Msijifunge Nira Pamoja na Wasioamini
“Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana . . . yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini?”—2 WAKORINTHO 6:14, 15.
1. Dada mmoja alikujaje kufunga ndoa na mtu asiye-amini?
MMOJA wa Mashahidi wa Yehova kutoka United States ya magharibi ya kati alifiwa na mume wake katika aksidenti ya gari miaka kadhaa iliyopita. “Kwanza nilizidiwa na hisia hata nisijue la kufanya,” akumbuka mwanamke huyo, “lakini nikapiga moyo konde nisiache jambo hili likatize utumishi wangu kwa Yehova. Ingawa hivyo, baada ya miaka kadhaa nilianza kuhisi kama gurudumu lisilo na mwenzi nilipokuwa karibu na wenzi waliofunga ndoa kundini. Binti yangu na mimi hatukualikwa sikuzote kwenye visafari vya kijamaa vya kwenda kujistarehesha nje. Nilipoona Wakristo walio wenzi wa ndoa wakionyeshana shauku, nilihisi kuwa nimekataliwa hata zaidi. Ilionekana ni kama hakuna mtu aliyeona kwamba nilikuwa ninaendelea kudhoofika kiroho. Kwa hiyo mwanamume mlimwengu niliyemjua kazini aliponiomba niende naye nje kula mlo mkuu, nilienda. Kabla sijang’amua mambo, nilianza kumwonea mapenzi. Mwishowe, nilidhoofika sana na kushindwa na upweke wangu hata nikakubali anioe.”
2. Kwa nini tamaa ya kufunga ndoa ni ya kiasili, na ndoa ilibuniwa ili ifanyize nini?
2 Ndiyo, tamaa ya kushirikiana maisha pamoja na mwenzi wa ndoa yaweza kuwa imara sana, na pia ni ya kiasili. Kama vile Yehova mwenyewe alivyoliweka wazo hilo: “Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake. Mimi nitafanya msaidiaji kwa ajili yake, awe kikamilisho chake [“sehemu ya mlingano,” kitu chenye kumfaa].” (Mwanzo 2:18, New World Translation Reference Bible, kielezi cha chini) Ndoa ilibuniwa kwa kusudi la kufanyiza kifungo cha muungano wenye ukaribiano na udumifu kati ya mwanamume na mwanamke. Si Adamu bali ni Yehova aliyesema hivi: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:22-24; linganisha Mathayo 19:4-6.) Labda moyo wako watamani sana kuwa na hiyo sehemu ya mlingano.
3, 4. (a) Biblia yaonyaje dhidi ya kufanyiza ufungamano wa karibu pamoja na wasioamini? (b) Shauri la Paulo kuhusu kujifunga nira isiyosawazika vizuri laweza kutumikaje kuhusu ndoa? (c) Wakristo Wakorintho wangeelewaje mtajo “wasioamini”? (Ona kielezi cha chini).
3 Ingawa hivyo, Biblia yaonya dhidi ya kufanyiza ufungamano wa karibu pamoja na wasioamini. Kama vile mtume Paulo alivyoweka wazo hilo: “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini,a kwa jinsi isivyo sawasawa [“Msijifunge wenyewe hatamu katika timu isiyosawazika vizuri,” The Jerusalem Bible], kwa maana . . . yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini?”b (2 Wakorintho 6:14, 15) Huenda ikawa Paulo alikuwa akifikiria katazo la Sheria ya Musa dhidi ya kufunga ng’ombe ndume na punda katika nira moja ili walime kwa plau. (Kumbukumbu 22:10) Punda ni mdogo zaidi naye hana imara kama mwenzake na angeteseka kwa kufungwa nira hiyo isiyosawazika vizuri. Kwa kuwa ndoa ni kama nira ambayo hufunga mume na mke pamoja, Mkristo akifunga ndoa na asiyeamini tokeo lingekuwa ni nira isiyosawazika vizuri. (Mathayo 19:6) Mara nyingi nira hiyo huleta mbano na mkazo wa ziada kwenye ndoa.—Linganisha 1 Wakorintho 7:28.
4 Hata hivyo, kama ilivyotolewa kielezi na tukio lile lililo katika utangulizi, Wakristo fulani wamechagua kufunga ndoa na wasioamini. Kwa nini watu fulani huona ni vigumu kufunga ndoa “katika Bwana tu”?—1 Wakorintho 7:39.
