Je! Utajiri Waweza Kununua Furaha?
KWA wazi kuwa na fedha nyingi zaidi hakufanyi watu wawe na furaha nyingi zaidi. Lasema hivi gazeti Psychology Today: “Mtu akiisha kupita kile kiwango cha umaskini, inashangaza kwamba maongezeko ya mapato yake hayamletei sana furaha ya kibinafsi.”[1]
Hili lilithibitishwa katika tanzia ya Oktoba 29, 1993 iliyokuwa katika New York Times, iliyokuwa na kichwa hiki: “Doris Duke, 80, Mrithi wa Kike Ambaye Utajiri Wake Mwingi Haungeweza Kununua Furaha, Amekufa.” Makala hiyo ilisema: “Usiku mmoja katika Roma katika 1945, Binti Duke, aliyekuwa na umri wa miaka 33 wakati huo, aliambia rafiki yake kwamba utajiri wake mkubwa ulikuwa ukimzuia kuwa na furaha kwa njia fulani-fulani.”[2]
“Fedha zote hizo ni tatizo nyakati fulani,” Duke akamwambia rafiki kwa usiri. “Nikiisha kwenda nje kirafiki na mwanamume mara chache, yeye huanza kuniambia anipenda sana. Lakini naweza kujuaje kama kweli amaanisha hivyo? Naweza kuwaje na uhakika?”[3] Times lilisema hivi: “Maneno yake usiku huo yalionyesha kwamba maisha yake yalikuwa yameathiriwa sana, hata kutiwa madhara makubwa, na utajiri wake.”[4]
Vivyo hivyo, Jean Paul Getty, aliyesifiwa wakati mmoja kuwa ndiye mwanamume tajiri zaidi ulimwenguni, alisema hivi: “Si lazima fedha zihusiane na furaha. Labda zahusiana na kukosa furaha.”[5] Na Jane Fonda, mwigizaji wa kike wa Hollywood aliye maarufu, ambaye katika miaka ya 1970 alipokea dola nusu-milioni kwa kila sinema aliyoigiza, alisema hivi: “Mimi mwenyewe nimeonja utajiri na vitu vyote vya kimwili kwa kadiri fulani. Vitu hivyo havina maana kamwe. Utajiri wa mtu kuweza hata kuwa na vidimbwi vyake mwenyewe vya kuogelea huambatana na magonjwa ya akili.”[6]
Ingawa utajiri pekee hautaleta furaha kamwe, wala umaskini wa kupindukia hautaileta. Hivyo, mwanamume mwenye hekima alisema hivi zamani za kale: “Usinipe umaskini wala utajiri.” (Mithali 30:8, 9) Mwandikaji mwingine wa Biblia alisema kwamba kile ambacho mtu huhitaji ili awe mwenye furaha ni ‘ujitoaji kimungu pamoja na ujitoshelevu. Kwa maana hatukuingiza kitu katika ulimwengu, na wala hatuwezi kuchukua kitu chochote kukipeleka nje. Kwa hiyo, tukiwa na riziki na cha kujifunika, tutakuwa wenye kuridhika na vitu hivi.’—1 Timotheo 6:6-10, NW.