Vijana Huuliza. . .
Michezo ya Kusisimua—Je! Niijasirie?
“HUU utakuwa ndio wakati wa kuogopesha zaidi maishani mwako,” waambiwa usimamapo juu ya jukwaa ukitetemeka. Hesabu inaanza ikirudi nyuma: “Tano, nne, tatu, mbili, moja—RUKA!” Lile anguko lakukata pumzi kwa hofu. Waporomoka mbiombio kuelekea kile kinachoonekana kuwa kifo cha hakika, lakini kwa ghafula wahisi ukivutwa upesi sana na kamba fulani yenye kunyumbulika. Hisi ya msisimuko wa kitulizo yakukumba. Lo, umeokoka!
Huo ni mchezo wa kuruka banji.a Mchezo huo umevutia washiriki wakadiriwao kuwa milioni moja hadi mbili katika Marekani pekee. Huo ni mmoja tu kati ya michezo mingi ambayo hivi majuzi imekuja kupendwa na watu wengi zaidi—kupanda miamba, kujifunga chandarua mwilini na kujitupa chini kutoka kilimani upande ulio na upepo, kupita na chelezo katika maporomoko ya maji, na kujirusha kutoka katika ndege na kupita hewani ukiwa umefungiwa mwilini kibao cha kuelea kwa hewa kisha kutumia mwavuli mkubwa kutua ardhini, kutaja michache tu. “Miaka ya 1990 ndio mwongo wa michezo ya kusisimua,” asema mdhamini mmoja wa mchezo wa kuruka banji.
Utendaji mbalimbali wenye hatari haufanywi na matajiri tu. Watafuta-msisimuko sehemu za mijini hujitia katika matendo hatari (tena ya haramu) ya kujasiria mambo kama kupanda juu ya mitambo ya kupandisha na kushusha watu ikiwa mwendoni, kupita kasi sana katika mahandaki ya majengo makubwa, kutembea juu ya paa za mabehewa ya magari-moshi ya chini ya ardhi, na kuteleza katika ngazi za majengo zilizopakwa mafuta ya utelezi.
Uvutio Ni Nini?
“Mimi nitajaribu chochote cha kuniogopesha,” asema kijana Norbert. “Mimi hufurahia michezo yote—besiboli, mpira wa vikapu—lakini kuruka kutoka darajani kwa kushikiliwa na kamba ya banji kulinipa msisimuko wa woga! Ni raha isiyo na kifani.” Kijana Douglas akubali. “Michezo ile ya kawaida ina raha, lakini ni lazima utumie akili,” yeye asema. “Sikuzote yakuwekea masharti fulani. Mimi napenda ile hisi ya kuanguka. Kisha kule kuporomoka kwenyewe . . . Hupati kamwe hisi kama hiyo kwa michezo mingineyo.”
Michezo ya msisimuko haijaribu uwezo wako wa kiriadha tu; hiyo hukukabilisha na kifo uso kwa uso! Washiriki huonekana kufurahia ule msisimuko wa mwili ambao huchochewa na ongezeko la adrenali. Wastadi fulani hudai kwamba watu fulani wana tabia za urithi za Namna-T, au ni watafuta-msisimuko. Hata hivyo, vijana walio wengi hujitia katika aina fulani ya kujihatarisha; hiyo ndiyo njia yao ya kutahini mipaka ya uwezo wao na kusitawisha hali ya kujitumaini.
Kwa kusikitisha, si sikuzote ambapo vijana hutumia uamuzi mwema katika kufanya hivyo. “Fahari ya vijana ni nguvu zao,” yasema Mithali 20:29. Lakini yaonekana baadhi yao hufikiri kwamba nguvu zao hazina mipaka. Dakt. David Elkind asema kwamba mara nyingi matineja huamini “wao ni watu wa pekee na wasio na kifani—wasioongozwa na sheria za uelekeo wa kupatwa na yasiyotazamiwa ambazo zawahusu wengine. Imani hii ya kuwa watu wa pekee, wa kutoweza kupatwa na madhara, ndiyo huchangia zaidi maamuzi ya matineja kujasiria mambo ya hatari.” Dakt. Robert Butterworth vilevile asema hivi: “Ufanyapo jambo kama kujirusha chini kutoka angani, hiyo hukupa hisi ya kwamba umeweza kufanya yasiyowezekana, kujiamulia mwenyewe jambo liwezalo na lisiloweza kukupata maishani.”
