Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 1/22 kur. 3-7
  • Waume na Wake—Je! Kweli Wao Huwasiliana kwa Njia Tofauti?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Waume na Wake—Je! Kweli Wao Huwasiliana kwa Njia Tofauti?
  • Amkeni!—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je! Ni kwa Sababu ya Tofauti ya Jinsia?
  • Maoni ya Mwanamume
  • Maoni ya Mwanamke
  • Mambo Waliyoona Kupitia Macho Yao Wenyewe
  • Kuona Mambo Kupitia Macho ya Kila Mmoja
  • Kutoka kwa Wasomaji Wetu
    Amkeni!—1994
  • Watu Wanawezaje Kuishi kwa Amani?
    Amkeni!—2014
  • Tulipata ‘Lulu Yenye Thamani Kubwa’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
  • Kutoka kwa Wasomaji Wetu
    Amkeni!—1994
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 1/22 kur. 3-7

Waume na Wake—Je! Kweli Wao Huwasiliana kwa Njia Tofauti?

EBU wazia tu kwamba Juma alijikokota kuingia ndani ya ofisi ya Musa, mabega yake yakiwa yamelegea kwa sababu ya mahangaiko yake. Musa alimtazama rafiki yake kwa upole na kumngojea aseme. “Sijui kama ninaweza kufanikiwa katika mkataba huu wa biashara,” Juma alisema akihema. “Kuna magumu mengi sana, na ofisi kuu inanikaza kwelikweli.” “Unahangaikia nini, Juma?” Musa aliuliza kwa uhakika. “Wajua wewe ndiye mtu bora zaidi kwa kazi hiyo, na mameneja wa ofisi kuu wajua hivyo pia. Wewe tulia tu. Wafikiri hilo ni tatizo kubwa? Mwezi uliopita tu . . .” Musa akamsimulia mambo madogo-madogo yanayochekesha ya mkasa wake mdogo na upesi rafiki yake aliondoka ofisini akicheka na akiwa hana mahangaiko. Musa alifurahi kusaidia.

Wazia pia aliporudi nyumbani alasiri hiyo, Musa angeweza kuona mara hiyo kwamba mke wake, Maria alikuwa amekasirika pia. Alimsalimia mke wake kwa uchangamfu usio wa kawaida na kisha akangojea aseme matatizo yake. Baada ya ukimya wa muda wenye wasiwasi mwingi, mke alianza kusema maneno haya: “Siwezi kuvumilia tena! Huyo mkubwa wetu mpya wa kazi ni mdhalimu!” Musa alimketisha, akamkumbatia mkewe, akisema: “Mpenzi, usikasirike sana. Hiyo ni kazi tu. Wakubwa wa kazi huwa hivyo tu. Ungesikia jinsi mkubwa wangu alinipigia kelele kwa muda mrefu leo. Lakini kama huwezani na hali hiyo, basi waweza kuacha kazi hiyo.”

“Wewe hata hujali nihisivyo!” Maria akajibu upesi. “Wewe hunisikilizi kamwe! Siwezi kuacha kazi! Huleti fedha za kutosha nyumbani!” Alikimbilia chumba cha kulala na kulia sana. Musa alisimama nyuma ya mlango uliofungwa wa chumba cha kulala, akiwa amepigwa na bumbuazi. Ni kwa nini mke huyo aliitika kwa njia tofauti kwa maneno ya Musa yenye kufariji?

Je! Ni kwa Sababu ya Tofauti ya Jinsia?

