Nidhamu Imekuwa Wokovu Wangu
NILIPOKUWA na umri wa miaka minne, wazazi wangu waliniandikisha katika darasa la mazoezi ya viungo vya mwili. Hilo lilihitaji mazoezi, na ilinilazimu kufanya kazi kwa umoja na wasichana wengine. Muda mfupi baadaye, nilianza kujizoeza kuwa mcheza-dansi. Nidhamu ikawa sehemu ya maisha yangu.
Wazazi wangu walikuwa watoa-nidhamu halisi na walitarajia watoto wao wawe na adabu nzuri, mwenendo mwema, na wenye staha. Niliwafikiria kuwa wabaya nyakati fulani, lakini sasa natazama nyuma—nikiwa nimelea watoto wangu watatu mwenyewe—nafahamu thamani ya nidhamu. Kwa kweli, nashukuru wazazi wangu kwa kujali sana.
Kujizoeza kwangu kwa mapema katika ujitiaji-nidhamu, na vilevile katika kufanya kazi nikiwa sehemu ya kikundi, kulinisaidia baadaye maishani.
Kukutana na Magumu
Katika umri wa miaka minane, nilipatwa na yabisi baridi, ugonjwa ulionifungia kitandani. Niliteseka kwa umivu kali katika magoti yangu mawili, na sikuruhusiwa kutembea kwa miezi 12. Familia yangu yenye upendo ilinibeba kila mahali. Hakuna mtu aliyewazia kwamba ningeweza kucheza dansi tena. Lakini hasa kwa sababu ya utunzi niliopata kutoka kwa wazazi wangu, pamoja na ustadi na subira ya daktari wetu wa familia, nilipata nafuu kabisa na kurudia kucheza kwangu dansi nikiwa nimeazimia zaidi ya wakati mwingineo wote kuwa mcheza-dansi bora kuliko wote.
Wazazi wangu waliniruhusu kuacha shule ya kawaida katika umri wa miaka 16 ili niweze kufuatia kazi-maisha yangu nikiwa mcheza-dansi. Nilifanya hili kwa bidii na idili. Hatimaye, nilianza kufanya mazoezi katika classical ballet. Jambo hilo lilitaka ujitiaji-nidhamu zaidi ya wakati mwingineo wote. Kwa miaka mitatu na nusu, nilijifunza na kufanya mazoezi siku sita kila juma.
Nilipokuwa na miaka 19, majaribio kwa ajili ya Australian Ballet School yalifanywa. Mashindano ya kukubaliwa katika shule hii yenye umashuhuri yalikuwa makali. Ni wachache tu waliokuwa wachaguliwe kutoka Australia yote. Kwa furaha yangu nilikuwa mmoja wa wale waliochaguliwa. Hivyo, nikaanza miezi 18 ya mazoezi makali. Shule hiyo ilitia ndani masomo katika ballet, miigizo, drama, na sanaa. Ballet ni aina ya dansi inayohusisha miendo yenye madaha, lakini huhitaji nguvu halisi ili kuifanya ionekane kana kwamba si kujikaza mno. Hivyo ili kutia nguvu miguu yetu, tulifanya mazoezi yaliyopangwa katika jumba la kufanyia mazoezi.
Mwishowe, katika Juni 1970, majaribio kwa ajili ya Australian Ballet Company yalifanywa. Mara nyingine tena nilichaguliwa, na mnamo juma moja nilikuwa nimejiunga na kampuni hiyo.
Maisha Katika Ulimwengu Tofauti
Kabla tu nijue kilichokuwa kikiendelea, nilikuwa mbali na nyumbani kwa mara ya kwanza katika maisha yangu na nilikuwa katika mazingira tofauti kabisa. Kampuni yetu ilitalii Australia, na kisha tukaenda Asia. Ilikuwa kama kuishi katika ulimwengu mwingine ulio na maagizo na viwango vyao wenyewe. Kulikuwa na siku na usiku mbalimbali mrefu wa kazi, pamoja na miguu yenye vidonda, iliyokuwa ikivuja damu, na yenye malengelenge. Lakini maonyesho yalifanya hiyo kazi ngumu istahiki. Kuwa kwenye jukwaa kulipendeza.
Baada ya kurudi kwetu Australia, ugonjwa wa flu ulienea kotekote katika kampuni, ukifanya wengi wetu tusiweze kufanya maonyesho. Sikuweza kucheza kwa miezi mitatu. Baada ya kurudi kwenye kampuni ya ballet, nilianza kuwa na taabu katika kushughulika na maisha ya mcheza-dansi—kung’ang’ania sikuzote ukamilifu na kujinyima aina yoyote ya utendaji wa kijamii nje ya ballet, kwa kuwa wakati na uchovu vilizuia maisha ya kushirikiana na wengine. Baada ya miaka yangu yote ya kujizoeza, je, huu ndio uliokuwa uwe mwisho wa kazi-maisha yangu?
