Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 6/8 kur. 17-19
  • Naweza Kuachaje Kuvutiwa Kimahaba na Mtu Fulani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Naweza Kuachaje Kuvutiwa Kimahaba na Mtu Fulani?
  • Amkeni!—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kupata Msaada
  • Kukomesha Uhusiano
  • Kupata Nafuu Kutokana na Uchungu Huo
  • Namna Gani Nikishikwa na Mahaba kwa Mtu Asiye Mwamini?
    Amkeni!—1994
  • Naweza Kuachaje Maisha Maradufu?
    Amkeni!—1994
  • Je, Ananifaa?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Naweza Kumkataaje?
    Amkeni!—2001
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 6/8 kur. 17-19

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kuachaje Kuvutiwa Kimahaba na Mtu Fulani?

“NINA umri wa miaka 20 nami ni Shahidi wa Yehova aliyebatizwa. Lakini nilianza kufanya urafiki na mtu [asiyeitikadi] mwenye umri wa miaka 28. Nilimpenda, nami naamini kwamba alinipenda. Wazazi wangu hawakujua juu yalo, kwa kuwa nilijua kwamba hawangependa jambo hilo. Walipopata kujua, walihuzunika sana na wakashtuka. Hawakuweza kuelewa ni kwa nini nilijihusisha kihisiamoyo na mtu wa ulimwengu.”[1]

Ndivyo alivyoandika kijana mwanamke Mkristo tutakayemwita Monique.a Kwa kusikitisha, vijana wengi wamejiingiza kwenye mashaka kama hayo—wakipumbazika au kujihusisha kimahaba na mtu asiyeitikadi, mtu ambaye hashiriki itikadi zao za Kikristo na viwango vya adili. Makala iliyotangulia katika mfululizo huu (Amkeni! ya Mei 22, 1994) ilionyesha kwamba uhusiano kama huo si kwamba haumpendezi Mungu tu bali pia ni tisho kubwa kwa furaha na usitawi wa mtu. Kijana Ruth alikuja kutambua ukweli huu. “Nilijihusisha na mtu asiyeitikadi,” yeye akiri. “Ingawa hivyo, nilitambua kwamba, ikiwa ningekuwa na uhusiano wowote na Yehova, ilinipasa nivunje uhusiano na mtu huyo.”[2]

Ikiwa wewe ni Mkristo, labda unaweza kukariri maneno ya Biblia kwenye Yakobo 4:4: “Hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.” Lakini ukiwa unajihusisha kihisia na mtu asiyeitikadi, maneno haya huenda yasiwe rahisi kutumia. Kweli, wazo la kuvunja uhusiano laweza kukulemea. Huenda ukahisi umeumia sana kindani. ‘Naweza kuachaje kuvutiwa kimahaba—au kumpenda—mtu fulani?’ huenda ukauliza.

Mtume Paulo wakati mmoja alisema: “Naifurahia sheria ya Mungu kwa utu wa ndani; lakini katika viungo vyangu naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya akili zangu, na kunifanya mateka ya ile sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu. Ole wangu, maskini mimi!” (Warumi 7:22-24) Kama vile Paulo, huenda ukawa unapatwa na mng’ang’ano wa hisia zako. Hata hivyo, vijana wengi Wakristo wameshinda vita hii na kama iwezavyo kusemwa, ‘wamenyakuliwa katika moto.’ (Linganisha Yuda 23.) Jinsi gani? Kwa kukomesha mahusiano yenye kuharibu kabla ya uharibifu usiorekebishwa haujafanyika.

