Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Kuwasiliana Leo nilipokea toleo la Januari 22, 1994 lenye ule mfululizo “Kuwasiliana Katika Ndoa.” Yawezekana sana huu ndio mfululizo bora zaidi wa makala ambao nimepata kusoma. Mume wangu nami tumekuwa katika ndoa mwaka mmoja na nusu. Tuna uhusiano mwema sana na tu wenye furaha sana, ingawa nyakati fulani uwasiliano usiofaa hutokea. Amkeni! liliandaa mafahamisho mazuri kwa nini hili hutokea. Nianzapo kuzisoma makala kwa mara ya tatu, acheni nishukuru Yehova na nyinyi kwa kuchapisha habari hizo za wakati ufaao.
C. M., Marekani
Mume wangu anaendelea vema akiwa mzee Mkristo na mweneza-evanjeli wa wakati wote. Hata hivyo, tumekuwa na pengo la kuwasiliana tangu tulipofunga ndoa na tumekuwa na nyakati fulani za kutatiza. Makala hizi zilituonyesha wazi visababishi vya tatizo hilo. Tuna uhakika zitatusaidia kuboresha uhusiano wetu.
C. A., Japani
Nilipokuwa nikisoma maitikio ya “Maria,” niling’amua singaliweza kuelezea hisia zangu vizuri kuliko alivyozieleza yeye. Hilohilo laweza kusemwa juu ya mume wangu na “Musa.” Makala hii yatatua kiini cha tatizo lenyewe, badala ya kutatua dalili zenyewe tu. Pia nilipendezwa na njia ya kuvutia ambayo makala zilitokeza habari hii ya maana.
E. F., Italia
Hata ingawa nina miaka 17 tu sasa hivi na sitaki kufunga ndoa kwa miaka kadhaa, bado nilithamini sana mpenyo huu wa habari juu ya kwa nini watu hutenda watendavyo. Ninapanga kuweka makala hii niwe nikiisomasoma muda wa miaka michache ijayo. Nitaihitaji hasa niwapo tayari kufunga ndoa!
N. B., Marekani
Baba yangu afanana sana na “Musa.” Lakini sasa naelewa kwamba ajinyamaziapo asiongee nami, hiyo ni haki yake. Hata ingawa makala hiyo iliangazia nuru, nahofu atatumia makala hiyo kuhakikisha kwamba afanyalo ni sawa tu.
A. B., Marekani
Makala hizo zilijitahidi kusaidia wasomaji waelewe kwa nini wanaume na wanawake huelekea kuhisi au kutenda kwa njia fulani. Hata hivyo, hatukukusudia kudokeza kwamba ama wanaume ama wanawake wana haki fulani ya kutowasiliana au ya tabia isiyofaa. Maandiko huhimiza akina baba waepuke ‘kuwachokoza watoto wao.’ (Wakolosai 3:21) Hiyo ingekataza kabisa kujitia katika vipindi virefu isivyofaa vya unyamavu wakati watoto watakapo na wahitajipo mwelekezo wa wazazi.—Mhariri.
Nina uhakika kwamba lazima barua ziwe zinamiminika zikiwa na maelezo chanya juu ya makala hizi. Tafadhali ongezeni maelezo yangu. Katika ile makala juu ya “Musa” na “Maria,” mngaliweza kuweka majina ya mke wangu nami badala ya “Musa” na “Maria.” Laiti ningaliweza kuelewa hisia za mke wangu! Nilikuwa sawasawa na “Musa,” nikijaribu kutimiza mahitaji yake lakini nikifanya hivyo kama vile ningalitaka mahitaji yangu mwenyewe yatimizwe. Sasa mke wangu wa miaka 20 amenitaliki. Labda moyo wa mke wangu utaguswa na makala hizi, nasi tuweze kujaribu kujenga ndoa yetu upya.
J. K., Marekani
Fumbo la Biblia Nilifurahia sana ule ukurasa “Je! Umepata Kujiuliza?” katika toleo la Januari 8, 1994. Nilifanya nakala za ukurasa huo nikapelekea marafiki, washiriki wa familia, na watu wengine wenye kupendezwa. Niliwatia moyo wachunguze kila Andiko na kuandika maswali yoyote wawezayo kuwa nayo. Hicho ni chombo kizuri sana cha kufanya mazungumzo ya Biblia na watu wa jinsi hiyo. Tafadhali endeleeni kuchapisha ukurasa huo!
M. S., Marekani