Kanisa Othodoksi la Kigiriki—Dini Iliyogawanyika
NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA UGIRIKI
KWA watu wanyoofu wanaompenda Mungu na ile kweli ambao wana staha ya kina kwa ibada yake, hali ya sasa katika Kanisa Othodoksi la Kigiriki, bila kutia chumvi, ni yenye kufadhaisha. Ukosefu wenye kuhuzunisha wa umoja, mikabiliano yenye jeuri kati ya mafarakano yenye kupigana ya kanisa, kashifa nyingi mno za adili zenye kuaibisha, na kushindwa kwa dini—ambayo hujifafanua kuwa “kanisa pekee la kweli la Mungu”—kuandaa mwongozo wa kiroho zinafanya Wagiriki wengi waudhike na kukirihishwa.
Watu wenye cheo cha chini wanakatishwa tamaa, hata kughadhabishwa, na hali hii. Profesa mmoja wa chuo kikuu, akiandika katika gazeti kuu la habari la Kigiriki, alalamika hivi: “Kanisa la Ugiriki linatenganishwa na tatizo lisilo na kifani katika ukuu walo na udumifu walo na ambalo hutokeza shaka kuhusiana na mamlaka [ya kanisa] na humomonyoa maadili ya kiasili ya desturi zalo. Kwa kuhuzunisha madhara yaendelea.”
Hali hii ilitokeaje? Je, uhusiano wa karibu kati ya Kanisa Othodoksi la Kigiriki na Serikali umekuwa wenye manufaa kikweli? Kuna wakati ujao gani kwa mahusiano haya ya Kanisa na Serikali? Kuna kibadala kipi kwa watu wanaotafuta kutaniko la Kristo la kweli lililo na umoja? Ebu tuchunguze mambo ya hakika tuone kile ambacho Biblia yasema kuhusu hilo jambo.
Kung’ang’ania Mamlaka
Udikteta wa kijeshi ulipotawala Ugiriki katika miaka ya 1967-1974, uliingilia sana mambo ya Kanisa Othodoksi la Kigiriki ili kuimarisha mamlaka yao yenyewe. Katika jitihada yao ya kudhibiti kikamili, kikundi cha kijeshi kilivunja Sinodi Takatifu iliyokuwa imechaguliwa mbeleni—baraza la juu zaidi ya yote la Kanisa Othodoksi la Kigiriki—na kuteua sinodi yalo lenyewe, “kulingana na ustahili,” kama ilivyosemwa. Demokrasia iliporudishwa katika 1974, baraza lenye kutawala la hilo kanisa lilichaguliwa tena kulingana na agizo la kanuni ya kanisa. Vivyohivyo, maaskofu waliokuwa wamefanyiza sehemu ya sinodi iliyochaguliwa na kikundi cha kijeshi waliondoshwa na wengine kuchukua mahali pao.
Hata hivyo, mswada wa serikali uliopitishwa katika 1990 uliwapa maaskofu walioondoshwa haki ya kudai upya vyeo vyao kwa kukata rufani kwenye mahakama za kilimwengu na hatimaye kwa mahakama ya juu zaidi ya kimamlaka, Baraza la Serikali. Watatu wa hao makasisi walifanya vivyo hivyo, na hatimaye wakashinda kesi zao. Leo, kama tokeo, dayosisi kubwa tatu tofauti za Kanisa Othodoksi katika Ugiriki zina maaskofu wawili kila moja—yule anayetambuliwa kirasmi na Kanisa Othodoksi la Kigiriki na yule anayekubaliwa kirasmi na Baraza la Serikali.