Kwa Nini Watu Fulani Hutazama Mahali Penginepo
5. Toa kielezi cha sababu ambayo hufanya watu fulani wahusike kimahaba pamoja na asiyeamini.
5 Si kwamba kwa lazima wao hujiondokea ili tu wakapuuze shauri la Mungu. Fikiria hali ya dada Mkristo ambaye huenda akataka kufunga ndoa. Huenda akatamani sana kuwa na mume Mkristo, lakini hakuonekani kukiwa na ndugu wengi wenye kufaa katika mzingo wake wa marafiki wanaoamini. Yeye ahangaishwa na umri wake. Huenda akatamani kuwa na jamaa. Hofu ya kuzeeka akiwa peke yake na uhitaji wa kuhisi akipendwa ni mambo yawezayo kumwingiza matatani kwa urahisi. Hapo, ikiwa mwanamume mlimwengu aonyesha kupendezwa naye, yaweza kuwa vigumu kukinza. Huenda mwanamume huyo akaonekana kuwa mfadhili na mwanana. Huenda ikawa havuti sigareti wala hatumii usemi mbaya. Ndipo dada aanza kuwaza-waza na kuwazua-wazua akitetea fikira zake za kwamba: ‘Mwanamume huyu ni mzuri kuliko ndugu wengi sana ambao nawajua!’ ‘Yeye apendezwa na kujifunza.’ ‘Mimi najua visa ambapo dada alifunga ndoa na mtu asiyeamini na hatimaye mtu huyo akawa mwamini mwenzi.’ ‘Kuna ndoa fulani za Kikristo zisizofaulu!’—Ona Yeremia 17:9.
6, 7. (a) Dada mmoja mseja alielezaje hali yake ya kuvurugika fikira? (b) Ni swali gani ambalo lastahili ufikirio wetu?
6 Ndiyo, laweza kuwa jambo lenye kuvuruga fikira za Mkristo mseja ambaye ataka kufunga ndoa. Baadhi yao hata huhisi wana shida kubwa ya kupata mwenzi. “Hesabu ya ndugu wenye kufaa ni ndogo sana tena sana,” ndivyo kasema dada mmoja mseja akieleza hali katika eneo lao. “Lakini hesabu ya dada waseja ni kubwa sana tena sana. Dada aonapo ujana wake ukipita mbiombio, hiari zake huchemka akachagua asifunge ndoa kamwe au afunge ndoa mara tu apatapo nafasi yake ya kwanza.”
7 Hata hivyo, shauri la Biblia liko wazi: ‘Msijifungie nira pamoja na wasioamini.’ (2 Wakorintho 6:14) Je! onyo hili la kimungu ni kali au lisilosababu mambo vizuri?
Wonyesho wa Utunzi wa Mungu Wenye Upendo
8. Yehova ameonyeshaje kwamba yeye afikiria masilahi yetu yaliyo bora zaidi katika moyo wake?
8 Yehova ahangaikia hali njema yetu ya daima kwa kina kirefu. Je! kwani yeye hakujiletea gharama kubwa akatoa Mwana wake awe “ukombozi badala ya wengi”? (Mathayo 20:28, NW) Je! yeye siye yule ‘Mmoja ambaye anatufundisha sisi kujinufaisha wenyewe’? (Isaya 48:17, NW) Je! yeye haahidi kwamba ‘hataacha tushawishwe kwa kadiri izidiyo ile ambayo twaweza kuhimili’? (1 Wakorintho 10:13, NW) Basi, kwa kusababu mambo vizuri, yeye atuambiapo tusijifunge nira pamoja na wasioamini, ni lazima moyoni mwake awe anafikiria masilahi yetu yaliyo bora zaidi! Fikiria jinsi onyo hili lilivyo wonyesho wa utunzi wake wenye upendo kwetu.
9. (a) Ni onyo gani ambalo Paulo atoa dhidi ya kufanyiza kwa Mkristo kifungo chenye ukaribiano pamoja na asiyeamini? (b) Ni nini maana ya neno la Kigiriki lililofasiriwa “upatano,” nalo latoaje kielezi cha ugumu ambao hutokea wakati Mkristo ajifungapo nira pamoja na asiyeamini?