Nilianza kuwa na hisia zisizofaa na zilizochanganyika. Nilikuja kuwa mwenye kujifikiria sana na kujitenga mwenyewe. Mwishowe, mwaka mmoja hivi baadaye, nilikuwa mgonjwa nikiwa na tatizo baya sana la kimzio liitwalo urticaria. Kama tokeo, mwili wangu wote ulijawa na vifundo vilivyofura vyekundu na vyenye kuwasha ambavyo vilikusanyana hadi nikawa kifundo kimoja kikubwa chekundu. Hili ndilo lilikuwa jambo la mwisho lililonifanya nishindwe kuvumilia zaidi—nilijiuzulu kutoka kwenye Australian Ballet Company. Miezi mingi ilipita kabla ya mimi kupata nafuu. Kwa mara nyingine tena wazazi wangu walinitunza na kunisaidia kurudia afya.
Ndoa na Familia
Katika 1974, nilikutana na mwanamume kijana mzuri. Yeye alikuwa mcheza-sinema aliyekuwa na biashara yake mwenyewe. Tulioana na kusafiri kotekote Ulaya. Baada ya kurudi Australia, mwana wetu wa kwanza, Justin, alizaliwa katika 1976. Baadaye, tulihamia Perth, jiji kuu la Australia Magharibi, tukanunua hoteli. Hili lilimaanisha badiliko kama nini katika mtindo-maisha!
Kiasi cha kazi kilikuwa kikubwa mno, kwa kuwa tulikuwa tukijaribu kuendesha hiyo hoteli sisi wenyewe. Niliamka saa kumi asubuhi na nyakati fulani sikumaliza kazi hadi asubuhi iliyofuata. Kwa kuongezea huo msongo, kulikuwa na uvutano wenye nguvu wa kishetani katika hoteli. Jambo hili polepole liliathiri hali yetu ya maisha, hasa hali ya maisha ya mume wangu mpendwa. Kwa hiyo baada ya miaka mitatu, kwa sababu ya matatizo ya ndoa na ya kifedha, tuliamua kuuza hiyo hoteli na kujaribu kuokoa ndoa yetu.
Familia yetu ilikuwa imeongozeka hadi washiriki watano kukiwa na kuzaliwa kwa binti zetu wawili, Bianca na Victoria. Hoteli haikupata mnunuaji haraka, na ulikuwa wakati huu kwamba nilianza kuelekeza uangalifu kwa Mungu kwa ajili ya msaada. Nilikumbuka ile sala ya Baba Yetu ambayo nilikuwa nimeikariri nikiwa mtoto. Ilikuwa kwenye akili yangu daima, na nilikuwa nikiisema sikuzote.
Hatimaye, hoteli ikapata mnunuaji. Hata hivyo, mume wangu alikufa kwa sababu ya kutanuka kwa mshipa wa ateri majuma matatu tu kabla ya kuondoka Perth kuelekea Melbourne. Yeye alikuwa na umri wa miaka 32 tu. Huzuni yangu ilikuwa nyingi mno, na haikupunguzwa wakati padri Mkatoliki katika Melbourne aliponiambia kwamba kwa sababu ya taabu ambayo mume wangu alikuwa nayo na mashetani, uvutano wao mbaya bila shaka ulikuwa nami pia. Kwa hiyo yeye alininyunyizia mwili wangu wote maji “matakatifu” na watoto na katika kila chumba cha nyumba ya mama yangu, ambapo tulikuwa tukikaa.
Maswali Yasiyojibiwa Bado
Miaka kadhaa ilipita, na niliendelea kuuliza maswali kuhusu Mungu, lakini sikupata majibu yoyote yenye kutosheleza kutoka kwa dini yangu ya Katoliki. Kisha nikafanya uamuzi wa kuhamisha familia yangu kutoka Melbourne hadi Queensland, ambapo kuna hali-anga yenye ujoto zaidi. Huko, katika Brisbane, tulijishughulisha sana na utendaji wa kanisa. Watoto walihudhuria shule za Kikatoliki, na sote tulienda kanisani kwa ukawaida, kufunga, kusema Rozari, na kufanya kila kitu nilichofikiria kwamba Mungu alihitaji tufanye.
