Kushinda Msiba kwa Nguvu za Yehova
NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA HISPANIA
MNAMO Februari wa mwaka huu, wengi wa Kutaniko la Bailén la Mashahidi wa Yehova nchini Hispania walifurahia siku nzuri wakiwa pamoja katika Milima ya Sierra Nevada iliyo karibu. Lakini wakiwa kilometa tano kutoka nyumbani, gari lililokuwa likija liliingia katika njia ya basi walimokuwa wakisafiria, likisababisha dafrao. Kukawa na mlipuko, basi likafunikwa kwa miale ya moto. Baadhi ya abiria waliweza kutoka nje haraka, lakini wengi waliokuwa sehemu ya nyuma ya basi walishindwa na moshi wakafa.
Kwa ujumla Mashahidi 26 walikufa, kutia ndani wahudumu wanne wa wakati wote pamoja na watoto kadhaa—karibu robo ya Kutaniko la Bailén. Mfalme wa Hispania, Juan Carlos, alitaja hisia za Wahispania wengi alipoandika hivi katika telegramu iliyopelekewa meya wa Bailén: “Nimeshtuliwa sana na aksidenti hiyo yenye kuhuzunisha. Pokea rambirambi zetu za moyoni. Tafadhali wape familia za waliokufa pole zetu na utegemezo wetu katika kipindi hiki chenye maumivu.”
Swali lililokuwa akilini mwa baadhi ya maelfu ya watu waliohudhuria maziko lilikuwa, Ni kwa nini misiba kama hiyo hutukia? Kwa wazi, aksidenti ambazo husababishwa na “wakati na tukio lisilotazamiwa” zaweza kuathiri watu wa Yehova kama watu wengine wowote. (Mhubiri 9:11, 12, NW) Hata hivyo, Yehova aahidi kwamba karibuni misiba kama hiyo itaondolewa isiwepo tena.—Ufunuo 21:4, 5.
Washiriki wengi wa familia ya ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Hispania na maelfu ya Mashahidi kutoka sehemu nyinginezo za nchi hiyo walisafiri Bailén ili kufariji na kutegemeza ndugu za huko. Watu wa Bailén, pamoja na wenye mamlaka wa huko na wenye mamlaka ya kimkoa, pia walihuzunika pamoja na familia za Mashahidi. Wachunguzi wengi walivutiwa na nguvu za kihisia-moyo za Mashahidi waliofiwa.
“Nimewajua Mashahidi kwa miaka mingi,” akaeleza Antonio Gómez, meya wa Bailén, “na ingawa mimi ni mwagnosti, navutiwa na imani yenu. Aksidenti hiyo ilipotokea, mara moja nilifikiri kwamba ushikamano wenu wa kidini na kibinadamu ungewawezesha kushinda msiba huo kuliko vikundi vingine. Nimeona jinsi mji mzima umetegemeza familia zilizofiwa. Labda awali, watu hawakuwafahamu vema, lakini nafurahi kuwaambia kwamba dhana mbaya zimeisha. Mna nguvu za ndani ambazo ni vigumu kwa mtu asiye Shahidi kuelewa.”
José Borrell, waziri wa ujenzi wa umma aliyehudhuria maziko akiwa mwakilishi wa serikali ya Hispania, alikiri hivi: “Unaweza kuwaambia nini wale ambao wamepoteza karibu familia nzima mara moja? Huwezi kusema lolote ambalo wao wenyewe hawajapata katika imani yao. . . . Mna imani ya ajabu sana.”
‘Farijianeni Kila Mtu na Mwenzake’
Wao walipata nini “katika imani yao”? Zaidi ya yote, wao walipata faraja kutoka kwa Yehova, “Mungu wa faraja yote; atufarijiye katika dhiki zetu zote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Japo huzuni yao, wao walipata nguvu za kufarijiana, wakitii maneno haya ya Paulo kwa Wathesalonike: “Farijianeni na kujengana kila mtu na mwenzake.”—1 Wathesalonike 5:11.
Lilikuwa ono lenye kugusa moyo sana kuona ndugu na dada Wakristo, baadhi yao wakiwa wamepoteza watu wa ukoo wapatao wanane, wakizuru washiriki wengine wa kutaniko wenye kuomboleza. “Tulipoonana, tulilia machozi. Lakini kati ya machozi hayo tulijikumbusha tumaini la ufufuo, nasi tukafarijika,” akaeleza Francisco Saez, mwangalizi-msimamizi, ambaye alipoteza watoto wake wa pekee wawili.
“Hatujaacha utendaji wetu wa kuhubiri, nasi tumejitahidi kuzuru watu wa ukoo waliofiwa ambao si Mashahidi, tukitumia broshua Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa.” Fransisco akaendelea kusema: “Mimi binafsi nilitaka kuhubiri, kwa kuwa nilijua kwamba ni kwa kuhuburi ningepata kuhisi vizuri. Na kwa kweli, ingawa nilienda nikilia machozi, nilirudi nyumbani nikiwa nimefarijika.”
Watu wa Bailén waliitikia vizuri sana kazi ya ushahidi. Juma moja baada ya aksidenti, Encarna, aliyekuwa akiomboleza kifo cha binti wawili na wajukuu wanne, alizuru bibi mmoja ambaye majuzi alikuwa ameanza kujifunza Biblia naye. Encarna alikuwa akifariji mwanamke huyu kupitia Maandiko, ambaye mume wake alikuwa amekufa miezi minne iliyokuwa imepita. “Sasa ni lazima tufarijiane,” yeye akasema, walipoendelea kujifunza broshua Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa.
Utegemezo wa udugu wa ulimwenguni pote ukaja upesi pia. “Kutaniko lote linahisi limetiwa moyo kwa maelfu ya barua na telegramu ambazo tumepokea,” akaeleza Francisco Capilla, mwandishi wa kutaniko. “Inalazimu posta itoe gari la kuleta barua hizo zote moja kwa moja kwetu. Tunashukuru sana kwa hangaiko lenye upendo la akina ndugu.”
Tumaini Kutokana na Msiba
Je, kuna lolote jema liwezalo kutokea kutokana na msiba huo? “Moyo wake mwenye hekima umo nyumbani mwa matanga,” akaandika Mfalme Sulemani wa kale. (Mhubiri 7:4) Kwa kupatana na kanuni hii, msiba wa Bailén umefanya watu wengine wafikirie kwa uzito zaidi uhusiano wao pamoja na Mungu. Faustino, mume asiyeamini ambaye alipoteza wawili kati ya watoto wake sita katika hiyo aksidenti alimwambia hivi mke wake Dolores: “Nina habari njema za kukueleza. Nitaanza kujifunza Biblia, kwa kuwa nataka kuwaona watoto wangu katika ulimwengu mpya.”
Ingawa ndugu na dada zetu katika Bailén hawatashinda huzuni yao upesi, wao wanafariji wengine nao wanafarijiwa. Yehova anawaimarisha kwa roho yake na kwa utegemezo wa ndugu na dada wengi wenye upendo. Tunaendelea kupeleka sala zetu juu kwa Baba yetu wa kimbingu kwa niaba yao.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Wanne kati ya wale waliokufa