Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g96 9/8 kur. 19-21
  • Je, Makasisi wa Othodoksi Wanakaa Macho?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Makasisi wa Othodoksi Wanakaa Macho?
  • Amkeni!—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je, Ni Sehemu ya Ulimwengu Huu?
  • Halina Muungano
  • “‘Ufunuo’ wa Starehe”
  • Kukuza Matumaini Yasiyo ya Kweli
  • Hawakai Macho
  • Kanisa Othodoksi la Kigiriki—Dini Iliyogawanyika
    Amkeni!—1996
  • Patmosi—Kisiwa cha Apokalipsi
    Amkeni!—2000
  • Jitihada za Kutafsiri Biblia Katika Kigiriki cha Kisasa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Iweni Wasomaji Wenye Furaha wa Kitabu cha Ufunuo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1996
g96 9/8 kur. 19-21

Je, Makasisi wa Othodoksi Wanakaa Macho?

NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA UGIRIKI

“YESU alipoingia hekaluni . . . na kuona ‘watu wakiendesha biashara,’ alikasirika na kupaaza sauti: ‘Komeni kufanya nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya bidhaa za biashara!’ Ikiwa yeye angaliabiri siku-hizi hadi kisiwa cha Patmosi, . . . yeye angalisema kwa ukali hata zaidi. Lakini sina uhakika ikiwa kuna yeyote ambaye angemsikiliza.” Ndivyo alivyoomboleza mwandikaji wa habari aliyekuwa akiripoti kile kilichoitwa “kikusanyiko cha Wakristo chenye umaana mkubwa” na “cha wakati wa maana sana katika Ukristo wa kisasa.”

Askofu mwenye kuwakilisha baraza la makanisa wa Constantinople, Bartholomew 1, aonwaye kuwa kichwa cha ufananisho cha Kanisa Othodoksi ulimwenguni pote, aliutangaza mwaka 1995 kuwa “Mwaka wa Apokalipsi.”a Toka Septemba 23 hadi 27, 1995, misherehekeo hiyo ilifikia upeo huku makasisi wa ngazi za juu wa vikundi vingi vya Othodoksi wakikusanyika kwenye kisiwa cha Patmosi. Wawakilishi wa Kanisa Katoliki ya Kiroma, Kanisa la Kianglikana, na dini kadhaa za Kiprotestanti walikuwapo pia. Wakuu wa juu kabisa wa kisiasa na kijeshi wa Ugiriki walihudhuria matukio hayo, pamoja na maofisa wa kigeni, wanasiasa, wafanyabiashara mashuhuri, na wageni wengine walioalikwa kutoka duniani kote.

Wanafunzi wa kitabu cha Ufunuo watakumbuka kikumbusha cha muhimu kilichotolewa hapo ndani na Yesu Kristo: “Tazama! Ninakuja kama mwizi. Mwenye furaha ni yeye akaaye macho.” (Ufunuo 16:15, NW) Kulingana na hili, mwadhimisho huu wa kidini uliotangazwa sana wenye kuhusiana na Ufunuo, twahisi kusukumwa kuuliza: Je, Jumuiya ya Wakristo inakaa macho? Je, wao wanakesha, wakingojea kwa hamu kuja kwa Yesu Kristo akiwa Mfalme aliyetawazwa? Je, karamu hizi zilikuwa zikikazia kichwa cha Biblia ambacho hufikia upeo katika Ufunuo—utakaso wa jina la Yehova na utukuzo wa enzi kuu yake kupitia Ufalme chini ya Kristo? Acheni tufikirie baadhi ya mambo ya hakika.

Je, Ni Sehemu ya Ulimwengu Huu?

Kwa watazamaji wengi muungano usio thabiti kati ya viongozi wa kidini, wanasiasa, na wafanyabiashara wakati wa karamu hizo ulikuwa wenye kuchukiza. Wengine walihisi kwamba vikundi vyote vilivyohusika vilijaribu kutumia hali hiyo kwa ajili ya faida yavyo vyenyewe. Makasisi walikazia uvutano wao kwa kuonekana karibu na wanasiasa mashuhuri, ilhali wanasiasa walijaribu kuboresha sura yao wenyewe kwa kutumia kwa faida yao maoni ya kidini ya umma. Msemaji wa Sinodi Takatifu ya Kanisa la Ugiriki hata alitaarifu: “Ufunuo ulikuwa pia na maana ya kisiasa . . . Ni matukio yanayofunuka katika mandhari ya kidunia.”—Italiki ni zetu.