Watu fulani wangesema kwamba tofauti iliyoko katika vielezi hivyo ni ukweli mmoja tu sahili: Juma ni mwanamume; Maria ni mwanamke. Watafiti wa lugha waamini kwamba matatizo ya uwasiliano katika ndoa hutokea kwa sababu ya jinsia. Vitabu kama vile You Just Don’t Understand na Men Are From Mars, Women Are From Venus huendeleza ile nadharia kwamba ingawa wanaume na wanawake husema lugha ileile moja, wao huwa na njia zao tofauti za kuwasiliana.[1]

Bila shaka, Yehova alipomuumba mwanamke kutoka kwa mwanamume, mwanamke hakuwa tu mfano wa mwanamume aliyefanyiwa marekebisho madogo tu. Mwanamume na mwanamke waliumbwa kwa ustadi na kwa uangalifu ili wakamilishane mmoja na mwenzake—kimwili, kihisia-moyo, kiakili, kiroho. Ongezea tofauti hizo za asili mambo yahusuyo malezi ya mtu na maono yake ya maishani pamoja na kugeuzwa kwa watu kupitia utamaduni, mazingira, na maoni ya jamii ya hali ya kiume au kike. Kwa sababu ya mavutano hayo, yawezekana kutambua vigezo fulani katika njia ambazo wanaume na wanawake huwasiliana. Lakini “mwanamume halisi” au “mwanamke halisi” wasioweza kupatikana huenda wakapatikana tu katika kurasa za vitabu vya saikolojia.[2]

Wanawake wajulikana sana kwa wepesi wao wa hisia, lakini wanaume wengi ni wenye wororo sana wanaposhughulika na watu. Wanaume waweza kusemwa kuwa wao hufikiri vizuri, lakini mara nyingi wanawake wana muono wa hali ya juu na wenye kuchanganua sana. Kwa hiyo ingawa yaweza kuwa vigumu kutaja tabia fulani hususa kuwa ni ya kiume ama ni ya kike pekee, kuna uhakika mmoja: Kuwa na utambuzi juu ya jinsi mwingine aonavyo mambo kwaweza kutokeza tofauti ya ama kuishi pamoja kwa amani ama kupigana, hasa katika ndoa.

Tatizo la uwasiliano la kila siku kati ya mwanamume na mwanamke katika ndoa ni gumu sana. Waume wengi wenye utambuzi wajua kwamba swali lionekanalo kuwa rahisi kama “Waonaje mtindo wangu mpya wa nywele?” laweza kuwa na hatari nyingi sana. Wake wengi wenye busara hujifunza kuepuka kuuliza waume zao kila wakati, “Mbona usiulize tu njia?” waume zao wanapopotea njia wasafiripo. Badala ya kudharau vitabia fulani vya mwenzi wako na kushikilia kwa ushupavu vitabia vyako mwenyewe eti kwa sababu “ndivyo nilivyo,” mume na mke wanaopendana hutazama ndani zaidi ya vitabia hivyo. Huo si uchunguzi wenye ukatili wa njia ya kuwasiliana ya kila mmoja bali ni mtazamo mchangamfu wa moyo na akili wa kila mmoja.

Kama vile kila mtu alivyo wa kipekee, ndivyo ilivyo na watu wawili walio katika ndoa. Kupatana kwa kweli kwa akili na mioyo ya watu tofauti hakutokei tu kiaksidenti bali kwahitaji kazi yenye bidii kwa sababu ya asili yetu ya kibinadamu isiyokamilika. Mathalani, ni rahisi sana kudhania kwamba watu wengine waona mambo jinsi tunavyoyaona. Mara nyingi sisi hutimiza mahitaji ya watu wengine kwa jinsi ambavyo tungependa tutimiziwe hayo, labda tukijaribu kufuata ile Kanuni ya Kidhahabu, “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Hata hivyo, Yesu hakumaanisha kwamba utakalo wewe lafaa wengine. Badala ya hivyo, ungetaka watu watoe unachohitaji wewe au kutaka. Kwa hiyo wapaswa utoe wanachohitaji wao. Hilo ni muhimu hasa katika ndoa, kwa sababu kila mmoja ameapa kutimiza mahitaji ya mwenzi wake wa ndoa kadiri iwezekanavyo.

