Je! Wewe Unaridhika na Kile Ulicho Nacho?
KUTAFUTA furaha ni tamaa wanayozaliwa nayo wanadamu. Hiyo ni tamaa inayofaa. Ilitiwa katika mioyo ya wanadamu na Muumba wao, kwa sababu, akiwa “Mungu wa furaha,” yeye hutaka viumbe wake wote wafurahi.—1 Tim. 1:11, NW.
Hata hivyo, ulizo ni hili: Mtu anawezaje kupata furaha? Kwa vile raha ya mambo ya kimwili inavyotiliwa mkazo leo, watu wengi wanashirikisha furaha na kuwa na vitu vya kimwili. Wanapoulizwa kama wanataka kujua namna ya kupata furaha maishani mwao, mara nyingi wanajibu hivi: ‘Kama ningekuwa na fedha, ningefurahi.’
Haipaswi kushangaza kwamba kuwaza kwa namna hiyo kunaenea kila mahali. Kwa kutumia njia za namna zote za utangazaji na propaganda—nyingine za waziwazi, nyingine za werevu—wanabiashara wa ulimwengu sikuzote wanatia watu moyo wanunue vitu zaidi na kutumia fedha nyingi zaidi. Watu wanafanywa waone kwamba wanaweza kuokoa fedha kwa kununua vitu vipya, ijapokuwa wanacho kitu kile kile, ingawa ni cha zamani kidogo au cha mwundo tofauti. Kwa mfano, tangazo fulani huko Hong Kong husihi watu hivi: “Ikiwa tayari una gari kubwa, jipatie gari hili, pia,” lililo imara zaidi. Mtangazaji mwingine anauliza: ‘Chombo cha kusawazisha hali ya hewa chumbani kinatumia nguvu (za umeme) nyingi?’ Ndipo laja pendekezo hili: ‘Kibadilishe sasa na chombo kinachofanya kazi vizuri zaidi.’
Kama matokeo ya matangazo hayo yote ya kibiashara, kuna kutoridhika miongoni mwa watu. Wengi wanajaribu kupata njia za kujipatia fedha zaidi ili waweze kununua vitu zaidi vya kimwili, wakifikiri kufanya hivyo kutawaletea furaha wanayotamani pamoja na usalama. Lakini ni mara nyingi kama nini jitihada zao hushindwa na kukatisha tamaa! Wengine, wakishindwa kujipatia utajiri katika njia halali, wametumia njia zisizo halali—kuiba, unyang’anyi wa kutumia nguvu, kuuza dawa za kulevya, na kadhalika. Jambo hilo lakazia ukweli wa mithali hii ya Biblia: “Yeye anayefanya haraka kuwa tajiri hataendelea kuwa bila hatia.”—Mit. 28:20, NW.
Lakini huenda watu fulani wakasema: ‘Je! si kweli kwamba, ijapokuwa wengi wameshindwa kuwa matajiri, wengine wamefaulu?’ Ndiyo, katika kila nchi kumekuwako wale ambao wamepata kuwa matajiri kwa kujitahidi sana katika kufanya kazi au kwa kutumia akili, ingawa hesabu yao iko chini sana kwa kulinganisha. Hata hivyo, ulizo lililo la maana zaidi ni hili: Je! wao wana uradhi na furaha? Ni lazima ikubaliwe kwamba hata wale ambao wameweza kujilundikia mali mara nyingi hawatosheki, sikuzote wakitaka kuwa matajiri zaidi. Muumba wa wanadamu anajua vizuri sana maelekeo ya namna hiyo ya wanadamu wasiokamilika. Neno lake lasema hivi: “Apendaye fedha hatashiba fedha, wala apendaye wingi hatashiba maongeo.” (Mhu. 5:10) Hiyo imekuwa kweli kama nini!
UBATILI WA UTAJIRI
Vilevile Muumba anajua vizuri sana madhara na kukosa furaha kunakoletwa na njia ya maisha ya kupenda mambo ya kimwili. Kwa sababu ya Mungu kuwahangaikia wanadamu kwa upendo, katika Neno lake ametoa mashauri mengi ya kuwaonya wanadamu juu ya hatari hii. Hata mtu awe amefaulu namna gani katika kujikusanyia mali, atapoteza kila kitu alicho nacho akifa. Bila shaka ni ubatili kutia jitihada zote za mtu katika kujipatia mali ambayo mtu atalazimika kuachia wengine. Hali hiyo inaelezwa kikweli na Mfalme Sulemani mwenye hekima katika maneno haya: “Alivyotoka tumboni mwa mamaye, atakwenda tena tupu-tupu kama alivyokuja; asichume kitu cho chote kwa ajili ya kazi yake, hata akichukue mkononi mwake.” Hivyo mwenye hekima alikuwa na sababu nzuri ya kukata maneno hivi: “[Huo ndio msiba mkubwa] sana, ya kwamba kama vile alivyokuja, vivyo hivyo atakwenda zake; naye amefaidiwa nini mwenye kujitaabisha kwa ajili ya upepo?”—Mhu. 5:15, 16.