9 Ndoa ilikusudiwa na Muumba ifanyize kifungo cha ukaribiano mwingi kabisa kati ya wanadamu, huku mume na mke wakiwa “mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Je! ni jambo la hekima Mkristo afanyize kifungo hicho cha ukaribiano pamoja na asiyeamini? Paulo ajibu kwa kutokeza mfululizo wa maswali yenye kupenya ndani, huku kila moja likitangulia kudokeza jibu la kukanusha: “Kwa maana pana urafiki gani kati ya haki [uadilifu, NW] na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu [Kigiriki, sym.phoʹne.sis] gani kati ya Kristo na Beliari [Shetani]? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini?” (2 Wakorintho 6:14, 15) Neno la Kigiriki sym.phoʹne.sis lamaanisha kwa uhalisi “kuvuma pamoja” (kutokana na syn, “pamoja,” na pho.neʹ, “mvumo”). Hilo hurejezea ulinganifu [upatano, NW] ambao hutokezwa na vyombo vya kimuziki. Bila shaka, hakuna upatano kati ya Kristo na Shetani. Vivyo hivyo, katika nira isiyosawazika vizuri, ni vigumu sana mume na mke ‘kuimba sauti moja.’ Wao ni kama vyombo viwili vya kimuziki visivyopatana, vinavyotokeza mivumo tengetenge badala ya kutokeza muziki.
10. Ni mambo gani yenye kuhitajiwa sana katika ndoa yenye furaha, na ni faida gani zilizopo wakati ambapo kuna nira iliyosawazika vizuri?
10 Basi, mtu wa kiroho aweza kuonaje shangwe ya upatano kamili pamoja na mtu wa kimwili? (1 Wakorintho 2:14) Ili kuwe na ndoa yenye furaha, yahitajiwa sana kuwe na upamoja wa kanuni, imani, na miradi. Hakuna kitu chenye kuletea ndoa imara kubwa kuliko ujitoaji wa watu wawili kwa Muumba. Iwapo kuna nira iliyosawazika vizuri, mume na mke waweza kutiana moyo katika ibada. Wote wawili waweza kutegemea Maandiko yatatue tofauti zao. Basi, je! ushuhuda hauonekani wazi kwamba Yehova atuambia tusijitie katika nira pamoja na wasioamini kwa sababu yeye ataka tuone shangwe ya kuwa na kifungo cha ukaribiano mwingi pamoja na mwenzi wetu wa ndoa kwa kadiri iwezekanayo?
11. Kwa nini mapatano ya ndoa pamoja na watu wasio waabudu yalikatazwa katika Israeli, na ni swali gani lenye kuamsha fikira ambalo latokezwa?
11 Kutii onyo la Biblia kwatuepusha pia na matokeo yenye maumivu ambayo hutokea mara nyingi Mkristo ajifungapo nira pamoja na asiyeamini. Kwa kielelezo, kuna uwezekano wa kwamba asiyeamini atageuza mwenzi Mkristo asitumikie Yehova. Fikiria onyo la Yehova kwa Israeli wa kale. Mapatano ya ndoa pamoja na watu wasio waabudu yalikatazwa. Kwa nini? “Kwa kuwa atamkengeusha mwanao mume asinifuate,” Yehova akaonya, “ili wapate kuabudu miungu mingine.” (Kumbukumbu 7:3, 4) Kwa kukabiliwa na upinzani kutoka kwa mwenzi asiyeamini, huenda mtu akawa na elekeo la kupeperuka pole kwa pole na kulegeza sana kinga zake. Ni rahisi kufikiri kwamba, ‘Hilo halitanipata mimi!’ Lakini lilipata mtu mwenye hekima ya kimo kile cha Sulemani. Je! jambo ilo hilo halingeweza kukupata wewe? — 1 Wafalme 11:1-6; linganisha 1 Wafalme 4:29, 30.
12. Sheria ya Mungu yenye kukataza kufunga ndoa pamoja na watu wa kigeni ilitumikaje kuwa ulinzi kwa Waisraeli? Toa kielezi.
