Mahali Ambapo Wazazi na Watoto Husikiliza na Kujifunza Pamoja
NA MLETA-HABARI ZA AMKENI! KATIKA JAPANI
“TUKIWA kampuni ya kutunza majumba, twaaibika, lakini [stediamu] yaonekana kuwa safi zaidi wakati nyinyi watu [mnapoisafisha].” Msimamizi wa kampuni ya kutunza majumba inayotunza Stediamu ya Kuba ya Fukuoka, katika Japani, alisema hayo kiangazi kilichopita, kuhusu matayarisho yanayofanywa na Mashahidi wa Yehova kwa ajili ya “Ufundishaji wa Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wao. Pia alihusika katika Stediamu ya Kuba ya Tokyo mwaka uliotangulia wakati “Wachukuaji Nuru” Mkusanyiko wa Wilaya wa Mashahidi wa Yehova ulipofanywa huko, naye alivutiwa sana. Mwishoni mwa mikusanyiko hiyo, stediamu ilikuwa safi zaidi ya vile ilivyokuwa kabla ya kukodiwa. Yeye aliendelea kusema hivi: “Mwenendo wa watoto ulivutia. Naweza tu kusema: ‘Ni ajabu!’”
Mwaka jana, “Ufundishaji wa Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya ulifanywa pia katika Jiji la Takamatsu. Mtu mmoja wa makamo aliyekuwa amechunguza wajumbe wa mkusanyiko aliwauliza hivi, “Je! nyinyi ni Wakristo?” halafu akaendelea hivi: “Mlikuwa na mkusanyiko mwaka jana pia, sivyo? Watoto wenu huwa wapi wakati wa mkusanyiko?” Wajumbe walipojibu: “Wao husikiliza hotuba na kufungua Biblia zao wenyewe pamoja na wazazi wao,” mtu huyo alisema hivi: “Hivyo ni vema! Mimi huona watu wenu kila kiangazi na sikuzote huvutiwa kwamba watoto wenu huwa na tabia njema.” Halafu akaendelea kusema kwamba ingawa yeye husikia sana juu ya ukosefu wa kuwasiliana kati ya wazazi na watoto, yeye aweza kujua kutokana na mwenendo wa watoto wa Mashahidi wa Yehova kwamba uhusiano kati ya mzazi na mtoto miongoni mwao ni mwema sana.
Mwalimu mmoja wa shule ya msingi, aliyehudhuria mkusanyiko wa wilaya wa Mashahidi wa Yehova uliofanywa katika Makuhari Messe mwaka uliopita, alishangaa kuona mtazamo wa watoto kwenye mahali pa mkusanyiko. Shuleni, mahali ambapo mafunzo huendelea huku wanafunzi wakiwasikiliza wengine wakisema, alikuwa amefikiri kwamba watoto hao hawakuwa tayari kusikiliza. Hata hivyo, yeye aliona jambo tofauti kwenye mkusanyiko. “Watoto hao walikuwa wakiketi wima kwa vipindi virefu. Isitoshe, walikuwa wakishika penseli zao imara mikononi na kuandika habari, wakiandika herufi kwa usahihi wajapolazimika kuweka vitabu vya kuandikia juu ya mapaja yao. Watoto wa Mashahidi ni tofauti na watoto wengine hata shuleni, katika njia yao ya kusema, kusikiliza, kuvaa, na kujipamba.” Kisha yeye aongeza hivi: “Nafikiri ni kwa sababu ya mazoezi yao ya kila siku, kumsifu Yehova, na familia zao kufanya kazi pamoja kwa umoja.”
Kama vile Waisraeli walivyofuata sheria ya kimungu iliyosema: “Wakusanye watu, wanaume na wanawake na watoto . . . , wapate kusikia na kujifunza,” Mashahidi wa Yehova leo, wazee kwa vijana, wanaume kwa wanawake, hukusanyika pamoja na kupokea ufundishaji uleule. Andiko lililo juu laendelea kusema hivi, likitoa sababu: “[Kwani ni lazima] kumcha BWANA, Mungu wenu, na kuangalia kutenda maneno yote ya torati hii.”—Kumbukumbu la Torati 31:12.