Licha ya hayo, wale walio na tamaa kubwa ya kutajirika mara nyingi wanataabishwa na magonjwa yanayoletwa na maono ya moyoni yenye kuharibu kama vile wasiwasi, hofu na wivu. Sulemani mtu aliyechunguza sana hali ya maisha katika nyakati za kale alisema kwa usahihi hivi: “Siku zake zote hula gizani, mwenye fadhaa nyingi, mwenye ugonjwa na uchungu.” (Mhu. 5:17) Uchunguzi wa kitiba (utabibu) wa kisasa umethibitisha kwa wingi sana matokeo yenye kuumiza sana yanayoletwa na maono yasiyofaa ya moyoni juu ya hali ya afya ya mwili wa mtu. Je! hali mbaya ya afya si ni hasara kubwa sana kupata kwa sababu ya utajiri wa mambo ya kimwili?
Tamaa isiyozuiliwa ya kujipatia raha nyingi zaidi ya mambo ya kimwili yaweza vilevile kuharibu furaha ya mtu. Kwa mfano, watu wengi hufanya kazi saa za ziada au wanakuwa na zaidi ya kazi moja ili waweze kununua vitu vya anasa, walakini wanapata kuona kwamba wamechoka sana au ni wenye shughuli sana kwamba hawawezi kujifurahisha vitu hivyo wanapovipata. Wengine wanakopa fedha ili wanunue vitu vya anasa au kwenda matembezi yenye kugharimu fedha nyingi, wakijiingiza kwenye deni na kuwa na mzigo mkubwa wa kifedha. Wengi wamelazimika kukubali kwamba wamefilisika kwa sababu ya kushindwa ‘kulipa deni zao, wakajiletea maumivu mengi pamoja na aibu juu yao wenyewe na jamaa zao. Ikiwa watu hao wangalitosheka na mambo ya lazima ya maisha, je! wangalijiletea maumivu kama hayo ya moyoni pamoja na taabu wao wenyewe na wapendwa wao?
FURAHA YA KWELI NA URADHI (KURIDHIKA)
Kwa sababu ya hekima yake kuu, Muumba wa wanadamu anajua mwendo unaoongoza kwenye furaha ya kweli na uradhi. Kupitia kwa mtume Mkristo Paulo, kwa upendo yeye anashauri hivi: “Utauwa pamoja na kuridhika ni faida kubwa. . . . Tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo.” (1 Tim. 6:6-8) Mtu anayeridhika na mambo ya lazima ya maisha hasukumwi aongeze mali yake kwa njia za pupa au kwa kujitahidi kusonga mbele. Anaepuka wasiwasi na kukosa furaha kunakoletwa na kutoridhika. Kwa kuridhika na kile alicho nacho, anaweza kutumia wakati na nguvu zake katika mambo yaliyo ya maana zaidi na yenye kuthawabisha zaidi kuliko utajiri wa mambo ya kimwili.
Ili tuweze kuwa na furaha kweli kweli, tunahitaji kuwa na uhusiano mwema pamoja na Mungu. Hilo linawezekana tu kwa kupata maarifa sahihi ya Muumba na kwa kumtumikia kwa moyo wote. Lakini wengine waweza kuuliza: ‘Ni kwa sababu gani inampasa mtu ajitoe kwa Mungu ili awe na furaha? Je! Si kuna watu wengi ulimwenguni ambao hawana maelekeo ya kidini hata kidogo na hata hivyo wanaonekana wakifurahia ufanisi wao wa mambo ya kimwili na mambo mengine mazuri ya maisha? ’ Ni kweli walakini lazima tukumbuke kwamba furaha ya kweli ni kubwa zaidi kuliko anasa tu au kufurahia kitu fulani kwa kitambo tu. Inahusu hali ya ndani ndani ya kujisikia vizuri pamoja na amani ya ndani ndani. Huenda mtu akapata furaha kutokana na alivyo navyo. Walakini, kwa sababu ya kutokuwa na uhakika na hali ya maisha, anawezaje kuwa na hakika kwamba atakuwa na furaha iyo hiyo kesho? Ajapojiona kuwa mwenye furaha, je! Jambo ambalo msingi wake ni wa kitambo tu laweza kufikiriwa kuwa furaha ya kweli?