“Wakristo Wanaopigana”
Maaskofu walioondoshwa mbeleni wamepata tena vyeo vyao, nao wanakataa katakata kutambua maaskofu wengine waliochaguliwa na kanisa rasmi. Isitoshe, kila kikundi kina wafuasi wengi walio “washupavu wa kidini”—kama gazeti moja la habari lilivyowafafanua—ambao hutetea kwa nguvu katika kuunga mkono mwelekeo wa askofu wao. Kwa hiyo hali hii ilianzisha maitikio makali na mengi huku viwambo vya televisheni kotekote nchini vikieneza mandhari za jeuri, vikionyesha wengi mno wa hao “Wakristo wanaopigana” wakiingia kinguvu makanisani, kuvunja-vunja sanamu za kidini, na kushambulia makasisi na watu wa kawaida wa mafarakano tofauti. Katika vingi vya visa hivi, ilibidi polisi wa kuzima fujo waingilie ili kurudisha utulivu. Matukio yalifikia upeo katika Oktoba na Novemba 1993 katika makanisa yaliyoko katika mtaa wa kiungani wa hali ya juu wa Athens uitwao Kifisia, na baadaye katika Julai na Desemba 1994 katika jiji la Larissa, huku matukio ya washupavu wa kidini wa wasiofikiri yakishangaza umma katika Ugiriki.
Mapigano yenye jeuri kuliko yote yalitokea Julai 28, 1994, wakati wa kutawazwa kwa Ignatius, askofu katika Larissa aliyechaguliwa na Sinodi Takatifu. Likionyesha kichwa kikuu chenye maandishi makubwa katika ukurasa wa mbele, “Larissa Lawa Uwanja wa Pigano Kwa Ajili Ya Askofu Mpya—Mihula ya Giza Yahuishwa,” gazeti la habari Ethnos liliripoti hivi: “Usemi mmoja tu ndio unaofaa: ile Mihula ya Giza. Mtu angeweza kufafanua kwa njia gani nyingine mambo yote yaliyotokea jana katika Larissa, . . . vita za barabarani, mapigano yenye fujo, majeraha mwilini?”
Majuma kadhaa baadaye, wapinzani walishambulia gari la Askofu Ignatius “wakitumia pau za chuma na vibao, baada ya kumkimbiza kufa kupona.” Mwandishi mmoja alishangaa: “Je, inawezekana mtu kukubali kwamba watendaji wa hayo mambo wametiwa moyoni mashauri ya Kikristo huku, kwa wakati huohuo, ushupavu wao ukiwaongoza kutenda matendo yanayofanana na yale ya majambazi, matendo ambayo yangeweza kusababisha kifo? . . . Na matendo haya yanatiwa moyo na kukubaliwa na viongozi wakuu wa kanisa.”
Hiyo hali ilikuja kuwa mbaya hata zaidi wakati wa kipindi cha Krismasi. Likirejezea matukio yenye kutamausha ya Desemba 23-26, 1994, katika Larissa, gazeti la habari Eleftherotipia liliandika hivi: “Ilikuwa Krismasi ya aibu katika Larissa, ambapo, kwa mara nyingine tena, migongano ya muda mrefu iliyoenea iliharibu [sherehe]. . . . Kengele za makanisa zilipokuwa zikitangaza kuzaliwa kwa Kristo, marungu ya polisi yalikuwa yakiangukia vichwa vya ‘waadilifu na wasio waadilifu.’ Fujo, mapigano, matukano, na kushikwa kulichukua mahali pa salamu za kutakiana mema na baraka za Krismasi katika uga wa Church of Saint Constantine katika Larissa. . . . Yale maandamano [dhidi ya Ignatius] mara moja yaligeuka kuwa maneno yenye matukano kisha mapigano na polisi. . . . Waligeuza uga wa kanisa kuwa uwanja wa pigano.”
Watu waliitikiaje hili? Mwanamume mmoja Mwothodoksi alisema hivi: “Sielewi jinsi watu wanaojiita Wakristo wawezavyo kutenda matendo ya jeuri hivyo wakati wa sikukuu takatifu za kidini. Nawezaje kwenda kanisani ninapokabiliwa na hatari ya kupigwa huko?” Na mwanamke mmoja mwenye kujitoa sana Mwothodoksi alitaarifu: “Naogopa kwenda kanisani sasa baada ya matukio yote haya.”
Isitoshe, pia kuna ufichuaji mwingi mno kuhusu kashifa za adili zinazohusu Kanisa Othodoksi la Kigiriki. Vyombo vya habari vimefunua kwa kurudia-rudia masimulizi yanayohusu adili zilizozorota za washiriki fulani wa jamii ya makasisi—makasisi walio wagoni-jinsia-moja na wenye kufanya ngono na watoto, utumizi mbaya wa fedha, na biashara isiyo halali ya vitu vya kale. Biashara ya vitu vya kale yawezekana kwa sababu makasisi wengi wana uwezo usiodhibitiwa wa kufikia hazina za sanamu zenye thamani na vitu vingine vya sanaa vyenye thamani.
Jinsi hali hii inavyovunja kwa kuchukiza onyo lenye nguvu lililotolewa na mtume Paulo kwa Wakristo kwamba wasiwe wafuasi wa wanadamu kwa sababu hili hutokeza “migawanyiko” na “mitengano”!—1 Wakorintho 1:10-13; 3:1-4, NW.
Mahusiano ya Kanisa na Serikali —Yana Wakati Ujao Gani?
Tangu mwanzo wa Serikali ya Kigiriki, Kanisa Othodoksi la Kigiriki limekuwa na cheo kilichopendelewa cha kuwa dini kuu. Katika Ugiriki, kufikia wakati huu, hakuna kitu kama utenganisho wa Kanisa na Serikali. Katiba yenyewe huhakikisha cheo cha Kanisa Othodoksi la Kigiriki kuwa “dini kuu” ya Ugiriki. Hili lamaanisha kwamba Kanisa Othodoksi la Kigiriki hupenya sekta zote za maisha ya umma, kutia ndani utawala juu ya umma, mfumo wa kihukumu, polisi, elimu ya umma, na karibu kila sehemu ya jamii. Kuwapo huku kwenye kuhusisha kila kitu kwa kanisa kumemaanisha kukandamizwa na magumu yasiyoweza kuelezeka kwa dini nyinginezo ndogo katika Ugiriki. Ingawa Katiba yahakikisha uhuru wa kidini, wakati wowote dini ndogo zijaribupo kudai haki zazo, karibu kila wakati hujipata zimenasika katika utando usiopenyeka wa ubaguzi, chuki, na upinzani wa kidini ambao umefumwa na uhusiano huu wa Kanisa na Serikali.
Kurekebishwa kwa Katiba kwaonekana kuwa uwezekano usiotilika shaka katika wakati ujao karibu, na kwa hivyo madai yenye nguvu kwa ajili ya kutenganishwa kwa Kanisa na Serikali tayari yasikika. Wataalamu na wachanganuzi mashuhuri wa katiba walio Wagiriki wanaelekeza uangalifu kwa matatizo yaliyotokezwa na ushirika huu wa karibu kati ya Kanisa na Serikali. Wanataja kwamba suluhisho pekee liwezalo kufanya kazi lingekuwa utenganisho kamili wa matengenezo haya mawili yanayotofautiana.
Wakati huohuo, viongozi wa kanisa wanatoa vipingamizi vyao kwa utenganisho huo uwezao kutokea. Ikigusia swala nyetivu, ambalo lingeathiriwa sana na matukio hayo katika mahusiano ya Kanisa na Serikali, askofu mmoja Mwothodoksi aliandika hivi: “Kama tokeo, je, Serikali itaacha kulipa makasisi mishahara? . . . Hilo lingemaanisha kwamba parishi nyingi zitaachwa bila mapadre.”—Linganisha Mathayo 6:33.
Tokeo jingine la huo uhusiano wa karibu kati ya Kanisa na Serikali katika Ugiriki ni kwamba sheria ya Kigiriki—ikipingana moja kwa moja na maagizo ya Muungano wa Ulaya na Masharti ya Mkataba wa Ulaya wa Haki za Binadamu, ambayo yanawajibisha Ugiriki—yanahitaji kwamba ni lazima vitambulisho vya wananchi wote Wagiriki vionyeshe dini ambayo kila mwananchi yuko. Watu wasio na upendeleo wanapinga hilo kwa nguvu kwa sababu washiriki wa dini ndogo kwa kawaida hubaguliwa. Mwandishi mmoja alitaarifu: “Uhakika huu yaelekea sana waweza kuwa na matokeo hasi juu ya haki za dini ndogo kuweza kuwa na uhuru wazo wa kidini.” Likitoa maelezo kuhusu hili, gazeti la habari Ta Nea liliandika: “Serikali yapaswa kufanya maamuzi yayo na kupitisha sheria bila kufikiria njia zenye kutawala na maitikio ya kanisa katika mambo kama vile kusajili dini ya mtu ambako ni wajibu kwenye kitambulisho chake cha kibinafsi.”
