Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Mikusanyiko ya Kimataifa Ningependa kuwashukuru kwa ule mfululizo “Ni Nini Kitakachounganisha Ulimwengu?” (Desemba 22, 1993) Nilifurahia kwelikweli ile sehemu iliyohusu mikusanyiko ya kimataifa ya Mashahidi wa Yehova katika Ulaya ya Mashariki. Ilitia moyo kusikia kwamba Wakristo fulani katika maeneo yaliyokumbwa na vita wangeweza kuhudhuria.
E. R., Marekani
Mume wangu na mimi pia ni wahudumu wa wakati wote; kwa hiyo, tulisikitika kwamba uwezo wetu wa kifedha haukutuwezesha kuwa wajumbe kwenye mkusanyiko wowote wa kimataifa. Hata hivyo, wakati wa kusoma makala zenu, mimi nilisafirishwa hadi ndani ya mazingira ya mkusanyiko. Ningeweza hata kujiwazia nikiimba kwa moyo mchangamfu pamoja na dada Wakristo walioonyeshwa katika ukurasa 9. Makala hiyo imenitia moyo kustahimili.
I. F., Ufaransa
Uwasiliano Baada ya kusoma ule mfululizo “Kuwasiliana Katika Ndoa” (Januari 22, 1994), niling’amua kwamba kwa muda wa miaka 28 ambayo nimefunga ndoa, nimekuwa simpi mke wangu upendo ahitajio. Kila mara alipoutafuta, niliupuuza kuwa ni ukosefu wa kukomaa. Makala hizi zilinisaidia mimi kuelewa jinsi hasa Mungu alivyowaumba wanawake. Wakati ujao, nitajaribu kumpa mke wangu upendo ahitajio. Asanteni kwa maarifa sahihi haya.
Y. K., Japani
Nashindwa kuwaeleza nilivyoufurahia mfululizo huo. Nilivutiwa sana na ule uchunguzi sahihi wa tofauti za kihisiamoyo na kisaikolojia zilizo kati ya wanaume na wanawake. Niliweza kujichunguza na kujielewa mwenyewe vizuri zaidi. Mimi sijafunga ndoa, lakini naamini kwamba makala hizi zitanisaidia niweze kuelewa vizuri zaidi maoni ya watu wengine.
D. R., Italia
Nyinyi mwasema kwamba kujitegemea ni jambo la thamani kubwa kwa wanaume. Lakini mimi najua wanawake kadhaa ambao pia huthamini kujitegemea. Nahangaishwa na jambo la kwamba nyinyi mwaonyesha fikira, hisia, na tamaa za wanaume kuwa tofauti kabisa na zile za wanawake.
U. B., Ujerumani
Makala hiyo ilikiri kwamba “yaweza kuwa vigumu kutaja tabia fulani hususa kuwa ni ya kiume ama ni ya kike” na kwamba “‘mwanamume halisi’ au ‘mwanamke halisi’ wasioweza kupatikana huenda wakapatikana tu katika kurasa za vitabu vya saikolojia.” Tabia ambazo wenzi wa ndoa “Musa” na “Maria” walitajwa kuwa nazo zilisaidia kuwa kielezi tu cha jinsi waume na wake mmoja-mmoja watofautianavyo katika namna za kuwasiliana.—MHARIRI.
Vitu vya Kuchezea vya Afrika Ile makala “Vitu vya Kuchezea vya Afrika Bila Malipo” (Machi 22, 1993) ilikuwa kama tunzo nzuri ajabu ya kukumbuka utoto wangu. Katika miji na vijiji vyetu vya Afrika, vitu vya kuchezea havikupatikana kwa watoto wote. Kwa hiyo sisi tulitumia wakati wetu tukitengeneza vitu vyetu wenyewe vya kuchezea ili tuwe kama watoto weupe walio matajiri. Ingawa hivyo, wao hawakuthamini vitu vyetu vya kuchezea vilivyotengenezewa nyumbani. Vyovyote vile, makala hiyo iliniletea shangwe kubwa.
A. A., Kamerun
Kutatua Matatizo Ninawaandikia kutoa shukrani yangu kwa ajili ya makala nzuri nyingi za “Vijana Huuliza . . . ” ambazo nyinyi hutuandalia. Mfululizo huo huwa ndilo jambo la kwanza mimi kuangalia nipokeapo toleo la karibuni zaidi la Amkeni! Hasa nilithamini ile makala “Ni Nani Awezaye Kunisaidia Kusuluhisha Matatizo Yangu?” (Desemba 8, 1993) Mimi ni mwanafunzi anayeelekea kuhitimu shule ya sekondari, nami hulemewa sana na kufanya maamuzi yahusuyo wakati wangu ujao. Wazazi wangu na mimi tumekuwa na mawasiliano ya wazi sikuzote, hata hivyo nyakati fulani bado mimi huhisi kwamba hawaelewi. Makala hii ilinisaidia kuona jinsi lilivyo jambo la maana kuomba ushauri wao na kuongea nao juu ya hisia na mahangaiko yangu.
H. L., Marekani