Hata hivyo, kujasiria kwaweza pia kuongozwa na makusudio mabaya. Katika kitabu chake Childstress!, mtungaji Mary Susan Miller aonyesha kwamba vijana wengi wajasiri hujasiria kipumbavu kwa sababu ya kushindwa kabisa kukabiliana na mikazo ya maisha zao. Hivyo huenda michezo ya msisimuko ikafunua mielekezo ya kujiangamiza au hata kujiua. “Wao hujitia makusudi katika hali za hatari,” asema Miller, “kama kukaidi kwamba msiba hauwezi kuwapata.”
Je! Ni Hatari Kwelikweli?
Hata michezo ya msisimuko iwe ina uvutio gani, yaweza kuwa hatari. ‘Hata kuvuka barabara ni hatari,’ wengine hubisha. Lakini mtu anayevuka barabara hatafuti hatari au misisimuko kwa makusudi. Na ingawa michezo mingi, kama vile kuruka banji, umekuwa na usalama mzuri, kasoro zaweza kutokea. Mark Bracker, M.D., alieleza hilo namna hii: “Kuhusiana na mingi ya michezo hii yenye hatari sana, kasoro itokeapo yaweza kuwa na msiba mkubwa. Kwa kadiri msisimuko uwavyo mkubwa zaidi, kwa kawaida hatari iliyopo huwa kubwa zaidi pia, iwe ni kuruka kutoka ndani ya ndege kwa mwavuli mkubwa au kuelea angani kwa kuning’inizwa juu sana au kuendesha pikipiki.” Kijana mmoja mruka-banji mwenye umri wa miaka 20 aliruka kutoka kibofu chenye hewa ya joto huku kibofu hicho kikielea meta 58 juu ya ardhi. Tatizo lilikuwa nini? Kamba yake ilikuwa na urefu wa meta 79! Aliruka akafa kifo kibaya sana.
Ni kweli kwamba utendaji fulani-fulani, kama vile kuendesha pikipiki, waweza kufurahiwa kwa njia yenye usalama wa kadiri fulani na isiyoruka mipaka. Lakini mstadi mmoja wa tiba ya wanamichezo asema hivi juu ya watafuta-msisimuko: “Kadiri ujuzi wao uwavyo mwingi zaidi na zaidi, ndivyo wachaguavyo jambo gumu zaidi na zaidi, na mwishowe hujikuta wakiwa na jeraha.” Kijana mmoja aliungama hivi: “Mimi ni mraibu. Sasa ni vigumu zaidi kujiwekea kiwango cha kuwa na hofu na cha kusisimuka.”
Je! Inafaa kwa Wakristo?
Je! Biblia hukataza kabisa michezo yote? Sivyo. Mapumbavu ya kupita kiasi ndiyo hushutumiwa vikali. Kama ilivyoandikwa kwenye Mhubiri 7:17, Sulemani aliuliza hivi: “Kwani ufe kabla ya wakati wako?”
‘Maisha ni mafupi. Cheza kwa bidii,’ lahimiza tangazo moja la biashara ya viatu vya wanariadha. Lakini sisi tuna daraka la kuhazini uhai wetu kuelekea sisi wenyewe, wale tuwapendao, na Muumba wetu. Uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu. (Zaburi 36:9) Katika nyakati za Biblia adhabu nzito zingeweza kutolewa ikiwa uhai uliondolewa kwa aksidenti. (Kutoka 21:29; Hesabu 35:22-25) Kwa njia hiyo watu wa Mungu walitiwa moyo kuepuka majasirio ya bure tu.—Linganisha Kumbukumbu la Torati 22:8.
Leo vilevile Wakristo wana wajibu wa kuonyesha staha kwa uhai. Je! ingefaa kufuatia utendaji wa michezo ambao ungeweza kukutia katika majasirio yasiyo ya lazima? Wakati Shetani Ibilisi alipojaribu kumshawishi Yesu, alitoa hoja ya kwamba malaika wangemshika Yesu kama angejibwaga chini kutoka kwenye ukuta wa paa ya hekalu. Yesu alijibu hivi: “Usimjaribu Bwana Mungu wako.”—Mathayo 4:5-7.
Zaidi ya hilo, ijapokuwa huenda ukahisi ukiwa mwenye nguvu na afya nyingi, wewe si mtu asiyeweza kupatwa na madhara kamwe. Si jambo la kweli kusababu kwamba: ‘Hilo haliwezi kunipata mimi.’ Biblia hutuonya kwamba ‘wakati na tukio lisilotazamiwa hutupata sisi sote.’—Mhubiri 9:11, NW.
