Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g96 9/22 kur. 8-10
  • Dhibiti Maisha Yako Sasa!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Dhibiti Maisha Yako Sasa!
  • Amkeni!—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Maoni ya Biblia Ni Nini?
  • Msaada Bora Zaidi Wapatikana
  • “Neno la Mungu Li Hai, Tena Lina Nguvu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Je, Ujilaumu Mwenyewe Au Chembe Zako za Urithi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Je! Mungu Anajali?
    Je! Mungu Anajali?
  • Jinsi Unavyoweza Kubadili Namna Ulivyo
    Amkeni!—1992
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1996
g96 9/22 kur. 8-10

Dhibiti Maisha Yako Sasa!

UTAFITI wa kisayansi kuhusu mwenendo na msukumo wa kibinadamu umetunufaisha kwa njia nyingi. Labda tumesaidiwa kukabiliana na ugonjwa kwa kuwa na ufahamu wa kina kuuhusu. Kwa wakati uo huo, ni jambo la busara kutahadhari kuhusu nadharia zenye kuchochea hisia, hasa zile ambazo yaonekana zapingana na kanuni zilizowekwa.

Kuhusu suala la jeni na mwenendo, maswali yazuka: Je, twaweza kuondosha lawama na kutokubali kulaumika kwa matendo yetu? Je, twaweza kutoa udhuru au hata kumlaumu mtu fulani au kitu kingine kwa ukosefu wowote wa busara au kosa tulilofanya, hivyo tukijiunga na idadi yenye kuongezeka katika kizazi hiki cha “si-mimi”? Sivyo hata kidogo. Watu walio wengi hukubali kwa utayari sifa kwa mafanikio yoyote maishani, kwa hiyo kwa nini wasikubali kwa utayari vilevile lawama kwa makosa yao?

Kwa hiyo, twaweza kuuliza, Neno la Mungu Biblia Takatifu, husema nini kuhusu ni nani au ni nini kiongozacho maisha yetu leo?

Maoni ya Biblia Ni Nini?

Jambo la kwanza tupaswalo kutambua ni kwamba sisi sote huzaliwa katika dhambi iliyorithiwa kutoka kwa wazazi wetu wa awali, Adamu na Hawa. (Zaburi 51:5) Kwa kuongezea, twaishi katika wakati wa kipekee, uitwao “siku za mwisho,” wakati ambapo watu wanajionea “nyakati zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1, NW) Hilo laonyesha kwamba, kwa ujumla, twakumbana na matatizo katika kudhibiti maisha yetu ifaavyo kuliko waliotutangulia walivyofanya.

Hata hivyo, wanadamu wote ni viumbe hai walio huru kuchagua mwendo watakaofuatia, wawezao kufanya machaguo yao ya kibinafsi. Kwa kadiri hiyo wanadhibiti maisha yao. Imekuwa hivyo tangu nyakati za mapema na inaweza kuonwa kwa maneno ya Yoshua kwa taifa la Israeli: “Chagueni hivi leo mtakayemtumikia.”—Yoshua 24:15.

Biblia hukubali kwamba Shetani Ibilisi ametupwa kutoka mbinguni na sasa, zaidi ya wakati mwingineo wote, ana uvutano wenye nguvu wa kuifanyia mabaya jamii yote ya kibinadamu. Hiyo pia hutuambia kwamba hata katika siku za mtume Yohana, ulimwengu wote ulikuwa chini ya uwezo wa yule mwovu. (1 Yohana 5:19; Ufunuo 12:9, 12) Hata hivyo, kama vile Mungu Mweza Yote hadhibiti kila kitendo chetu au kupanga kimbele mwisho anaoujua yeye pekee, hatupaswi kumwekea Shetani lawama moja kwa moja kwa kila kosa au ukosefu wetu wa mafanikio. Kweli ya Kimaandiko yenye kusawazisha ni kwamba “kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa. Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi.” (Yakobo 1:14, 15) Mtume Paulo aliandika maneno haya yaliyopuliziwa: “Msidanganyike, Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.”—Wagalatia 6:7.

Kwa hiyo Yehova Mungu anatutoza hesabu mtu mmoja-mmoja kwa matendo yetu. Twapaswa kuwa waangalifu tusijaribu kujiondolea lawama kwa sababu ya mfanyizo wetu wa kijeni na kutokamilika tulikorithi. Mungu aliitaka jumuiya yenye jeuri, ya ugoni-jinsia-moja ya Sodoma na Gomora ya kale itoe hesabu kwa matendo yayo yenye ufisadi. Kwa wazi, yeye hakuona wakazi hao kuwa viumbe maskini, wa kuhurumiwa ambao hawakuweza kujizuia eti kwa sababu ya kasoro fulani ya kijeni. Sawa na hivyo; watu walioishi katika siku za Noa walikuwa na uvutano mwingi mwovu kuwazunguka; hata hivyo iliwabidi wafanye chaguo, uamuzi wa kibinafsi, ikiwa wangalisalimika Gharika iliyokuwa karibu kutokea. Ni wachache waliofanya chaguo lifaalo. Wengi hawakufanya hivyo.