Kwa kuwa sikuwa nimepata majibu kwa maswali yangu, niliamua kusoma sehemu fulani ya Biblia kibinafsi kila siku ili kuona ikiwa ningepata majibu kupitia jitihada zangu mwenyewe. Hatimaye nilisoma Mathayo 7:7, ambalo lilinishangaza. Lilisema tu kwamba tuendelee kuomba na kutafuta. ‘Hili ni rahisi,’ niliwaza. Kwa hiyo nikafanya hivyo tu. Niliendelea kumwomba Mungu msaada ili kupata majibu kwa maswali yangu.
Majibu Yanaandaliwa Hatimaye
Ninapofikiria nyuma, naweza kuona kwamba haikuwa aksidenti kwamba Mashahidi wa Yehova walibisha mlangoni pangu muda mfupi baada ya hapo. Walichosema kilisikika kuwa cha ajabu mno. Hata ingawa nilisikiliza kwa upendezi, nilikosa kutambua kwamba hiki ndicho nilikuwa nikitafuta. Kwa hiyo, baada ya ziara chache, niliwaambia hao wanawake walionitembelea wasijisumbue kurudi tena.
Nilikuwa mwenye shughuli nyingi mno wakati huo mapema katika 1987. Nyumba yangu ilikuwa katika hatua za mwisho za ukarabatishaji, na mpaka-rangi mzuri alihitajika ili kumalizia kila kitu. Mjenzi alipendekeza mpaka nyumba rangi mwenye urafiki, aliye na staha, na mchanga na mwenye msaada aliyeitwa Peter. Peter alizungumza kwa upendo kuhusu mke wake na watoto, na alikuwa na sura nzuri na safi. Nilitaka kuwa na sura kama iyo hiyo, kwa hiyo asubuhi moja alipokuwa akijisawazisha kwenye jukwaa la kusimamia ili kupaka rangi nikamuuliza: “Wewe huenda kanisani wapi?”
Nilipojua kwamba alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, nilimsumbua na maswali kutoka wakati alipowasili kazini asubuhi hadi alipoondoka akiwa amechoka alasiri. Na aliweza kuyajibu yote. Nilianza kujifunza mchana na usiku, na Biblia ikaanza kuwa yenye kupendeza na yenye uhalisi. Nikiwa nimefurikwa na shangwe, nilikubali funzo la Biblia nyumbani kwa ajili ya familia yote. Ulikuwa wakati wenye kusisimua kuliko wote wa maisha zetu kwa sababu ya shangwe ya kujua kwamba tulikuwa tumepata kweli.
Tulitupa takataka zote—mawazo katika akili zetu na vitu tulivyokuwa navyo vilivyohusiana na ibada ya sanamu. Mifuko iliyojaa ilitolewa kutoka nyumba yetu na kupelekwa kwenye jaa la takataka. Haukuwa muda mrefu kabla ya watoto wangu kuombwa kwa upole kuondoka katika shule za Kikatoliki. Kutoa kwao ushahidi juu ya Yehova hakukuthaminiwa.
Wenye Umoja Katika Ibada ya Kweli
Sote wanne sasa ni Mashahidi waliobatizwa. Justin na Bianca wamemaliza shule na wanatumikia katika huduma ya wakati wote wakiwa mapainia. Victoria ana umri wa miaka 16 na bado yuko shuleni. Nami niko katika mwaka wangu wa sita nikiwa painia.
Nilikuwa katika kutaniko la Brisbane kwa miaka sita, ambapo nilisaidia wanawake wawili wapendwa walio wazee-wazee, ambao muda si muda walitoa maisha zao wakfu kwa Yehova Mungu. Katika 1994 tulihamia mahali ambapo uhitaji wa wahubiri wa Ufalme ulikuwa mkubwa zaidi. Sasa tunatumikia katika mji mdogo wa mashambani unaoitwa Charleville kusini-magharibi mwa Queensland. Eneo letu la kuhubiri linatia ndani sehemu kubwa, lenye ukubwa ulio karibu sawa na kisiwa-jimbo cha Australia cha Tasmania!
Nikirudisha mawazo nyuma hadi utotoni mwangu na mazoezi yangu, nimekuja kutambua jinsi nilivyonufaika kutokana na nidhamu. Imenisaidia kutumia kanuni za Biblia na kufanya mabadiliko ya lazima maishani. Kwa kweli, kutiwa nidhamu sasa na Yehova huleta shangwe tupu na tumaini la baraka zisizo na mwisho kwangu na kwa familia yangu pendwa.—Mithali 6:23; 15:33.—Kama ilivyosimuliwa na Sue Burke.
[Picha katika ukurasa wa 21]
Nikiwa na watoto wangu watatu