Maria na Musa wameapa hivyo. Na muungano wao wa ndoa wa miaka miwili umekuwa wenye furaha. Hata hivyo, ingawa wanahisi kwamba wajuana vizuri sana, nyakati nyingine hali hutokea ambazo hufunua pengo kubwa katika uwasiliano ambalo makusudi mazuri pekee hayawezi kuziba. “Moyo wake mwenye hekima hufundisha kinywa chake,” yasema Mithali 16:23. Naam, kuwa na utambuzi katika kuwasiliana ndiko ufunguo unaohitajiwa. Ebu tuone utafungua milango gani kwa Musa na Maria.

Maoni ya Mwanamume

Musa hufanya kazi katika ulimwengu wenye mashindano makali ambapo ni lazima kila mtu ajithibitishe katika jamii, awe ni mfanyakazi wa chini au mkubwa mahali fulani. Uwasiliano wamfanya athibitishe cheo chake, uwezo wake, ustadi wake, au kufaa kwake. Uhuru wake ni wenye thamani kubwa kwake. Kwa hiyo akipewa maagizo kwa njia ya kuamriwa, Musa hujikuta akiwa mkaidi. Ule ujumbe wa kichinichini “Hufanyi kazi yako” wamfanya awe mkaidi, hata kama ombi hilo lilikuwa lenye kufaa.[3]

Kwa msingi Musa huzungumza ili kupashana habari. Yeye hupenda kuongea juu ya mambo ya hakika, mawazo, na mambo mapya ambayo amejifunza.[4]

Anaposikiliza, Musa humkatiza msemaji mara chache sana, hata kwa maitikio madogo, kama “eh-eeh, ndiyo,” kwa sababu anasikiliza kwa uangalifu. Lakini asipokubali jambo, huenda asisite kusema hivyo, hasa kwa rafiki. Hilo laonyesha kwamba yeye apendezwa na mambo asemayo rafiki yake, akichimba zaidi.[5]

Musa akiwa na tatizo, yeye hupendelea kujisuluhishia matatizo yake. Kwa hiyo aweza kujitenga na kila mtu na kila kitu. Au aweza kutafuta kustarehe akijaribu kusahau tatizo lake kwa muda. Atalizungumzia ikiwa tu anatafuta shauri.[6]

Mtu akimjia Musa akiwa na tatizo kama alivyofanya Juma, Musa atambua kwamba ni kazi yake kusaidia, akiwa mwangalifu asifanye rafiki yake ajione kuwa mtu asiyejiweza. Mara nyingi atashiriki baadhi ya matatizo yake anapomshauri ili rafiki yake asihisi mpweke katika tatizo hilo.[7]

Musa hupenda kushiriki katika utendaji mbalimbali pamoja na marafiki. Kwake, urafiki wamaanisha kufanya vitu pamoja.[8]

Kwa Musa, nyumbani ni mahali pa usalama kutokana na utendaji wa nje, mahali ambapo hapamlazimu kusema ili kujithibitisha, mahali ambapo amekubaliwa, ametumainiwa, amependwa, na kuthaminiwa. Hata hivyo, mara moja-moja Musa huona uhitaji wake wa kuwa peke yake. Huenda kufanya hivyo kusisababishwe na Maria au kitu chochote alichofanya. Yeye ahitaji tu muda fulani akiwa peke yake. Musa hupata ugumu wa kumfunulia mke wake hofu zake, ukosefu wake wa usalama, na uchungu wake wa moyoni. Yeye hataki mke wake ahangaike. Kazi yake ni kumtunza na kumlinda, na ataka Maria amtumaini kwamba atafanya hivyo. Ingawa Musa ataka utegemezo, yeye hataki kuonewa huruma. Kufanya hivyo kwamfanya ajihisi kuwa mtu asiyejiweza au asiyefaa.[9]