Nabii Mwebrania Ezekieli athibitisha udhibiti wa kibinafsi wahitajiwa ikiwa tutapata upendeleo wa Mungu: “Lakini ukimwonya mtu mbaya, wala yeye hauachi ubaya wake, wala njia yake mbaya, atakufa katika uovu wake; bali wewe umejiokoa roho yako.”—Ezekieli 3:19.

Msaada Bora Zaidi Wapatikana

Bila shaka, sote twahitaji msaada ili kujidhibiti kibinafsi katika maisha yetu ya kila siku, na kwa wengi wetu, hili ni tatizo gumu sana. Lakini hatuhitaji kukata tumaini. Ingawa mielekeo yetu iliyorithiwa ya kutenda dhambi haikubaliwi na Mungu, ikiwa tunataka kurekebisha mwenendo wetu, yeye atatuandalia msaada bora zaidi upatikanao—roho yake takatifu na kweli yake iliyopuliziwa. Licha ya mwelekeo wa kijeni ambao huenda tukawa nao na uvutano wowote wa nje ambao huenda ukatuathiri, twaweza ‘kuuvua utu wa zamani pamoja na mazoea ya huo, na kujivika wenyewe utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba.’—Wakolosai 3:9, 10, NW.

Wakristo wengi katika kutaniko la Korintho walifanya mabadiliko yenye kutazamisha katika mwenendo wao. Rekodi iliyopuliziwa hutuambia: “Waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi. Na baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa, lakini mlitakaswa, lakini mlihesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo na katika Roho wa Mungu wetu.”—1 Wakorintho 6:9-11.

Kwa hiyo ikiwa twang’ang’ana na kutokamilika, tusijiache tushindwe, Wakristo wengi wa siku ya kisasa wamethibitisha kwamba kwa msaada wa Yehova, waliweza ‘kugeuzwa kwa kufanya upya nia zao, wapate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.’ Wao hulisha akili zao na mambo yoyote yaliyo ya kweli, ya uadilifu, safi, yenye kupendeka, yenye sifa njema, na yenye kusifika; nao huendelea ‘kuyatafakari hayo.’ Wao hula chakula kigumu cha kiroho na kwa kukitumia wanazoeza uwezo wao wa kufahamu ili kutofautisha lililo jema na baya.—Warumi 12:2; Wafilipi 4:8; Waebrania 5:14.

Inachangamsha moyo kujua juu ya ming’ang’ano yao, kutofaulu kwao kwa muda, na mafanikio yao ya hatimaye kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu. Mungu atuhakikishia kwamba kubadili mwenendo wetu mara nyingi huhusisha moyo na tamaa zao: “Hekima itaingia moyoni mwako, na maarifa yatakupendeza nafsi yako, busara itakulinda; Ufahamu utakuhifadhi. Ili kukuokoa na njia ya uovu.”—Mithali 2:10-12.

Kwa hivyo, ikiwa wataka kufanya uhai udumuo milele uwe mradi wako—maisha yasiyo na taabu za ulimwengu huu mwovu na yasiyo na kutokamilika kwenye kudhoofisha—‘jitahidi’ kudhibiti maisha yako sasa na kuongozwa na hekima ya kimbingu. (Luka 13:24) Jiache usaidiwe na roho takatifu ya Yehova ili uweze kutokeza matunda ya kujidhibiti. Fanya kupatanisha maisha yako na sheria za Mungu kuwe tamaa ya moyo wako, na utii shauri hili: “Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.” (Mithali 4:23) Kupata “uzima ulio kweli kweli” katika ulimwengu mpya wa Mungu—ambao katika huo Yehova Mungu atarekebisha mapungukio yoyote ya kijeni kwa msingi wa imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo—kwastahili jitihada zote unazofanya za kudhibiti maisha yako katika ulimwengu huu!—1 Timotheo 6:19; Yohana 3:16.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kujifunza Biblia kwaweza kutupatia nguvu ya kushinda udhaifu mbalimbali uliotushika sana

[Picha katika ukurasa wa 9]

Funzo la Biblia laweza kutusaidia kushikamana na viwango vya adili vya Mungu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki