Chakula cha Kutosha kwa Wote!
NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA BRAZILI
NI JAMBO linalowezekana kufurahia chakula kingi kilicho bora, na bado uwe bila furaha. Ili kuwa na furaha ya kweli na yenye kudumu, kitu kingine kinahitajika—chakula cha kiroho. Yesu alitaarifu hivi: “Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.”—Mathayo 4:4.
Kwa upande ule mwingine, kukataa Neno la Mungu huongoza kwenye njaa ya kiroho, kama ilivyotabiriwa kwenye Amosi 8:11: “Nitaleta njaa katika nchi; si njaa ya kukosa chakula, wala kiu ya kukosa maji, bali ya kukosa kuyasikia maneno ya BWANA.” Hata hivyo, utapiamlo wa kiroho waweza kuepukwa. Yesu alitangaza hivi: “Wenye furaha ni wale wenye kufahamu uhitaji wao wa kiroho . . . Wenye furaha ni wale walio na njaa na walio na kiu kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa wao watashibishwa.” (Mathayo 5:3, 6, NW) Kama vile chakula chenye lishe bora kwa viwango vifaavyo kinavyotosheleza mwili wetu, chakula cha kiroho chenye kujenga hutia nguvu imani yetu na tumaini letu la wakati ujao. Ni ulimwengu wa aina gani tunaoweza kutumainia?
Chakula Kingi kwa Wote
Wazia ulimwengu ulio na wingi wa chakula kitamu na chenye kujenga. Ulimwengu usio na vita, misiba, au misiba ambayo husababisha njaa kali au utapiamlo, mambo ambayo hudhoofisha au kushusha watu moyo. Hakutakuwako tena watu wasio na makao au wasioajiriwa wanaotegemea ugawaji wa supu au vitu vya kupewa bure, wala bei zenye kupanda za chakula hazitalazimisha watu wale chochote tu ili kujaza tumbo. ‘Kutakuwapo wingi wa nafaka katika ardhi na juu ya milima.’ (Zaburi 72:16) Lakini hili litatokeaje? Ni nani atakayetatua tatizo la utapiamlo?
Muumba wetu ataelekeza uangalifu wenye upendo kwa mahitaji ya mwanadamu ya chakula cha kutosha. Hata tabia-nchi ya dunia itadhibitiwa, jambo hilo likihakikisha kwamba mavuno hayatakosekana tena. “BWANA atatoa kilicho chema, na nchi yetu itatoa mazao yake.” (Zaburi 85:12) Isitoshe, ingawa dunia ina uwezo wa kutokeza chakula cha kutosha, ni Ufalme wa Mungu tu utakaomaliza pupa na ukandamizaji, mambo ambayo huongoza kwenye ugawaji usiotosha, utapiamlo, na taabu.
Ndiyo, serikali ya Yehova ya kimbingu itahakikisha kwamba mifumo yoyote ya kilimo na usafirishaji ipatikanayo itaandaa chakula chenye kujenga mahali kinapohitajiwa. Mamlaka ya huo Ufalme haitafaidi watu wachache tu na kuacha walio wengi kujiruzuku kwa taabu. Badala ya utamausho na kukata tamaa, baraka za Ufalme zitaleta shangwe inayodhihirishwa katika karamu kuu ya vinono iliyotabiriwa kwenye Isaya 25:6: “BWANA wa majeshi atawafanyia mataifa yote karamu ya vitu vinono, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, karamu ya vinono vilivyojaa mafuta.”
Sasa, ona akilini mtindo-maisha wa leo, wenye roho ya mashindano, wenye mkazo na wenye ukatili ukiwa umetoweka milele. Hakuna yeyote atakayelishwa chini ya ipasavyo au atakayekuwa mgonjwa. Kwa hivyo, ikiwa wataka kikweli kufurahia maisha katika ulimwengu huo mpya, tii maneno ya Yesu: “Msikitendee kazi chakula chenye kuharibika, bali chakula kidumucho hata uzima wa milele.”—Yohana 6:27.