Maoni ya Mwanamke

Maria ajiona mwenyewe kuwa mtu katika ulimwengu wake wa urafiki na wengine. Kwa maoni yake ni muhimu kufanyiza na kuimarisha vifungo vya mahusiano hayo. Mazungumzo ni njia muhimu ya kufanyiza na kuhakikisha ukaribu wa uhusiano.[10]

Ni jambo la asili kwa Maria kutegemea mwingine. Yeye ahisi anapendwa Musa aulizapo maoni yake kabla ya kufanya uamuzi fulani, ingawa yeye ataka mume wake achukue uongozi. Ikiwa ni lazima afanye uamuzi, yeye hupenda kushauriana kwanza na mumewe, si ili mume amwambie jambo la kufanya, bali ili amwonyeshe ukaribiano wake na jinsi anavyomtegemea yeye.[11]

Ni vigumu sana kwa Maria kusema moja kwa moja kwamba anahitaji kitu fulani. Hataki kuwa mwenye chokochoko kwa Musa au kumfanya Musa ahisi kuwa yeye Maria ni mwenye huzuni. Badala ya hivyo, yeye angojea aonwe au adokeza mambo kichinichini.[12]

Maria anapozungumza, yeye hufikiria mambo mengi madogo-madogo sana na kuuliza maswali mengi. Hilo ni jambo la asili kwa sababu ya wepesi wake wa hisia na kupendezwa kwake kwingi na watu na mahusiano.[13]

Maria asikilizapo, yeye huitikia maneno ya msemaji kwa maneno mafupi ya mshangao, maitikio, au maswali ya kuonyesha kwamba anasikiliza msemaji na anajali maneno anayosema huyo.[14]

Yeye hujitahidi kujua pasipo kuambiwa mahitaji ya watu. Kutoa msaada bila kuombwa ni njia nzuri ajabu ya kuonyesha upendo. Yeye ataka hasa kusaidia mume wake kukua na kufanya maendeleo.[15]

Maria anapokabili tatizo, anaweza kuhisi ameshindwa na hali. Ni lazima aseme, si hasa kwamba apate suluhisho, bali aeleze hisia zake. Ahitaji kujua kwamba mtu fulani anaelewa na kujali hali yake. Anapokuwa na hisia yenye kusisimka, Maria hutoa maneno makali yenye kutazamisha. Hamaanishi kihalisi anaposema: “Wewe husikilizi kamwe!”[16]

Rafiki wa Maria wa wakati wa utotoni wa karibu zaidi hakuwa yule ambaye alifanya mambo pamoja naye bali yule Maria alisema naye kila kitu. Kwa hiyo katika ndoa yeye hapendezwi sana na utendaji mbalimbali wa nje kuliko jinsi apendezwavyo na msikilizaji mwenye huruma ambaye yeye aweza kumweleza hisia zake.[17]

Nyumbani ni mahali ambapo Maria aweza kusema bila kuhukumiwa. Yeye hasiti kumfunulia Musa hofu zake na matatizo yake. Ikiwa anahitaji msaada yeye haoni haya kuutaja kwa sababu anatumaini kwamba mume wake yuko kwa ajili yake na humjali kiasi cha kuweza kumsikiliza.[18]

Maria huhisi kupendwa na mwenye usalama katika ndoa yake. Lakini mara kwa mara, pasipo sababu yoyote, yeye huanza kuhisi ukosefu wa usalama na asiyependwa na yeye huhitaji kwa haraka uhakikisho na urafiki.[19]

Naam, Musa na Maria, ambao wanakamilishana sana, ni watu tofauti sana. Tofauti zilizoko kati yao hutokeza uwezekano wa kuelewana vibaya, hata kama wote huenda wakawa na makusudi mazuri ya kupendana na kutegemezana. Kama tungesikia maoni ya kila mmoja juu ya hali iliyotajwa juu, wao wangesemaje?

