Chanzo cha Mabishano
MKE ahitaji kueleza hisia zake. Mume ataka kutoa masuluhisho. Yale mamilioni ya mabishano katika ndoa ambayo yametokea kwa muda wa wakati ambao umepita huenda yalikuwa katika hali tofauti-tofauti, lakini mara nyingi mabishano hayo yamekuwa na utofauti katika mambo fulani machache ya msingi. Kuelewa maoni tofauti ya mwenzi wako wa ndoa au njia yake tofauti ya kuwasiliana kwaweza kusaidia kupunguza magombano hayo makali yawe mambo madogo-madogo tu katika nyumba yenye furaha.
“Usitawale Maisha Yangu!”
Mwanamke mwenye kutawala na mwenye chokochoko kwa mume aweza kuwa mfano wa visa vya waume kujikuta wamebanwa kwa kila hali kwa mashauri, maombi, na uchambuzi. Biblia hukiri kuwapo kwa hisia kama hizo, isemapo hivi: “Ugomvi wa mke [ni] kama kutona-tona daima.” (Mithali 19:13) Mke aweza kutoa ombi ambalo mume wake apuuza kwa ukimya kwa sababu ambazo mke hajui. Akifikiri kwamba mume hakumsikia, sasa amwambia mume jambo la kufanya. Mume apuuza hata zaidi. Je! huyo ni mke mwenye chokochoko na mume mwenye kutawalwa na mke? Au ni watu wawili ambao hawajawasiliana vizuri tu?[1]
Kwa maoni ya mke, yeye aonyesha upendo wake kwa njia bora zaidi kwa mume wake anapotoa shauri lenye kusaidia. Kwa maoni ya mume wake, mke huyo amtawala-tawala sana na kudokeza kwamba yeye hajiwezi. Kwa maoni ya mke, maneno kama “Usisahau mfuko wako” ni wonyesho wa kujali kwake, akihakikisha kwamba mume wake ana kitu anachohitaji. Jambo hilo lamkumbusha mume wake mama yake akimwambia kwa sauti kutoka mlangoni, “Ulichukua sweta yako?”
Mke mchovu aweza kusema hivi kwa upole, “Je! wataka kula hotelini usiku huu?” akimaanisha hasa, “Mbona usinipeleke hotelini? Nimechoka mno kuweza kupika.” Lakini mume wake mwenye kujitolea sana aweza kutumia nafasi hiyo kupongeza upishi wake na kusisitiza kwamba apenda upishi wake kuliko upishi mwingine wowote. Au huenda mume akahisi, ‘Anajaribu kunitawala!’ Wakati uo huo, mke aweza kujiambia hivi kwa udhiko, ‘Kwa nini ni lazima niombe?’[2]
“Hunipendi!”
“Mbona afikirie hivyo?” amaka mume anayefadhaika na kutatanishwa. “Ninafanya kazi, nalipia matumizi ya nyumbani, na nyakati nyingine mimi hata humletea maua!”
Ingawa wanadamu wote wahitaji kuhisi kupendwa, mwanamke ana uhitaji wa pekee wa kuhakikishiwa upendo kila mara. Huenda asiseme hivyo kwa sauti, lakini ndani aweza kuhisi akiwa kama mzigo usiotakikana, hasa wakati kipindi chake cha hedhi kinapomfanya ahisi mshuko wa moyo kwa muda. Katika pindi kama hizo mume wake huenda akamwepuka akifikiri kwamba mke wake ahitaji wakati wa kuwa peke yake. Mke naye huenda akaona ukosefu wake wa kuwa karibu kuwa uthibitisho wa hofu yake kuu—kwamba hampendi tena. Huenda mke akamfokea, akijaribu kumlazimisha ampende na kumtegemeza.[3]
“Kuna Tatizo Gani, Mpenzi?”
Njia ya mwanamume ya kusuluhisha tatizo yaweza kuwa ni kutafuta mahali pakimya ili alifikirie tatizo hilo. Mwanamke huenda akahisi tu kwamba kuna mikazo fulani na kuitikia mambo kwa kujaribu kumtia mume wake moyo amweleze tatizo lenyewe. Hata jitihada hizo ziwe zenye makusudi mazuri kama nini, mume huenda akaziona kuwa ni za kumwingilia na zenye kumshusha. Mume anapojitenga afikirie tatizo lake, aangalia nyuma na kuona mke wake mwaminifu akimfuata mbio. Yeye asikia sauti yake yenye upendo ikisema: “Mpenzi, kuna kitu kibaya? Kuna tatizo gani? Tuzungumze juu ya tatizo hilo.”
