Msiba Utakwisha Lini?
NI LINI watoto wataacha kuwa majeruhi wa kutekwa, kutendwa vibaya, kutumiwa vibaya, na mara nyingi wa ile athari mbaya ya marika wao? Je, kutekelezwa zaidi kwa sheria na adhabu kali zaidi kwa uhalifu unaotendwa dhidi ya watoto kungeweza kuwalinda? Je, programu zaidi za kijamii ili kuandaa chakula, nyumba, na elimu zingeweza kusimamisha kule kutendwa vibaya na kutoroka? Je, kufunza wazazi wanaowajali watoto wao stadi bora za uwasiliano kungeweza kusaidia kukinza ile ndoto ya msisimuko ishawishiyo watoto wao ndani ya mazingira yenye kuharibu?
Ingawa hatua kama hizo huenda zisaidie, mpaka kisababishi kikuu cha misiba kama hiyo kiondolewe, watoto watabaki chini ya mateseko mengi. Kulingana na kijana mmoja, hatua yoyote ya kushughulika na tatizo la watoto watoro ambayo haizuii kutendwa vibaya au kupuuzwa nyumbani ni kama haielekei kuwa na matokeo zaidi, kwani tayari madhara yamefanywa.
Kisababishi Kikuu
Ni nini kisababishi cha matatizo haya yote? Yatamalizwaje? Biblia hueleza kwamba kiungo cha familia kinashambuliwa na viumbe wa kiroho walio waovu, Shetani na roho waovu wake, wafurahiao ukatili, kutumiwa vibaya kingono, na upotovu. (Mwanzo 6:1-6; Waefeso 6:12) Yesu alipokuwa duniani, watoto walishambuliwa na roho waovu hawa. Kivulana kimoja kilipatwa na teseko la mifurukuto ndani ya moto.—Marko 9:20-22.
Hata karne nyingi kabla ya Yesu kuwa duniani, roho waovu walifurahia kutesa na kuwachoma hadi kuwaua watoto wachanga waliotolewa kwa miungu ya kipagani wabaya kama vile, Baali, Kemoshi, na Moleki. (1 Wafalme 11:7; 2 Wafalme 3:26, 27; Zaburi 106:37, 38; Yeremia 19:5; 32:35) Hivyo basi, katika ulimwengu huu unaoshuka tabia zaidi na zaidi, haishangazi kwamba roho waovu hulenga watoto wanaoteseka mikononi mwa maajenti wa wanadamu walio radhi ambao hupasha aibisho, uchungu, na kifo kwa walio wachanga. Watekelezaji wa uhalifu kama huo wa kinyama hujilisha akili zao kwa ponografia, ichemshayo upotovu wao.
Msongo ambao roho waovu huweka juu ya jamii ya wanadamu umeongezeka katika wakati wetu, kwani Biblia huita kipindi hiki cha historia “siku za mwisho” za mfumo wa sasa wa mambo. Ilitabiri kwamba hizi zingekuwa “nyakati ngumu kushughulika nazo.” Sasa zaidi ya wakati uwao wote, athari ya roho waovu ina matokeo ya kufanya wanadamu waonyeshe mshuko wa tabia wa viumbe waovu hawa wa kiroho. Biblia ilitabiri kwamba watu katika siku yetu wangekuwa wakali, bila kujidhibiti, wakiwa bila shauku ya kiasili, bila upendo wa wema.—2 Timotheo 3:1-5, 13, linganisha New World Translation.
Hilo hufafanua vizuri watu wenye pupa watoao filamu, marekodi, magazeti, na vitabu vitukuzavyo uzinzi, madawa ya kulevya, kuua kikusudi, kulala watu kinguvu, ndoa ya kiukoo, kufungia utumwani, na kutesa-tesa. Kupitia njia hizi na nyingine, roho waovu wamekuza utamaduni ambao, kama hewa iliyovunda, umechafua akili na mioyo ya vijana na wazee sawia, ukimomonyoa viwango vya familia na adili za kimungu.
