Maoni ya Biblia
Je, Mungu Apendezwa Kutuona Tukiteseka?
AKIJIKAKAMUA chini ya uzito wa msalaba mkubwa wa mbao, mwanamume fulani ajikwaa kupitia umati huku damu ikitiririka kutoka taji ya miiba kichwani pake. Baada ya kufika mahali pa “kuuawa,” ananyooshwa kwenye msalaba; misumari mikubwa inapigiliwa ndani ya mikono yake. Ajigeuza-geuza kwa maumivu makali misumari ichomwapo kwenye mnofu. Msalaba unaposimamishwa wima, maumivu yanakuwa makali sana. Kulingana na Panorama, gazeti la Filipino, kawaida kama hizo za kidini huonyeshwa kwa ukawaida wakati wa sherehe za Juma Takatifu katika Filipino.
Kilichotoka tu kuelezewa ni ufananisho wa siku ya kisasa wa miteseko ya Yesu. Lakini mwanamume huyu haigizi tu mandhari katika tamthilia fulani. Ile misumari, damu, maumivu—yote ni halisi kabisa.
Mahali kwingine, wafuasi wa Katoliki ya Kiroma waweza kuonekana wakijipiga mijeledi hadharani kwa kutamani kwao kupata miteseko aliyopata Kristo. Kwa nini? Baadhi yao hufanya hivi katika itikadi ya kwamba miteseko yao itatokeza miujiza, kama vile kuponywa kwa wapendwa wao walio wagonjwa. Wengine hufanya hilo ili kulipia dhambi zao ambazo, wanahofu, hakuna msamaha isipokuwa damu yao wenyewe imwagike. Kitabu The Filipinos chaelezea hivi: “Maumivu ni kisafishaji chema cha akili na nafsi. . . . Mtenda-dhambi apaswa kuibuka kutoka kwenye maumivu akiwa amesafishwa dhambi na kuondolewa taabu.”
Hata hivyo, maumivu ya kujipa hayafanywi tu na Wakatoliki wa Filipino. Watu kutoka dini mbalimbali na nchi tofauti-tofauti huamini kuwa miteseko ya kujipa inakubaliwa na Mungu.
Kwa kielelezo, katika kutafuta kwake ukweli, yule Buddha, Siddhārtha Gautama, alimwacha mkeye na mwanaye na kukimbilia jangwani, ambapo kwa miaka sita aliishi maisha ya mjinyimaji sana. Alikaa vikao vigumu na vyenye maumivu kwa saa nyingi na baadaye alidai kuishi kwa muda mwingi wa wakati akila tu chembe moja ya mchele kwa siku, akikonda sana hivi kwamba alisema: “Ngozi ya tumbo langu ilirudi ndani na kushikana na uti wa mgongo.” Lakini hakuna kiwango cha mteseko wa kujipa kilichoweza kuleta mnuriko aliotafuta.
Vilevile, Wahindu wa India wenye kufuata maisha ya kijinyima walipitia vitubio ambavyo nyakati fulani vilipita kiasi—kujilaza katikati ya moto, kutazama jua hadi kuwa vipofu, kusimama kwa mguu mmoja au kwa vikao vingine vigumu kwa vipindi virefu vya wakati. Wema-adili wa baadhi ya wale wenye maisha ya ujinyimaji sana ulifikiriwa kuwa mkubwa sana hivi kwamba ungeweza kulinda jiji kutokana na ushambulizi wa adui.
Vivyo hivyo, Biblia husema juu ya waabudu wa Baali ambao walijikata-kata wenyewe “kwa visu na vyembe kama ilivyo[kuwa] desturi yao, hata damu ikawachuruzika” katika jitihada ya bure ya kujaribu kupata uangalifu wa mungu wao.—1 Wafalme 18:28.
“Lazima Mjitaabishe Nafsi Zenu”
Ingawa ni kweli kwamba Yehova aliamuru taifa lake teule: “lazima mjitaabishe nafsi zenu,” hili kwa kawaida hueleweka kumaanisha kufunga kula. (Mambo ya Walawi 16:31, New World Translation) Kufunga kula huko kulikuwa wonyesho wa huzuni na toba kwa dhambi au kulifanywa wakati wa kuwa chini ya hali zenye kutaabisha. Hivyo, kufunga kula hakukuwa namna ya adhabu ya kujipa bali kuliwakilisha kujinyenyekeza mbele za Mungu.—Ezra 8:21.
