Je, Yafaa Kujiingiza Katika Deni?
“KAMWE usitumie fedha zako kabla ya kuwa nazo.” Kwa kuwa kujiingiza katika deni kwa watu wengi ni njia ya maisha leo, je, shauri hili lililotolewa na aliyekuwa rais wa Marekani Thomas Jefferson lasikika kuwa la kikale?
Katika mabara mengi mishahara hubaki chini ikilinganishwa na bei, na infleshoni humeza akiba. Pia, hali ya kiuchumi huathiri hisi za watu za thamani. Hata hivyo, ufuatiaji haki ni muhimu. Kwa kuwa mambo kama vile kuepuka kodi na kukosa kulipa madeni kumeenea, kwa kweli ni mwito wa ushindani kudumisha dhamiri njema. Si ajabu basi, kwamba uchumi mara nyingi ndio jambo kubwa la mazungumzo ya watu, na madokezo juu ya kuweka akiba au kuchuma fedha yamejaa katika magazeti ya habari na magazeti na kwenye televisheni huku watu wakijaribu kutafuta jinsi ya kushughulika na utata wa kiuchumi. Wakati uleule, kwa kufaa unahangaishwa juu ya jinsi utakavyojiandalia pamoja na familia yako.—1 Timotheo 5:8.
Kwa kuwa kwa kulinganishwa ni watu wachache wafurahiao ustawi wa kiuchumi, waweza kufanya nini ili uiepushie familia yako magumu? Jambo moja ni kwamba, kuna somo moja muhimu sana la kuweka akilini.
Epuka Deni Nyingi Mno
Kwa nini watu fulani hujiingiza katika deni? Kukopa sikuzote si kwa sababu ya hali yenye msiba, kama vile ugonjwa. Tamaa ya kuwa na vitu fulani vya kimwili yaweza kuwa yenye nguvu sana. Kwa upande ule mwingine, ushawishi wa kujiingiza katika deni huenda usiwe mbaya wenyewe. Kwa hakika, yaweza kuwa bora kuwekea nyumba rehani kuliko kulipa kodi ya nyumba, au yaweza kuwa muhimu kununua gari. Mtoa-riziki hutaka familia yake iwe na furaha. Yeye hutaka kuwa mfanikiwa akiwa mume na baba. Yaelekea, yeye huhisi kwamba familia yake ina haki ya kufurahia vitu vingi vya kimwili ambavyo wengine wanavyo.
Ni kweli kwamba, huenda ikashawishi kukopa fedha ili kununua kitu kitamaniwacho lakini kisicho muhimu. Kuwa na vitu humfanya mtu ahisi vyema, sivyo? Ni nani asiyefurahia nguo yenye kupendeza, jozi mpya ya viatu, au hata kitu kama gari jipya? Na ni nani ambaye hangependa kuwa na nyumba yenye kuvutia zaidi? Lakini, jihadhari! Wanabiashara wanaweza kuwa wenye kushawishi, na fedha nyingi sana hupatikana katika kuuzia watu bidhaa wasizohitaji na wasizoweza kugharimia.
Kumbuka pia, kwamba kulipa madeni kwa wakati unaohitajiwa kwaweza kusababisha mkazo wa mahusiano ya familia. Kutoafikiana na uchungu vyaweza kutokea. Mwanatamthilia Henrik Ibsen alikuwa sahihi aliposema: “Maisha ya nyumbani hukoma kuwa huru na yenye kupendeza mara tu yawekewapo msingi wa ukopaji na deni.” Ikiwa hulipi kwa wakati, sifa yako nzuri yaweza kufifishwa. Kwa kuwa ni rahisi zaidi kutumia fedha zilizokopwa kuliko kuzilipa kwa riba, wengi hupata kwamba kile walichonunua hakileti ile shangwe waliyotazamia.
Kwa kawaida, serikali huendelea kukopa zaidi na zaidi, zikiongeza ulipaji wazo wa riba. Ingawa hili laweza kuwa la kawaida, kwa nini uige mataifa yaliyojawa na madeni? Badala ya kufanyiza utajiri kwa ajili ya watu, deni nyingi mno yaweza kuongeza umaskini na ukosefu wa usalama. Kama methali ya Kidenmark inavyosema, “ni vigumu kulipia mkate ambao umekwisha liwa.”
Kwa kufurahisha, mkazo kwa sababu ya mzigo wa deni hupungua mno unapojua kufanya matumizi kihekima. Kwa hiyo, chukua wakati kupangia ununuzi wako ili kuepuka misongo ya kukopa. Hata katika nchi ambazo infleshoni iko juu sana, kuna njia za kuhifadhi fedha—kwa kununua vitu vilivyopunguzwa bei na kununua vitu vya lazima tu. Yahitaji kuishi kulingana na uwezo wako, ukiwa tayari kungoja au kukaa bila.
Jiulize mwenyewe: Je, kujiingiza kwangu katika deni kutasababisha magumu kwa familia yangu? Namna gani sifa yangu ikiwa sitaweza kulipa huo mkopo? Yaweza kuchukua muda mrefu kabla ya kutumainika tena! Kuhusu hili, shauri bora na lenye kutumika lapatikana. Kwa nini usichunguze Biblia ili uone ikiwa yaweza kukusaidia wewe na familia yako kushughulika na suala la deni?
Je, Biblia Yaweza Kukusaidia?
La maana zaidi, Biblia yaweza kutusaidia sisi sote tukuze tumaini kamili katika Yehova. Kwa hakika twahitaji msaada katika hizi “nyakati zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1, NW) Twaonywa hivi: “Namna yenu ya maisha na iwe bila upendo wa pesa, huku nyinyi mkiridhika na vitu vilivyopo. Kwa maana yeye amesema: ‘Hakika sitakuacha kwa vyovyote wala kukuachilia mbali kwa vyovyote.’ Ili kwamba tupate kuwa wenye moyo mkuu na kusema: ‘Yehova ni msaidiaji wangu; hakika sitaogopa. Mtu aweza kunifanya nini?’” (Waebrania 13:5, 6, NW) Jinsi ilivyo muhimu kukuza imani yenye nguvu katika Mungu akiwa Mwandalizi wetu!
Ingawa Biblia haielezi kila mtu jinsi ya kujiruzuku, hiyo hutoa miongozo isiyo na dosari. Yesu Kristo alihimiza wasikilizaji wake washughulikie kwanza hali yao ya kiroho: “Wenye furaha ni wale wenye kutambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3, NW) Twaambiwa pia tuweke miradi: “Mjitahidi kutulia, na kutenda shughuli zenu, na kufanya kazi kwa mikono yenu wenyewe, kama tulivyowaagiza; ili mwenende kwa adabu mbele yao walio nje, wala msiwe na haja ya kitu chochote.” (1 Wathesalonike 4:11, 12) Kuishi kwa utulivu na kufurahia kiwango fulani cha amani ya akili, je, hakuhitaji kuishi kulingana na uwezo wetu?
Neno la Mungu laweza kutusaidia kurekebisha kufikiri kwetu. Mwandikaji wa Mithali alionyesha maoni yenye usawaziko katika kumwomba Mungu hivi: “Usinipe umaskini wala utajiri, unilishe chakula kilicho kadiri yangu. Nisije nikashiba nikakukana, nikasema, BWANA ni nani? Wala nisiwe maskini sana nikaiba, na kulitaja bure jina la Mungu wangu.” (Mithali 30:8, 9) Kwa hivyo usione haya ikiwa walazimika kuishi ukiwa na uhaba, angalau kwa muda. Usiache kamwe furaha yako itegemee vitu vya kimwili, kama wengi wafanyavyo, wakijilinganisha na wengine au kuwa na wasiwasi isivyofaa kuhusu mali za kimwili.—Mathayo 6:31-33.
Kwa kuongezea, Biblia yaweza kukusaidia kusitawisha mazoea mazuri. Jifunze kuwa mwenye ufanisi bila kuwa mchoyo, ukipata uradhi katika vitu uwezavyo kuvigharimia. Ikiwa wewe ni kijana, usitarajie kupata mara moja kile ambacho watu wazima wamepata kwa kazi ya miaka mingi. Epuka kutumikishwa na upendaji wa vitu vya kimwili. Kwa kufaa, Biblia hutuonya si kuhusu fedha, bali “kupenda fedha,” ikisema hivi: “Hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha, ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani na kujichoma kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:9, 10) Jinsi ilivyo muhimu kwamba utambue tofauti kati ya kile unachohitaji kikweli na kile unachotaka tu!
Hata hivyo, je, wahisi kwamba mapato yako ni ya chini mno? Ni kweli, kwamba si rahisi kuvumilia ujinyimaji bila kuhuzunika. Ingawa hivyo, uwe mwenye utayari kuendelea bila vitu visivyo vya lazima badala ya kujiingiza katika deni kwa ajili yavyo, jambo ambalo laweza kukusababishia mizigo mizito na hata hasara ya kifedha. Panga kwa uangalifu, na uwe mwenye kupunguza matumizi. Unaweza kupata madokezo yenye kutumika kwa kuzungumza na rafiki mwenye uzoefu. Je, yaweza kusaidia kujifunza ustadi mpya? Kumbuka: Kufuata kanuni za Biblia, kuweka mambo ya kiroho kwanza na kumtumaini Yehova kikamili ni muhimu sana—hata hali ziwe zipi.—Wafilipi 4:11-13.
Ndiyo, kujiingiza katika deni huenda kusifae. Imesemekana hivi: “Mtu aliye na deni amenaswa wavuni.” Mzigo wa deni waweza kuharibu maisha ya familia, afya na hali ya kiroho. Deni laweza kumfanya mkopaji awe maskini hata zaidi. Yasema Mithali 22:7: “Tajiri humtawala maskini, naye akopaye ni mtumwa wake akopeshaye.” Hivyo, epuka deni lisilo la lazima. Bado twaweza kunufaika na kanuni inayohusika katika kile alichopendekeza mtume Paulo kwa Wakristo: “Msiwiwe na mtu cho chote, isipokuwa kupendana; kwa maana ampendaye mwenzake ameitimiza sheria.”—Warumi 13:8.
Pasipo kujali hali ya kiuchumi katika nchi yako, tazama mbele ukiwa na uhakika kuelekea ulimwengu mpya wa Mungu. Karibuni wanadamu hawatagawanywa kuwa wakopeshaji na wakopaji. Chini ya Ufalme wa Mungu, hakuna atakayekuwa maskini. Ahadi ya Yehova itatimizwa: “Atamwokoa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa.” (Zaburi 72:12, 13) Badala ya kujikakamua ili kuishi tu, wakazi wa dunia wakati huo “watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.
[Picha katika ukurasa wa 12]
Thomas Jefferson
[Hisani]
Mchoro umefanywa na Gilbert Stuart. Kwa hisani ya Bowdoin College Museum of Art/Dictionary of American Portraits/Dover
[Picha katika ukurasa wa 13]
Kujiingiza katika deni mno kwaweza kuweka mkazo kwenye ndoa yako