Nyota kwa Kweli Zina Ujumbe Fulani Kwako!
KAMA ilivyoonyeshwa katika makala zilizotangulia, ujapokuwa utukufu ambazo nyota hudhihirisha, mwanadamu alikusudiwa kuziona kama vile zilivyo tu—vitu visivyo na uhai vilivyowekwa katika mbingu na Muumba kwa kusudi lake. Hazikupasa kuabudiwa. Zikiwa sehemu kuu ya uumbaji mzuri ajabu wa Yehova ulio chini ya sheria zake, nyota zilipasa ‘kuhubiri utukufu wa Mungu’ na wakati uleule ziwe chanzo cha nuru kwa mwanadamu atekelezapo kusudi la Muumba kwake.—Zaburi 19:1; Kumbukumbu la Torati 4:19.
Katika Biblia twasoma hivi: “Asionekane kwako mtu . . . atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri, wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu. Kwa maana mtu atendaye hayo ni chukizo kwa BWANA.” (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Isaya alisema hivi: “Acha [washauri wako] wasimame, sasa, na wawaokoe, waabudu wa anga, wazitazamao nyota . . . Wamekuwa kama mabua.”—Isaya 47:13, 14, NW.
Yale Tuwezayo Kujifunza Kutokana na Nyota
Hata hivyo, nyota zisizo na uhai zaweza kutuambia jambo fulani ikiwa tuko tayari kusikiliza. Edwin Way Teale aliandika hivi: “Nyota zasema juu ya uduni wa binadamu katika umilele mrefu wa wakati.” Ndiyo, tung’amuapo kwamba zile nyota nyingi tuzionazo kwa macho yetu matupu katika usiku mwangavu zilionwa na babu zetu wa kale karne nyingi zilizopita, je, hiyo haitunyenyekezi? Je! hatuhisi kicho kwa Yule Mwadhamu aliyeziumba “hapo mwanzo” na baadaye akatokeza wanadamu? Mfalme Daudi wa Israeli aliandika hivi kwa kicho: “Nikiziangalia mbingu zako, kazi ya vidole vyako, mwezi na nyota ulizoziratibisha; mtu ni kitu gani hata umkumbuke, na binadamu hata umwangalie?” Mbingu zapasa zitunyenyekeze na kutufanya tujiulize tunafanya nini na maisha zetu.—Mwanzo 1:1; Zaburi 8:3, 4.
Katika pindi moja Daudi alisali hivi: “Unifundishe kuyatenda mapenzi yako, kwa maana ndiwe Mungu wangu.” (Zaburi 143:10) Kumbukumbu la maisha ya Daudi laonyesha kwamba sala yake ilijibiwa. Yeye alijifunza kufanya mapenzi ya Mungu kama yalivyopangiliwa katika Sheria Yake. Vilevile alijifunza kusudi la Muumba kwa wanadamu, naye akaandika juu yalo. “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo . . . Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani. . . . Jiepue na uovu, utende mema, na kukaa hata milele. . . . Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” Kujua kusudi hilo kuliambatana na daraka: “Jiepue na uovu, utende mema.”—Zaburi 37:10, 11, 27-29.
Nyota zina ujumbe uleule mmoja kwa wanadamu wote. Bila kuziabudu wala ‘kuziomba ushauri,’ twaweza kuona upendo, hekima, na nguvu za Muumba zikionyeshwa katika nyota hizo. Kujifunza astronomia, tofauti na unajimu, kwapasa kukazie kicho katika mioyo yetu. Lakini zaidi ya hilo, je, hakutii ndani yetu tamaa ya kujifunza mengi zaidi juu ya Mungu? Yeye ameandaa Neno lake, Biblia, kwa kusudi lilohilo. Ikiwa umetambua ujumbe huu utokao kwenye nyota, waweza kujifunza yale ambayo Yehova atafanyia wanadamu na, la maana zaidi, jinsi uwezavyo kushiriki katika baraka ambazo amewatayarishia. Ikiwa una maswali juu ya Mungu na kusudi la maisha, uwe huru kupashana habari na Mashahidi wa Yehova katika eneo lako, au uandikie anwani iliyo karibu zaidi iliyoonyeshwa katika ukurasa 5.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Nyota zaweza kutufundisha unyenyekevu