Ongezeko la utekwaji nyara wa watoto, kusumbuliwa kingono, na kuuliwa ni sehemu ya ishara ya siku za mwisho. Kwa kuongezea, Biblia ilisema kwamba ‘watu wangekuwa wenye kujipenda wenyewe, wasiotaka kufanya suluhu, wasio safi, wasaliti.’ Basi siku hizi vifungo vya ndoa vinavunjwa mara tu baada ya kufanywa. Kadiri talaka zinavyoongezeka, ndivyo na mitorosho ya kimzazi. Na kuchapa na kuua wenzi wa ndoa wa sasa na wa awali kwaongezeka, wengi wa majeruhi wakiwa wanawake. Basi, twaona kizazi cha watoto ambacho wazazi wao huwatia moyo kutoroka kwa kuwapuuza na kuwatenda vibaya. Zaidi, wakati wetu umetiwa alama na watoto “wasiotii wazazi wao,” “wakaidi,” na wapendeleao kutoroka pamoja na marika wao kuliko kustahi viwango vya kimungu.—2 Timotheo 3:2-4.
Karibuni Msiba Huu Utakwisha
Hata hivyo, karibuni athari ya Shetani na roho wake waovu itakwisha. (Ufunuo 12:12) Unabii wa Ufunuo 20:1-3 hutaarifu kwamba Mungu ataagiza Shetani na roho wake waovu waondolewe. Baada ya hilo, Ufalme wa kimbingu wa Mungu, mikononi mwa Yesu Kristo, utatawala dunia hii kwa uadilifu, utatekeleza haki na wote watahakikishiwa usalama. (Zaburi 72:7, 8; Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10) Mfumo wa kibiashara wenye pupa utakuwa umetoweka ambao hukandamiza maskini na kutumia vibaya udhaifu wa wanadamu kwa faida, kwani “ulimwengu pamoja na vitu vyake vyote vyenye kutamanika unapita.” (1 Yohana 2:17, Habari Njema kwa Watu Wote) Wote wazoeao uovu wataondolewa, kama Mithali 2:22 itabirivyo: “Waovu watatengwa na nchi.”
Mika 4:4 hueleza kwamba katika ulimwengu mpya wa Mungu kutakuwa na usalama na amani kwa wote: “Hapana mtu atakayewatia hofu.” Hilo lawezekanaje? Kupitia ile sheria ya kifalme ya upendo. Sheria hiyo kuu itatawala mawazo na matendo yote. Wale watakaoishi wakati huo watakuwa wamejifunza kuonyesha utu wa Yesu na Baba yake, Yehova Mungu, kwani ikiwa hawataweza, hawataruhusiwa kuendelea kuishi. Kwa kujivisha wenyewe na “moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, na upole,” ubinafsi utang’olewa kutoka kwa mfanyizo wa wanadamu. (Wakolosai 3:12) Maisha yatang’aa kwa furaha; nyumba zitachachawa na uchangamfu na shauku itakuwa kawaida duniani pote.
Isaya 65:21-23 yaahidi chakula kingi na nyumba nzuri kwa kila mtu: “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. . . . Hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu.” Hakuna kutendwa vibaya tena. Hakuna kuteseka tena kwa watoto au kwa wazazi.
Kunufaika Sasa
Hata sasa, katika saa za mwisho za mfumo huu mwovu, ujuzi juu ya Yehova na kusudi lake la kurudisha dunia hii ili kuwa paradiso huleta manufaa. Umewapa vijana na wazazi wengi tumaini na sababu ya kufurahi, hata ikiwa wamekuwa majeruhi wa nyakati zetu. Kwa kielelezo, Tamara, aliyetajwa katika makala yetu ya awali, aeleza kilichotukia katika maisha yake.