Kupata Msaada

Mark, kwa mfano, alikuza kile alichoita “upendo wa kupumbaza” kwa mtu asiyeitikadi alipokuwa na miaka 14 tu. Badala ya kutafuta msaada, alijaribu kuweka hisia zake ziwe siri. Lakini hisia zake kwa msichana huyo ziliendelea kuongezeka. Upesi alianza kumpigia simu za siri. Msichana huyo alipoanza kumpigia simu, haikuchukua muda mrefu kabla wazazi wake kugundua kilichokuwa kikiendelea.[3]

Usifanye makosa hayohayo ya kujaribu kutatua tatizo lako mwenyewe. Mithali 28:26 yasema: “Mwenye kujitumainia moyo wake ni mjinga; bali yeye aendaye kwa busara ataokolewa.” Je! kweli, ungekuwa katika hali hii ikiwa uamuzi wako haukuwa na kasoro? Wakati mwingine hisia zetu hushinda kusababu kwetu, na twahitaji msaada wa mtu fulani mwenye kuelewa na mwenye kusaidia. Pengine wazazi wako ndio wanaofaa kukusaidia wewe, hasa ikiwa wao ni wenye kuhofu Mungu. Yaelekea, wanakujua vizuri kuliko mtu yeyote. Wao walikuwa vijana wakati mmoja nao waweza kukusaidia kuelewa mambo yanayokupata. Kwenye Mithali 23:26, mwandikaji wa Biblia Sulemani asihi hivi: “Mwanangu, nipe moyo wako; macho yako yapendezwe na njia zangu.” Kwa nini usiwape wazazi wako moyo wako, nao wajue kuwa unahitaji msaada?

Kijana Jim alifanya vivyo hivyo. Alikuwa na mng’ang’ano wa hisia zake kuhusu mapenzi ya kupumbaza na msichana mmoja shuleni. Yeye asema: “Hatimaye niliuliza wazazi wangu msaada. Huo ndio ulikuwa ufunguo wa kushinda hisia hizi. Walinisaidia sana.” Akiwa ameona tegemezo la wazazi wake lenye upendo, Jim atoa ushauri huu: “Nafikiri vijana wengine Wakristo hawapaswi kusita kuongea na wazazi wao. Wasiliana nao. Watakuelewa.”[4]

Akiwa katika hali hiyohiyo, kijana aitwaye Andrew alitumia kwa mafaa msaada mwingine. Kuhusu kuhudhuria kwake kusanyiko la mzunguko la Mashahidi wa Yehova, yeye asema: “Mojapo hotuba hizo ilinifanya nifikiri kwa uzito. Mwangalizi wa mzunguko alitoa shauri kali dhidi ya kusitawisha mahusiano na washiriki wa jinsia tofauti wasio Wakristo. Nilijua kwamba nilipaswa kurekebisha kufikiri kwangu mara hiyo.” Kwa hiyo alifanya nini? Kwanza aliongea na mama yake, mzazi aliye peke yake, naye akanufaika na ushauri wake. Kisha pia alimwendea mzee katika kutaniko la kwao la Mashahidi wa Yehova, ambaye aliweza kutoa msaada wa kuendelea.[5] Wazee wa kutaniko wanaweza kuwa “kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba” kwa walioshuka moyo. (Isaya 32:2) Kwa nini usiendee mmoja wao, nawe umjulishe kinachokutatiza?

Kukomesha Uhusiano

Wazazi wa Mark walipogundua uhusiano wake wa siri, walitenda mara moja. “Wao waliniambia moja kwa moja niache uhusiano huo,” asema Mark. “Itikio langu la kwanza lilikuwa la uasi. Tulijibizana kwa sauti ya juu, na nikajifungia chumbani mwangu. Lakini upesi nikafikiria juu ya mambo ya kweli kuhusu hali hiyo. Uhusiano huo haungefaulu.”[6] Naam, kutafakari juu ya mambo ya kweli ya hali kwaweza kusaidia kutuliza hisia zako. Jiulize mwenyewe: ‘Je! mtu huyu anashiriki miradi yangu, masadikisho yangu, viwango vyangu vya adili? Ikiwa tungeoana, je, mtu huyu angetemeza jitihada zangu za kumwabudu Mungu? Mtu huyu anashiriki idili yangu ya mambo ya kiroho? Kwa kweli, ni upatano gani uwezao kuwa katika uhusiano kama huo?’—Linganisha 2 Wakorintho 6:14-18.

