saa za chakula cha mchana alikuwa akija na kula pamoja nami. Vipindi vya mafunzo katika maktaba, alikuwa akinitafuta.” Hisia za Sheila kwa mvulana huyo zilianza kuongezeka.[5] Mark, aliyetajwa mapema kidogo, vilevile akumbuka hivi: “Sikuzote mimi nilikuwa nikiona msichana huyo kwenye somo letu la mazoezi ya mwili. Alikuwa akifanya bidii kuja kuongea nami. Haikuwa vigumu urafiki kusitawi.” [6] Katika kisa cha Pam wa miaka 14, mvulana wa ujirani hata alifikia hatua ya kumpa pete iwe wonyesho wa shauku yake kwake.[7]
Ni wazi kwamba si sikuzote ambapo Shahidi asiye na hatia ndiye tu amekuwa akitongozwa. Msichana mmoja alikuwa akirudisha tu ule upendezi wa wazi alioonyeshwa na mvulana Mkristo jina lake Jim. Ingawa hivyo, siku moja alibanwa wakati msichana huyo alipojitokeza siku moja kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, akimtafuta![8]
Hali zozote ziwazo, huenda ikawa ulijua lilikuwa kosa kuhusika. Lakini nyakati fulani ni vigumu kukinza uelekezeo wa fikira kutoka kwa mtu wa jinsia tofauti. Fikiria Andrew. Wakati wa mwaka wake wa kwanza katika shule ya sekondari, wazazi wake walikuwa katika hatua za kutalikiana. “Mimi nilihitaji mtu wa kuongea naye,” akumbuka. Msichana mmoja katika shule yao alionekana sikuzote akiwa na neno lifaalo la kumtia moyo. Upesi hisia za kuoneana mahaba zikasitawi.[9]
Hatari Zilizopo
Hisia za jinsi hiyo zisipozuiwa, zaweza kukuingiza matatani. Mithali 6:27 husema hivi: “Je! mtu aweza kutia moto kifuani pake, na nguo zake zisiteketezwe?” Kwa kielelezo, fikiria ono la msichana mmoja jina lake Kim. Ingawa alilelewa akiwa Mkristo, alijiruhusu ahusike kihisiamoyo na mvulana shuleni. “Mvulana yule alikuwa mmoja wa jamaa wenye kupendwa na kusisimua sana shuleni,” Kim akumbuka. Muda si muda Kim akawa akihudhuria karamu ambazo dawa za kulevya zilitumiwa waziwazi. “Niliogopa sana, lakini nilipendana naye. Nilipata mimba.” Kim aliolewa na mvulana-rafiki yake, lakini mvulana huyo akajikuta gerezani kwa wizi wa kutumia silaha.[10] Kwa mara nyingine onyo la Biblia lilithibitika kuwa kweli: “Urafiki mbaya huharibu tabia njema.”—1 Wakorintho 15:33, Habari Njema kwa Watu Wote.
Hiyo si kudokeza kwamba vijana wote wasio Mashahidi wa Yehova ni wakosefu wa adili au hutumia dawa za kulevya. Hata hivyo, angalau vijana hao hawashiriki na vijana Mashahidi viwango, maoni, au miradi ileile. Wakorintho wa Kwanza 2:14 hueleza kwamba mtu asiye mwamini “hayapokei mambo ya Roho wa [roho ya, NW] Mungu; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana [yachunguzwa, NW] kwa jinsi ya rohoni.” Fikiria ni kwa kadiri gani viwango vyako vya kidini vimefanyiza hisiamoyo zako—shangwe upatayo kwenye mikutano ya Kikristo, msisimko wa kushiriki ujumbe wa Biblia pamoja na mtu mpokevu, furaha ya kujifunza Biblia yenyewe. Je! yawezekana mtu asiyeamini akazielewa—sembuse kuzishiriki—hisia hizo? Hata kidogo.
Hivyo Paulo awasihi Wakristo hivi: “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini?” (2 Wakorintho 6:14, 15) Kijana Sonya alijifunza somo hilo kwa kujionea mambo mwenyewe alipohusika kihisiamoyo pamoja na mtu asiye mwamini. Msichana huyo akiri hivi: “Kuwa na mwandamani asiyeshiriki bidii na upendo wako kwa Yehova ndio upweke mbaya zaidi uwezao kuwaziwa. Ni jambo la kuvunja hisiamoyo. Kweli iwapo ndiyo kani yenye kuchochea maisha yako, ni lazima uishiriki—ni lazima tu ufanye hivyo! Ni hisia ya kusikitisha sana wakati ambapo huwezi kuishiriki pamoja na mwenzi wako wa ndoa kwa sababu wewe upo pamoja na mtu asiye mwamini.”[11]
Basi, katika uhusiano wa jinsi hiyo dini haitaelekea kuwa ya kufuatwa na wahusika wote kwa pamoja, bali itakuwa jambo kuu watakaloshindania. Ungeweza kwa urahisi kuhisi walazimishwa kupuuza kidogo masilahi yako ya kiroho ili udumishe amani. Lakini kufanya hivyo kungekuachia ukiwa wa kiroho tu. Mwanamke mmoja kijana asimulia hivi: “Mimi nilipata kukaribiana sana na jamaa ambaye hakuwa Shahidi. Lakini urafiki ulipokuwa wa karibu zaidi, niling’amua kwamba nilikuwa nimeshikwa na mahaba kwake. Kidogokidogo uhusiano wangu pamoja na Yehova ulifuliza kupungua umaana kwangu; uhusiano wangu na mvulana huyo ukawa ndilo jambo la maana zaidi kwangu. Sikutaka tena kwenda mikutanoni, kushirikiana na ndugu zangu Wakristo, wala kwenda nje katika kazi ya kuhubiri. Nilitaka kuwa naye na basi. Nikawa Shahidi asiye mtendaji miaka miwili iliyofuata. Na katika yote hayo, ‘rafiki’ yangu hakurudisha kamwe upendo wangu kwake. Nilifuliza kufikiri kwamba siku fulani angefanya hivyo hatimaye, lakini wapi.”[12]
Ndiyo, kuhusika pamoja na mtu asiyeshiriki viwango vyako vya kidini na vya kiadili hakika kutakuletea majonzi na huzuni. Mwendo wa hekima ni kujiondoa katika nira hiyo isiyoingiana sawasawa. Lakini wawezaje kufanya hivyo na hali wahisi ukivutwa sana na mtu fulani? Hiyo ndiyo habari ya makala yetu inayokuja katika mfululizo huu.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
b Ona sura ya 28 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 19]
Je! mtu asiye mwamini atashiriki idili yako kwa mambo ya kiroho?