“Nilipokuwa na miaka 18, niliolewa na kwa kadiri fulani nikaacha genge langu la ‘marafiki,’ wengine wao wakiyoyomea gerezani, kwa kubanwa na madawa au na umalaya. Lakini bado nilikuwa na utu uleule, hivyo mabishano yalianza na mume wangu. Hata hivyo, mara baada ya kumzaa mwana wetu, jambo fulani lilitukia lililobadili maisha yangu. Nilipata Biblia nikaanza kuisoma. Jioni moja nilisoma ile sura katika Mithali isemayo ‘kupata hekima ni kama kupata hazina iliyofichika.’ (Mithali 2:1-6) Kabla ya kwenda kulala jioni hiyo, nilisali nipate hekima hiyo. Asubuhi iliyofuata, Mashahidi wa Yehova walipiga kengele mlangoni pangu. Nilianza kujifunza Biblia pamoja nao, lakini ilinichukua muda kufanya niliyokuwa nikisoma kutoka kwa Biblia. Hatimaye, niliazimia kufuata njia ya maisha ya Kikristo nikabatizwa. Sasa, pamoja na mume wangu, nasaidia wengine kupokea kitulizo ambacho Mungu huandaa.”
Naam, Tamara alipata Chanzo cha utulizo wote, Yehova Mungu. Yeye ni Baba wa kimbingu ambaye kamwe hatawaacha wanaoshikamana naye. Zaburi 27:10 hutuambia hivi: “Baba yangu na mama yangu wameniacha [“wangeniacha,” NW], bali BWANA atanikaribisha kwake.”
Domingos, aliyetajwa awali, pia alipata familia halisi ambayo imeandaa faraja, kitia-moyo, na utegemezo. Yeye asimulia hivi: “Siku moja nilipata nakala ya kitabu Kumsikiliza Mwalimu Mkuu nikashangaa kujifunza kwamba Mungu ana jina, Yehova.a Nilihudhuria mmojapo wa mikutano ya Mashahidi wa Yehova nikamaka kuona kwamba hakuna ubaguzi wa kiwango cha kijamii. Mashahidi walianza kujifunza Biblia pamoja nami nijapovaa mararuraru, kwa kukosa tabia, na yenye kuaibisha. Polepole walinisaidia kuacha njia yangu ya maisha ya awali. Hata walinisaidia kupata kazi. Hatimaye nilisaidiwa kufanya maendeleo kuelekea ubatizo.”
Makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ni kama wavu wa ulinzi kwa vijana. Mashahidi ni wenye furaha kusaidia yeyote anayetaka kujifunza kuhusu tumaini zuri ajabu lililo mbele. Faraja inayoletwa kwa wale wanaotafuta uhusiano na Baba yao wa kimbingu ni kubwa, kwa sababu Mashahidi wamezoezwa kuandaa mashauri na mwongozo kutoka kwa Neno la Mungu Biblia. Shahidi mmoja aeleza kwamba vijana huhitaji kuonyeshwa kwamba hali yenye kunyarafisha wajipatayo kwayo yanyarafisha kwa Yehova pia. Shahidi huyo ataarifu hivi: “Yehova hataki watoto watendwe vibaya. Yeye hataki wakose furaha. Lakini hawataki wabadilishe aina moja ya kutendwa vibaya kwa nyingine—kutendwa vibaya hivi kwamba watorokee mitaani. Wanaweza kuwafikia watu wakomavu mmoja-mmoja katika tengenezo la Yehova ili kuongea kuhusu matatizo yao na kuonyeshwa suluhisho.”
Kwa watoto ambao mioyo yao ni yenye kuitikia, Neno la Mungu huandaa kichochezi chenye nguvu ili kuepuka mtego wa msongo wa marika. Frances, msichana mwenye miaka 17, alichochewa na wanashule wenzake kuhepa shule mara kadhaa bila kuwaambia wazazi wake. Mwishowe, alitoroka nyumbani. Baada ya kusababisha saa kadhaa za taabu kwa wazazi wake, alirudi. Baadaye, Mashahidi wawili kutoka kutaniko lake walizuru. Walifahamu kwamba hali ya familia haikuwa ndiyo kisababishi cha tatizo hilo, na kwa upendo waliandaa shauri. Walieleza jukumu la Kikristo la vijana kuwastahi wazazi wao (Waefeso 6:1, 2); uhitaji wa kuepuka kutofuatia haki, kwani alikuwa amehepa shule bila kuwaambia wazazi wake (Waefeso 4:25); na umuhimu wa kuepuka mashirika mabaya. (1 Wakorintho 15:33) Aliitikia kwa uchanya.