Tahadhari Kabla ya Hatari
Ni jambo la akili kufikiria kwa uzito matokeo ambayo yaweza kutokea ukiruka kutoka kwenye kreni, kujirusha nje ya ndege, au kufanya lolote liwezalo kuonekana kuwa la kujasiria mno. Usitegemee uvumi tu wala ripoti za idili za vijana wengine. (Mithali 14:15) Pata mambo ya uhakika.
Kwa kielelezo, aksidenti hutokea kwa kadiri gani katika mchezo fulani hususa? Ni tahadhari gani ambazo hufanywa? Mstadi mmoja asema hivi kuhusu mchezo wa kujizamisha chini sana ndani ya maji: “[Watu hufikiri kwamba] kuliacha eneo lenye hewa na kuingia ndani ya maji ni hatari . . . . Lakini ni hatari ikiwa tu wafanya hivyo bila kufunzwa ifaavyo.” Kwa hiyo yakupasa uulize hivi pia, Ni mazoezi na vifaa gani vihitajiwavyo kwa mchezo huu? Je! kuna manufaa zozote halali, kama kupata mazoezi ya mwili? Je! kunaweza kutokea hatari zozote, au lengo kuu la mchezo huo ni kukaidi kifo?
Ikiwa jibu ni kukaidi kifo, ungeweza kujiuliza kwa nini wewe huvutiwa sana na kujasiria. Je! hilo ni tokeo tu la ukosefu wa jambo la kupendeza au mkazo? Basi mbona usitafute njia salama zaidi, yenye kufaa zaidi ya kushughulika na hisia za jinsi hiyo?b Kitabu Teenage Stress chatukumbusha kwamba kujasiria ni “njia hatari ambayo mwishowe hukosa matokeo katika kukabiliana na mkazo usiofaa.”—Linganisha Mithali 21:17.
Baada ya kufanya utafiti kamili juu ya mambo—na kuongea na wazazi wako—huenda ukakata shauri kwamba ingekuwa vizuri zaidi ujiepushe kabisa na michezo ya kusisimua kupita kiasi. Huenda wazazi wako wakapendelea ufuatie utendaji mbalimbali ambao kwa asili si wenye kutisha sana uhai, kama vile kuendesha baiskeli, kupiga mbizi, kwa kutaja mambo machache tu. Bila shaka, hata utendaji mbalimbali ulio salama kwa kiasi waweza kuwa hatari ikiwa tahadhari zifaazo hazifanywi.
Hili lilipata kikundi kidogo cha vijana Wakristo walioamua kufanya matembezi marefu. Waliacha njia waliyokuwa wakifuata wakaanza kupanda ukingo mwembamba juu ya genge lililoinama sana. Muda si muda wakajipata ni kama wamenaswa mtegoni, wasiweze kwenda mbele wala kurudi nyuma kwa usalama. Kijana aliyekuwa akiongoza kikundi hicho akasikia kelele ya ghafula. Wawili kati ya waandamani wake walikuwa wameanguka na kufa. Lo, ni msiba ulioje!
Kwa hiyo tafadhali tahadhari! ‘Furahia ujana wako,’ ukifurahia nguvu na siha ambayo umebarikiwa kuwa nayo. (Mhubiri 11:9) Lakini kabla ya kukubali mwaliko kufanya jambo fulani la kujasiria hatari, fanya afanyalo Brian mchanga. Yeye asema hivi: “Mimi hujiuliza, ‘Yehova angehisije juu ya jambo hilo? Lingeonyeshaje mtazamo wangu kuelekea zawadi ya uhai ambayo amenipa?’” Ndiyo, pima uzito wa hatari zihusikazo, pekua makusudio yako. Haingefaa ufanye kinyume cha hilo kwa sababu uhai ni wa thamani kubwa sana.
[Maelezo ya Chini]
a “Kuruka banji” ni mchezo ambamo warukaji, wakiwa wameshikamanishwa na kamba ndefu yenye kunyumbuka iitwayo banji, huruka kutoka kwenye madaraja, kreni, na hata vibofu vilivyopuliziwa hewa yenye joto. Hii huwezesha kuwe na anguko la kuelekea chini moja-kwa-moja kabla ile kamba haijajikaza, ikizuia lile anguko la kasi.
b Ikiwa umeshuka moyo au unapambana na vihimizo vya kujiangamiza, kwa nini usiongee na mtu fulani upate msaada badala ya kufanya majasirio yasiyo ya lazima?—Ona “Vijana Huuliza . . . Je! Suluhisho Ni Kujiua?” katika toleo letu la Aprili 8, 1994 la Amkeni!
[Picha katika ukurasa wa 10]
Je! vijana Wakristo wapaswa kucheza michezo ya msisimuko kama kuruka banji?