Hata hivyo, kukomesha uhusiano ghafula na kabisa si rahisi. Monique, aliyetajwa mwanzoni, akubali: “Nilijaribu katika pindi mbili kuvunja uhusiano lakini bila mafanikio. Sikutaka kumwacha kabisa. Nilijaribu kumhubiria, nikitumainia kwamba angemkubali Yehova. Hata alikuja kwenye mkutano wa Jumapili mara moja. Lakini hakupendezwa kikweli na Yehova. Nilitambua kuwa mwendo ufaao ni kumwacha kabisa.”[7]

Hilo latukumbusha maneno ya Yesu kwenye Mathayo 5:30. Hapo alizungumzia mambo yanayoweza kumzuia mtu asiingie kwenye Ufalme wa Mungu—vitu ambavyo vyaweza kuwa vyenye thamani kama mkono wa kulia. Kwa hiyo, Yesu alishauri: “Ukate uutupe mbali nawe; kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee, wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanum [ufananisho wa uharibifu wa milele].” Kupatana na kanuni hiyo, mkabili mtu uliye na uhusiano naye ukiwa na moyo mkuu na ‘ukaseme kweli.’ (Waefeso 4:25) Mkiwa mahali peupe—si peke yenu au katika hali ya kimahaba—mwache ajue waziwazi bila mashaka kwamba uhusiano umekwisha. Kijana Sheila akumbuka: “Jambo lililofaulu kwangu lilikuwa hatua isiyo na shaka. Hakuna tena kwenda kula chakula cha mchana pamoja. Hakuna kuonana tena wakati wa masomo. Nilimwonyesha msimamo wangu waziwazi.”[8] Msichana Mkristo aitwaye Pam alisema waziwazi: “Hatimaye nilimwambia aniache, na nikampuuza tu.”[9]

Kupata Nafuu Kutokana na Uchungu Huo

Katika matokeo ya baada ya mvunjiko huo, huenda ukahisi kama vile mtunga-zaburi ambaye alisema: “Nimepindika na kuinama sana, mchana kutwa nimekwenda nikihuzunika.” (Zaburi 38:6) Kipindi fulani cha kuhuzunika ni cha asili tu. Biblia hujulisha kwamba kuna “wakati wa kulia.” (Mhubiri 3:4) Lakini hauhitaji kulia milele. Uchungu huo utakwisha kwa wakati. “Ndiyo,” akubali Mark, “Nilikuwa katika kipindi cha huzuni. Wazazi wangu walitambua jambo hilo nao wakaniongezea mashirika ya vijana wengine Wakristo. Jambo hilo lilikuwa lenye msaada sana.”[10] Andrew, ambaye alihisi mshuko wa moyo vivyo hivyo baada ya mvunjiko wake, asema: “Wazee walinisaidia. Pia nilijihusisha zaidi katika kazi ya kuhubiri na nikawa karibu na ndugu fulani Wakristo ambao tulisikilizana sana.”[11] Naam, jishughulishe na kazi za kiroho. (1 Wakorintho 15:58) Utendaji fulani wa kimwili au mazoezi yaweza kusaidia pia. Epuka kujitenga. (Mithali 18:1) Kazia akili yako mambo yenye kufurahisha na yajengayo.—Wafilipi 4:8.

Kumbuka, pia, kwamba Yehova atafurahia msimamo wako wa moyo mkuu. Jihisi huru kumwendea katika sala kwa ajili ya msaada na tegemezo. (Zaburi 55:22; 65:2) “Nilisali sana,” akumbuka kijana Sheila. Hasha, si rahisi kukomesha uhusiano wenye kudhuru. Akubali Sheila: “Hata kama umepita, wakati mwingine mimi humfikiria na kujiuliza anachofanya. Lakini unashikilia azimio lako, ukijua unampendeza Yehova.”[12]

[Maelezo ya Chini]

a Majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mwache mtu huyo ajue waziwazi kwamba uhusiano wenu umeisha

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki