Lile Pambano Dhidi ya Misiba Lashindwa
ZILE jitihada za Umoja wa Mataifa na serikali moja-moja za kupunguza athari za misiba ya asili kwa hakika zasifika. Miradi kama vile Mwongo wa Kimataifa Kuhusu Upunguzaji wa Misiba ya Asili yadokeza kwamba jamii ya kibinadamu haihitaji kukata tamaa ikabilipo maafa kama hayo. Ikiwa mtu mmoja-mmoja, jamii mbalimbali, na serikali zachukua hatua zifaazo, uhai mwingi waweza kuokolewa.
Jambo hili ni lenye kupendeza sana, kwa sababu Biblia hutuambia kwamba karibuni kutakuwa na mbadiliko katika usimamizi wa jamii ya kibinadamu wa kiserikali. Tangu siku za Yesu, Wakristo wamekuwa wakisali Sala ya Bwana (ile ya “Baba Yetu”), ambayo hutia ndani yale maneno: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Ufalme wa Mungu ni serikali halisi. Kulingana na unabii wa Biblia, hivi karibuni sana “utavunja falme hizi zote [za binadamu] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” (Danieli 2:44) Ebu wazia jamii yote ya kibinadamu chini ya serikali moja kamilifu. Hilo litakuwa badiliko lililoje!
Ikiwa serikali za sasa zaona uhitaji wa kuchukua hatua ili kwamba hatari za asili zisije kuwa misiba ya asili, tunaweza kuwa na uhakika kwamba serikali ya Mungu itahakikisha kwamba raia wake hawatateseka kamwe katika njia hii. Ufalme wa Mungu utaleta amani ya kudumu kwenye sayari hii kwa mara ya kwanza tangu Kaini alipomwua Abeli. Chini ya Ufalme huo, “wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:11) Huo Ufalme utaelimisha jamii ya kibinadamu hivi kwamba katika maana halisi ‘watu wote watafundishwa na BWANA; na amani yao itakuwa nyingi.’—Isaya 54:13.
Leo, wengi wa majeruhi wa misiba ya asili wako miongoni mwa maskini. Hata hivyo, kukiwa na usimamizi mkamilifu na elimu inayofaa chini ya Ufalme wa Mungu, jamii ya binadamu haitateseka na umivu kali la umaskini. Akitabiri hali kama hizo katika njia ambayo watu wa siku yake wangeelewa, nabii Isaya aliandika hivi: “BWANA wa majeshi atawafanyia mataifa yote karamu ya vitu vinono, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, karamu ya vinono vilivyojaa mafuta, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, uliochujwa sana.” (Isaya 25:6) Naam, karamu ya vitu vizuri! Akieleza zaidi juu ya maisha chini ya utawala wa Ufalme, mtunga-zaburi aliandika hivi: “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima; Matunda yake na yawaye-waye kama Lebanoni, na watu wa mjini wasitawi kama majani ya nchi.”—Zaburi 72:16.
Kwa wazi, pambano la mwanadamu dhidi ya misiba ya asili litakuwa limefikia kikomo. Kwa mwongozo wa roho ya Mungu na usimamizi wa Ufalme wa Mungu, binadamu wenye kuhofu Mungu watakuwa wameshinda pambano hilo. Hicho kitakuwa kitulizo kilichoje!