Hata hivyo, kulikuwa na Wayahudi fulani ambao kwa kukosea walifikiri kuwa yale maumivu hasa yaliyo katika kujitaabisha nafsi yalistahili na kwamba yalimpa Mungu daraka la kuwathawabisha. Wakati thawabu hizo hazikupatikana, walimwomba Mungu kwa umbelembele kuhusu malipo waliyofikiri ni haki yao: “Mbona tumefunga, lakini huoni? Mbona tumejitaabisha nafsi zetu, lakini huangalii?”—Isaya 58:3.
Lakini walikosea. Kufunga kula kunakofaa kwa kidini hakukuhusisha maisha ya ujinyimaji, kutaabisha mwili kwa njaa kana kwamba maumivu ya kimwili au adha ilikuwa na thawabu yoyote. Hisia-moyo zenye nguvu zingaliweza kupunguza njaa yao. Akili ikishikwa na matatizo yenye mkazo, huenda mwili usitamani chakula. Hili laashiria Mungu hisia za ndani za yule anayefunga kula.
Je, Mungu Afurahishwa na Maumivu ya Kujipa?
Je, Muumba mwenye upendo hupata furaha yoyote kutokana na kutazama watu wakijitesa wenyewe? Ingawa ni kweli kuwa nyakati fulani Wakristo huenda wakalazimika kuwa ‘washiriki wa mateso ya Kristo,’ hii haimaanishi kwamba watende kwa njia ya kuongeza uwezekano wa kupata taabu au kuwa mfia-imani.—1 Petro 4:13.
Kwa hakika, Yesu hakuwa kamwe mjinyimaji. Viongozi wa kidini walilalamika kwa sababu wanafunzi wake hawakufunga kula, na hata walimshitaki kuwa “mwanamume aliye mlafi na mwenye tabia ya kunywa divai.” (Mathayo 9:14; 11:19, NW) Yesu alidhihirisha kiasi katika kila kitu na hakujilazimisha wala kulazimisha wengine kuzidi kiasi.—Marko 6:31; Yohana 4:6.
Hakuna mahali popote katika Maandiko tupatapo msingi wowote wa maisha ya ujinyimaji kana kwamba kujinyima wenyewe mahitaji ya lazima au hata raha za maisha kungeleta upendeleo wa Mungu. Angalia maneno ya mtume Paulo kuhusu mazoea hayo yenye maumivu: “Mambo hayo yanaonekana kana kwamba yana hekima, katika namna ya ibada mliyojitungia wenyewe, na katika kunyenyekea, na katika kuutawala mwili kwa ukali; lakini hayafai kitu kwa kuzuia tamaa za mwili.”—Wakolosai 2:23.Alipokuwa mtawa, Martin Luther alijitesa kihalisi. Hata hivyo, baadaye alikataa mazoea kama hayo, akisema kuwa yalitia moyo wazo la kuwa kuna njia mbili za kumwendea Mungu, ya hali juu na ya hali chini, hali Maandiko yalifundisha kuwa kuna njia moja tu ya kupata wokovu—kupitia kudhihirisha imani katika Yesu Kristo na Baba yake, Yehova. (Yohana 17:3) Kawaida za kidini zenye maumivu, kwa upande ule mwingine, zilionekana na wengine kama njia ya wokovu wa kibinafsi.
Kitabu Church History in Plain Language hutoa maelezo juu ya maisha ya ujinyimaji: “Kutegemeza utawa kulikuwa maoni ya kimakosa juu ya mwanadamu. Kulingana na maoni ya watawa, nafsi, imefungwa mnyororo kwenye mwili kama mfungwa kwenye maiti. Hayo si maoni ya Kibiblia kwa uhai wa kibinadamu.” Ndiyo, wazo la kwamba maumivu ya kujipa yaweza kumfurahisha Mungu ni la kigeni katika Maandiko. Wazo hilo hupata msingi katika hoja ya uongo ya Kignosti kwamba chochote kinachohusiana na mwili ni kiovu na chapaswa kutumiwa vibaya kadiri iwezekanavyo ili mtu apate wokovu.
Kwa kuwa Yehova ataka tuwe na furaha, kutumikia Mungu mwenye furaha jinsi hiyo hakuhitaji kuwa na maisha ya ujinyimaji. (Mhubiri 7:16) Hivyo, hakuna mahali katika Maandiko tuambiwapo kuwa miteseko ya kujipa wenyewe ni njia ya kupata wokovu. Kinyume cha hilo, Neno la Mungu huelewesha wazi kuwa ni damu ya Kristo, pamoja na imani yetu katika hiyo, ambayo hutusafisha kutoka dhambi zote.—Warumi 5:1; 1 Yohana 1:7.y