12 Hata ikiwa asiyeamini hageuzwi mbali kutoka kwenye ibada ya kweli, kungali kuna matatizo na mibano ambayo mara nyingi hushirikishwa na nyumba iliyogawanyika kidini. Fikiria, tena, sheria ya Mungu kwa Israeli. Tuseme msichana Mwisraeli alikubali kufunga ndoa na mwanamume Mkanaani. Kwa kupewa mazoea ya ngono yaliyoenea sana katika bara la Kanaani, mwanamume huyo angekuwa na staha gani kwa sheria ya Mungu wa msichana huyo? Kwa kielelezo, je! mwanamume huyo angekuwa na nia ya kujizuia asifanye ngono wakati wa hedhi, kama ilivyotakwa na Sheria ya Musa?c (Walawi 18:19; 20:18; linganisha Walawi 18:27.) Katika kisa cha mwanamume Mwisraeli ambaye angefunga ndoa na msichana Mkanaani, msichana huyo angemuunga mkono kwa kadiri gani wakati mwanamume huyo angefunga safari kwenda Yerusalemu mara tatu kila mwaka akahudhurie zile sikukuu za majira? (Kumbukumbu 16:16) Ni wazi kwamba sheria ya Mungu yenye kukataza ndoa hizo ilitumika kuwa ulinzi kwa Waisraeli.
13. (a) Kwa nini mlimwengu hana dhamiri ya Kikristo yenye kuzoezwa na Biblia? (b) Ni mibano na matatizo gani ambayo yaelekewa na watu fulani katika nyumba zilizogawanyika kidini?
13 Namna gani leo? Viwango vya kiadili vya walimwengu ni kama kisauti hafifu chenye kusikika kwa mbali vikilinganishwa na vile vya Biblia. Hata walimwengu fulani waonekane kuwa wanyoofu kama nini, wao hawana dhamiri ya Kikristo yenye kuzoezwa na Biblia. Wao hawajatumia miaka ya kujifunza Neno la Mungu, ‘wakigeuza akili zao’ na ‘kuvua kabisa utu wa kale.’ (Warumi 12:2, NW; Wakolosai 3:9) Kwa sababu hiyo, mara nyingi Mkristo ambaye ajifunga nira pamoja na asiyeamini huwa ajifunua wazi aingiwe na maumivu mengi ya moyoni na kihoro. Baadhi yao hukabili mbano wa mara kwa mara ili washiriki katika mazoea ya ngono za upotovu au kuadhimisha sikukuu za kilimwengu. Na baadhi yao hata hulalamika juu ya kuwa wapweke. Kama vile alivyoandika dada mmoja: “Upweke ambao wewe wahisi ikiwa umefunga ndoa na mtu asiyependa Yehova ndio upweke mbaya zaidi uwezao kuwaziwa. Wajua, wewe huwi na mtu yeyote wa kushirikiana ukweli naye, na hilo ndilo jambo la maana kuliko yote katika maisha yako.”
14. (a) Katika nyumba iliyogawanyika, kwa nini ni vigumu kulea watoto katika “nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova”? (b) Huenda athari ikawa nini juu ya watoto katika nyumba iliyogawanyika?
14 Katika nyumba iliyogawanyika, yaweza kuwa vigumu sana kulea watoto katika “nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4, NW) Kwa kielelezo, je! asiyeamini atakuwa na nia ya kuruhusu watoto wahudhurie mikutano au washiriki katika huduma ya shambani? Mara nyingi watoto hujikuta mwishowe wakiwa wamevurugika waelekeze wapi shauku zao—wao wawapenda wazazi wote wawili, lakini mzazi mmoja tu ndiye ampenda Yehova. Alisema hivi dada mmoja aliyefunga ndoa na mtu asiyeamini: “Nilipita katika maumivu mengi sana ya moyoni wakati wa ndoa yangu ya miaka 20. Wana wangu walikua wakiwa na msukosuko mwingi na maudhiko ya hisia-moyo na sasa wao ni sehemu ya ulimwengu. Mara nyingi binti yangu huudhika kwa kulazimika kuwa mbali na mimi muda mwingi kwa sababu ya haki za utembeleaji ambazo baba yake anazo. Matatizo yote haya yametokea kwa sababu mimi nilipokuwa na miaka 18, nilichagua kupuuza moja ya kanuni za Yehova.” Kanuni gani? Msijifunge nira pamoja na wasioamini!
