Kuuzwa Utumwani
Na mleta-habari wa Amkeni! katika Afrika
OLAUDAH EQUIANO alizaliwa katika 1745 mashariki mwa Nigeria kama inavyojulikana sasa. Maisha katika kijiji chake yafanana na kipindi cha wakati alimoishi. Familia zilifanya kazi pamoja ili kupalilia mahindi, pamba, viazi vikuu, na maharagwe. Wanaume walichunga ng’ombe na mbuzi. Wanawake walisokota na kufuma pamba.
Baba ya Equiano alikuwa mzee wa mbari aliyejulikana sana na hakimu katika hiyo jamii. Kilikuwa cheo ambacho Equiano alikuwa katika msururu wa kukirithi siku moja. Jambo ambalo halikutukia kamwe. Equiano, alipokuwa kijana mchanga, alitekwa nyara na kuuzwa utumwani.
Akiuzwa kutoka kwa mfanyabiashara hadi mfanyabiashara, hakukutana na Wanaulaya mpaka akafika mwambao wa pwani. Miaka mingi baadaye, alieleza maoni yake hivi: “Kitu cha kwanza nilichokiona nilipowasili kwenye mwambao wa pwani kilikuwa bahari, na meli ya watumwa ikiwa imetia nanga na kungoja shehena yayo. Vitu hivi vilinijaza mshangao, ambao muda mfupi baadaye uligeuka kuwa tisho nilipopanda meli. Mara nilichunguzwa-chunguzwa na kurushwa juu na baadhi ya wanameli ili kuona kama nilikuwa mzima, na sasa nilishurutishwa kwamba nilikuwa nimeingia katika ulimwengu wa mazimwi na kwamba wataniua.”
Akitazama kumzunguka, Equiano aliona “halaiki ya watu weusi wa mifanyizo yote wakiwa wamefungwa kwa minyororo pamoja, kila moja ya nyuso zao ikionyesha simanzi na msononeko.” Kwa kushindwa na hisia, alizirai. Waafrika wenzake walimpa ari upya na wakajaribu kumfariji. Equiano asema hivi: “Niliwauliza kama hatungeliwa na wanaume hao weupe.”
Equiano alisafirishwa hadi Barbados, kisha hadi Virginia, na baadaye hadi Uingereza. Akiwa amenunuliwa na nahodha wa meli, alisafiri mapana na marefu. Alijifunza kusoma na kuandika, na hatimaye alilipa fedha ili aachiliwe huru, naye alichangia fungu kubwa katika harakati ya kumaliza utumwa katika Uingereza. Katika 1789 alichapisha hadithi ya maisha yake, mojapo kati ya maandishi machache (na yaelekea bora zaidi) yaliyoandikwa kuhusu biashara ya watumwa na jeruhi wayo wa Kiafrika.
Mamilioni ya Waafrika wengine hawakupata mazuri sana. Wakiwa wamekwanyuliwa kutoka nyumba na familia zao, walisafirishwa kuvuka Atlantiki katika hali za ujeuri mkubwa. Wao, pamoja na watoto wao waliowazaa, walinunuliwa na kuuzwa kama ng’ombe na wakashurutishwa kumwaga jasho bila malipo ili kuongezea utajiri wa watu wasiowajua. Wengi wao hawakuwa na haki zao na wangeweza kuadhibiwa, kutendewa vibaya, ama hata kuuliwa kulingana na upendezi wa wale waliowamiliki. Kwa wengi wa hao walionyanyaswa, ukombozi pekee kutoka kwa utumwa ulikuwa kifo.