Mke asipojibiwa, anaweza kuhisi vibaya. Anapokuwa na tatizo, yeye hutaka azungumze pamoja na mume. Lakini mtu apendaye hataki kumwambia hisia zake. “Ni lazima iwe hanipendi tena” huenda ukawa mkataa wake. Kwa hiyo hatimaye yule mtu asiye na habari anapotoka katika ulimwengu wake wa ndani, akiwa ameridhika na suluhisho alilopata, apata pia mke aliyekasirishwa ambaye yuko tayari kumpinga kwa sababu alimwacha bila kumshirikisha katika tatizo lake bali si mke mwenye upendo mwenye kumhangaikia aliyempuuza.[4]
“Wewe Hunisikilizi Kamwe!”
Shtaka hilo laonekana kuwa la ajabu. Mume aona kwamba yeye husikiliza tu. Lakini mke wake asemapo, mke ahisi kwamba maneno yake yanachunguzwa na kuchanganuliwa kama kompyuta inayofanya hesabu. Shuku zake zathibitishwa wakati, akiwa katikati ya sentensi, mume asema: “Naam, mbona usifanye tu . . . ?”
Mke anapomjia mume wake na tatizo, mara nyingi sana yeye hamlaumu mume wala hamwendei ili kupata suluhisho kutoka kwake. Jambo ahitajilo zaidi ni kusikilizwa kwa hisia-mwenzi, si tu mambo ya hakika yasiyomfaa, bali hisia zake juu ya jambo hilo. Kisha hataki shauri, bali kuthibitishiwa kwamba hisia zake zafaa. Hiyo ndiyo sababu waume wenye makusudi mazuri wametokeza mfyatuko waliposema tu hivi: “Mpenzi, hupaswi kuhisi hivyo. Si jambo baya hivyo.”
Mara nyingi, watu hutarajia wenzi wao wa ndoa wajue wanayofikiria. “Ndoa yetu imekuwa ya miaka 25,” akasema mtu mmoja. “Kama hajui kitu ninachotaka kufikia sasa, basi ni lazima mke awe hajali au yeye si mwangalifu.” Mtungaji mmoja wa vitabu asema hivi katika kitabu chake cha uhusiano katika ndoa: “Mume na mke wakiwa hawaambiani mambo wanayotaka na kuchambuana kila wakati kwa kukosa kufanya jambo fulani, haishangazi kwamba ile roho ya upendo na ushirikiano hupotea. Mahali payo huchukuliwa na . . . mng’ang’ano wa mamlaka, unaofanya kila mwenzi ajaribu kulazimisha mwenzake atimize mahitaji yake.”[5]
“Hujali Kabisa Daraka Lako!”
Huenda mke asiseme hivyo moja kwa moja kwa mume wake, lakini aweza kulidokeza jambo hilo waziwazi katika sauti yake. “Kwa nini umechelewa sana?” yaweza kuonwa kuwa ombi la kutaka kujua habari. Lakini yaelekea zaidi kwamba mtazamo wake wenye kushuku na mikono yake iliyoshika kiuno yamwambia mume wake hivi: “Wewe kijana asiyechukua daraka, umenifanya nihangaike. Mbona hukunipigia simu? Wewe hufikirii kabisa hisia za wengine! Sasa mpango wetu wa mlo umeharibika!”[6]
Bila shaka, mke huyo asema ukweli kuhusu chakula. Lakini mabishano yakitokea, je, uhusiano wao utakuwa hatarini vilevile? “Mabishano mengi hayatokei kwa sababu ya watu wawili kukosa kusikilizana, bali hutokea kwa sababu mume ahisi kwamba mke anakataa maoni yake ama mke hapendi jinsi mume anavyoongea naye,” asema Dakt. John Gray.[6a]
Watu wengine wahisi kwamba mtu apaswa kuwa huru kusema jambo lolote analofikiri bila kujizuia nyumbani. Lakini mwasilianaji mzuri hutafuta upatano na kupata amani, akizingatia hisia za msikilizaji. Kidogo twaweza kulinganisha mazungumzo kama hayo na kumpatia mwenzi wako wa ndoa glasi ya maji baridi badala ya kumwaga maji hayo kwenye uso wake. Twaweza kusema kwamba tofauti iko katika namna tunavyozungumza.[7]
Kutumia maneno ya Wakolosai 3:12-14 kutaondoa kabisa mabishano na kuleta familia yenye furaha: “Jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake: kama Bwana [Yehova, New World Translation] alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi. Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.”
[Picha katika ukurasa wa 9]
Mume atetea mambo ya hakika, mke atetea hisia zake