15. Kwa nini Yehova atushauri sisi tusijifunge nira pamoja na wasioamini?
15 Ni wazi kwamba Yehova ataka sisi tupate manufaa bora zaidi kutokana na maisha. Mambo ambayo yeye ataka kwetu, kutia na shauri lake kwamba tusijifunge nira pamoja na wasioamini, ni kwa faida yetu. (Kumbukumbu 10:12, 13) Kufunga ndoa na mtu asiyeamini ni kupuuza shauri la Kimaandiko, hekima yenye kutumika kwa mafaa, na maumivu ambayo huwapata wengi mara nyingi.
Maswali Ambayo Huulizwa Kikawaida
16, 17. (a) Tusipojiangalia, huenda hisia-moyo zikavurugaje fikira za utimamu? (b) Je! shauri la Mungu lapasa kupuuzwa kwa sababu ya hali zenye utofauti usio wa kikawaida ambamo Mkristo alifunga ndoa pamoja na mtu asiyeamini na sasa wote wawili wanatumikia Yehova? Eleza.
16 Hata hivyo, tusipojiangalia, hisia-moyo zaweza kuvuruga fikira za utimamu. Huenda tukaanza kuhisi kwamba utofauti fulani usio wa kikawaida waweza kufanywa katika kisa chetu. Fikiria baadhi ya maswali ambayo huulizwa zaidi.
17 Namna gani hali ambamo ndugu au dada alifunga ndoa na mtu asiyeamini, na sasa wote wawili wanatumikia Yehova? Ingawa hivyo, kanuni za Yehova zilivunjwa. Je! kufaulu kwa jambo kwapaswa kutetea uhaki wa njia iliyotumiwa hata kama haikufaa? Kinachotoa kielezi cha maoni ya Mungu kuhusu wale ambao hupuuza shauri lake ni kisa cha Wayahudi waliokuwa wanarudi kutoka utekwa wa Kibabuloni. Baadhi yao walipochukua wake wapagani, waandikaji wa Biblia Ezra na Nehemia hawakukawia kulaani vikali vitendo vyao. Wayahudi hao ‘walitenda kwa ukosefu wa imani,’ walitenda ‘ubaya mkubwa,’ na wakajiletea “uhatia.” (Ezra 10:10-14; Nehemia 13:27, NW) Jambo jingine la kufikiria: Wakati ambapo twapuuza shauri la Mungu, huenda tukajijeruhi kiroho, huku tukitia makovu katika dhamiri yetu. Dada mmoja ambaye mume wake asiyeamini alikuja hatimaye kuwa mwamini alisema hivi: “Mimi ningali ninashughulika na makovu ya kihisia-moyo. Nashindwa na maneno ya kuwaeleza hisia mbaya ambazo mimi huwa nazo wakati wengine waelekezapo kidole kwetu na kusema, “Lakini wale walifanikiwa.”’
18. Mwendo wa hekima ni nini ikiwa wewe wavutiwa na mtu fulani ambaye hajabatizwa bado, na kwa kufanya hivyo utaonyesha nini?
18 Namna gani ikiwa wewe wavutiwa na mtu fulani ambaye anajifunza Biblia na anahudhuria mikutano, ingawa hajabatizwa bado? Sisi hushangilia wakati mtu yeyote aonyeshapo kupendezwa na ukweli wa Biblia. Ingawa hivyo, swali ni hili: Je! wewe wapaswa kufuatia mbetuko wako? Kwa kusema wazi, mwendo wa hekima ni kungoja mpaka muda fulani baada ya rafiki yako kubatizwa na awe anafanya maendeleo katika kuonyesha matunda ya roho ya Mungu kabla hujaanza matembezi ya kirafiki naye. (Wagalatia 5:22, 23) Huenda isiwe rahisi kutumia ushauri huo, lakini kwa kufanya hivyo utaonyesha kwamba una ujitoaji kwa kanuni za Biblia; hiyo itaweka msingi mzuri kwa ajili ya furaha ya kweli katika ndoa. Ikiwa rafiki yako akujali wewe kihalisi na anaendelea kupata kumpenda Yehova kikweli, bila shaka yeye atakuwa na nia ya kungoja mpaka nyinyi wote wawili mwe “katika Bwana”—mwe mmejiweka wakfu na kubatizwa—kabla ya kuchumbiana. Kumbuka, pia, kwamba upendo wa kweli hauumizwi na kupita kwa wakati. — 1 Wakorintho 7:39; Mwanzo 29:20.