Hii yahusiana vizuri kama nini na ufafanuzi upatikanao kwenye Ufunuo 17:1, 2, ambapo “kahaba mkuu” wa ufananisho, milki ya ulimwengu ya dini zisizo za kweli ambayo Jumuiya ya Wakristo ni sehemu yayo kuu, huelezwa kuwa inafanya “uasherati” na “wafalme wa nchi”! Badala ya kubaki likiwa safi kiroho na lenye kukesha, Kanisa Othodoksi, kama sehemu nyinginezo za Jumuiya ya Wakristo, limeshawishi watawala wa kisiasa kuingia katika urafiki usio mtakatifu pamoja nalo, likichochea mnyanyaso wa kidini, hasa dhidi ya Mashahidi wa Yehova.

Halina Muungano

Yafaa kuonwa kwamba maaskofu wawili wa Othodoksi hawakuwepo katika sherehe hizo. Kwa nini? Katika tendo la kupinga, askofu Alexios 2 wa Moscow alikataa kuhudhuria kwa sababu ofisi za usimamizi za Constantinople ziliitikia vema maombi yaliyofanywa na dayosisi kuu za Estonia na Ukrainia ya kujiweka chini ya usimamizi wa Constantinople badala ya Moscow. Kulingana na ripoti, “hili ndilo tatizo zito sana kupata kuzuka katika mahusiano kati ya [ofisi za usimamizi za Constantinople] na Kanisa Othodoksi la Urusi lenye nguvu zaidi,” likitisha kutokeza “matokeo yasiyotabirika kwa muungano na mamlaka ya Uothodoksi.”

Kwa kuongezea, askofu wa Yerusalemu alisusia sinodi. Kwa nini? Inaripotiwa kwamba ni kwa sababu alikasirishwa na toba aliyokuwa ameagizwa afanye na ofisi ya usimamizi ya Constantinople miaka mitatu iliyopita kwa kujaribu kuchukua udhibiti wa Kanisa Othodoksi la Australia.

Mwanzoni, Papa John Paul 2 alikuwa aalikwe, lakini hilo likabadilishwa dakika ya mwisho kwa sababu ya upinzani mkali uliozushwa na watu wasiotaka mabadiliko katika Kanisa Othodoksi. Katika Mei 1995 kasisi mkuu wa Othodoksi katika Athene alimbandika papa jina kuwa “mhalifu wa vita.” Kisha ikatangazwa kwamba chini ya hali kama hizo “papa . . . hawezi kushiriki katika sherehe hizo katika Patmosi.”

Kilichoongezea hali hii yenye kuhuzunisha ni hali yenye kupingana kwamba sherehe hizo zilipokuwa zikiendelea, kilometa 1,500 tu kaskazini-magharibi ya Patmosi, “Wakristo” wa Othodoksi na wa Katoliki ya Kiroma walikuwa wakiuana katika Bosnia na Herzegovina!

Kwa wazi, watu wavivu kiroho wanaodai kuwa Wakristo huruhusu mafarakano yawagawanye! Akikataa waziwazi ukosefu huu wa muungano, Iakovos, askofu mkuu Mwothodoksi wa Amerika Kaskazini na Kusini, alitaarifu hivi katika mahojiano: “Tumeshindwa katika jitihada yetu ya kufanya makanisa yaunganike ili kuandaa huduma kwa wanadamu na si kwa wenye uwezo wa ulimwengu huu. . . . Watu wamechoka na . . . baraka za maaskofu.”

“‘Ufunuo’ wa Starehe”

Kile kilichoitwa kuwa “tamasha ya utajiri” kilikuja kuchunguzwa sana. Ripoti moja ya gazeti la habari ilitaarifu: “Siku hizo nne za karamu katika Patmosi hatimaye zilithibitika kuwa ‘ufunuo’ wa starehe. . . . . Uvutio huo wa Byzantium ulipita mipaka ya sherehe ya kikanisa, ukitoa ishara za kugeuza tukio la kidini kuwa msherehekeo wa gharama ya juu.” Wengi walihangaikia kiwango cha fedha kilichotumiwa kwa karamu hizi, hasa kwa wakati ambapo kusalimika kwa watu katika Balkani iliyo jirani na Ulaya Mashariki kulikuwa hatarini. Makadirio fulani hupiga hesabu ya gharama ya huku “kusherehekea kusiko na kifani” kuwa karibu dola milioni 17 (za Marekani). Meli za abiria za starehe zilifika kwenye bandari ya Patmosi zikiwa na baadhi ya wageni matajiri walioalikwa kuhudhuria kusanyiko hilo. Kwa tamauko la wakazi wa hapo, kisiwa hicho kilifanyiwa rekebisho la dakika ya mwisho ili kuonyesha sura nzuri kwa wageni hao wa ngazi za juu—ingawa hakina majengo mazuri ya hospitali na shule.

