Maoni ya Biblia
Je, Mariamu Ni “Mama ya Mungu”?
“TWATAFUTA KIMBILIO CHINI YA ULINZI WA REHEMA ZAKO, EE MAMA YA MUNGU; USIKATAE MAOMBI YETU WAKATI WA UHITAJI LAKINI UTUOKOE TUSIANGAMIZWE MILELE, EE WEWE AMBAYE PEKEE NDIWE MBARIKIWA.”
SALA kama hiyo hujumlisha hisia za mamilioni ya wanaume na wanawake waliojitoa kwa Mariamu, mama ya Yesu Kristo. Kwa maoni yao yeye ni kiwakilishi chenye fadhili cha mama ambaye anaweza kuwaombea kwa Mungu na kwa njia fulani kupunguza hukumu zake kuwaelekea.
Hata hivyo, je, Mariamu kweli ni “Mama ya Mungu”?
Mariamu—“Alipendelewa Sana” na Mungu
Bila shaka Mariamu “alipendelewa sana”—alipendelewa zaidi, kwa hakika, kuliko mwanamke yeyote ambaye amepata kuishi. (Luka 1:28, The Jerusalem Bible) Malaika Gabrieli alimtokea na kumweleza jinsi angependelewa. “Sikiliza!” yeye akasema. “Utapata mimba na kuzaa mwana, na ni lazima umwite Yesu. Yeye atakuwa mkuu naye ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi Sana.” Tukio hili la kimuujiza lingewezekanaje? Gabrieli aliendelea hivi: “Roho Takatifu itakuja juu yako, . . . na uwezo wa Aliye Juu Zaidi Sana utakufunika kwa kivuli chao. Na kwa hiyo, huyo mtoto atakuwa mtakatifu naye ataitwa Mwana wa Mungu.”—Luka 1:31, 32, 35, JB.
“‘Mimi ni kijakazi wa Bwana,’ akasema Mariamu, ‘yale umesema na yanipate.’” (Luka 1:38, JB) Kwa hiyo Mariamu kwa unyenyekevu akakubali mwelekezo huu wa kimungu na baada ya muda akamzaa Yesu.
Hata hivyo, katika karne kadhaa zilizofuata, wenye kujitoa kwake walimkweza kutoka kuwa “kijakazi wa Bwana” wa hali ya chini hadi cheo cha “mama malkia” mwenye uvutano mwingi sana katika mbingu. Viongozi wa kanisa walimtangaza kirasmi kuwa “Mama ya Mungu” katika 431 W.K. kwenye Baraza la Efeso. Ni nini kilichochochea badiliko hilo? Papa John Paul 2 aeleza sababu moja hivi: “Ujitoaji wa kweli kwa Mama ya Mungu . . . umetegemezwa kabisa katika Fumbo la Ule Utatu Uliobarikiwa.”—Crossing the Threshold of Hope.
Kwa hivyo, kumkubali Mariamu kuwa “Mama ya Mungu” hutegemea kuamini Utatu. Hata hivyo, je, Utatu ni fundisho la Biblia?a Chunguza, tafadhali, kile ambacho mtume Petro aliandika katika Biblia. Yeye alionya kwamba “walimu bandia . . . kwa hila wataingiza uzushi [nao] watajaribu kuwatumia vibaya ninyi pia kwa mabishano yao yasiyo na maana.” (2 Petro 2:1, 3, The New Testament in Modern English, iliyoandikwa na J. B. Phillips) Uzushi mmoja kama huo ulikuwa fundisho la Utatu. Mara lilipokubaliwa, hilo wazo kwamba Mariamu alikuwa “Mama ya Mungu” (Kigiriki: Theotokos, ikimaanisha “Mzaa-Mungu”) lilikuwa la kiakili kabisa. Katika kitabu chake The Virgin, Geoffrey Ashe hutaarifu kwamba “ikiwa Kristo alikuwa Mungu, Mtu wa Pili wa Utatu,” kama walivyosababu Wanautatu, “basi mama yake katika udhihirisho wake wa kibinadamu alikuwa Mama ya Mungu.”
Ikiwa Yesu alikuwa “Mungu kamili na kabisa,” kama kinavyotaarifu Catechism of the Catholic Church iliyo mpya, basi Mariamu angeweza kuitwa kwa haki “Mama ya Mungu.” Ingawa hivyo, ni lazima isemwe kwamba Wanautatu wengi wa mapema waliona likiwa jambo gumu kukubali fundisho hili lilipotolewa mara ya kwanza—kama ilivyo na Wanautatu Waprotestanti leo. Limeitwa “fumbo la kiibada, ‘yeye ambaye hangeweza kutoshea katika mbingu alitoshea katika tumbo la uzazi la Mariamu.’” (The Virgin)—Linganisha 1 Wafalme 8:27.
Lakini je, Yesu Kristo kweli ni “Mungu kamili na kabisa”? La, yeye hakudai hivyo kamwe. Badala ya hivyo, sikuzote yeye alikubali cheo chake cha chini ya Mungu.—Ona Mathayo 26:39; Marko 13:32; Yohana 14:28; 1 Wakorintho 15:27, 28.
‘Abuduni Katika Njia Ambayo Inastahili Viumbe Wanaofikiri’
Hata hivyo, Biblia hutia moyo Wakristo watumie uwezo wao wa kufikiri katika ibada. Hatuambiwi tuamini kwa wepesi bila ushuhuda katika kitu ambacho kimefichika kama fumbo. Badala ya hivyo, asema mtume Paulo, twapaswa ‘kuabudu katika njia ambayo inastahili viumbe wanaofikiri.’—Warumi 12:1, JB.
“Hatukutiwa moyo kamwe kufikiri kuhusu hilo,” asema Anne, ambaye alilelewa akiwa Mkatoliki. “Hatukulitilia shaka. Tuliamini tu kwamba Yesu alikuwa Mungu, kwa hiyo Mariamu alikuwa ‘Mama ya Mungu’—kwa kushangaza hatukufikiria kamwe kuhusu itikadi hii!” Kumbuka, Catechism of the Catholic Church husema kwamba kila mshiriki wa “Umoja wa kimungu” ni “Mungu kamili na kabisa.” Hutaarifu kwamba hakuna miungu watatu tofauti. Basi, je, tuamini kwamba kadiri chembe zenye kuishi katika tumbo la uzazi la Mariamu zilivyogawanyika na kuzidi kugawanyika, “Mungu kamili na kabisa” alitoshea katika kiinitete ambacho katika mwezi wa kwanza wa mimba kilikua hadi kufikia urefu usiozidi robo moja ya inchi na kilikuwa na macho na masikio madogo mno?
Kumbuka kwamba malaika Gabrieli alimwambia Mariamu kwamba mtoto wake angeitwa “Mwana wa Aliye Juu Zaidi Sana” na “Mwana wa Mungu,” si “Mungu Mwana.” Ikiwa, kwa hakika, Yesu alikuwa Mungu Mweza Yote, kwa nini malaika Gabrieli hakutumia usemi uleule unaotumiwa na Wanautatu leo—“Mungu Mwana”? Gabrieli hakutumia usemi huo kwa kuwa hilo fundisho halipatikani katika Biblia.
Bila shaka, tumepungukiwa katika uelewevu wetu wa kazi za Mungu. Lakini kuelewa Maandiko ifaavyo hutusaidia kuamini kwamba Mungu Mweza Yote, Muumba wa uhai wote, alikuwa na uwezo wa kuhamisha kimuujiza uhai wa Mwana wake mpendwa, Yesu Kristo, katika tumbo la uzazi la Mariamu na kisha kulinda ukuzi wao kupitia kani Yake ya utendaji, au roho takatifu, hadi Mariamu alipokuwa mama ya Yesu—Mwana wa Mungu.
Ndiyo, Mariamu alibarikiwa sana kuwa mama ya yule ambaye alikuja kuwa Kristo. Si kumkosea heshima kukubali kwamba fundisho la wazi la Biblia—kutia ndani rekodi ya unyenyekevu wa Mariamu mwenyewe—hupinga kumpatia cheo “Mama ya Mungu.”
[Maelezo ya Chini]
a Tafadhali ona Je! Uamini Utatu? kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]
Museo del Prado, Madrid