Mambo Waliyoona Kupitia Macho Yao Wenyewe

“Mara tu nilipofika kutoka kazini, nilitambua kwamba Maria alikuwa amekasirika,” Musa angesema. “Nilidhani kwamba mara atakapokuwa tayari, angeniambia sababu. Tatizo hilo halikuonekana kuwa kubwa sana kwangu. Nilifikiri kwamba nikimsaidia tu aone kwamba hakuhitaji kukasirika sana na kwamba suluhisho lilikuwa rahisi, angehisi vema zaidi. Niliumia sana baada ya kumsikiliza, aliposema, ‘Wewe hunisikilizi kamwe!’ Nilihisi ni kama ananilaumu kwa ajili ya mfadhaiko wake wote!”[20]

“Siku nzima imekuwa yenye msiba mkubwa,” Maria angeeleza. “Nilijua kwamba halikuwa kosa la Musa. Lakini aliporudi nyumbani akiwa mchangamfu, nilihisi anapuuza kukasirika kwangu. Mbona hakuniuliza tatizo langu? Nilipomwambia tatizo lenyewe, kwa msingi yeye alidokeza tu kwamba nilikuwa mpumbavu, kwamba hilo lilikuwa ni jambo dogo tu. Badala ya kuniambia anaelewa jinsi ninavyohisi, Musa, msuluhisha matatizo, aliniambia jinsi ya kusuluhisha tatizo langu. Mimi sikutaka suluhisho, nilitaka nihurumiwe!”[21]

Ujapokuwa mgogoro huo wa muda tu, Musa na Maria wapendana sana. Ni utambuzi gani utawasaidia waonyeshe upendo kwa wazi zaidi?

Kuona Mambo Kupitia Macho ya Kila Mmoja

Musa alihisi kwamba ingekuwa ni kumwingilia Maria kumuuliza tatizo lake, kwa hiyo alimfanyia jambo ambalo kwa kawaida angetaka wengine wamfanyie. Alimngojea amwambie wazi tatizo lake. Sasa Maria alikuwa amekasirika si kwa sababu tu ya tatizo lake bali kwa sababu Musa alionekana kuwa amepuuza uhitaji wake wa kutegemezwa. Yeye hakuona ukimya wake kuwa ishara ya staha yake yenye uanana—yeye aliliona kuwa kutojali. Hatimaye Maria aliposema, Musa alisikiliza bila kumkatiza. Lakini alihisi kwamba Musa hasa hakuwa akisikia hisia zake. Kisha akatoa suluhisho badala ya hisia mwenzi. Jambo hilo lilimfanya ahisi hivi: ‘Hufai kuwa na hisia hizo; waitikia mambo kupita kiasi. Waona jinsi lilivyo jambo rahisi kusuluhisha tatizo hili dogo?’

Mambo yangekuwa tofauti kama nini ikiwa kila mmoja wao angeweza kuona mambo kwa maoni ya mwingine! Labda mambo yangeenda hivi:

Musa aja nyumbani na kumpata Maria akiwa amekasirika. “Kuna tatizo gani, mpenzi?” auliza kwa upole. Machozi yaanza kutiririka, nayo maneno yaanza kutoka. Maria hasemi, “Ni kosa lako!” au kwamba tu Musa hamtoshelezi. Musa amkumbatia na kusikiliza kwa saburi. Anapomaliza kusema, Musa asema: “Pole kwa kujisikia umeudhika. Naweza kuona sababu inayokufanya ukasirike.” Maria ajibu: “Asante sana kwa kusikiliza. Nahisi vema zaidi kwa kujua kwamba unaelewa hali yangu.”

Inasikitisha kwamba badala ya kusuluhisha tofauti zao, waume na wake wengi huchagua kumaliza tu ndoa zao kwa talaka. Ukosefu wa kuwasiliana ni jambo linaloangamiza kabisa familia nyingi. Mabishano hutokea kiasi cha kutikisa misingi halisi ya ndoa. Hilo hutokeaje? Makala ifuatayo yasema jinsi jambo hilo hutokea na jinsi ya kuliepuka.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki