Maoni ya Biblia
Kile “Chombo Dhaifu Zaidi”—Je, Ni Kuvunjia Wanawake Heshima?
“KWA NINI WANAWAKE HUHUKUMIWA KWA KUANGALIA JINSIA YAO BADALA YA KUANGALIA MAARIFA YAO, UWEZO, NA AKILI?”—BETTY A.
“WANAWAKE WAMEKAZIWA NDANI YAO FIKIRA YA KWAMBA WAO NI VIUMBE WAPUNGUFU ZAIDI.”—LYNN H.
JE, ULE usemi wa Biblia “chombo dhaifu zaidi” hushushia wanawake hadhi? Mstari wa Biblia uhusikao ni 1 Petro 3:7, NW, utaarifuo: “Nyinyi waume, endeleeni kukaa pamoja nao kwa namna kama hiyo kulingana na ujuzi, mkiwahesabia heshima kama kwa chombo dhaifu zaidi, kile cha kike, kwa kuwa nyinyi pia ni warithi pamoja nao wa pendeleo lisilostahiliwa la uhai, kusudi sala zenu zisizuiwe.”
Petro alipowaandikia Wakristo wenzake maneno haya, wanawake walikuwa na haki chache sana, si katika ulimwengu wa kale wa kipagani tu bali pia miongoni mwa jumuiya ya Kiyahudi yenye uasi-imani. Je, Petro na Wakristo wa mapema walikuwa wakitetea maoni yaliyoenea sana wakati huo juu ya wanawake?
Vyombo Vipungufu Zaidi?
Wasomaji wa karne ya kwanza wa maneno ya Petro wangeelewaje mtajo huo “chombo dhaifu zaidi”? Neno la Kigiriki kwa chombo (skeuʹos) lilitumiwa mara kadhaa katika Maandiko ya Kigiriki nalo hurejezea viwekeo, zana, vyombo vya jikoni, na ala mbalimbali. Kwa kuita wanawake kile “chombo dhaifu zaidi,” Petro hakuwa akishushia wanawake hadhi, kwa maana usemi huo ulidokeza kwamba mume pia alikuwa chombo rahisi kuvunjika au kilicho dhaifu. Maandiko mengine ya Biblia hutumia jazanda kama hiyo katika kurejezea wote wanawake na wanaume, kama vile “vyombo vya udongo” (2 Wakorintho 4:7, NW) na “vyombo vya rehema” (Warumi 9:23). Ni kweli, Petro aonyesha wanawake kuwa ndio “dhaifu zaidi” kati ya zile jinsia. Lakini Warumi 5:6, NW, hutumia “dhaifu” kuwahusu wanadamu wote—wa kiume na wa kike. Kwa hiyo, Wakristo wa mapema hawangeufikiria mtajo “chombo dhaifu zaidi” kuwa wa kimadharau kwa wanawake.
Badala ya hivyo, maneno ya Petro yangalionwa kuwa ya kupandisha hadhi ya wanawake. Katika siku ya Petro ilikuwa shida wanawake kupewa staha. Kama vile Mungu alivyokuwa ametangulia kuona, mara nyingi waume waliwatawala na kuwatenda vibaya wake zao kimwili, kingono, na kihisiamoyo. (Mwanzo 3:16) Hivyo, shauri la Petro kwa waume Wakristo lilikuwa ni kama likidokeza hivi: Msiitumie mamlaka ambayo jamii ya kilimwengu imewapa wanaume.
Acheni tuutazame karibu zaidi mtajo “dhaifu zaidi.” Petro katika mstari huu alikuwa akirejezea, si vitabia vya kihisiamoyo, bali vya kimwili. Wanaume ni vyombo dhaifu; katika maana ya ulinganisho, wanawake ni vyombo dhaifu zaidi. Jinsi gani hivyo? Muundo wa mifupa na misuli ni wa hali ya kwamba wanaume kwa kawaida wamejaliwa nguvu nyingi zaidi za kimwili. Hata hivyo, hakuna kionyeshi cha kwamba Petro alikuwa akifanya ulinganisho wa nguvu za kiadili, kiroho, au kiakili. Kwa kweli, kwa habari ya maitikio ya kihisia-moyo kwa matukio, wanawake huenda wakaelezwa vizuri zaidi kuwa tofauti na wanaume, si walio dhaifu zaidi au wenye nguvu zaidi kwa lazima. Biblia hueleza utabia wenye nguvu za kiadili, uvumilivu, na utambuzi wa wanawake waliofuata njia ya Mungu—kama vile Sara, Debora, Ruthu, na Esta, kutaja wachache tu. Wanaume wanyenyekevu hawaoni ugumu wa kukubali kwamba wanawake waweza kuwa wenye akili kuliko wao.
Hata hivyo, watu fulani huamini kwamba rejezeo la wanawake kuwa “dhaifu zaidi” hudokeza kwamba wao ni watu wapungufu zaidi. Lakini fikiria kielelezo hiki. Mtu ana viwekeo (vyombo) viwili vyenye mafaa. Kimoja ni thabiti, kingine cha uthabiti mpungufu. Je, kile chombo cha pili huthaminiwa kidogo zaidi kwa sababu hakina uthabiti kama kile kingine? Kwa kweli, kile chenye uthabiti mpungufu kwa kawaida hutendewa kwa uangalifu na heshima zaidi ya kile kilicho thabiti zaidi. Kwa hiyo, je, mwanamke ana thamani pungufu zaidi kwa sababu ana nguvu pungufu za kimwili kuliko mwanamume? Hakika sivyo! Petro autumia mtajo “chombo dhaifu zaidi,” si kuvunjia wanawake sifa, bali kukuza staha.
“Kwa Namna Kama Hiyo . . . Kulingana na Ujuzi”
Petro alihimiza waume ‘waendelee kukaa pamoja na wake zao kwa namna kama hiyo kulingana na ujuzi.’ “Kwa namna kama hiyo” kwa nani? Katika mistari iliyotangulia Petro alikuwa akizungumzia utunzaji wa Kristo wenye upendo kwa wafuasi wake, na aliagiza waume wawatunze wake zao “kwa namna kama hiyo.” (1 Petro 2:21-25; 3:7, NW) Kristo sikuzote aliweka hali njema na masilahi ya wanafunzi wake mbele ya tamaa na mapendeleo yake mwenyewe ya kibinafsi. Yeye alipendezwa na hali njema yao ya kiroho na ya kimwili, na aliifikiria mipaka yao. Waume wapaswa kuigiza kielelezo cha Kristo chenye upendo, kujiendesha kuelekea wake zao “kwa namna kama hiyo.”
Ndoa inayoendelea kwa ulaini haitokei kiaksidenti. Wote wawili mume na mke ni lazima wajue jinsi ya kuchangia mafanikio ya ndoa. Ndiyo sababu ushauri wa Petro ni kwamba waume waendelee kukaa na wake zao “kulingana na ujuzi.” Waume wahitaji kujifunza jinsi Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo, walivyoshughulika na wanawake. Wao wahitaji kujua jinsi Mungu awatakavyo wawatendee wake zao.
Kwa kuongezea, waume wahitaji kuwajua sana wake zao—hisia zao, nguvu zao, mipaka yao, yawapendezayo, na yasiyowapendeza. Wao wahitaji kujua jinsi ya kustahi akili, maarifa, na fahari ya wake zao. Biblia husema: “Waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile yule Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujikabidhi mwenyewe kwa ajili yalo. Katika njia hii waume wapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Yeye apendaye mke wake ajipenda mwenyewe, kwa maana hakuna mtu aliyepata wakati wowote kuuchukia mwili wake mwenyewe; bali huulisha na kuutunza sana.”—Waefeso 5:25, 28, 29, NW.
Wahesabieni Heshima
Petro aliporejezea wanawake kuwa “chombo dhaifu zaidi,” pia alitaarifu kwamba waume wapaswa kuwa ‘wakiwahesabia heshima.’ Katika Kigiriki, nomino ti·meʹ ina maana ya heshima, ustahifu, thamani, kuwa na bei. Yaani, kuhesabia heshima si kitendo cha kuonyesha hisani tu bali cha kutambua yawastahiliyo. Paulo aliwaagiza Wakristo wote, wanaume na wanawake pia, kama ifuatavyo: “Katika upendo wa kidugu iweni na shauku yenye wororo kwa mtu na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima nyinyi kwa nyinyi iweni wenye kuongoza.”—Warumi 12:10, NW.
Yehova Mungu hakika hawaoni wanawake kuwa vidude vya mapambo tu. Katika Israeli, sheria ya Mungu ilitumika kwa nguvu zilezile kuhusu wote wanaume na wanawake waliokuwa na hatia ya uzinzi, ngono za kiukoo, kulala na mnyama na uhalifu mwingine. (Mambo ya Walawi 18:6-17, 23, 29; 20:10-12) Wanawake wangeweza kupata manufaa za siku za Sabato, sheria zilizosimamia Wanaziri, misherehekeo, na maandalizi mengine mengi ya ile Sheria. (Kutoka 20:10; Hesabu 6:2; Kumbukumbu la Torati 12:18; 16:11, 14) Mama, vilevile baba, alipasa kuheshimiwa na kutiiwa.—Mambo ya Walawi 19:3; 20:9; Kumbukumbu la Torati 5:16; 27:16; Mithali 1:8.
Mistari 10 hadi 31 ya Mithali sura 31 huheshimu “mke mwema” kwa sababu ya uaminifu wake, bidii, na hekima katika kutunza madaraka yake mengi. Yeye alitambuliwa ipasavyo kwa ushiriki wake katika kushughulikia shughuli ya familia, na pia mambo mengine ya kifedha. Lo, ni tofauti kama nini na mtazamo wa wanaume fulani wafikirio wanawake ni vipambo tu! Baadaye, katika kutaniko la mapema la Kikristo, wanawake walitiwa nguvu na roho takatifu kuwa mashahidi wa Kristo. (Matendo 1:14, 15; 2:3, 4; linganisha Yoeli 2:28, 29.) Hivyo, wanawake fulani wamekusudiwa mwishowe kuwa mahakimu wa kimbingu wa wanaume, wanawake, na hata malaika. (1 Wakorintho 6:2, 3) Ni kweli, wanawake hawakupaswa kufundisha katika kusanyiko la kutaniko; hata hivyo, kulikuwako hali ambazo wanawake Wakristo wangeweza kusali au kutoa unabii. Waligawiwa kuwa walimu wa wanawake wachanga zaidi, watoto, na kwa wale walio nje ya kutaniko.—Mathayo 24:14; 1 Wakorintho 11:3-6; Tito 2:3-5; linganisha Zaburi 68:11.
Kionyeshi kingine chema cha fikira aliyokuwa nayo Petro aliposema juu ya kuwahesabia heshima yapatikana kwenye 2 Petro 1:17. Hapo twasoma kwamba Yehova alimheshimu Yesu kwa kuonyesha ukubali wake kwake mbele ya wengine kwa kutaarifu hivi: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu.” Vivyohivyo, mume apaswa kuonyesha kwa matendo yake, hadharani na faraghani pia, kwamba yeye humhesabia mke wake heshima.
Warithi wa Uhai
Muda wote wa historia, mara nyingi wanaume wamewaona wanawake kuwa wenye kustahili heshima au staha kidogo—kama mtumwa, au kama chombo tu cha kutosheleza wanaume. Wazo la Kikristo la kuhesabia wanawake heshima hakika huwapandisha hadhi kwenye kiwango cha juu zaidi cha staha. Barnes’ Notes on the New Testament chasema kwamba onyo la upole la Petro “lina kweli ya maana sana kuhusiana na ile jinsia ya kike. Mwanamke ameonwa kuwa duni kuliko mwanamume kwa kila njia chini ya kila mfumo wa dini isipokuwa mfumo wa Kikristo. Ukristo hufundisha kwamba . . . yeye ana haki ya kupewa matumaini na ahadi zote ambazo dini hutoa. . . . Kweli moja hii pekee ingeinua ile jinsia ya kike kila mahali iache kushushiwa hadhi, na kurekebisha moja kwa moja nusu ya maovu ya kijamii ya wanadamu.”
Kwa kuwa Kristo ndiye mwenye umiliki wa wote wanaume na wanawake, kuna sababu nzito kwa waume kuwatunza sana wake zao kama mali ya Kristo. Mara tu baada ya kurejezea wanawake kuwa kile “chombo dhaifu zaidi,” maneno ya Petro yaendelea hivi: “Kwa kuwa nyinyi pia ni warithi pamoja nao wa pendeleo lisilostahiliwa la uhai, kusudi sala zenu zisizuiwe.” (1 Petro 3:7b, NW) Petro alionyesha kwamba kutenda mke vibaya kungeharibu uhusiano wa mume pamoja na Mungu, kukizuia sala zake.
Mtajo “chombo dhaifu zaidi” haukusudiwi kuwavunjia wanawake heshima kwa vyovyote. Ingawa Yehova aliwaweka waume wawe kichwa cha nyumba, yeye hakubalii wanaume kuwatenda vibaya wanawake. Badala ya hivyo, yeye huelekeza kwamba mwanamume, kwa kumjua mwanamke, apaswa kumtolea utunzaji na heshima.
Biblia huelekeza wote wanaume waliooa na waseja wawahesabie wanawake heshima, si kuwatendea kama watu wapungufu. Wanaume na wanawake wamwabuduo Mungu kwa bidii na waheshimianao watapokea baraka nyingi kutoka mkono wa Mungu.—Linganisha 1 Wakorintho 7:16.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 19]
Miss G. E. K. /Mchoraji: Alice D. Kellogg 1862-1900
Hisani ya Joanne W. Bowie