Akikazia uhitaji wa haraka wa utenganisho huo, Dimitris Tsatsos, profesa wa sheria ya kikatiba na pia mshiriki wa Bunge la Ulaya, alitaarifu hivi: “Ni lazima Kanisa [la Ugiriki] liache kutawala maisha ya jamii, kisiasa, na kielimu. Njia ambayo kwayo Kanisa la Kigiriki linatenda ni yenye kukandamiza. Ni utawala wa kimabavu juu ya mfumo wetu wa kielimu na jamii yetu.” Katika mahojiano mengine profesa huyohuyo alisema: “Kanisa lina uwezo wenye kuhofisha katika Ugiriki, ambao kwa kuhuzunisha umepita mipaka kuhusiana na uhusiano walo pamoja na wanasiasa wenye kushikilia sana maoni yao, na kufaulu pia kupenyeza sekta huru ya jamii ya Kigiriki. Mimi binafsi, nadai utenganisho wa Kanisa na Serikali. Nadai kwamba Wagiriki wa Othodoksi wawekwe kwenye kiwango sawa na wawe na usawa na waumini wa dini nyinginezo katika Ugiriki.”
Wakristo wa Kweli Wameungana
Kwa kweli ni vigumu kupata alama ya Ukristo wa kweli katika Kanisa Othodoksi la Kigiriki. Yesu Kristo hakunuia mitengano na migawanyiko ikue miongoni mwa Ukristo. Akisali kwa Baba yake, yeye aliomba kwamba wafuasi wake “wote wapate kuwa mmoja.” (Yohana 17:21, NW) Na wafuasi hawa walikuwa ‘wawe na upendo wao kwa wao,’ upendo huu ukiwa alama ya kutofautisha wafuasi wa kweli wa Kristo.—Yohana 13:35.
Yaonekana umoja wahepa Kanisa Othodoksi la Kigiriki. Hata hivyo, hiki si kisa cha kipekee kamwe katika dini mashuhuri leo. Badala ya hivyo, ni kiwakilishi cha mgawanyiko unaokumba dini za Jumuiya ya Wakristo.
Wapenda-Mungu wanyoofu huona hali hii yenye kuhuzunisha kuwa ngumu kupatanisha na maneno ya mtume Paulo kwa Wakristo wa kweli kwenye 1 Wakorintho 1:10 (NW): “Sasa nawahimiza nyinyi kwa bidii, akina ndugu, kupitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kwamba nyote mseme kwa upatano, na kwamba kusiwe na migawanyiko miongoni mwenu, bali kwamba mpate kuunganishwa kwa kufaa katika akili ileile na katika namna ileile ya fikira.”
Ndiyo, wafuasi wa kweli wa Yesu huwa na muungano usioweza kuvunjika miongoni mwao. Kwa sababu wameunganishwa na kifungo cha upendo wa Kikristo, hawana tofauti za kisiasa, kifarakano, au kimafundisho. Yesu alieleza waziwazi kwamba kila mtu ataweza kutambua wafuasi wake kwa “matunda yao,” au utendaji. (Mathayo 7:16) Wachapishaji wa gazeti hili wanakukaribisha uchunguze “matunda” ya Mashahidi wa Yehova, ambao wana muungano wa kweli wa Kikristo katika Ugiriki na vilevile mahali penginepo pote ulimwenguni.
[Picha katika ukurasa wa 18]
Makasisi walipigana na polisi
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 15]
Kutoka kitabu The Pictorial History of the World