Maneno ya Ufunuo 18:2, 3, 7 (NW) yanafaa hali hii kama nini: “Wafanya-biashara wanaosafiri wa dunia wakawa matajiri kwa sababu ya nguvu ya anasa yake [Babiloni Mkubwa] isiyo na aibu. Kwa kadiri ambayo alijitukuza mwenyewe na kuishi katika anasa isiyo na aibu, kwa kadiri hiyo mteseni-teseni na kumpa ombolezo”! Wakati ambapo watu wa kawaida wanateseka, Kanisa Othodoksi, badala ya kukaa macho kuandaa faraja na msaada wa kiroho, lilikuwa likijishughulisha sana na karamu za starehe zisizo na thamani kiroho.

Kukuza Matumaini Yasiyo ya Kweli

Wakati wa sherehe hiyo, kulikuwa na mikutano kadhaa na makongamano. Masuluhisho yalitajwa ya kushughulika na matatizo mazito yanayokabili wanadamu. Azimio lilitolewa likiomba wanasayansi watende kwa uharaka kutatua matatizo ya wanadamu. Ufalme wa Mungu haukutajwa hata mara moja. Kinyume cha hilo, kitabu cha Ufunuo, kupatana na Biblia nzima, hukazia kwamba Ufalme wa Mungu mikononi mwa Yesu Kristo ndio suluhisho pekee kwa matatizo yote ya binadamu.—Ufunuo 11:15-18; 12:10; 21:1-5.

Si ajabu kwamba Jumuiya ya Wakristo haichukui kwa uzito tumaini la Ufalme lenye kutegemea Biblia. Akirudia kutaja mtazamo wa wengi, mmoja wa watawa wa makao ya watawa ya Patmosi alikiri hivi waziwazi: “Sisi hatuchukui Ufunuo kuwa andiko lenye mamlaka. Ni aina ya andiko ambalo halisomwi katika makanisa.” Vivyo hivyo, mwanatheolojia mmoja alisema: “Ni hatari kuhusianisha Ufunuo na historia ya ulimwengu huu kama kwamba ni andiko linalofafanua kwa kina kile kitakachotukia. . . . Kufanya hivyo ni ujinga na ufafanuzi wenye hatari.” Ni usingizi wa kiroho mzito kama nini!

Hawakai Macho

Kwa wazi, basi, Jumuiya ya Wakristo haikai macho. Sherehe hii, badala ya kukazia uangalifu kwenye Neno la Mungu na ahadi zake, ilikuwa “sikukuu [ya kidini] ya ufurahiaji na kutumbuizwa” isiyo na thamani na iliyo bure. Hali ya yaitwayo eti makanisa ya Kikristo inafanana sana na ile ya kutaniko katika Laodikia, ambalo Yesu aliliambia hivi: “Wasema, Mimi ni tajiri, nimejitajirisha, wala sina haja ya kitu; nawe hujui ya kuwa wewe u mnyonge, na mwenye mashaka, na maskini, na kipofu, na uchi.”—Ufunuo 3:17

Kwa kupendeza, muungaji-mkono mwenye bidii wa Kanisa Othodoksi aliandikia gazeti la habari kulalamika kwamba “wale tu walionufaika kutokana na” sherehe hii ni Mashahidi wa Yehova. Kwa nini alifikiri hivyo? Yeye alieleza kwamba ufunuo kwa Yohana “una msingi mmoja katika fundisho la mwisho wa ulimwengu na msimamo wa kimafundisho wa Mashahidi wa Yehova.” Ndiyo, ni kweli kwamba Mashahidi wanajitahidi kwa bidii “kufuliza kulinda,” kwa kuendelea kuwa chonjo kwa kutimizwa kwa kusudi la Mungu. Wao wana hamu pia ya kuwasaidia watu wenye mioyo ya kufuatia haki ‘wakae macho ili wapate kufanikiwa kusimama mbele za Mwana wa binadamu,’ Yesu Kristo.—Mathayo 24:42; Luka 21:36, NW.

[Maelezo ya Chini]

a Kulingana na kronolojia ya Jumuiya ya Wakristo, mwaka huo ulitia alama mwaka wa 1,900 wa kuandikwa kwa kitabu cha Ufunuo (Kigiriki, a·po·kaʹly·psis) kwenye kisiwa cha Patmosi. Uthibitisho wenye kutegemeka huonyesha kwamba Ufunuo kiliandikwa katika 96 W.K.

[Blabu katika ukurasa wa 20]

“Tamasha ya utajiri” na “kusherehekea kusiko na kifani”

[Blabu katika ukurasa wa 21]

“Watu wamechoka na . . . baraka za maaskofu”

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 19]

Picha: Garo Nalbandian

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki