Vijana huuliza...
Je, Nijifunze Mbinu za Kujikinga?
“Kuna hiki kikundi kibaya sana shuleni,” asema Jesse. “Wakikuona katika ukumbi wa shule na wanataka viatu vyako, koti, au hata suruali yako, watachukua. Ukiripoti, watakushambulia tena.”
KUKABILI jeuri kumekuwa njia ya maisha kwa vijana wengi. Likasema gazeti USA Today: “Karibu mwanafunzi mmoja kati ya watano wa shule ya sekondari hubeba, bastola, kisu, wembe, rungu, au silaha nyingineyo kwa ukawaida. Wengi huenda na vitu hivyo shuleni.” Mvulana tineja aitwaye Jairo anajua hili kwa kujionea mwenyewe. “Shule yetu ilikuwa ya kwanza [katika New York City] kuwa na vitambua-chuma,” yeye asema, “lakini hilo halizuii watoto kuwa na visu na bunduki. Sijui wanavyoviingiza, lakini wanafanya hivyo.”
Kwa kueleweka, tisho la kushambuliwa lafanya vijana wengi wafikirie jinsi watakavyojikinga. Lola mchanga aonelea hivi: “Baada ya msichana mmoja katika shule yangu kudungwa kisu hadi kufa kwa sababu ya vipuli vyake, walianza kufunza mbinu za kujikinga shuleni. Karibu kila mtu alijiandikisha.” Vijana wengine waamua kubeba vipulizio vya kikemikali na silaha nyinginezo. Swali ni, Je, mbinu za kujikinga hukulinda kikweli?
Mbinu za Kupigana
Zinaonyeshwa katika televisheni nyakati zote—wataalamu wa mbinu za kupigana wakipinduka hewani, huku wakirusha mateke na ngumi kwa urahisi na mnyumbuko kama wa mcheza-dansi. Mnamo sekunde chache jamaa wabaya wanalala ardhini bila kusonga. Inastaajabisha! Mbinu za kupigana huonekana kama ulinzi kamili. Ingawa hivyo, kwa uhalisi maisha si kama sinema. Mwanamume mmoja aliye na miaka mingi ya uzoefu wa mbinu za kupigana asema hivi: “Risasi moja tu inatosha. Ikiwa mtu aliye mbali ana bunduki, huna fursa yoyote. Ikiwa mmesongamana sana bila nafasi yoyote ya kusongea, huwi na matokeo vile.”
Tambua pia, kwamba, ili kuwa mwenye ustadi katika mbinu za kupigana, ni lazima mtu atumie pesa nyingi mno na apitie miaka mingi ya mazoezi makali mno. Na isipokuwa unadumu katika kufanya mazoezi, uwezo wako wa kurusha mateke na ngumi kwa njia hiyo yenye ufundi na madaha waweza kuzorota kwa haraka sana. Ndivyo iwezavyo kusemwa pia kuhusu namna nyinginezo za mbinu za kujikinga, kama vile ndondi. Isitoshe, sifa ya kujua kupigana yaelekea itavuta uangalifu usiotakwa. Wachokozi huenda wakaamua kupigana nawe ukiwa kama mshindani wao.
Hata hivyo, kuna hatari kubwa zaidi katika kujifunza mbinu za kupigana. Gazeti The Economist liliripoti majuzi hivi: “Nyingi za mbinu za kupigana, ikiwa si zote, zinahusiana kabisa, na dini tatu za Asia Mashariki, Dini ya Buddha, Dini ya Tao na Dini ya Confucius.” Chanzo kingine kinaongezea hivi: “Kila kitu kinachofanywa katika kupigana—kila msogeo, kila hisi—kinaweza kufuatiwa hadi kanuni fulani ya Zen.” Zen ni farakano la Dini ya Buddha linalokazia kutafakari kwa kidini. Vyanzo hivi vya kidini vyatokeza tatizo zito kwa Wakristo kulingana na maoni ya maneno ya Biblia kwenye 2 Wakorintho 6:17: “Kwa hiyo, tokeni kati yao [waabudu wa uwongo], mkatengwe nao, asema Bwana, msiguse kitu kilicho kichafu.”
Utumizi wa Silaha
Lakini, namna gani kubeba bunduki au kisu? Kufanya hivyo kwaweza kwa kweli kukufanya uhisi kutotishika. Lakini kutotishika huko kwaweza kuthibitika kuwa hatari ikiwa ungeanza kujihatarisha isivyofaa au kutenda kwa njia ya kutokeza fujo. Yaonya Biblia: “Atafutaye madhara, hayo yatamjia.” (Mithali 11:27) Na ikiwa fujo usiyoisababisha yakujia, kutoa silaha kwa hakika kutaongeza migongano. Unaweza kuuawa—au umuue mtu mwingine. Je, Mungu, Chanzo cha uhai, angeonaje matendo yako ikiwa ungaliweza kuepuka kutumia jeuri?—Zaburi 11:5; 36:9.
Ni kweli, wengine hawakusudii kutumia nguvu zenye kufisha. Huenda wakasema kwamba wanabeba silaha tu ili kuogopesha washambuliaji. Lakini gazeti Health lasema hivi: “Wakufunzi wa bunduki wanakubali hivi: Usibebe bunduki ikiwa hunuii kuitumia. Kupunga-punga bunduki kwa kutisha tu kwaweza kuogopesha washambulizi fulani, lakini kutakasirisha tu wengine.”
Namna gani silaha “salama zaidi,” kama vile vipulizio vya kikemikali? Licha ya uhakika wa kwamba hivyo si halali mahali fulani-fulani, silaha hizi zina matokeo mabaya. Badala ya kumzuia mshambulizi aliyetumia dawa za kulevya mno, hizo silaha huenda zikamghadhabisha. Hata kuna uwezekano kwamba upepo upulize hiyo kemikali usoni mwako badala ya usoni mwa mshambulizi—ikiwa ulifaulu kutoa kipulizio hicho. Akikuona ukitafuta-tafuta mifukoni au pochini mwako, huenda mshambulizi adhanie unataka kutoa bunduki na aamue kuchukua hatua kali. Hivyo mpelelezi mmoja wa polisi alieleza hivi: “Hakuna uhakikisho kwamba mace [kipulizio cha kikemikali], au silaha nyingineyo, itafanya kazi. Au kwamba utaitoa mfukoni kwa wakati. Silaha hazisaidii hali kamwe. Watu huzitumaini kupita kiasi.”
Silaha—Maoni ya Kimungu
Tisho la jeuri lilikuwa halisi huko nyuma katika siku za Yesu. Moja ya mifano yake ijulikanayo sana, iitwayo kwa kawaida mfano wa Msamaria Mwema, ulisimulia kisa fulani kilichohusisha unyang’anyi wenye jeuri. (Luka 10:30-35) Yesu alipowaambia wanafunzi wake wajihami kwa panga, haikuwa kwa kusudi la kujikinga. Kwa hakika, ilimwongoza kutaarifu ile kanuni: “Wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga.”—Mathayo 26:51, 52; Luka 22:36-38.
Kwa hivyo, Wakristo wa kweli, hawajihami ili kuumiza mwanadamu mwenzao. (Linganisha Isaya 2:4.) Wao wanafuata shauri la Biblia kwenye Warumi 12:18: “Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote.” Je, hili lamaanisha kutojikinga? Sivyo hata kidogo!
Hekima—Ni Bora Kuliko Silaha
Katika muhula ambapo yaonekana kuna vidude vya kila kitu, huenda ikakushangaza kujua kwamba waweza kuwa na namna ya kujikinga yenye matokeo sana kuliko kitu chochote kilichotengenezwa na mwanadamu. Kwenye Mhubiri 9:18, twasoma hivi: “Hekima ndiyo bora kupita silaha za vita.” Hekima hii ni zaidi ya kile mtu aitacho “werevu wa mitaani.” Ni utumizi wa kanuni za Biblia, na mara nyingi yaweza kukusaidia kuepuka hali zenye jeuri.
Kwa kielelezo, Jairo, ambaye mapema alikuwa amefafanua shule yake yenye jeuri, huepuka fujo kwa kutumia maneno ya Biblia kwenye 1 Wathesalonike 4:11: “Mjitahidi kutulia, na kutenda shughuli zenu.” Jairo asema: “Ukijua kutakuwa na vita, usijihusishe na uende nyumbani. Wengine hubaki wakingojea, na hapo ndipo waingiapo taabani.”
“Kuacha kila mtu ajue kwamba mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova ndio ulinzi wangu bora zaidi,” ataarifu Lola mchanga. “Watu hawanisumbui kwa kuwa wanajua sitakuwa tisho kwao.” “Ni zaidi ya kusema tu kwamba wewe ni Shahidi,” aongeza Eliu. “Wanapaswa kuona kwamba wewe ni tofauti.” Lazima Wakristo ‘wasiwe sehemu ya ulimwengu.’ (Yohana 15:19) Lakini uwe mwangalifu usitoe wonyesho wa mtazamo wa kuwa bora. (Mithali 11:2) Kijana mmoja alisema hivi: “Usitembee kumbini kama kwamba hizo ni mali yako.” Hili laweza kusababisha chuki. Kijana mmoja Mkristo aitwaye Luchy asimulia hivi: “Mimi ni mwenye urafiki, na huzungumza na wanadarasa wenzangu; lakini sitendi kama wao.”
Namna unavyovaa pia ni jambo la maana. “Mimi ni mwangalifu kutovaa vitu ambavyo huvuta uangalifu,” asema kijana mmoja. “Naamua kwamba sihitaji kuvaa aina ghali mno za nguo ili nionekane vizuri.” Kufuata shauri la Biblia la kuvaa kwa kiasi kwaweza kukusaidia kutovuta sana uangalifu wa watu na kuepuka fujo.—1 Timotheo 2:9.
Ukikabiliwa na Jeuri
Namna gani, basi, ikiwa licha ya jitihada zako za kuepuka dhara, unatishwa na jeuri? Kwanza, jaribu kutumia kanuni inayopatikana kwenye Mithali 15:1: “Jawabu la upole hugeuza hasira; bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.” Eliu mchanga alifanya hivyo alipokuwa shuleni. Yeye asema hivi: “Nyakati fulani jambo kuu ni kupuuza maneno makali. Katika visa vingi, ni namna unavyoitikia ambayo husababisha fujo.” Kwa kukataa “kulipa ovu kwa ovu,” huenda ukaweza kudhibiti hali.—Warumi 12:17.
Hata hivyo, werevu usipofaulu, lazima uchukue hatua za kujikinga. Ikiwa kikundi cha vijana kinadai uwapatie viatu vyako au vitu vyako vyenye bei, wape! Uhai wako ni wenye thamani sana kuliko vitu ulivyo navyo. (Luka 12:15) Ikiwa jeuri yaelekea kutokea, nenda zako—na vema zaidi, kimbia! “Acheni ugomvi kabla haujafurika,” yasema Mithali 17:14. (Linganisha Luka 4:29, 30; Yohana 8:59.) Ikiwa kutoroka hakuwezekani, huenda usiwe na chaguo ila kuondosha jeuri uwezavyo. Baadaye, hakikisha umeeleza wazazi wako kilichotokea. Labda wanaweza kusaidia katika njia fulani.
Kama tu Biblia ilivyotabiri, tunaishi katika nyakati zenye jeuri. (2 Timotheo 3:1-5) Lakini kubeba bunduki au kujifunza mateke ya kupigana hakutakufanya uwe salama hata kidogo. Tahadhari. Tumia hekima ya kimungu unapokabiliwa na fujo. Na zaidi ya yote, uwe na imani na tumaini katika Yehova. Kama mtunga-zaburi, unaweza kwa uhakika kusali hivi: ‘Waniponya na mtu wa jeuri.’—Zaburi 18:48.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Mbinu za kupigana si suluhisho kwa Wakristo