Msaada Kutoka Juu
Cheryl pia alipata msaada kutoka kwa Yehova katika kushughulika na kutoroshwa kwa watoto wake na mwenzi wake wa ndoa wa awali.b Alipoulizwa ni nini kilichomsaidia kukabiliana na ogofyo hili, alisema hivi: “Jambo la kwanza nililofanya ni kusoma Zaburi, hasa Zaburi 35. Lilikuwa jambo la kufariji kujua kwamba Yehova aliona ukosefu wa haki wa yale niliyokuwa nikikabili.” Zaburi 35:22, 23 husema hivi: “Wewe, BWANA, umeona, usinyamaze; Ee Bwana, usiwe mbali nami. Uamke, uwe macho ili kunipatia hukumu kwa ajili ya madai yangu.”
Baada ya miaka miwili, kwa utegemezo wa Yehova na msaada kutoka kwa Mashahidi, Cheryl alimkabili mume wake wa awali, akazuru watoto wake. Aliweza kuandaa majibu yenye faraja juu ya sababu hili lilikuwa limetukia kwao na kuwahakikishia kwamba yeye alikuwa hajawaacha. Kwa sababu Cheryl alizoeza watoto wake kumheshimu Yehova, aliweza kuwaambia uhakika aliokuwa nao kwao. Aliwaeleza: “Ninajua watoto wangu wanampenda Yehova, naye hataacha dhara lenye kudumu liwapate.”
Hivyo ndivyo suluhisho lilivyopatikana. Kwa jitihada zenye kuendelea za Cheryl kuhusu maofisa wa usafiri wa nje na kwa utegemeo wake kwa Yehova kwa sala ya bidii, watoto wake walirudishwa kwake. Cheryl alitaarifu hivi: “Hakika ningeweza kusema kwamba ni kwa mkono wa Yehova tu kwamba niliwapata tena.”
Ni umuhimu ulioje kuwafunza watoto wetu kujua Yehova ni nani na kumwabudu! Biblia kwenye 1 Petro 3:12 hutaarifu kwamba macho ya Yehova “huwaelekea wenye haki, na masikio yake husikiliza maombi yao.” Hakika Yehova ni kimbilio kwa watoto wetu. Jina lake ni “ngome imara; mwenye haki huikimbilia, akawa salama.”—Mithali 18:10.
Ingawa twaishi katika nyakati hatari sana na sikuzote hatujui ni nini kitawafika watoto wetu, wazazi wanaomwabudu Yehova wajua kwamba hakuna dhara lenye kudumu litakalowapata watoto wao waaminifu. Yeye hata ameahidi kuwarudisha kutoka kwa wafu walioteseka wakiwa majeruhi wa wakati wetu na kufuta uchungu na kuteseka walikotendwa.—Isaya 65:17, 18; Yohana 5:28, 29.
Lile tumaini la ulimwengu mpya wa Mungu ni zuri ajabu. Na ndivyo kulivyo kung’amua kwamba karibuni Mungu ataondoa Shetani duniani na mfumo wake mwovu. Tisho kwa watoto wetu litakuwa limetoweka. Mmojapo wa nyimbo ambazo Mashahidi wa Yehova huimba kwenye mikutano yao ya kutaniko hufafanua mfumo mpya huo kwa njia hii: “Na watoto waimbapo,/furaha, amani kote,/na kuona ufufuo,/kazia zawadi macho”!
Wakati ujao ukikutana na wengine wa Mashahidi wa Yehova, waombe wakuonyeshe jinsi wewe pia uwezavyo kujifunza zaidi kuhusu ile shangwe iliyo tu mbele katika ulimwengu mpya unaokuja wa Mungu wa uadilifu. Watafurahi kukusaidia kuona jinsi Neno la Mungu liwezavyo kuleta faraja nyingi sasa na uhai wa milele baadaye.—Zaburi 37:29; Ufunuo 21:4, 5.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Ona makala kwenye ukurasa 6.
[Blabu katika ukurasa wa 12]
“Yehova hataki watoto watendwe vibaya”