Biblia inaeleza watu wanaojiona kuwa wenye furaha kwa sababu ya ufanisi wao wa mambo ya kimwili. Wanaonyeshwa wakisema hivi: “Ghala zetu zimejaa, zikitoa mazao ya namna moja baada ya nyingine, makundi yetu yakiongezeka kwa maelfu, elfu kumi kwa moja, katika barabara za miji yetu, ng’ombe wetu wakiwa mazito, pasipo kupasuka na pasipo kutoa mimba, na pasipo kilio katika njia kuu zetu. Wenye furaha ni watu wenye hali hiyo! ” Walakini, ndipo Biblia huonyesha furaha kuu zaidi: “Wenye furaha ni watu ambao Yehova ndiye Mungu wao!”—Zab. 144:13-15, NW.
Mtu ambaye amejitoa kwa Mungu na anayefurahia uhusiano wa karibu pamoja na Muumba anakuwa na hali ya kujiona kuwa salama sana na kuwa na amani, jambo ambalo ni la maana katika kupata amani ya kweli. Mtu huyo anajua kwamba hata apatwe na msiba gani, amehakikishiwa uangalizi wa Mungu wenye upendo. (Ebr. 13:5, 6) Kwa sababu ya kuwa mtumishi wa Mungu, vilevile mtu huyo anakuwa na kusudi maishani pamoja na tumaini zuri la wakati ujao. Yeye anajua kwamba yeye Aliye Juu Zaidi ataondoa chuki yote na uovu mambo ambayo yameleta maumivu mengi sana na huzuni duniani. Mahali pa taratibu ya sasa patachukuliwa na utawala wa haki, ambao chini yake watu “hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu,” bali watajifurahisha matunda ya kazi yao milele.—Isa. 65:17-25.
Ulimwenguni pote leo, kuna maelfu ya watu ambao hapo kwanza walishindwa kupata furaha katika kufuatilia mambo ya kimwili, lakini baadaye walipata furaha ya kweli na kuridhika. Hiyo ilikuwa wakati walipojifunza kweli ya Neno la Mungu wakaanza kuishi kupatana nayo.
Katika nchi moja ya Kusini-magharibi ya Asia, mwanamume mmoja kijana kutoka jamaa moja tajiri alikuwa amejaribu kupata furaha kwa kujaribu kuleta mabadiliko ya kisiasa. Jambo hilo lilimletea taabu tu kutoka kwa wenye mamlaka ya kiserikali. Kisha akajaribu kufanya biashara na akafaulu kujilundikia fedha nyingi sana kwa muda mfupi tu. Walakini bado hakupata furaha. Kugeukia kwenye dawa za kulevya hakukumletea uradhi. Mwishowe, kwa kukata tamaa, alitafuta msaada kutoka kwa Mashahidi wa Yehova na upesi akatambua kwamba alikuwa amepata kweli. Baada ya kujifunza kwa bidii sana katika muda mfupi tu, alijiweka wakf kwa yeye Aliye Juu Zaidi afanye mapenzi yake. Jambo hilo lilimfanya mwanamume huyo kijana abadili kabisa maoni yake juu ya maisha. Kwa kujua kwamba furaha ya kweli inaweza kupatikana tu kwa kumtumikia Mungu kwa moyo wote, akawa mtangazaji wa habari njema za ufalme wa Mungu wa wakati wote. Tangu wakati huo amefurahia baraka nyingi katika kazi yake hiyo mpya, kutia na furaha yenye kuridhisha nafsi ambayo hakupata kuona hata kidogo alipokuwa akifuatia mambo ya kimwili.
Ndiyo, kuridhika kwa kweli na furaha vinapatikana tu kwa kuyaona mambo ya kimwili katika maoni yanayofaa. Ingawa yametolewa na Muumba wetu mwenye upendo ili tuyafurahie, bila shaka si ndicho chanzo cha furaha peke yake. Kwa kweli, kuyafuatia bila kumfikiria Mungu kunaweza tu kuongoza kwenye hali ya kupoteza furaha. Furaha ya kweli na kuridhika hupatikana tu kwa kumtumikia Muumba wetu mkuu na kwa kufanya mapenzi yake. Kufanya hivyo kunatuwezesha kupata furaha kamili kutokana na mambo ya kimwili aliyoyaumba Mungu pamoja na furaha kuu kutokana na mambo ya kiroho.