19. Yapasa ukumbuke nini ikiwa unaona ni vigumu kupata mwenzi wa ndoa miongoni mwa waamini wenzi?
19 Namna gani ikiwa inakuwa vigumu kwako kupata mwenzi wa ndoa mwenye kufaa miongoni mwa waamini wenzako? “Mimi nina miaka 26, niko mseja, na nina upweke kweli kweli,” akasema dada mmoja. Ni kweli kwamba kuwa mseja kwaweza kufanya mambo yawe magumu kwako, lakini matatizo yanayotokana na kufungwa nira isiyosawazika vizuri katika ndoa yaweza kuwa magumu hata zaidi! Kutii shauri la Mungu kwaweza kutaka imani, kujidhibiti na saburi, lakini uwe na uhakikishio wa kwamba Yehova ajua na atamani yaliyo bora zaidi kwako. (1 Petro 5:6, 7) Tia jambo hilo katika sala, halafu mngojee Yehova. (Zaburi 55:22) Katika mfumo huu wa mambo, hakuna mtu aliye na maisha yenye kuridhisha kikamilifu. Huenda moyo wako ukawa na uchu mwingi wa kutaka mwenzi wa ndoa. Ingawa hivyo, wengine wana fungu lao pia la matatizo, baadhi yayo yakiwa yasiyoponyeka katika mfumo huu. Ni katika ulimwengu mpya tu unaokuja kwamba “tamaa ya kila kilicho hai” itaridhishwa kikamili.—Zaburi 145:16, NW.
20. Dada mmoja mseja alielezaje hali yake ya kupiga moyo konde, na wewe waweza kuwa na uradhi gani kwa kupiga moyo konde vivyo hivyo?
20 Kwa sasa, piga moyo konde usijifunge nira pamoja na asiyeamini. Dada mseja wa miaka 36 alieleza hivi hali yake ya kupiga moyo konde: “Mimi hupelekea Yehova sala kila siku ili nipate mwenzi wa ndoa. Sina tamaa ya kutafuta nje ya tengenezo la Yehova, lakini kungali kuna vishawishi vya kufanya hivyo. Kwa sasa, mimi napanga kutengeneza sifa ambazo zitanipa maendeleo ya kiutu ili niwe mwanamke wa kiroho wa aina ambayo mwanamume wa kiroho anatafuta.” Je! wewe umepiga moyo konde vivyo hivyo? Ikiwa ndivyo, waweza kuwa na uradhi ambao huja kwa kuthibitisha uaminifu wako mshikamanifu kwa yule Mungu wa haki ya kimungu.—Zaburi 37:27, 28.
[Maelezo ya Chini]
a Kwenye 1 Wakorintho 14:22, Paulo alitumia mtajo “wasioamini” kwa kuutofautisha na “waaminio,” au watu waliobatizwa. Basi, Wakorintho wangeelewa neno “wasioamini” kuwa larejezea watu wasiobatizwa.—Ona Matendo 8:13; 16:31-34; 18:8.
b “Katika namna iliyopanuliwa, kanuni hii ingeweza kuelezwa hivi: ‘Msifanyize uhusiano wowote, uwe ni wa muda tu au ni wa kudumu, pamoja na wasioamini ambao ungeongoza kwenye kuridhiana msimamo wa viwango vya Kikristo au kuhatarisha upatani wa ushahidi wa Kikristo. Na kwa nini kuwe na utengano huo? Kwa sababu asiyeamini hashiriki viwango, maoni, au miradi mimoja na Mkristo.’”—The Expositor’s Bible Commentary, Buku la 10, ukurasa wa 359.
c Ona Mnara wa Mlinzi (wa Kiingereza) wa Septemba 15, 1972, kurasa 575-6.
Wewe Waweza Kueleza?
◻ Biblia yaonyaje dhidi ya kufanyiza ufungamano wa karibu pamoja na wasioamini?
◻ Kwa nini Wakristo fulani waliojiweka wakfu hutafuta mwenzi wa ndoa nje ya kundi?
◻ Ni jinsi gani onyo la Yehova kuhusu kujifunga nira isiyosawazika vizuri lilivyo wonyesho wa utunzi wake wenye upendo kwetu?
◻ Ni maswali gani kuhusu kupata mwenzi wa ndoa huulizwa kikawaida, nawe ungeyajibuje?